Friday 5 December 2014

KUKUZA VIONGOZI WA KANISA

[Front Cover]
MBWEHA
TALLY HO!
Msingi Kwa Ajili Ya Kujenga
Wanafunzi Wa Yesu
Wanaojiongeza Na Wenye Maono
Ya Kuigusa Dunia Nzima
Kimeandikwa Na
Herb Hodges
Kimefasiriwa Na
Mch. Simon Joel Vomo
ii
[Back Cover]
Herb Hodges aliyezaliwa na kukulia jimbo la Arkansas Marekani, aliokoka siku alipotimiza miaka kumi na nane, na akaitwa kuwa mhubiri muda mfupi baada ya hapo.
Ndugu Hodges alisoma katika Chuo Kikuu cha Biblia kiitwacho Southwestern Seminary huko Fort Worth Texas, na kuhitimu shahada ya Masters of Divinity mwaka wa 1962. Alichunga makanisa kwa miaka 27 katika majimbo ya Arkansas, Texas na Tennessee. Mwaka wa 1980, Ndugu huyu akawa mwinjilisti, mwenye kufanya mikutano ya uamsho, makongamano ya Biblia, makongamano ya Maisha ya Kiroho na Ufuasi. Huduma hii imemfanya atembelee karibu majimbo yote hamsini ya Marekani.
Amesafiri sana katika nchi za nje kwa ajili ya kufundisha wachungaji na viongozi kuhusu mkakati wa kujenga wanafunzi wa Yesu wanaojiongeza na wenye maono ya kuigusa dunia nzima katika kutimiza Agizo Kuu la Kristo. Amefanya safari kwa ajili ya kusudi hilo katika nchi za nje ni zaidi ya 70.
Ndugu Hodges na Judy mkewe wanakaa mjini Memphis, jimbo la Tennessee.
iii
ORODHA YA YALIYOMO
UTANGULIZI .................................................................................................................... IV
SHUKRANI ...................................................................................................................... VII
SURA YA 1 ........................................................................................................................... 1
MAONO NI MUHIMU KIASI GANI? ...................................................................................... 1
SURA YA 2 ......................................................................................................................... 34
AGIZO LENYE KUAMUA WAJIBU WETU ............................................................................ 34
SURA YA 3 ......................................................................................................................... 85
WAZO LENYE KUAMUA NJIA TUTAKAYOTUMIA ............................................................... 85
SURA YA 4 ....................................................................................................................... 104
UFUNGUO ULIOKO MLANGONI MWA HISTORIA YA KANISA ........................................... 104
SURA YA 5 ....................................................................................................................... 133
VINAVYOTAKIWA ILI KUFANYA WANAFUNZI ................................................................. 133
DAWA YA DAKTARI KUTIBU TATIZO LA KUACHA AGIZO KUU ....................................... 133
SURA YA 6 ....................................................................................................................... 158
MPANGO WA MUNGU WA KUONGEZA ........................................................................... 158
SURA YA 7 ....................................................................................................................... 177
HEKIMA YA MKAKATI WA YESU ................................................................................... 177
SURA YA 8 ....................................................................................................................... 197
JINSI KIWANGO HIKI KIFANYAVYO KAZI KANISANI ........................................................ 197
SURA YA 9 ....................................................................................................................... 219
MANENO YAKE YA MWISHO, WOSIA WAKE .................................................................. 219
SURA YA 10 ..................................................................................................................... 241
MBWEHA TALLY HO! ..................................................................................................... 241
Maana Ya Jina La Kitabu ........................................................................................ 241
KUMALIZIA .................................................................................................................... 253
MAISHA YA MBWA WA MWITUNI .................................................................................. 253
MUHTASARI WA KILA SURA .................................................................................... 264
MASWALI NA MAPENDEKEZO KWA AJILI YA KUJIFUNZA HIKI KITABU . 270
iv
Utangulizi
Kanisa la kawaida mahali popote lina kundi kubwa la “watendaji” wasiotumiwa ndani ya washirika wake. Mkristo wa kawaida hana kazi kulingana na viwango vya Kristo vya ajira, na yule Mkristo wa kawaida ambaye ana ajira, mara nyingi “hana kazi ya kutosha”. Basi anatumia muda mwingi na juhudi nyingi katika shughuli zenye kutoa matokeo madogo sana kwa habari ya kuwafikia na kuwajenga watu. Kanisa la kawaida la Kikristo hukutana Jumapili kwa Jumapili katika “jengo” na washirika wake ni “wasikilizaji” binafsi, ambao ni sehemu ya “wasikilizaji” wengine. Kwa kifupi ni kwamba, kanisa la kawaida limejaa “walioketi” ambao kusudi lao pekee ni kuja kanisani, kusikiliza mahubiri na kuondoka, wakitazamia kwamba mpango huo utasaidia katika kufikisha roho zao mbinguni kwa namna fulani na kuwawezesha kuwa na maisha mazuri kabla ya kufika huko. Kufanana kwa maisha hayo na maisha ya Kikristo yanayo-onekana katika Agano Jipya ni kwa bahati tu.
Ni dhahiri kwamba sisi Wakristo lazima tujifunze tena Agano Jipya, ambalo ndicho kitabu chetu cha kuongoza utendaji, na tujilazimishe kuona mambo kama yalivyo wakati tunapofanya hivyo. Lazima tujitangaze kuwa huru kutokana na mapokeo na desturi, na tugundue Agano Jipya linatuambia nini juu yetu sisi wenyewe, na kazi ambayo tumepewa na Mungu.
v
Mwandishi maarufu aitwaye Charles Swindoll aliandika hivi: “Hakuna kundi katika historia lililojithibitisha kuwa na uwezo katika utendaji kama ile timu ya uinjilisti ya karne ya kwanza – wale watu waliokuwa karibu sana na Kristo.” Huo ni ukweli usiokanika. Kwa nini? Bila shaka kilichochangia sana ni utaratibu ule ambao Yesu aliutumia katika kuwafundisha. Utaratibu huo umejengwa juu ya neno kubwa sana – “mwanafunzi”. Neno hilo linaonekana kwa nguvu sana katika vitabu vitano vya kwanza vya Agano Jipya, likitokea mara 269 (katika Injili ya Mathayo hadi Kitabu cha Matendo). Linatumika kama jina na tendo. Tena, linapotumika kama tendo, neno lenyewe ndilo amri pekee katika Agizo Kuu ambalo Yesu aliwapa wanafunzi Wake. Alisema hivi, “Wafanyeni watu kuwa wanafunzi”. Sasa, kwa uhalisi wa makundi makubwa ya waamini wasioendelezwa katika kanisa la leo (tena wengi wao wako kanisani kila tunapokutana), ni halali kwetu kuendelea kusema kwamba tumelifafanua vizuri neno ‘mwanafunzi’? Au kwamba sisi tumeelewa ipasavyo maana (au utaratibu) ya “kuwafanya watu kuwa wanafunzi”? Kwa uhalisi wa kanisa kutokuwa na mguso mkubwa kwa ujumla, pamoja na mabilioni ya watu ambao hawafikiwi na Injili duniani siku hizi, tunaweza kweli kuendelea kuamini kwamba tunatimiza Agizo Kuu? Sidhani.
Kurasa hizi ni mtazamo mpya na juhudi mpya za kutafsiri kwa kifupi sana kwamba sisi ni nani kama waamini wa Kristo, na kazi yetu kama wafuasi Wake. Ni maombi yangu kwamba Mungu
vi
atatusumbua na kutuamsha kupitia kurasa hizi kuwa na mtazamo mpya, kutaka kujihusisha kwa upya, na kuwa na matokeo mapya katika kutimiza Agizo Kuu la Bwana wetu.
Ninawiwa na marafiki wengi sana na waandishi wasio na idadi – wa kawaida na wa kanisa – kwa ajili ya mawazo tele na mbinu ambazo zimefupishwa na kuandikwa hapa. Pia, ninawiwa na wengi ambao wamenitia moyo kuandika vitu hivi, na wachache ambao wamenisaidia kufanya hivyo. Ushawishi wao ninauacha mpaka tutakapofika kwenye Kiti cha Hukumu cha Kristo, ambapo utatathminiwa kwa ubora sana na kupewa thawabu nzuri na bora kuliko niwezayo kuitoa mimi.
Herb Hodges - Mwandishi
vii
Shukrani
Haiwezekani hata kuzaliwa kama mwanadamu bila kudaiwa sana. Kila mwanadamu anapozaliwa anakuwa na deni la pango la miezi tisa huko alikokuwa anakaa!
Kati ya wote wenye madeni, mimi ni mmoja mwenye kudaiwa sana, japo si kifedha. Watu wengi sana – walio hai na walikwisha pumzika – wamechangia faida nyingi sana maishani mwangu – hata siwezi kutaja yote. Ukweli ni kwamba siwezi hata kulipia riba ya kile walichowekeza kwangu.
Kwa habari ya kijitabu hiki, ninawiwa sana na makundi ya waandishi walioandika mawazo yao na kuhakikisha kwamba nimeyapata. Ninawiwa na wahubiri, waalimu na wenzangu ambao wametia kweli nyingi katika akili zangu, katika kipindi chote cha Ukristo wangu. Ninawiwa na watu kama Dom Fosco, ambaye kwa uvumilivu na uangalifu sana alihariri na kupanga upya kurasa hizi mara kadhaa; na Clint Davis, aliyeandika sura inayohusu Utangulizi wa Injili ya Luka (akitumia maandishi niliyotoa pamoja na kanda). Zaidi, ninawiwa sana kwa mke wangu mpenzi Judy, anayehudumia vile vile kama msaidizi wangu na mwandishi wangu, kwa sababu ya kunipenda na kuniunga mkono kwa hali yake tulivu, na kwa kuongezea hekima yake kubwa katika yangu ndogo niliyo nayo.
viii
Ninawathamini na kuwaheshimu na kuwashukuru hao na wengine wengi. Wamenibariki sana! Narudia kusema tena – wamenipa deni kubwa sana. Rafiki zangu, asanteni mno. Herb Hodges
1
Sura Ya 1
Maono Ni Muhimu Kiasi Gani?
“Mahali ambapo hakuna maono, watu huangamia.”
Mithali 29:18
Katika lugha ya kiroho, “mtazamo wa KiMungu”, “hekima”, “uwezo wa kuona”, “kuangaziwa” na “maono” ni maneno yanayofanana kwa kiasi fulani. Maandiko mengi katika Neno la Mungu hudhihirisha umuhimu wa maono kama hayo. Tunasoma hivi katika Zaburi 119:18, “Unifumbue macho yangu niyatazame maajabu yatokayo katika Sheria Yako”. Na katika Zaburi 119:130 tunasoma hivi, “Kufafanusha maneno yako kuwatia nuru, na kumfahamisha mjinga.” Katika Yakobo 1:5 tunaambiwa hivi, “Lakini mtu wa kwenu akipungukiwa na hekima, na aombe dua kwa Mungu”. Katika Waefeso 1:15-19 – pamoja na mantiki yake – Paulo ameandika mojawapo ya sala zake kuu. Ninaamini kwamba hii ndiyo sala muhimu zaidi ambayo mwanadamu anaweza kumwombea mwenzake. Ni maombi ya “kuangaziwa”, kitu kimoja muhimu sana kwa ajili ya kuelewa mambo ya Mungu baada ya Kuzaliwa Mara Ya Pili. “Mtu asipozaliwa mara ya pili, hawezi kuona”. Mambo mawili ya lazima kwa ajili ya ufahamu wa kiroho ni kuzaliwa upya na kuangaziwa.
2
Andiko kiongozi katika somo hili linatuonyesha kwa hali ya kinyume jinsi ambavyo “maono” ni muhimu. Kuona kwa mtu hutegemea “vioo” anavyotumia kuonea, kama ambavyo kusikia kwake kunavyotegemea “chujio” analotumia kusikiliza. Tunapoanza mafunzo haya kuhusu Agizo Kuu la Bwana Yesu kwa watu Wake, ni muhimu sana tuelewe thamani ya maono. Tunaambiwa na Mithali 29:18 kwamba, “Mahali ambapo hakuna maono, watu huangamia.” Huu ni mstari kamili: unafanya kazi kila mahali kwa ukamilifu kabisa.
WAZO LA KIROHO
Kwanza kabisa, fikiri kuhusu wazo la kiroho litolewalo hapa – wazo la “maono”. Likitazamwa katika mantiki yake, ni dhahiri kwamba maono yanayotajwa hapa ni ya aina pekee, maalum. Hapa kinachosemwa ni maono ya kiroho, ambayo ni maono ya maana sana mtu anayoweza kuwa nayo.
Kila kitu huanza kwa maono. Utakuwa kama unavyoona. Usichokiona huwezi kuwa. Utakuwa unachotazama, lakini usichokitazama, huwezi kuwa. Yaani, kile unachotazama kwa upendo sana, kwa kutamani, na kwa muda mrefu, ndivyo utakavyokuwa. Utakuwa kama kitu unachokitazama.
Hili jambo ni dhahiri katika dunia ya teknolojia ya vitu vya umeme siku hizi. Ukiacha picha fulani kwenye kioo cha kompyuta kwa muda mrefu sana, kitajiingiza mpaka katika mfumo mzima wa
3
kompyuta na kuingia katika kila eneo na programu yoyote itakayotumika baada ya hapo. Kanuni hiyo ni halisi hata kwako: Kile unachotazama kwa muda mrefu sana kitaamua maisha yako.
Mkayun mmoja kutoka jimbo la Louisiana alikuwa anamwuza punda wake. Mtu mmoja aliyetaka kumnunua akamwuliza hivi: “Je, punda mwenyewe ana matatizo yoyote?” Yule Mkayun akajibu, “Haonekani vizuri” (japo kwa lugha yake alimaanisha haoni vizuri). Mnunuzi akasema, “Sijali sana kwa hilo. Je, anafanya kazi sana?” Akajibiwa, “Naam, ana bidii sana katika kazi, ila, haonekani vizuri tu” (kumbuka maana yake). Basi yule mtu akamnunua, na mwenye kumwuza akampandisha kwenye gari la huyo bwana mpya. Alipofika shambani kwake, alifungua nyuma ya gari lake na kumshusha yule punda. Mara, punda akagonga mti, halafu akajigonga kwenye zizi. Mkulima akapiga kelele kwa hasira, “Nimedanganywa! Huyu punda ni kipofu!” Akampakia punda kwenye gari, akamrudisha kwa mwenyewe na alipomfikisha, alipiga kelele na kusema, “Wewe ulinidanganya kuhusu huyu punda. Punda mwenyewe kipofu. Uliniambia uongo!” Yule mwuza punda akasema, “Hapana, sikukudanganya. Nilikwambia vizuri kabisa kwamba, ‘punda haonekani vizuri’!” (Bila shaka unakumbuka maana yake kwa kikwao.)
Ndugu Oswald Chambers ambaye ni mwandishi maarufu wa kitabu kiitwacho My Utmost For His Highest na vitabu vingine vizuri sana vya kujisomea kwa ajili ya kukua kiroho, aliandika kwa
4
utambuzi mkubwa sana, kama ifuatavyo: “Ni rahisi zaidi kumtumikia Mungu bila maono. Ni rahisi kumfanyia Mungu kazi bila ya mwito. Kwa sababu, hapo husumbuliwi na yale Mungu anayotaka. Unaongozwa na akili za kawaida, ila juu yake unatia hisia za Kikristo. Lakini kama ukisikia agizo kamilifu la Yesu Kristo hata mara moja tu, ufahamu wa kile Mungu anachotaka kitakuwa lengo lako tangu wakati huo na kuendelea, nawe hutaweza kumtumikia kwa msingi wa akili zako za kawaida.” Hebu soma maneno hayo mara kadhaa kabla ya kuendelea mbele katika mafunzo haya. Nimetumia wino mwepesi kutilia mkazo.
Kuona kimwili ni muunganiko wa vidokezo vyenye kuonekana (yaani, kitu halisi katika dunia inayomzunguka mtu) na ujuzi pekee (jinsi mtu anavyotambua hivyo vidokezo vinavyo-onekana). Kidokezo chenye kuonekana kinaweza kisibadilike kamwe, lakini kikiisha onekana na kunasa kwenye macho ya mtu, kinaweza kupotoshwa, kukataliwa, au kupokelewa – yaani, kinategemea tafsiri ya mtu aliyekiona
Katika zile hisia tano za asili, kuona ni hisia mojawapo ambayo mtu hafai kupoteza. Ralph Sockman alikuwa sahihi aliposema hivi, “Jicho ndiyo askofu wa hisia”. Claud Monet, mchora picha maarufu wa Kifaransa alisema hivi, “Mimi ni mfungwa kamili wa macho yangu”. Kwa sehemu kubwa, hiyo ni kweli kwa kila mtu. Kuona (au kutambua) ndicho kiini cha kila kitu. Kanuni ifuatayo itakuwa kweli: Kuona hupelekea kwenye Hatua (au Utaratibu), na
5
Hatua zitaongoza kwenye Matokeo. Ni dhahiri kwamba katika kanisa la Yesu Kristo tuna matatizo sana kwa habari ya matokeo. Ni kwamba hatutoi aina ya Wakristo waliosababisha Kitabu cha Matendo! Basi, kama tunachotoa kina upungufu, ni kwamba kuona kwetu kuna upungufu pia.
Maono ya kiroho ni kitu gani? Tafsiri moja ya Biblia kwa lugha rahisi inafafanua Wakolosai 1:9 kwa njia itakayotusaidia. Paulo aliandika hivi, “Ninaomba kwamba mwone mambo kwa mtazamo wa Mungu.” Maono ya kiroho ni kuona mambo kwa mtazamo wa Mungu. Lakini Biblia inatuambia wazi kwamba mtazamo Wake hautakubaliana na wa kwetu (ktk Isaya 55:10). Basi, ni muhimu kuwepo na urekebishwaji wa dhati kiroho ili tuweze kufikisha mtazamo wetu kwenye hali ya kukubaliana na mtazamo wa Mungu.
Ndugu Dawson Trotman, mtu mwenye maono makubwa kiroho, alisema hivi, “Maono ni kupata moyoni mwako kile kilicho moyoni mwa Mungu.” Lakini, Mungu ana nini moyoni Mwake? Mstari wetu kiongozi unajibu swali hilo kwa neno moja tu: “watu”. Moyoni mwa Mungu kuna watu. Watu wangapi? Watu wote. Moyoni mwa Mungu yuko kila mtu aliyeko duniani. Naye anatazamia watoto Wake kukubaliana Naye katika jambo hili linalomgusa sana.
Anatazamia sana kwamba watoto Wake wataigusa dunia nzima. Basi, utume wa dunia nzima unahitaji maono ya dunia nzima.
6
Hii inamaanisha kwamba Wakristo wengi wanahitaji kufikishwa mahali ambapo wataanza kuona wajibu wao wa kuibeba dunia nzima ili waweze kuanza kuigusa kwa ajili ya Kristo.
Hebu fikiri tena swali hili: Je, moyoni mwa Mungu kuna nini? Je, kinachotakiwa kuwa kiini cha moyo wa kila aaminiye, na katika ndoto zake na maono yake ni nini? Mstari wetu unatoa jibu: watu. “Mahali ambapo hakuna maono, watu huangamia.” Basi, ni kwa nini kiasi cha 4 kwa 5 ya watu wa duniani ndiyo wamepelekewa Injili kwa udhaifu sana, na kufundishwa kwa udhaifu sana kuhusu yaliyomo katika Injili na mkakati wake, huku nusu ya binadamu hawajawahi kusikia jina la Yesu kwa kiwango cha kufikia ukombozi? Je, Ukristo uliofunuliwa katika Kitabu cha Matendo ungevumilia hali hii? Hapana kamwe! Basi, nini tofauti kati ya Ukristo wa Kitabu cha Matendo na Ukristo wa siku za leo, ulioko katika kanisa? Je, Yesu wa kanisa la leo ni tofauti na yule wa kanisa la kwanza? Hapana. Je, Roho Mtakatifu ni tofauti. Hapana. Je, Biblia ni tofauti? Ndiyo, lakini uzuri wa hili uko kwetu, si kwa Wakristo wa kwanza. Wao hata hawakuwa na Agano Jipya lililokamilika. Sisi tunalo, lakini pamoja na hilo, hatujafikia karibu na jinsi wao walivyoweza kuigusa dunia yao.
Basi, nini tofauti kati ya Ukristo uliosababisha Kitabu cha Matendo, na Ukristo wetu sisi? Pamoja na kwamba itaonekana kama nimerahisisha sana, mawazo yangu ni kwamba tofauti ya msingi kati ya “Ukristo wao” na “wetu” ni mkakati. Mkakati wao ulionyesha
7
kutokujali kwao kujenga taasisi na kukazia zaidi kuwajenga watu. Mkakati wao ulikuwa wa kulipuka (kuelekea nje) badala ya kubomokea ndani. Yesu alifundisha watu kumi na mbili, “ambao aliwaita mitume” (ktk Luka 6:13). Kwa nini akawapa jina tofauti? Ni kitu gani kikubwa, ni kitu gani anachokazia, na anataka tuone nini wakati mtindo Wake mkuu (hata unaweza kusema, wa pekee) wa kufundisha uliwalenga watu kumi na mbili, na kuacha neno la kawaida la “mwanafunzi” na kuwapa jina tofauti na la kipekee sana la “Mtume”? Nadhani siri iko katika maana ya neno lenyewe. Ni neno la Kiyunani linalotokana na kuunganika kwa maneno mawili madogo. “Stolos” maana yake ni “kutuma”. “Apo” maana yake ni “mbali na.” Hapo ndipo penye siri. Aliwajenga hao watu maalum waliochaguliwa ili “kuwa pamoja Naye” (ktk Marko 3:14) kwa muda aliohitaji tu kuwafundisha na kuwaingizia uzima Wake, maono Yake, na mkakati Wake. Baada ya hapo, mpango Wake ulikuwa kuwatuma waende mbali na eneo lao la mafunzo kiasi ambacho wangeweza, au ingewezekana, au wangetaka kwenda. Mwongozo Wake ulikuwa: Kuingia ndani kwa muda, lakini Kutoka kikazi! Na ukweli kwamba orodha ya Zawadi (Watu Wenye Karama) alizotoa kwa Kanisa Lake inaanza kwa neno “mitume” (ktk Waefeso 4:11) unaonyesha kwamba mtume alitolewa kwa kanisa ili kuwafanya washirika na huduma ya kanisa kuelekea nje.
Imani yangu thabiti kabisa ni kwamba, Yesu Kristo anamtazamia kila mtu aliyeokoka atawaliwe na maono ambayo
8
daima yanafanya macho yake na miguu yake kutoka nje – kwenda hadi miisho ya dunia. Ni kweli alitupa sisi utume wa dunia nzima, lakini lazima nirudie tena kwamba utume wa dunia nzima unahitaji maono ya dunia nzima. Pia ninaamini kwamba maono na shughuli yenyewe vinapaswa kuwa kitu binafsi, wala siyo kitu kinachofanywa kitaasisi. Mkristo wa kanisa la siku hizi “asiyefanya kitu”, asiyejihusisha katika kazi ya kugusa dunia nzima, hafikiriki na hawezi kuvumiliwa katika mpango wa Mungu. Ninaamini kwamba Yesu anamtazamia kila mtu aliyeokoka awe na maono na mkakati (ambao ulionyeshwa na Yeye Mwenyewe) wa kuigusa dunia nzima hadi miisho ya dunia na mpaka ukamilifu wa dahari!
Kumbuka kwamba Mungu anao watu wote katika moyo Wake, Naye anatazamia sisi pia tuwe hivyo. Henrietta Mears, mwalimu maarufu sana Mkristo, alisema hivi: “Ninapoitazama huduma yangu, nafikiria dunia nzima. Kingine chochote hakitamsahili Kristo wala mapenzi Yake kwa ajili ya maisha yangu.” Mkristo asiyekuwa na maono kama hayo ni kama chombo cha kusafiria katika anga za juu kilichopoteza ratiba yake ya safari. Mwendo kasi wake utakifanya kufika mahali, lakini lengo lake linaweza kufutwa kama kitakataa kufanya kazi kulingana na ratiba yake. Sisi kama Wakristo ratiba yetu siku zote ni ile yenye kulenga Kugusa Dunia Nzima, na mkakati wake maalum umetamka katika Agizo Kuu la Bwana wetu. Kitu chochote kinyume cha hicho kimetokana na mwanadamu, na hakimtoshelezi Mungu.
9
Ni kitu muhimu sana kutambua kwamba, Roho Mtakatifu aliposhuka siku ile ya Pentekoste katika uwezo mkamilifu wa ukombozi, tokeo la kwanza linalotajwa la kuja Kwake ni kwamba “vijana wenu wataona maono na wazee wenu wataota ndoto” (ktk Matendo 2:17). Mara nyingi hili limegeuzwa na kuonekana ni kitu cha kipekee na cha siri sana kiasi kwamba kimetengwa kwa ajili ya watu waonaji wasiokaa na watu. Sivyo. Ukweli ni kwamba hii inapaswa kuwa kawaida ya maisha kwa Wakristo wa kiroho. Kulingana na mantiki, hayo maono na ndoto si yale yanayotokea wakati watu wamelala, bali ni yale yanayopatikana na kujulikana na moyo uliojaa Roho Mtakatifu. Kwa mantiki hiyo, ndoto hizi na maono ni ndoto za mkakati pamoja na maono yatakayopelekea kwenye kufanya kikamilifu kabisa Agizo Kuu la Bwana wetu. Ndoto na maono ya mikakati aina hiyo vinatakiwa kuwa vitu vya kawaida na vya kila siku katika maisha ya Wakristo wa Agano Jipya wa kawaida, wala si mambo ya kiajabu na kushangaza yanatokea kwa watu fulani wachache wenye aina fulani ya maisha.
[USHUHUDA WA MWANDISHI – Nilikuwa nafundisha kwenye mkutano wa viongozi wa kanisa miaka kadhaa iliyopita. Nikapewa kisa hiki kifuatacho na ndugu asiyekuwa mchungaji. Alianza kwa kunionyesha jengo lenye ghorofa kumi na nne, kisha akasema kitu alichokuwa ameambiwa kuhusu wakuu wa shirika la hapo.
10
“Lile jengo ni makao ya shirika tajiri sana. Wakati fulani huko nyuma, viongozi kadhaa wa ngazi ya juu katika shirika hilo walimwendea kiongozi mkuu wakamwuliza, ‘Hivi huyo makamu wako wa kwanza ana nini juu yako kiasi kwamba inabidi aendelee kuwepo? Mbona unamlipa mshahara mkubwa kiasi hicho wakati hazalishi chochote?’ Yule mkuu alipowauliza maana yao, walimpeleka hadi ofisini kwa msaidizi wake huyo na kumwambia achungulie dirishani. Makamu wake alikuwa ameegama kwenye kiti chake kinachozunguka, na hakikuwa kinatazama mezani. Alikuwa ameweka mikono nyuma ya kichwa chake, na miguu ameiweka kwenye dirisha. Hakuwa anajigusa – pengine alikuwa kalala au alikuwa anachungulia nje. Wakamwambia, ‘Unaona tunachosema? Hiyo tu ndiyo kazi yake, lakini analipwa mshahara mzuri sana. Kwa nini?’ Yule mkuu wa shirika akajibu kwa upole sana, hivi: ‘Nisikilizeni kwa makini sana. Mwaka jana, huyo jamaa aliyeketi kwenye hicho kiti katika hiyo ofisi alipata wazo lililoletea shirika hili zaidi ya Dola milioni 85 za Marekani… Mwaka huu, ana kazi moja tu ….’!” MWISHO WA USHUHUDA]
Wapendwa waamini wenzangu, yuko wapi mtu katika kanisa la leo anayefikiri kuhusu wazo la Mungu la Dola milioni 85? Yuko wapi mtu anayeona maono ya Mungu ya Dola milioni 85, au mwenye kuota ndoto ya mkakati wa Mungu wa Dola milioni 85? Mungu Muumbaji wa Biblia hakosi mawazo makubwa ya kiumbaji, lakini, wako wapi watakatifu Wake wa kawaida kabisa ambao
11
wanaona mkakati kwa mtazamo Wake, na kupata moyoni mwao yale ambayo Mungu anayo moyoni Mwake kimkakati?
Hebu nitaje kanuni nyingine inayohusu maono.
Hakuna maono = kushindwa kabisa;
Maono yenye mpaka = mafanikio kidogo;
Maono – mpango – matendo = ni ndoto tu;
Maono + mpango – matendo = ndoto yenye kutisha (kusikia hatia); ila
Maono + mpango + matendo = huduma ya kiroho yenye matokeo.
Ona kwamba kipimo cha maono ya mtu ni matendo yanayosababishwa na maono hayo. Pasipo matendo, wewe na vipawa ulivyo navyo mnabakia kwenye kiwango cha “kuwa na uwezo wa kufanya kitu”. Hali hiyo ni uwezo uliolala ambao haufanyiwi kazi kamwe kupitia maono.
Myles Munroe ambaye ni kiongozi Mkristo alisema hivi kuhusu uwezo wa mwamini kufanya kitu katika kitabu chake kiitwacho Understanding Your Potential: “Mahali penye utajiri sana hapa duniani si katika maeneo ya mafuta huko Kuwaiti, Iraki au Saudi Arabia. Wala si katika machimbo ya dhahabu na almasi huko Afrika Kusini, au machimbo ya uranium huko Urusi au katika machimbo ya shaba yaliyoko Bara Afrika. Utashangaa tu lakini, utajiri mkubwa sana katika dunia yetu uko mita chache tu kutoka nyumbani kwako. Uko katika makaburi yenu. Huko chini, kumezikwa ndoto ambazo hazikuwahi kutimizwa, nyimbo ambazo
12
hazikuwahi kuimbwa, vitabu ambavyo havikuandikwa, picha ambazo hazikuchorwa, mawazo ambayo hayakutolewa, maono ambayo hayakufanyika uhalisi, vitu vilivyobuniwa ambavyo havikutengenezwa, mipango ambayo haikutoka kwenye mawazo ya mtu na makusudi ambayo hayakutimizwa. Makaburi yetu yamejaa uwezo wa kufanya vitu ambao haukufanikiwa.
“Uwezo wa kufanya vitu unadai kwamba usikubali kutosheka na kitu ulichofanikisha. Adui mmoja ambaye ni mkubwa sana wa uwezo wako kufanya vitu ni mafanikio. Mafanikio kidogo huharibu uwezekano mkubwa! Ili uweze kufikia uwezo wako kamili wa kufanya vitu, hutakiwi kutosheka na ulichofanikisha. Pia ni muhimu kwamba usiruhusu kile usichoweza kufanya kiingiliane na kile unachoweza kufanya. Janga kuu maishani si kifo, bali ni maisha ambayo hayakufikia kilele chake katika uwezo wa kufanya vitu.
“Katika kurahisisha dhana hii, hebu tutazame kitu kimoja katika uumbaji ambacho kina nguvu sana … mbegu. Nikishika mbegu mkononi na kuukuliza, ‘Nina nini mkononi?’ utasemaje? Pengine utajibu kilicho wazi kabisa … ni mbegu. Lakini, ukielewa asili ya mbegu, jibu lako linaweza kuwa uhalisi japo halitakuwa ukweli. Ukweli ni kwamba nimeshika msitu mkononi mwangu. Ni hivi: Katika kila mbegu kuna mti, na katika kila mti kuna matunda au maua yenye mbegu ndani yake. Na hizo mbegu nazo zina miti ambayo ina matunda yenye mbegu ndani yake … ambazo zina miti yenye matunda yenye mbegu, na kadhalika na kuendelea.
13
Unachokiona hapa si yote. Kwa hiyo, tofauti kati ya mbegu moja na utoaji wa chakula kama vile ngano inayoweza kulisha dunia nzima ni kitu kinachoitwa ‘uwezo wa kufanya vitu.’ Hicho ndicho kiwango cha tofauti kati ya unachoona na kinachowezekana.
“Kama Musa angekufa kabla hajaona kile kichaka kilichokuwa kinawaka moto … au Paulo kabla ya kukutana na Yesu akiwa njiani kwenda Dameski … au Ibrahimu kabla ya Isaka kuzaliwa. Maandiko na historia vingekuwa tofauti sana. Kama Martin Luther angekufa bila ya kuandika yale matangazo yake … au Charles Wesley bila ya kutunga nyimbo zake … au John Wycliff bila kufasiri Biblia katika lugha ya Kiingereza. Historia ya Kanisa ingekuwa tofauti sana.
“Sijui ingekuwaje kama baba yako angekufa kabla hujatungwa mimba, au mama yako kabla hujazaliwa. Dunia ingepoteza nini kama usingezaliwa? Je, dunia itakosa nini kwa sababu unashindwa kuishi kufikia kiwango cha uwezo wako wote? Je, utakwenda kaburini na nyimbo, vitabu, magunduzi au dawa?” Mimi nimetumia wino mwepesi hapa kuweka msisitizo maneno ya mwandishi.
Je, inawezekana kwamba dhambi kuu ya Wakristo imo katika uwezo wao wa kufanya mambo ambao haujafikiwa? Tena, uwezo mkuu wa kufanya mambo ambao haujatumiwa katika siku za leo ni katika eneo la kutimizwa Agizo Kuu la Bwana wetu. Yeye amekupa wewe nafasi maalum katika Kuufikia Ulimwengu Kikamilifu, na ni
14
nafasi kubwa kuliko yoyote uliyowahi kuwa nayo. Hii nafasi haiwezekani bila ya maono kwamba inawezekana. Basi, kitu muhimu kuliko vyote katika maisha yako ni kuwa na maono yanayokubaliana na Mungu, na kuyafuatilia. Kwa kuwa kazi uliyopewa inahusu dunia nzima, maono yako lazima yawe hivyo hivyo. Je, una maono ya aina hiyo?
Sasa – watu kama wewe na mimi – wenye ubinafsi, kujijali, wenye kujali kwao na wenye kujiona wanapataje maono ya Mungu? Angalia kanuni hii, inayoweza kufanya kazi: habari sahihi ukijumlisha na kuangaziwa kiroho vitaleta maono, ambayo yatasababisha motisha, na hiyo motisha itapelekea utendaji wa kiroho wenye matokeo. Hapo, ona kwamba maono huanza kwa kupata habari sahihi. Sawa na ambavyo kuona kimwili kunavyoanza kwa kuwepo kwa kivutio cha nje, ndivyo na maono kiroho yanavyoanza kwa ukweli wa Mungu katika Maandiko na kila kitu ambacho kinahusiana na Maandiko. “Matofali” ya kujengea maono hayo ni: kufahamu Maandiko kiasi cha kutosha na moyo sikivu wa kusikia Maandiko na kuyatii, halafu ufahamu wa jiografia ya dunia na tamaduni za nchi mbalimbali, utambuzi kiroho wa matukio, maombi, kujisomea ili kupata habari, ujuzi binafsi (“njoo uone” katika Maandiko) wa baadhi ya maeneo ya kimisheni duniani, ushirikiano na waamini wenye maono, kujitoa kwa ajili ya kutoa kuhusu mambo ya umisheni, kukutana na wamishenari na Wakristo wenye kugusa dunia, na maamuzi mbalimbali katika maisha.
15
Unaweza kuanza kushirikiana na Mungu katika kujenga maono ya kiroho katika maisha yako leo. Lakini, ni dhahiri – na inasikitisha sana – kwamba Wakristo wengi unaoshirikiana nao mara kwa mara hawana maono kama hayo.
HALI YA KUSIKITISHA
Pili – fikiri kuhusu hali ya kusikitisha ambayo inatajwa hapa, kwamba, “Mahali pasipo na maono.” Neno “mahali” linaweza pia kutamkwa hivi: “popote”. Basi, haya ni maneno yanayohusu kila mahali. Kwa lugha ya KiBiblia, nini maana ya “pasipo maono”? Maana yake ni kwamba Mungu hatambuliwi, wala mpango Wake mkamilifu. Maana yake ni kwamba Shetani, “mungu wa dunia hii” ame”pofusha mawazo ya watu” wasione mambo ambayo ni ya muhimu na yenye maana! Hawawezi kuona wala kuyaelewa mambo haya bila ya kuzaliwa upya pamoja na kuangaziwa (ona 1Wakor. 2:9-14). Basi, hakuna mawasiliano ya kudumu baina ya mbingu na mioyo ya watu. Hakuna biashara na kile kisichoonekana, cha milele, cha kiroho, na ambacho ni halisi. Hakuna kumsikiliza Mungu na kumtazama Yeye. Kwa kifupi ni kwamba, “pasipo maono” maana yake ni kwamba watu hawamwoni “Aliye Juu na Mtakatifu, mwenye kutamalaki Milele.” Basi, tunakuwa na mipaka na kuona maeneo yetu madogo pamoja na upeo wetu, na mipango yetu midogo, ya kibinafsi, ya kidhambi tu. Mtu mwenye mipaka kiasi hicho, na mwenye mipango yenye mipaka kiasi hicho hatimaye anabomokea
16
ndani yake mwenyewe. Ni hivi: Kila kitu huanza kwa maono ya kweli. Ona lile neno “kweli”. Ninalitumia kama kinyume cha kutokuwa na maono, maono bandia na maono yenye mipaka.
Lazima tukubali – kwa huzuni sana – kwamba, watu wengi walio-okoka wana ubinafsi, wanajipenda wenyewe na wametawaliwa na hali ya kujilinda kwa kiwango sawa na watu waliopotea tu. Yaani, wengi katika watu walio-okoka ni wenye dhambi (tafsiri “dhambi” kuwa ni ubinafsi) kama waliopotea tu. Kwa nini? Hapo tena, andiko letu la msingi linatoa jibu: Hakuna maono. Si mara nyingi tunaona mambo “kwa mtazamo wa Mungu”. Si mara nyingi mioyo yetu inakuwa na kile ambacho Mungu anacho moyoni Mwake – dunia nzima ya watu mmoja mmoja waliopotea.
Mtazamo ni muhimu sana. Kuona kwa mtu hutegemeana na aina ya vioo anavyotazamia, sawa na jinsi kusikia kwa mtu kunavyotegemeana na chujio analotumia kusikilizia. Hebu tutoe mfano wa kusaidia kueleweka kweli hiyo.
Mwaka wa 1877, mtaalamu wa nyota Mmarekani aliyeitwa Percival Lowell aliushangaza ulimwengu wa sayansi kwa kutoa wazo kwamba, kutokana na ushahidi aliokuwa amekusanya, kulikuwepo na dalili za uhai na viumbe wenye akili katika sayari ya Mars. Nadharia yake – kwa sehemu – ilitokana na yeye kuona vitu alivyoita “mifereji” kwenye sayari hiyo. Wanasayansi wakabebwa na tamko hilo kwa kishindo. Lakini, walikuwepo watu wachache ambao tangu mwanzo walikuwa wamefahamu kwamba hiyo sayari haina mifereji.
17
Baadaye, Bwana Lowell alipata tatizo kubwa kiafya, lililoanza kujitokeza. Jopo la matabibu walimpima na kugundua tatizo lenyewe. Ugonjwa wake haukuwa umejulikana sana siku zile, basi wakauita jina lake – “Lowell’s Syndrome”. Ishara mojawapo ilikuwa kwamba, alipoketi muda mrefu akichunguza kitu fulani, sura na ukubwa wa mishipa ya kupitisha damu katika macho yake ilikuwa inaonekana kwenye hicho kitu alichokuwa anakichunguza. Basi, badala ya kuona “mifereji” kwenye sayari ya Mars kwa njia ya darubini, alichokuwa anakiona ni mishipa yake mwenyewe ya damu. “Alibeba” kile alichodhani anakiona, katika kichwa chake mwenyewe. Mtazamo!
Ufuatao ni mfano mwingine tena.
Dakta Harold Lindsell, mhariri mstaafu wa jarida liitwalo Christianity Today, alihudhuria kliniki ya macho ya Kijapani zamani kidogo. Akiwa darasani siku moja, mkufunzi aliinua chati kwa ghafula mbele ya darasa. Akauliza hivi: “Ni wangapi mnao-ona namba nane?” Lindsell peke yake ndiye aliinua mkono wakati huo. Alisema baadaye kwamba alidhani ni njama – kwamba darasa lote lilikuwa limekusudia kumcheza shere. Lakini, mkufunzi akauliza, “Ni wangapi mnaoweza kuona namba kumi na nne?” Kila mtu darasani aliinua mkono! Ndipo mwalimu akazungumza na Ndugu Lindsell na kumwambia, “Mheshimiwa! Kuna mtu ambaye amewahi kukwambia kwamba wewe una matatizo ya kuona rangi?” Ni kwamba hapakuwa na hila yoyote. Kila mtu siku hiyo katika lile darasa alikuwa anasema ukweli – kulingana na alivyouona. Mtu mmoja kweli aliona
18
mamba nane huku wengine wote wakiona namba kumi na nne. Mtazamo huo!
Ni hivi: Mtazamo hufunika kila kitu ambacho hakihusiki, na kusababisha maono yatawaliwe na kile ambacho kinahusika. Kwa hiyo ni muhimu sana.
Mwanamke mmoja alisogea karibu na Dakta G. Campbell Morgan, mwalimu maarufu wa Biblia wa zamani. Akamwuliza huvi: “Hivi Dakta Morgan, unaamini kweli kwamba Mungu anajali mambo madogo madogo ya maishani mwetu?” Dakta Morgan akamjibu kwa upole sana, hivi: “Mama. Hivi kweli unaamini kwamba katika maisha yako kuna kitu kikubwa sana kwa Mungu?” Mtazamo huo.
Hayo ndiyo yanayofanywa na mtazamo. Yanaondolea mbali habari fulani au mambo fulani kuwa si ya maana, na kukuza mengine kuwa muhimu mpaka kufikia kiwango cha “kweli”. Lakini, mtazamo unaweza kutokana na mtazamaji mwenyewe kiasi cha kutokuwa halisi katika hali ya kawaida kabisa. Yaani, hata unaweza usitoe nafasi ya kitu halisi kabisa kilichopo kuonekana. Acha nikupe mfano wa KiBiblia kuhusu mtazamo.
Sura ya kumi na tatu ya kitabu cha Hesabu ni taarifa ya hadithi ya taifa la Israeli wakiwa Kadeshi Barnea, kusini kidogo tu ya nchi ambayo Mungu alikuwa amewaahidi. Bila shaka walikuwa tayari kuingia katika Nchi yenyewe. Lakini, walipatwa na hali ya kutokuamini, wakatuma kikundi cha wapelelezi kumi na mbili
19
kwenda kutazama udhaifu wa nchi ile. Wapelelezi wake wakarudi na taarifa iliyogawanyika. Wote walikubaliana kwamba nchi ilikuwa inakaliwa na watu ambao hawakuwa na wazo la kuiachia. Halafu, wapelelezi kumi – idadi kubwa kabisa – wakapendekeza kwamba wasiiteke nchi kwa msingi kwamba wakazi waliokuwemo nchini “wana nguvu kuliko sisi,” na kwamba wana wa Israeli walionekana kama mapanzi, wakilinganishwa na majitu. Wapelelezi wawili walitosha ushauri “wa wachache”. Wakikiri ukweli ule ule, wao waliendelea na kusema hivi: “Hebu na tupande mara moja na kuitwaa nchi, kwa sababu tuna uwezo kabisa wa kuiteka” (ktk Hesabu 13:30). Ni hivi: Wale wachache walimwingiza Mungu katika uamuzi wao, kitu ambacho wale wengi hawakukifanya. Basi, mitazamo miwili ikaamua mashauri yale mawili yaliyotolewa: mtazamo mmoja ulimhusisha Mungu, ule wa pili haukufanya hivyo. Wote waliona “majitu”; wengi wao walijiona kuwa “mapanzi”. Wawili tu ndiyo walimwona Mungu. Au basi: wengi walimwona Mungu kupitia hao majitu, na hao wakaonekana kuwa wakubwa kuliko Mungu. Wale wachache waliwaona majitu kupitia Mungu, na Mungu akawa mkubwa kuliko majibu. Basi, mtazamo wao uliamua mapendekezo yao na utendaji wao. Hapo ndipo penye tofauti kati ya “maono” na “pasipo maono”!
Akili ya kibinadamu siku zote itakupa mtazamo wako kulingana na maoni yako. Muujiza tu wa kuangaziwa ndiyo utakaokupa mtazamo wa Mungu. Hapo ndipo kuna tofauti kati ya
20
“pasipo maono” ambayo hatima yake ni “watu huangamia”, na “maono” ambayo kwa hiyo watu hustawi na kufanikiwa.
Jaribu kufikiri kutokuwepo na maono ya kiroho katika madhabahu ya kanisani unapoabudu. Huna haja ya kufikiri sana kama utatembelea makanisa mengi! 1Samweli 3:1 inasema, “Neno la Mungu lilikuwa adimu katika siku hizo. Hayakuwepo maono ya wazi (au, ya mara kwa mara).” Ukisoma historia ya taifa iliyotokana na wakati huo utagundua kwamba mambo ya kusikitisha sana yalitokea kwa sababu ya kutokuwepo na maono.
Ingekuwaje kama isingekuwepo Injili inayohubiriwa kutoka madhabahu ya kanisa unalohudhuria? Kutokuwepo kwa kutambua kwamba mtu amepotea pasipo Kristo? Kutokuwepo na kuamini nguvu zenye kubadili maisha za Roho Mtakatifu? Kutokuwepo kwa mafafanuzi ya ndani sana na wa milele wa mausia ya Mungu? Kutokuwepo kwa mafunuo ya hazina nyingi sana zisizomalizika zilizomo katika Neno la Mungu? Kutokuwawezesha wasikilizaji “waishi mbinguni na duniani kwa wakati mmoja”? Kutofundishwa kwa upana wa maisha ya Kikristo yaliyojaa Roho, yanayofuata Neno, yaliyo na mwelekeo wa maombi, na yenye kujenga wanafunzi? Jaribu kufikiri madhabahu “pasipo maono”.
Mchungaji: Una mashaka kiasi gani kuhusu uwezo wa kile unachofanya sasa? Mashaka mazuri ndiyo nyundo yenye kuvunja madirisha yaliyofunikwa na kiwingu cha mambo yanayowavutia wanadamu. Mashaka aina hiyo ni ishara yenye kuleta matumaini.
21
Bila ya ukiri wa kweli kuhusu mashaka kama hayo, na uchunguzi kwa njia ya maombi kuhusu njia mbadala itolewayo na Mungu, madhabahu unayosimama ndani yake itadumu kutokuwa na maono.
Miaka kadhaa iliyopita, mchungaji maarufu wa Kibaptisti alikuwa kwenye maombi ofisini mwake asubuhi moja. Alikuwa amelala kifudifudi akimwomba Mungu upako wa nguvu za Roho Mtakatifu juu ya huduma yake. Alimsihi Mungu tena na tena, “Ee Bwana! Nipe nguvu Zako. Usiache nihubiri na kufanya huduma pasipo nguvu Zako.” Kila mhubiri wa maana amewahi kuomba sala hii kwa uzito sana na mzigo. Anasema, mara ikaonekana kama paa juu yake limefunguka na mkono ukamshukia na kumgusa kwenye bega. Ikawa ni kama sauti ya Mungu imezungumza ndani yake, hivi: “Mwanangu, acha kuomba!” Alipotulia, Sauti ni kama ilimwambia hivi, “Mwanangu! Kwa mipango yako isivyokuwa mikubwa, huhitaji nguvu Zangu!”
Ewe Mkristo – maono yako ni makubwa kama ya Mungu, kwa ajili ya utukufu Wake? Iko wapi mipango, ndoto, maono, mikakati kwa ajili ya kuifikia dunia nzima – vitu ambavyo kwa kweli vinasukuma rasilmali ya miujiza ya Mungu? Uko wapi mkakati unaotaka miujiza endelevu ili kuudumisha? Yako wapi maono ambayo ni makubwa kiasi kwamba rasilmali za kibinadamu (za aina yoyote na kiwango chochote) hazina uwezo wa kuyategemeza? Maono pekee yenye ukubwa wa umilele ambayo yeyote kati yetu anaweza kuyahitaji yanapatikana katika lile Agizo Kuu ambalo
22
tumepewa na Bwana Yesu Kristo. Kama madhabahu yako haisumbuliwi na maneno “kuwafanya kuwa wanafunzi” na “mataifa yote”, Mungu anawezaje kutazamiwa kuunga mkono kutoka mbinguni? Bila kutatizwa na hilo, madhabahu ya kanisa lako ina ubao unaosema hivi: “hakuna maono”.
Halafu, ni hatua ndogo tu kufikia kwenye viti, watu ambao hawana maono ya kiroho ya hayo. Sheria ya maisha ya ndani ya kanisa ni hii: “watu wako kama mchungaji alivyo”. Watu watapokea jinsi mchungaji wao alivyo kiroho. Hebu tuseme katika mfuatano huu, watu waketio kanisani hawana, au wamepoteza maono yao kuhusu utukufu wa kushangaza sana wa Injili. Inakuwaje? Na wamepoteza uzuri wa pekee wa Yesu Kristo. Inakuwaje? Na wamepoteza maono ya ukuu na utukufu wa kazi yetu ya dunia nzima. Inakuwaje? Na wamepoteza maono ya uwezekano wa kuigusa dunia nzima kwa ujumbe wa Injili na uwezo wa Yesu Kristo kama Wakristo wa kwanza walivyofanya. Inakuwaje? Mtu mmoja amesema, na ni kweli kabisa, “Hatua kutoka aliye tayari kujitoa hadi mtunzaji na hatimaye mzikaji ni fupi sana.”
Kwa nini washirika wa makanisa wanasisimka zaidi kuhusu vitu vingine elfu na zaidi, kuliko kuhusu Mungu, mambo ya kiroho, mbinguni, jehanamu, na umilele? Jibu lake: Hakuna maono, kwa hiyo hakuna motisha. Maana, motisha hutokana na maono.
Kujifunza Injili na Kitabu cha Matendo kwa makini sana kutadhihirisha kwamba Kanisa la kawaida la Kikristo linaendeshwa
23
kwa misingi ya desturi na taratibu kuliko kwa misingi ya kuangaziwa [na Roho Mtakatifu]. Mtu mmoja – kwa mzaha tu – alisema hivi: “Ni vizuri makanisa yafanye na kusema kila kitu kwa usahihi mara ya kwanza, kwa sababu yatafanya na kusema kwa njia hiyo hiyo tangu sasa na kuendelea.”
Maono yanapotoweka katika madhabahu na kwa washirika, tuwe na uhakika kabisa kwamba hayatakuwepo maono ya kiroho katika maisha ya kila siku. Itakuwaje ikiwa Wakristo watapoteza kabisa maono ya nafasi yao kama chumvi na nuru (ktk Mathayo 5:14-16) katika dunia inayoharibika na yenye giza? Itakuwaje kama sisi tutapoteza maono juu yetu kwamba ni wawakilishi wa Yesu Kristo (ktk 2Wakor. 5:20), “katikati ya kizazi kiovu kilichopotoka, ambacho kati yake tunang’aa kama taa duniani, tukilishika na kulitangaza Neno la Uzima” (ktk Wafilipi 2:14-16)? Itakuwaje ikiwa tutapoteza maono yetu juu ya daraja yetu kuu kama “mabalozi kwa ajili ya Kristo”, tulioagizwa kusemea jambo la Mfalme wetu katika dunia hii yenye giza na uhasama? Mbona si kitu cha kufikiri na kukisia kabisa. Kutokuwepo na maono ni kitu kinacho-onekana waziwazi katika madhabahu, kwa washirika, na katika maisha ya kila siku – ukitazama tu mambo yanayotokea, kama yanavyotajwa katika maandiko haya.
24
MATOKEO YAKE, MAZITO
Hebu fikiri juu ya matokeo mazito yanayofuata hali ile ya kusikitisha sana ya “pasipo maono”. Mahali ambapo hakuna maono, watu huangamia.” Neno linalotafsiriwa “kuangamia” ni la Kiebrania, lenye kushangaza sana. Yaani – limejaa maneno, na linatisha. Lina maana kadhaa tofauti. Maana yake ni “kutokuwa na kujizuia, kujiachilia, kuyeyuka, kuvunjika, kusambaratika vipande-vipande, kutembea uchi, kuangamia.” Sasa, tazama matokeo ya kusikitisha sana ya kupotea kwa maono miongoni mwa Wakristo.
Kwanza – maono yanapokuwa hayapo, watu wa jamii, wa jumuiya, wa kanisa, wa nyumbani “huacha kujizuia”. Hayo ni matokeo ya kiadili ya maono kupotea. Kupoteza maono husababisha vurugu kiadili, ambapo “kila mtu hufanya kilicho sawa machoni pake mwenyewe”. Ona kwamba, kunapokuwa hakuna utambuzi wa uhalisi kamili, watu hufanya “yaliyo sawa machoni pao wenyewe”, wala si kile ambacho kinaonekana kuwa makosa kwao. Kumbuka pia kwamba “sawa” na “kosa” siku zote ni maneno tu kwa wale wenye akili za kawaida au za kimwili. “Sawa” na “kosa” ni vitu halisi kwa wale tu ambao wana akili timamu kiroho. “Iko njia ionekanayo kuwa sawa kwa mtu, lakini mwisho wake ni mauti” (ktk Mithali 14:12). Ona kwamba huyo mtu ana uhakika kwamba njia yake ni sawa – kamwe haoti kwamba njia yake ni ya KiShetani na yenye uharibifu. Hapo tena, tofauti ni katika ufunuo, katika maono na mtazamo wa mtu binafsi. Inashangaza sana kuona jinsi ambavyo watu walio
25
vipofu kwa mambo ya kiroho wanavyohalalisha ukweli wa kuelewa kwao!
Kwamba watu kila mahali siku hizi wameacha kujizuia ni kitu kinachokubaliwa na kila mmoja. Kujitawala, fujo na vurugu na kujiamulia mambo mwenyewe ni mambo yanayozidi kuenea. Tofauti kati ya Mwana wa Mungu na wenye dhambi inadhihirishwa hapo. Yesu alisema hivi: “Siku zote mimi hufanya mambo ambayo yanampendeza Baba Yangu” (ktk Yohana 8:29). Lakini, kauli mbiu ya wenye dhambi (au kiini cha dhambi) ni: “Siku zote mimi hufanya mambo yanayonipendeza”. Pengine atatokea msanii wa siku zijazo atakayetengeneza sanamu au kuchora picha itakayomwonyesha mtu wa karne ya ishirini akiwa amejikumbatia mwenyewe kwa upendo sana, akijipiga busu mwenyewe katika kioo. Lakini, bila ya kupoteza uzito wa hali halisi katika maneno ya utani, hebu maneno ya Shetani aliyopewa na John Milton katika kitabu kinachoitwa Paradise Lost yaturekebishe. Shetani alionyesha ukiri usioepukika wa wenye dhambi wenye kufuata ubinafsi wao bila ya mipaka aliposema hivi: “Mimi mwenyewe ndiye jehanamu”.
Miaka kadhaa iliyopita, magazeti yaliandika kisa cha msaidizi wa fundi uchundo wa Uwanja wa Ndege wa Idlewild huko New York, Marekani. Huyu alikuwa na miaka ishirini, naye alimwandikia rafiki yake mmoja barua, aliyekuwa katika Jeshi la Anga la Marekani katika jimbo la Texas. Barua ilieleza jinsi ambavyo kijana huyo alikuwa ameachana na mchumba wake, na
26
jinsi alivyopanga kuchukua ndege mojawapo ya shirika la Pan American. Akaiba ndege aina ya DC-3 yenye injini mbili, akaanza kuiendesha. Ikashindwa kupaa, ikaanguka, naye akafa. Habari gazetini zilimalizika kwa maneno yake kutoka kwenye ile barua, kwamba, “Nitakuwa nikiendesha mimi mwenyewe, kama ambavyo nimekuwa siku zote – peke yangu.” Kisa hiki hurudiwa tena na tena, katika mavazi tofauti, kila siku – na matokeo ni yale yale. Kujisimamia mwenyewe ni kujiharibu mwenyewe. Mtu anayejisimamia mwenyewe siku zote ataanguka na kuungua! Kwa kuwa mawazo ya wanadamu hupingana sana wakati kila mmoja anapochukuwa sheria yake mwenyewe, machafuko duniani yanaendelea kukua na kuongezeka, na hali ya wasiwasi itokanayo nayo. Mahali ambapo hakuna maono ya mara kwa mara miongoni mwa watu, ambapo hakuna neno lililo wazi kutoka kwa Mungu aliye hai, ambapo hakuna Ukristo halisi wenye maana, basi watu hutupilia mbali vizuizi.
Pili – neno hili lenye nguvu sana la Kiebrania pia linamaanisha “kusambaratika”. “Mahali ambapo hakuna maono, watu husambaratika”. Hayo ni matokeo ya kijamii ya kupoteza maono. Dhambi, inayozidi kuongezeka katika jamii yenye utovu wa maono ya kiroho, ina nguvu ya mvutano fulani. Inawafukuza watu watoke kwenye Kiini cha Kweli cha Uzima ambacho ni Mungu Mwenyewe, na kwa njia hiyo kuwatenganisha wao kwa wao. Basi, tunakuwa na dunia iliyotengana, iliyogawanyikana. Jamii huanza
27
“kulegea, kuyeyuka, kuvunjika, kuwa vipande-vipande”. Neno “kugawanyika” linaelezea hali nyingi tofauti zilizomo katika dunia yetu. Tunazo familia zilizogawanyika, mataifa yaliyogawanyika, dunia iliyogawanyika, na watu wenye haiba zilizogawanyika. Siku moja, daktari wa magonjwa ya akili aliingia kwenye kituo cha mafuta akiwa na gari aina ya pikap. Nyuma alikuwa amebeba viti vitatu. Alipoulizwa anakwenda wapi, alijibu, “Ninakwenda kumtembelea mwenda wazimu (ambaye tatizo lake ni kuona kwamba yeye si mmoja, bali wengi)!” Mara nyingi sana watu binafsi wana”sambaratika”. Binti mmoja msomi wa chuo kikuu fulani alimwambia mwenzake wanayekaa chumba kimoja, “Ninajisikia kama Vita ya Wenyewe kwa Wenyewe, inayotembea”. Mwenzake akamjibu, “Wala hiyo si kitu. Mimi ni Vita Kuu ya Dunia, inayotembea!” Mtu binafsi anaweza kuvumilia tatizo la aina yoyote ile kama ameunganika ndani, lakini atashindwa na shambulio la aina yoyote ile kama ndani yake mwenyewe kuna ubishi na hali ya kutoelewana.
Habari za Yuda katika Agano Jipya zinamalizika kwa maneno haya: “Basi, mtu huyu alinunua konde kwa ijara ya udhalimu; akaanguka kwa kasi akapasuka, matumbo yake yote yakatoka” (Matendo 1:18). Kama mjuavyo, Yuda alijinyonga, na huku kuharibikiwa kimwili pengine kulitokana na kutokufanikiwa katika kujaribu kujinyonga, au kama matokeo ya kuvimba na kuharibika kulikotokana na maiti yake kuning’inia kwenye kamba yake kwa
28
muda mrefu. Tafsiri ya Biblia Fafanuzi inasema hivi, “Alipasuka katikati ya mwili wake”. Pamoja na kwamba maelezo hayo hayavutii, tunapata picha nzuri. Tafsiri nyingine inasema kwamba Yuda “alisambaratika”. Yaani, “aliachana”. Lakini hii ilikuwa ni tokeo la mwisho la kimwili la yale ambayo yalikuwa yametokea kwa miaka mitatu huko nyuma. Alikuwa ameharibu kile kiini pekee – “saruji” ya KiMungu ambayo ingeunganisha na kushikamanisha haiba yake na kuifanya kamilifu na yenye umoja. Kweli,“alisambaratika katikati”. Na Yuda angefaa kabisa kuwa “mtakatifu mwangalizi” wa majira ya siku hizi. Biblia inatuambia (ktk Wakolosai 1:17) kwamba “vitu vyote hushikamana pamoja” katika Yesu Kristo tu. Lakini, watu wanapopoteza “Maono ya Kuvutia Sana ya Yesu Kristo,” basi jamii inakosa nguvu za kuunganisha, za kufanya vitu kuwa umoja, za kushikamanisha vitu vyote.
Katika mchezo uitwao Green Pastures uliotungwa na Marc Conally, malaika Gabrieli anaonekana akipita hapa na pale katika kumbi na maeneo mbalimbali ya mbinguni, huku akizidi kusumbuka kutokana na vurugu na fujo anazo-ona hapa duniani. Mwishowe anamgeukia Mungu na kusema, “Bwana! Bwana! Inaonekana kwamba kila kitu kilichopigiliwa ili kushikamana kinaanza kuachana!”Watu binafsi na taasisi husambaratika wakati Kristo anapokosa kutawala. Hayo ni matokeo ya kijamii ya upotevu wa maono ya kiroho.
29
Tatu – hili neno katika Kiebrania lina maana nyingine ya “kutokuvaa” au “kutembea uchi”. Sasa – kwa kuwa kila matumizi ya neno hili yamekuwa ya kiroho, bila shaka maana hii ni ya kiroho pia. Tunapata uwanja mpana kiasi gani kwa ajili ya kujifunza Biblia kama tutaona maana hii kuwa inahusu hali ya kiroho ya wanadamu. Tafsiri kwamba “watu hawajavaa nguo” hudhihirisha matokeo binafsi ya kutokuwa na maono. Katika Biblia – tena kwa mtiririko dhahiri kabisa – kuokolewa kwa wenye dhambi, “kuhesabiwa haki” kwao, ni kitu kinachoonekana kwa lugha ya wao “kuvikwa” na ile haki yenye kulinda na kuhifadhi ya Kristo, na kuhukumiwa kwao kunaonekana katika wao kutokuwa na mavazi na walio wazi kwa ajili ya hukumu. Ukweli ni kwamba, katika Biblia nzima, mavazi ni mfano wa dhambi na haki pia. Mavazi machafu mara nyingi hutumika kama picha ya dhambi na kujihesabia haki, na mavazi safi na meupe hutumika kama picha ya ile haki ya Kristo ifunikayo, inayohifadhi. Ukitaka kufuatilia wazo hilo kwa upana zaidi katika Maandiko, mafungu yafuatayo yatakuwa na maana sana kwako: Mwanzo 3:7, 21; Zekaria 3:1-5; Mathayo 22:11-13; Luka 15:22; Warumi 13:11-14; Waefeso 4:22-24; Wakolosai 3:5-14 na Ufunuo 19:7, 8.
Kitu kimojawapo cha kufurahisha sana katika kuwa Mkristo ni kujua kwamba Mungu amenivika Vazi Bora Zaidi la Mbinguni – tena, kwa gharama Yake Mwenyewe! Hili linaonekana katika simulizi maarufu sana la John Bunyan liitwalo, Safari ya Msafiri.
30
Wakati yule msafiri aliyetambua hatia yake anapofika Msalabani pa Yesu na kumwamini, mzigo wa dhambi zake unamwacha na kuanguka, naye anainuka akiwa anasherehekea msamaha na uzima wa milele. Ndipo anapokutana njiani na “Watatu Wenye Kung’aa” ambao ni mfano wa Mungu baba, Mungu Mwana, na Mungu Roho Mtakatifu. Mungu Baba anamwambia msafiri huyo aliyeokoka, “Amani iwe kwako. Dhambi zako zimesamehewa.” Mungu Mwana anamvua zile nguo chafu alizokuwa amevaa, na badala yake, anampa joho jipya, safi, jeupe. Na Mungu Roho Mtakatifu anaweka alama kwenye uso wake (ambayo ni mfano wa muhuri wa Roho Mtakatifu), na kumpa mkononi mwake gombo lililokunjwa vizuri (ambalo ni mfano wa Biblia).
Hiyo kazi ya pili – kazi ya kumvua mwenye dhambi mavazi yake ya kale na kumvika upya – ndiyo inayolengwa wakati andiko letu la msingi linaposema, “Mahali ambapo hakuna maono, watu hawana mavazi.” Tunasoma hivi katika Yohana 3:36, “Yeye amwaminiye Mwana anao uzima wa milele, lakini yeye asiyemwamini Mwana hataona uzima, bali hasira ya Mungu inakaa juu yake.” Mwamini anayemtumaini Kristo amefunikwa kwa haki ya Kristo naye huepuka hasira ya Mungu kuhusu dhambi. Lakini, mwenye dhambi asiyeamini hana nguo, na kwa hali hiyo, yuko wazi kupatikana na kila kitu kinachotaka kumharibu.
31
“Mahali ambapo hakuna maono,” watu zaidi na zaidi hubaki “bila nguo” au, pasipo ulinzi kwa kitambo na milele. Hayo ndiyo matokeo binafsi ya kutokuwa na maono.
Mwisho, neno la Kiebrania linatafsiriwa kwa usahihi kabisa hapa. Maana yake ni “kuangamia”. “Mahali ambapo hakuna maono, watu huangamia.” Kweli, huruma inahitajika hapa kwa sababu, kilicho hatarini ni “watu”. Wangekuwa wanyama au mimea, mambo yasingekuwa mabaya sana. Lakini ni watu – kama wewe na kama mimi. “Wanaangamia”. Katika Yohana 3:16, neno “kuangamia” linawekwa kinyume na kuwa na “uzima wa milele”. Kuangamia maana yake ni kuhusika milele katika kifo hai na maisha ya kufa katika mahali paitwapo jehanamu. Hapo hapo tena, 1Wakor. 1:18 inaonyesha kwamba watu wasiokuwa na Kristo wako katika hali ya sasa ya kuangamia. Huku kuangamia kwa watu ni matokeo ya kiroho na ya milele ya kutokuwa na maono katika Wakristo. Watu watatu huangamia pasipo Kristo kila sekunde, na Kanisa kwa sehemu kubwa limepoteza maono yake! Jehanamu inajaa, na Mbingu bado ina nafasi tele za kujazwa! Yote kwa sababu maono ya Kanisa yamechuja!
Zamani kidogo, mfanya biashara tajiri alisafiri kwenda India kuwinda simba marara wa Bengali. Akakaa huko majuma sita. Aliporudi nyumbani, alihudhuria ibada ya katikati ya juma katika kanisa lake kubwa sana. Alikuta wanajadili kuhusu bajeti ya mwaka ya kanisa. Mfanya biashara huyo alishtua kanisa zima kwa kutoa pendekezo kwamba sadaka zote kwa ajili ya utume wa nchi za nje
32
ziondolewe kwenye bajeti. Mzee mmoja akauliza sababu ya pendekezo hilo la ajabu sana. Jibu likatoka, hivi: “Ndiyo nimerudi kutoka safari ya majuma sita huko India, na katika kipindi chote hicho, sikuona mishenari hata mmoja.” Yule mzee akauliza tena, “Na kusudi la safari yako hasa lilikuwa nini?” Jibu: “Nilikwenda kuwinda simba marara wa Bengali.” Akaulizwa, “Na ulifanikiwa kuona wangapi?” Akajibu, “Niliwaona sita.” Yule mzee akasema, “Hiyo ni ajabu kabisa. Mimi nimekaa India miaka kumi na tatu kama mishenari, na niliwaona wamishenari mamia kwa mamia. Lakini mpaka sasa sijaweza kumwona simba marara mmoja wa Bengali huko India!” Kwa hiyo, mengi sana yanategemeana na mtazamo wetu, na maono yetu.
Maneno ya Mithali 29:18 yaliandikwa na Mfalme Sulemani, mtu ambaye katika utawala wake, maono yalipotea. Na hapakuwa na kushindwa kubaya zaidi katika historia ya Israeli kuliko kule kwa Sulemani. Watu walisambaratika! Taifa liliporomoka! Ufalme uligawanyika!
Basi, uchaguzi mbele yetu ni dhahiri kabisa: Aidha ni “maono au mgawanyiko”! Hii ni kweli duniani kote, kitaifa, katika mahali pamoja, lakini sana ni kweli katika Kanisa la Yesu Kristo na katika maisha ya Mkristo binafsi!
Ni lazima – na ni lazima – tumngoje Mungu katika utulivu na maombi, tukiwa na hali ya ndani sana ya uhitaji na moyo wenye kufundishika, na kumwomba Yeye arejeshe maono ya Utukufu Wake
33
mkuu sana, naya Mpango Wake mkuu mno kwa ajili yetu, na dunia! Maono yanaporejezwa, tutagundua tena kwamba Mpango Wake wote umefunuliwa katika Agizo Kuu la Bwana wetu, na kwamba jukumu hapo ni “kuwageuza watu wawe wanafunzi”.
Dawson Trotman alikuwa sawa aliposema hivi: “Maono ya kiroho ni kupata moyoni mwako kile kilicho kwenye moyo wa Mungu – yaani, dunia!” Paulo aliomba kwamba Wakristo wa Kolosai wapate “kuona mambo kwa mtazamo wa Mungu” (ktk Wakolosai 1:9, TLR). Kama tungefanikiwa hapo, yangekuwepo mapinduzi makubwa sana!
“Mtu mmoja aliyeamka
Anaweza kumwamsha mwingine;
Na huyo wa pili anaweza kumwamsha
Ndugu yake aliyeko jirani.
Hao watatu walioamka
Wanaweza kuamsha mji mzima
Kwa kugeuza hapo pote
Juu chini.
Wengi walioamka
Wanaweza kufanya vurugu
Kiasi kwamba hatimaye
Sisi wote tunaamshwa.
Mtu mmoja aliyeamka,
Alfajiri ikiwa machoni mwake,
HUONGEZEKA!”
34
Sura Ya 2
Agizo Lenye Kuamua Wajibu Wetu
“Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani. Basi, enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza kwa jina la Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu; na kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi. Na tazama, mimi nipo pamoja nanyi sikuzote, hata ukamilifu wa dahari.”
Mathayo 28:18-20
Tunapoondoka nyumbani, mara nyingi tunatoa maagizo yetu muhimu sana na maelezo – mambo ambayo hatutaki watu wengine wasahau. Mke wangu mimi huyaweka mezani au kwenye mlango wa friji. Nini maana yake? Kwamba, hayo ni muhimu!
George Peters katika kitabu chake kiitwacho A Biblical Theology of Missions aliandika hivi: “Agizo Kuu ndiyo taa yenye kutuongoza katikati ya ukungu wa kibinadamu na mawazo. Tunahitaji sana kujifunza upya na kwa undani sana Agizo Kuu. Ni waalimu wachache sana na wafafanuzi wanaoshughulika kwa upana sana na mafungu yanayohusu Agizo Kuu. Kanisa linahitaji kufikiri upya na kwa uzito sana lile Agizo la kufanya watu kuwa wanafunzi.” Mishenari mstaafu John McGee aliyefanya kazi huko Nigeria, alisema hivi: “Kuna mengi sana katika Agizo Kuu kuliko mtu
35
anavyoweza kuota, au kufikiri, au kutenda, hata kama angekuwa na uwezo wa kuishi mara kumi.”
Katika fungu la Maandiko ambayo ni pamoja na Agizo Kuu (ktk Mathayo 28:16-20), tunasoma kwamba “wale wanafunzi kumi na moja wakaenda Galilaya hadi kwenye mlima ambao Yesu alikuwa amewaagizia.” Huku ndiko kuonekana kwa Yesu kwa kipekee baada ya ufufuo ambako kulikuwa kumepangwa kabla. Alipoonekana mara zile nyingine zote, alikuwa anatokea tu. Bila shaka kulikuwa na kitu fulani cha muhimu sana alichotaka kukisema au kukifanya wakati huu. Na kweli, ndivyo ilivyokuwa! Hapa “alibandika” maagizo Yake ya Mwisho. Kuna msemo mmoja wa kawaida sana miongoni mwa watu wenye kutumia vyombo aina mbalimbali – “Kila Kitu Kikishindikana, Soma Maelekezo”. Katika sura hii, tunakwenda kujifunza na kusoma Maelekezo Yake ya Mwisho. Tutagawanya maelekezo hayo katika mafungu mawili: Uhakikisho Ulioko Katika Hilo Agizo, na Kazi Iliyoko Katika Hilo Agizo. Ikiwa tunataka kuelewa na kutimiza Agizo Kuu, ni lazima tuchunguze kwa makini sana mambo hayo mawili.
UHAKIKISHO ULIOKO KATIKA HILO AGIZO (MS. 18, 20A)
Agizo lenyewe linaanza kwa tamko la kushangaza sana lililowahi kutolewa. Yesu alisema, “Mamlaka yote nimepewa Mimi,mbinguni na duniani.” Hapo, sifa Yake na agizo letu
36
vinategemea sentensi hiyo. Nini maana yake, na ni muhimu kiasi gani maneno hayo?
“Mamlaka” yanayotajwa hapa ni mamlaka ya KiMungu. Kanuni kuu katika Maandiko yote ni kwamba, “hakuna mamlaka isipokuwa itokayo kwa Mungu” (ktk Warumi 13:1), na kanuni hiyo inaonekana hapa pia. Katika Kiyunani, neno linalotumiwa kueleza mamlaka ni exousia, ambalo maana yake halisi ni “kutokana na kuwa”. Fikiri kidogo jambo hili. Maana yake ni kwamba mamlaka yote ya lazima kutoka kwa Mungu mwenyewe yametolewa kwetu kwa njia ya mahusiano yetu na Kristo ili kutimiza Agizo hilo.
Halafu, mamlaka hii ni mamlaka iliyotolewa. Yesu Kristo anayo mamlaka katika Nafsi Yake, ambayo anaimiliki kwa sababu ya kuwa Yeye. Mamlaka aliyokuwa nayo wakati wa maisha Yake hapa duniani ilionyeshwa kwa njia nyingi zilizo wazi.
Alionyesha mamlaka Yake juu ya nguvu za asili wakati alipotuliza dhoruba kali iliyokuwa imewatisha hata wavuvi waliozoea, kwa neno tu la kinywa Chake na kunyoosha mkono Wake. Alikuwa amesema na mtini nao ukakauka mbele ya macho ya wanafunzi, waliokuwa wameshangaa sana.
Vile vile alikuwa na mamlaka juu ya dhamiri ya mwanadamu. Kwa kutumia mazungumzo rahisi tu naye, Mwokozi wetu aliamsha dhamiri ya mwanamke Msamaria aliyekuwa amejaa dhambi, na kuanzisha hali ya matumaini katika nafsi yake. Wakati mwingine, akiwa amezungukwa kabisa na kundi lililotaka kujua mambo mengi,
37
kwa kutaja tu jina la mtu na kumwambia ashuke kutoka kwenye mti, aliweza kuiamsha dhamiri ya Zakayo, Myahudi aliyechukiwa na asiyemcha Mungu, wa mjini Yeriko.
Vile vile alionyesha mamlaka makuu juu ya ile dunia ya kiroho isiyoonekana wakati wa maisha Yake hapa duniani. Kwa neno tu au mguso, aliweza kufukuza falme na mamlaka za uovu zilizokuwa zimetawala maisha ya mtu.
Tena alikuwa na mamlaka ya kupendeza sana katika eneo la udhaifu na magonjwa ya mwanadamu. Akitumia nguvu Zake bila kutaka kujionyesha, lakini kwa ajili ya kusaidia maisha ya watu waliokuwa wanateseka, aliwafanya viziwi wasikie, vipofu waone, bubu waseme, viwete watembee, vilema wanyooke katika viungo vyao, na wafu warudie uhai wao.
Hata mafundisho Yake pia yalikuwa na mamlaka. Baada ya mafundisho Yake ya kwanza katika sinagogi fulani, watu “walishangazwa na mafundisho Yake, kwa sababu aliwafundisha kama mtu aliyekuwa na mamlaka, si kama waandishi” (ktk Marko 1:22, TLR). Yesu hakusita kuchukua mamlaka kamili kabisa. Alidai kuwa na mamlaka ya kusamehe dhambi (ktk Marko 2:10). Alitoa matamko yaliyorekebisha kanuni za Torati ya Musa, ambayo kila mtu aliikubali kuwa ilitokana na Mungu (ktk Mathayo 5:21, 27, 33). Hata alidai kwamba Yeye Mwenyewe ndiye angemhukumu kila mtu (ktk Yohana 5:27).
38
Lakini, mamlaka inayoonekana katika madai haya si ile mamlaka inayotajwa katika Mathayo 28:18. Yesu alisema kwamba haya mamlaka “yametolewa” bila shaka kwa msingi wa mafanikio Yake katika Kifo na Kufufuka Kwake. Mamlaka ambayo alikuwa nayo wakati huo katika utukufu Wake wa ufufuo yalizidi sana yale aliyokuwa nayo wakati wa maisha Yake. Kila aina ya mamlaka ilikuwa Yake kwa sasa. Mamlaka hiyo alikuwa amepewa kwa amri ya Baba Yake mbinguni. Wanafunzi walijua kwamba wao walikuwa watumishi wa Bwana ambaye mamlaka Yake mbinguni na duniani haikuwa na utata hata kidogo wala swali la aina yoyote ile. Tunasoma hivi katika Warumi 1:4, “Alitangazwa kuwa Mwana wa Mungu kwa nguvu (mamlaka) … kwa ufufuo kutoka kwa wafu” (TLR). Hayo mamlaka ndiyo msingi wa Agizo analotoa kwa wanafunzi Wake.
Ni dai la ajabu sana! A.T. Robertson alisema hivi: “Ni onyesho la hali ya juu sana katika historia ya dunia, kumwona Kristo aliyefufuka, pasipo fedha wala jeshi wala taifa, akiwaagiza kundi hili la watu mia tano – waume kwa wake – waende kuiteka dunia na kuwafikisha mahali pa kuamini kwamba inawezekana kufanyika, kwa mguso na udhati na nguvu.”
Vile vile, mamlaka hii ni mamlaka anayostahili Yeye. Yesu alisema hivi: “Mimi nimepewa mamlaka yote.” Ona kwamba hii mamlaka hatujapewa sisi, bali kapewa Yeye. Lakini, hilo lisitupe
39
hofu, kwa sababu chochote kilicho Chake ni mali ya kila mtu aliyeokoka. Kila mtu aliyezaliwa mara ya pili ni mrithi wa Mungu kwa sababu yeye ni “mrithi pamoja na Kristo” (ktk Warumi 8:17). Kila kitu katika milki ya Baba ambacho kihalali ni mali ya Kristo kwa sasa ni mali yangu pia kwa sababu ya mahusiano yangu kiimani, au kujitambulisha kwangu kiimani, na Yeye. Chochote kilicho Chake ni changu, si kwa sababu mimi ninastahili kuwa nacho, bali kwa sababu mimi niko ndani Yake. Ona pia kwamba, hakupewa mamlaka haya kwa sababu Yeye ni Mwana wa Mungu. Kama Mungu, hakuna kitu anachoweza kuongezewa, na hakuna kitu kinachoweza kupunguzwa Kwake. Mamlaka ambayo Yesu anadai hapa ni mamlaka ambayo ameipata (ameistahili) kama Mwana wa Mtu. Neno “aliyopewa” linaonyesha tendo la wakati uliopita, na bila shaka humaanisha kukabidhiwa mamlaka hiyo siku ile alipofufuka toka kwa wafu. Hii inakubaliana na yale maandiko katika Wafilipi 2:5-11, yanayohusu Kunyenyekezwa na Kutukuzwa Kwake. Baada ya Paulo kuonyesha jinsi Yesu alivyoshushwa na kunyenyekezwa, ndipo anapodhihirisha kutukuzwa Kwake kulikofuata. “Kwa hiyo tena Mungu alimwadhimisha mno, akamkirimia Jina lile lipitalo kila jina; ili kwa jina la Yesu kila goti lipigwe, la vitu vya mbinguni, na vya duniani, na vya chini ya nchi; na kila ulimi ukiri ya kuwa Yesu Kristo ni Bwana, kwa utukufu wa Mungu Baba” (ktk Wafilipi 2:9-11). Kwa hiyo, kutukuzwa Kwake na mamlaka Yake vilimstahili kutokana na kifo na kufufuka Kwake.
40
Mwisho – mamlaka aliyodai kabla ya kutoa Agizo Lake Kuu yalikuwa mamlaka yaliyoelezwa na kuwekwa wazi. “Nimepewa mamlaka yote, mbinguni na duniani.” Maeneo hayo mawili yanayotajwa ndiyo pekee ambayo sisi tunahusika nayo, na bila shaka Yesu Kristo anatenda kazi katika maeneo hayo pia. “Mbinguni na duniani.” Mamlaka yote ya mbinguni ni Yake, na mamlaka yote ya duniani ni Yake. Anawatangazia wanafunzi Wake kwamba “nimepewa Mimi mamlaka yote mbinguni”, mahali alipopokea “Jina lipitalo majina yote”, mahali ambapo “ametukuzwa na kuketishwa mkono wa kuume wa mamlaka”, mahali ambapo “ametiwa taji ya heshima na utukufu”. Anatangaza pia kwamba “Mimi nimepewa mamlaka yote duniani”. Hivyo, Yeye ndiye Bwana mkuu wa kote kuwili.
Katika mchezo maarufu sana wa Shakespeare, mwandishi Mwingereza maarufu, anaonekana Liwali wa Kent akimjia mfalme kwa siri, akiwa amejibadilisha. Mfalme huyo Lear anamwambia, “Unataka nini wewe?” Yule Liwali anamjibu, “Nataka nikutumikie.” Mfalme anamwuliza, “Kwa nini?” Ndipo linatoka jibu maarufu la Liwali wa Kent, kwamba, “Kwa sababu katika uso wako naona kitu ambacho kwa hiari yangu mwenyewe naweza kukiita bwana”. Mfalme akamwuliza, “Kitu gani hicho?” Liwali anajibu, “Mamlaka”.
Yesu anatoa madai halali kabisa kwamba mamlaka yote ni Yake. Na katika mamlaka hiyo ndipo tunapaswa kutekeleza ule mradi wa utume (na ile amri ya kufanya watu kuwa wanafunzi).
41
Mamlaka Yake hayajapungua wala kumalizika kutokana na miaka kupita. Basi, kwa msingi wa mamlaka hiyo, tunapaswa kutekeleza agizo au kazi tuliyopewa katika Agizo Kuu.
KAZI ILIYOKO KATIKA HILO AGIZO (MS. 19, 20)
AMRI PEKEE KWA KANISA (KWA MKRISTO) KUSONGA MBELE
Agizo Kuu ndiyo “amri pekee ya kusonga mbele” iliyowahi kutolewa na Yesu Kristo kwa Kanisa Lake. Agizo Kuu ni kazi ya kuvuna roho na utume, lakini ni zaidi ya hayo. Kuna maelezo kuhusu Agizo Kuu la Bwana wetu katika Agano Jipya mara tano. Linatajwa kwa njia tofauti katika Mathayo 28:18-20 (kwa maelezo yaliyo dhahiri zaidi), katika Marko 16:15 (kwa kifupi lakini wazi), katika Luka 24:47, Yohana 20:21 na Matendo 1:8 (kwa ufafanuzi mpana zaidi).
Katika maelezo ya Mathayo, Kanisa la Yesu Kristo linapata msingi kwa ajili ya kazi yake. Hakuna swali kabisa katika maneno anayotoa Mathayo kuhusu kile ambacho Yesu alikusudia wafuasi Wake kufanya. Si swala la hisia au kujisikia. Si kazi ya kufanywa tutakapoona inafaa. Yesu aliacha maagizo dhahiri. Maagizo hayo ni kamilifu (yaani, hayapitwi na wakati wala kubadilika) na ni ya mara moja. Agizo Kuu ni la sasa hivi, na linamfunga kila Mkristo kulitimiza wakati huu. Maneno ya Agizo hili ni maneno tendaji: Enendeni, fanyeni watu kuwa wanafunzi, batizeni, na fundisheni.
42
Kwa kifupi tu, Kanisa liko chini ya amri, lakini uhalisi wa hiyo amri unaweza kuwashangaza waamini wengi.
KULIGAWA AGIZO SEHEMU SEHEMU
Ningependa kuligawa Agizo Kuu katika sehemu saba. Muhtasari ni kama ifuatavyo: Kwanza, sisi tunawajibika kutumia kila mtenda kazi anayepatikana (neno “ninyi” la ms. 19 liko katika wingi). Halafu, tunatakiwa kuingia shambani (“enendeni”). Tatu, tunatakiwa kila wakati kupanua maono yetu (“mataifa yote”). Nne, tunapaswa kuwashuhudia wahusika (“kufanya wanafunzi”). Tano, tunapaswa kuwahusisha walioshuhudiwa (“mkiwabatiza katika jina la Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu”). Sita, tunatakiwa kuwaelimisha na kuwajenga waliojiunga nasi (“na kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi”). Na mwisho, tunapaswa kutarajia Yeye kutenda kazi (“na tazama, Mimi niko pamoja nanyi siku zote, hata mwisho wa dunia”). Bila shaka unaona sasa kwamba, yapo mengine mengi sana kuhusu Agizo Kuu la Bwana wetu kuliko ambavyo sisi tumekuwa tukiheshimu!
Tunapochunguza kwa makini na dhati kabisa hili Agizo, tunagundua kitu cha kushangaza sana. Tunapata kwamba, kwa karibu karne mbili, Agizo lilifanya kazi vizuri kabisa na kuigusa dunia iliyokuwa inajulikana siku zile kwa haraka sana. Lakini, kitu cha ajabu kikatokea. Kitu fulani kiliharibika kabisa. Ili kuona hilo, ningependa tutazame kila hoja katika zile saba ambazo nimetaja.
43
Chini ya kila hoja, ninataka utazame vichwa vidogo viwili. Kimoja ni “Mkakati wa Mwokozi”, na kingine kinaitwa “Mbadala wa Shetani”. Tutafanya hivyo na kila hoja.
1. KUTUMIA KILA MTENDA KAZI
Hoja ya kwanza katika Agizo Kuu ni kutumia kila mtenda kazi. Katika mstari wa 19, neno “ninyi” liko katika wingi, na maana yake hasa ni “ninyi wote”.
Mkakati Wa Mwokozi
Mtu mmoja ameeleza nia ya Yesu kuhusu kutimizwa kwa Agizo hili Kuu kwa maneno haya: “Waamini wote wanatakiwa kuhusika, na wanapaswa kutenda wakati wote”. Kitu kimoja – licha ya nguvu za Mungu – kilichofanya Agizo Kuu kufanikiwa sana hapo mwanzoni ni kwamba, watenda kazi wake wote walihusishwa kufanya huduma mahali palipotakiwa. Lengo lilikuwa kwamba kila mwanafunzi awe mzalishaji wa wavuna roho na wafanya watu kuwa wanafunzi kama yeye. Wote walikuwa wasemaji, waenezaji na wainjilisti! Ukweli ni kwamba, kushiriki kulikuwa kwa kila mtu miongoni mwao mpaka ikabidi sheria ziwekwe ili kuondoa vurugu au kuchanganyikiwa (ona 1Wakor. 14:31). Hapakuwepo na watazamaji miongoni mwao. Adolph Harnack, mwanahistoria maarufu wa kanisa, alisema hivi: “Wakati kanisa liliposhinda sana katika siku za mwanzo za Dola ya Rumi, halikufanya hivyo kwa
44
waalimu au wahubiri au mitume, bali kwa wamishenari wa kawaida kabisa.” Hili Agizo linataka huduma binafsi kutoka kwa kila aaminiye. Wote walio viungo vya Mwili wa Kristo hawawezi kufanya hivyo bila ya kila mshirika kufanya hivyo. Kanisa moja katika eneo la Manhattan huko Marekani lina ujumbe ufuatao kwenye kibao chake: “Mchungaji, --------“. “Wahudumu: Kila mshirika.” Huo ndiyo mkakati wa Mwokozi kwa ajili ya kila mtenda kazi kutumika.
Mbadala Wa Shetani
Sasa, tazama mbadala alioleta Shetani. Ukweli ni kwamba Agizo Kuu lilifanya kazi. Yaani, lilifanya kazi mpaka Shetani akaona vibaya. Lilifanya kazi vizuri sana kiasi kwamba ilimchukua miaka 200 kuondokana na kipigo alichopata na kupanga upya majeshi yake. Hatimaye, akapambana na Agizo Kuu kwa mpango mbadala wake. Si vigumu kuona kwamba Agizo Kuu la kwanza limevurugwa kiasi. Limerekebishwa, na kwa karne nyingi sana, makanisa mengi yameangukia katika mpango wa Shetani. Pigo kubwa sana la Shetani dhidi ya Agizo Kuu lilielekezwa kwenye ile hoja ya kwanza, ya kutumika kila mtenda kazi.
Mapema kabisa katika historia ya Kanisa, Shetani alianzisha mgawanyo katika Kanisa. Likawa na sehemu mbili, naye akakazia kupita kiasi zile tofauti. Walio wengi aliwaita “walei – wasiokuwa wachungaji” na wale wachache akawaita “wachungaji – watumishi”.
45
Na hoja yake kubwa ilikuwa kwamba walei hawana uwezo na hawana vipawa, na kwamba hawahusiki katika kazi halisi ya kanisa hata hivyo. Shetani basi akasimamia ujenzi wa tabaka ya watu wa dini walio wataalamu. Hawa wataalamu walitakiwa (1) kupigana vita zote za kiroho, na (2) kufanya kazi zote za kiroho. Vipi shughuli ya “walei”? Kumtegemeza na kumsaidia huyo mtaalamu kiongozi na kulipia mpango wake kufanyika (ambapo katika Agano Jipya, watu ndiyo mpango mkuu).
Basi, “ngazi ya kiroho” ikatengenezwa Kanisani. Juu kabisa ya ngazi alikuwepo “mishenari”, halafu anayefuata ni mchungaji, halafu watendaji wengine wataalamu wa kidini, na mwisho wa ngazi, mshirika wa kawaida. Kuna mtu amesema kwamba kizazi chetu ni “kizazi cha mtazamaji”. Mpira wa miguu una wachezaji 22 kwa mara moja, lakini unaweza kuwa na watazamaji mamilioni wakati huo huo! Michezo mingine ina wachezaji 18. Mpira wa vikapu una wachezaji kumi, ngumi wachezaji ni wawili, na kuna michezo mingine katika Olimpiki yenye mchezaji mmoja tu. Lakini michezo hiyo yote ina mashabiki mamilioni. Mchekeshaji mmoja aitwaye Fred Allen alisema hivi: “Kama jamii itaendelea kama ilivyo, baada ya muda tutakuwa na dunia iliyojaa watu wenye macho makubwa kama sahani za vikombe vya chai, na akili zenye ukubwa wa harage” (kwa kuwa wakati wote watu wanakodoa macho, na kutumia muda mwingi katika ushabiki)!
46
Matatizo Kanisani Ya Watu Kutokuwa Na Kazi, Na Kazi Kidogo
Kanisa limetengeneza matatizo mawili ya “kutokuwa na ajira” na hayo yanaungana mkono mara zote, na kufanya mambo kuwa mabaya zaidi. Kuna tatizo la kutokuwa na kazi kwa washirika katika kusanyiko la mahali. Kwa kuwa mshirika wa kawaida katika kanisa la kawaida hatimizi kazi yake aliyopangiwa na Mungu, “mshahara” wake unapunguzwa na kuwa posho tu kwa ajili ya kuishi. Wajibu wake hautimizwi, thawabu yake inapotea, dunia inabakia gizani, na Shetani anatosheka vizuri sana.
Halafu kuna tatizo linalokaribiana na lile, ambalo ni mtumishi kutofanya kazi ipasavyo. Mchungaji wa kawaida katika kanisa la siku hizi ana kazi nyingi, lakini hafanyi kazi ipasavyo! Wakati Henry M. Stanley aliporudi kutoka Afrika kwenye kumtafuta David Livingstone, mwanahabari mmoja alimwuliza swali hivi: “Ni kitu gani kilichokusumbua zaidi wakati ukiwa Afrika? Ni wale simba, au ni nyoka?” Stanley akajibu hivi, “Wala! Walionisumbua zaidi ni mbu!” Wachungaji wetu hawapati kuona simba na chui kwa sababu daima wako kwenye mapambano na mbu. Wakati vita kuu za atomiki zinapiganwa katika ulimwengu wa roho, wao wanajitahidi kupambana na kukabiliana na mashambulizi ya mbegu ndogo ndogo tu! Ongezeko la vitu vingi vidogo vidogo – vishughuli vingi vya kidini ambavyo vinachokesha, pamoja na picha bandia ya huduma ya mchungaji ambazo zimechorwa njiani mwake vinamfanya mchungaji ashindwe kutekeleza kazi pekee ambayo Mungu amempa.
47
Hivi karibuni nilipata taarifa kutoka Ofisi Kuu ya Jimbo kwamba wachungaji 300 wa Kibaptisti wanaondolewa makanisani kila mwezi. Sina uhakika na idadi hiyo, lakini najua kwamba tatizo hilo ni kubwa sana. Pia nilisikia taarifa miaka kadhaa iliyopita kwamba wachungaji zaidi ya elfu moja wa Kibaptisti wanaachana na madhabahu zao. Sina uwezo wa kuthibitisha idadi hiyo, lakini najua kwamba tatizo hilo ni kubwa sana pia. Pengine sababu kubwa ya huko kutatizika kwa uongozi unaoitwa ni kwamba kiongozi huyo hatosheki kwa “ajira ndogo” inayomkabili – hana kazi za kumtosha kuridhika!
Ukristo Tazamaji Katika Kanisa
Tumetengeneza Ukristo tazamaji katika kanisa, ambao katika huo, wachache ndiyo wasemaji, na wengi ni wasikilizaji. Kanisa limejaa “umoja wa mashabiki” – mashabiki wa imani. Hebu fikiri kuhusu duka la kuuza vitu jumla, ambalo lina meneja mauzo ambaye kazi yake ni kuuza hivyo vitu na kufundisha kuhusu sifa ya vitu hivyo na mbinu za uuzaji. Tuseme pia kwamba duka hilo lina kundi kubwa tu la “wauzaji” ambao kazi yao kubwa ni kuwatafuta wasikilizaji na kuwatia moyo kusikiliza tu mafundisho ya meneja mauzo. Kingekuwa kituko cha namna gani hicho? Je, duka hilo lingedumu kwa muda gani? Ndugu James S. Stewart wa Edinburgh, Uskochi, alisema hivi: “Tatizo hasa la Ukristo si wasemao hakuna Mungu wala wenye mashaka, bali ni Mkristo asiyeshuhudia, asiyezaa
48
matunda, anayejaribu kuingiza roho yake mbinguni kwa njia ya magendo, yeye mwenyewe.” Huo ndiyo mkakati wa Shetani, na zaidi ya hayo, ametumia sana neno “ninyi” mpaka imefikia kwamba hata hao “watumishi” si wote wanaoshuhudia!
Hebu tazama jamii ya Kikristo. Kanisa liko upande gani – upande wa Mkakati wa Mwokozi, au upande wa Mbadala wa Shetani? Nadhani jibu liko wazi kabisa, na linasikitisha. Ni lazima tutazame upya Amri yetu ya Kusonga Mbele!
2. KUINGIA SHAMBANI
Hoja ya pili katika muhtasari wetu kuhusu Agizo Kuu ni kuingia shambani kote. Neno “enendeni” ni neno tendaji, lenye nguvu – neno linalo-onyesha kwenda au kutembea.
Mkakati Wa Mwokozi
Mkakati wa Mwokozi ni dhahiri. Katika Mathayo 13:38, alisema hivi: “Shamba ni dunia”. Hili si shamba kwa ajili ya kanisa, bali ni shamba kwa ajili ya kanisa lako la mahali! Yesu Kristo anakutazamia uhusike na dunia nzima! Mifano ambayo Yesu anatumia kusema kuhusu Wakristo na Injili imefungamanishwa pamoja kwa kitu kimoja. Yote ina tabia ya kupenya – kuingia ndani. Yesu alitumia mfano kama nuru, chumvi, funguo, mkate, na maji. Nuru haina faida kama haipenyi na kufukuza giza. Chumvi haina faida kama inabakia ndani ya chupa yake. Lazima ipenye na kuingia
49
katika mboga au viazi. Mtoto mmoja mvulana alisema hivi, “Chumvi ndiyo huharibu viazi – ukiacha kuiweka.” Funguo hazina maana kama haziingii katika kitasa. Mkate hauna faida ukiwa nje ya mlaji, na maji hayatoshelezi hitaji la mtu mwenye kiu kama yasipomwingia. Vivyo hivyo, Wakristo wanatakiwa kuingia na kupenya duniani kila mara.
“Huwezi kumtaja Mungu bila kwenda. Hakuna uzuri bila kwenda. Huwezi kutamka neno Injili bila kwenda, na huwezi kuitii Injili na kuwa mtumishi mzuri wa Mungu usipokwenda – kwa masharti Yake. Ukristo ni kitu cha kwenda kwa asili yake na msukumo – si cha kushikilia. Kila Mkristo anapaswa kuishi kikazi (yaani, kama Mkristo) kwenye eneo la kupenya – iwe ni katika maabara ya kisayansi, maktaba, kiwandani, shamba la matunda, kazi ya kugawa vitu, cheo kikubwa, kwenye ndege ya kisasa, katika hospitali ya tabibu wa magonjwa ya akili, au katika ofisi ya mchungaji. “Dunia” yetu ni popote tulipo, penye watu. Katika Luka 10:1-3, Biblia inatuambia, “Basi, baada ya hayo Bwana aliweka na wengine, sabini, akawatuma wawili wawili wamtangulie kwenda kila mji na kila mahali alipokusudia kwenda mwenyewe. Akawaambia, ‘Mavuno ni mengi, lakini watenda kazi ni wachache; basi mwombeni Bwana wa mavuno apeleke watenda kazi katika mavuno yake. Enendeni. Angalieni, nawatuma kama wanakondoo kati ya mbwamwitu”. Ona maeneo ambayo nimekazia kwa kutumia wino mwepesi. Maneno hayo yamejaa! Kila Mkristo anapaswa kuwa
50
mwanzilishi, mtangulizi kwa ajili ya ujio wa Kristo “kila mahali alipokusudia kwenda mwenyewe.” Wanakondoo kati ya mbwamwitu watarajie kupona kwa muujiza tu!
Tena – neno “enendeni” katika Agizo Kuu SI AMRI. Kulihesabu kwamba ni amri ni kuendeleza ile dhana ya “ngazi ya kiroho katika Ukristo”. Lingekuwa ni amri, kila ambaye angekwenda mbali ili kuihubiri Injili au kumshuhudia Kristo angehesabiwa kuwa mtu maalum. Lakini, neno tendaji lina maana hii: “Mnapokuwa mkienda”, au hata, “Kwa kuwa mnakwenda”. Yesu asingekosa akili kiasi hicho, atuagize kufanya kitu ambacho tunafanya tayari! Je, kanisa lako liko wapi Jumanne mchana saa tisa? Kwani liko kanisani? Hapana, “linakwenda”. Swala hapa si kwamba mbona kanisa haliendi duniani? Swala ni hili: Je, kanisa linatimiza kazi yake linapoingia na kupenyeza?
Nilikuwa katika mji mkubwa mzuri sana katika nchi ya kigeni fulani, miaka kadhaa iliyopita. Nilihubiri kwenye kanisa la Kiingereza hapo Jumapili asubuhi. Nikawahi ili nipate nafasi ya kuzungumza na watu walipokuwa wanafika ibadani. Mbona nilishtushwa sana na watu wenyewe! Walikuwepo Wamarekani wengi, na walikuwa wafanya kazi katika shirika la mafuta la kimataifa, wenye mishahara mikubwa sana. Nilipowauliza jinsi walivyokuwa wanafurahia kukaa huko, wote walilalamika kwamba wanachoshwa na mambo yale yale kila siku. Wengi wao walikuwa hapo kwa mikataba ya miaka miwili. Katika mahubiri yangu,
51
niliuliza ni kwa nini wasijifunze lugha ya pale na wawe na vipeperushi vyenye ujumbe wa Injili katika lugha ya pale na wafanye umisheni, uinjilisti na kuleta watu kwa Yesu wakiwa huko. Nadhani walipuuza wazo hilo bila hata ya kulifikiria! Ni hivi: Kuna mtu ambaye ametuuzia wazo baya kabisa lenye kupelekea usaliti mkubwa sana wa Yesu na Agizo Lake. Wao walikuwa “wamekwenda” (tena, kwa kulipwa na shirika la mafuta), lakini hawakutambua wajibu wao “wakiwa katika kwenda”.
Mbadala Wa Shetani
Shetani ameingiza mbadala wa kijanja na siri sana katika akili za Kanisa. Maneno makuu mawili katika Injili ni “njoo” na “enenda”. Tukisha kuja kwa Kristo (Mathayo 11:28-30, kwa mfano), tunapaswa “kwenda na kuwaeleza” watu wote yale tuliyopata katika Kristo. Shetani ni bingwa wa kutumia watu, na kubadili maneno. Yeye akaingiza upotofu wa polepole kanisani, kuliondoa kwenye “nenda ukaeleze” na kulitia kwenye “njoo usikie”. Mkomunisti mmoja alitania Kanisa kwa maneno haya, “Kauli mbiu ya Wakristo inaonekana ni, ‘Njooni hapa mpate ujumbe wa Mungu, mwende mbinguni. Au acheni kuja, mwende jehanamu’!” Ndugu mmoja aitwaye Paul Little alisema hivi, “Tatizo si kwamba Injili imepoteza nguvu yake. Tatizo ni kwamba kanisa limepoteza walengwa wake.” Mwingine naye akasema, “Roho Mtakatifu hawezi kuwaokoa watakatifu na viti – lakini Kanisa limejaa vyote!”
52
Fikiri mfano wa kimatibabu. Tuseme kwamba Wizara ya Afya inaogopa kwamba kutatokea mlipuko wa surua. Ingefanya nini ili kuzuia kuenea kwa ugonjwa huo? Bila shaka ingewatenga wenye ugonjwa huo na kuwaweka karantini wote ambao wamekwisha upata, na kwa njia hiyo ugonjwa ungezuilika. Sasa hebu fikiri – Wizara ya Jehanamu itake kuzuia mlipuko wa Ukristo wa Agano Jipya. Bila shaka ingefanya kila liwezekanalo kuwatenga “wabebaji” na kwa njia hiyo kuzuia kuenea kwake. Na hicho ndicho kinachotokea Kanisani kwa sehemu kubwa. Tunakaa ndani ya Kanisa kwa “mkao mtakatifu”. Timu yetu haiendi uwanjani, mahali ambapo ili kupata ushindi mchezo lazima ufanyikie. Na kuna wanaopenda mpango huu na uzuri wake na usalama wake. Maana, umewahi kumsikia mchezaji aliyeumizwa akiwa hajaingia uwanjani? Kwa hiyo, tunapanga mikakati yetu, tunafanya uchambuzi kuhusu adui yetu, tunarudiarudia mambo na hata kulaumu wachezaji wenzetu. Tunawaza kuhusu uanachama, mipango yetu, majengo na fedha. Kila juma tunakuwa na “gwaride” na amri yetu kuu ni “tubaki kama tulivyo”. Nimechanganya mifano hapo, lakini nadhani ujumbe umefika. Daima tunaongeza shughuli zetu za kidini, tunakamilisha mipango yetu kishirika, tunapanua na kukuza taasisi zetu za kidini, na kuimarisha taratibu zetu kiuongozi katika dini, na yote tunayofanya katika makanisa mengi ni kudumisha kawaida na kujistarehesha sisi wenyewe tu! Bila shaka Shetani anafurahi sana!
53
Kanisa la kawaida linafanya kazi kwa kufuata mpango mbadala wa Shetani, badala ya kufuata mkakati wa Mwokozi.
3. KUPANUA MAONO
Sehemu ya tatu katika Agizo la Bwana wetu ni kuendelea kupanua maono. Upana wa eneo letu la utendaji katika Agizo hili ni “mataifa yote”.
Mkakati Wa Mwokozi
Hebu tujikumbushe tena – Yesu Kristo hafanyi mchezo nasi. Anatutazamia kabisa “tukabiliane” na dunia nzima! Naye ametupa Mpango ambao kwa huo tunaweza kufanikiwa! Je Mkristo – ni nia yako kugusa mataifa yote kwa “kuwageuza watu kuwa wanafunzi”? Hiyo kazi kuu ndiyo agizo la Bwana wetu. Kugusa dunia ndiyo utume wetu. Lengo letu lazima liwe kujulisha na kugusa dunia nzima mpaka mwisho wa nchi, mpaka ukamilifu wa dahari.
Hii hoja ya tatu katika Agizo inawezekana kuwa ndiyo ya maana kuliko zote. Hapa ndipo motisha kwa ajili ya kuwafanya watu kuwa wanafunzi inapotokea. Ningependa kutumia nafasi zaidi hapa ili kuhakikisha kwamba sote tunatambua ukuu wa Agizo la kuigusa dunia nzima. Dakta D. Martyn Lloyd-Jones alisema hivi katika kitabu chake kiitwacho The Miracle of Grace, “Sitasita kusema kwamba hatimaye, hakuna kipimo kamili cha ukiri wetu binafsi wa imani kama hali tuliyo nayo moyoni juu ya shughuli ya umisheni ya
54
Kanisa.” Mimi niongeze maneno yangu hapa kwamba, “shughuli ya umisheni ya Kanisa” si kutuma waamini wenye mzigo maalum kwenda nchi za mbali tu. Huanza katika moyo wa kila aaminiye, na hutekelezwa kwa kila aaminiye kuwa mwanafunzi wa Yesu Kristo anayetambua kuhusu dunia nzima, anayelemewa na dunia nzima, anayeona dunia nzima, na mwenye kuwajenga na kuwaongeza wanafunzi wengine wenye kuiona dunia nzima na kuigusa dunia nzima.
Je, maono yako binafsi ni maono “makubwa kama ya Mungu”? Je, unakusudia kufika wapi na kugusa watu? Kipimo cha kufanikiwa kwako kama mwanafunzi wa Kristo kunaweza kuonekana katika jinsi unavyojibu maswali haya: Je, ushawishi ulio nao unafika mbali kiasi gani? Je, nini ukubwa wa eneo lako la uwezo? Isaya 54:2 inasema, “Panua mahali pa hema yako, na wayatandaze mapazia ya maskani yako; usiwakataze. Ongeza urefu wa kamba zako, vikaze vigingi vya hema yako.” Mstari huu unatoa kauli mbiu kamili kabisa kwa ajili ya wote wanaofanya wengine kuwa wanafunzi (yaani, wanafunzi wote wa kweli wa Kristo), na hutoa mwito kwa ajili ya kukuza maono kusikokoma kwa kila aaminiye, ili kuigusa dunia nzima.
Hapa tena naomba ukabiliane na swali hili: Je, nini ukubwa wa eneo lako la uwezo na ushawishi? Je, unatenda kazi chini ya maono kama kofia, ambapo maisha ya Kikristo yanaanza na kuishia kwa ajili ya manufaa yako binafsi – ili uishi na upate kitu? Au je,
55
maono yako ni kama mwavuli, yenye nafasi kwa ajili ya watu wawili au watatu hivi? Au je, maono yako ni kama kibanda cha simu, yenye nafasi ya kufunika watu kati ya watu hadi wanne? Au je, ni kama chumba, yenye kuwaingiza marafiki kadhaa? Au pengine yako kama nyumba, yenye uwezo wa watu kama 25 hadi 50 hivi? Au ni kama duka kubwa, yenye uwezo wa watu mia kadhaa, na hata elfu kadhaa? Au ni kama uwanja wa michezo, yaliyo na upana wa kutosheleza makumi elfu? Au pengine unatamani kuwa na maono kama anga, ambayo yanaweza kuwahusisha watu wote duniani na vizazi vyote vitakavyokuja? Kumbuka kwamba Agizo linahitaji maono yanayolingana na Yesu, yenye ukubwa wa Mungu, nasi tunatakiwa tuzidi kufanana na Kristo, kwa hali hiyo kuendeleza Tabia ya Mungu Mwenyewe. Tunakuwa “washiriki wa asili Yake ya Uungu” (ktk 2Petro 1:4) tunapo-okoka, na sehemu inayobaki ya maisha yetu inapaswa kutumika katika kushirikiana na kupanuliwa kwa Asili Yake ndani yetu. “Yeye hana budi kuzidi, bali mimi nipungue” (ktk Yohana 3:30). Sehemu ya huku kupanuka inamaanisha kuongezeka katika kujitambulisha na “Kinachomsumbua” Mungu – kumjulisha na kugusa kila mtu duniani kwa Ujumbe wa Injili Tukufu ya Kristo.
Ni dhahiri kutokana na kusoma Injili hata kwa juu juu tu kwamba, Yesu alikuja ili kuvamia, kufahamisha na kugusa dunia nzima. Angeweza kusema, “Mimi ni nuru ya Galilaya”, lakini hakufanya hivyo. Alisema, “Mimi ni nuru ya dunia” (ktk Yohana 8:12). Hakusema, “Mimi ni nuru ya Wabaptisti au WaPresbiterian au
56
WaMethodisti”. Hakusema, “Mimi ni nuru ya waliolelewa vema au waliosoma vizuri au waliolishwa vizuri”. Angeweza kusema, “Mungu aliwapenda sana Wayahudi” lakini hakufanya hivyo. Alisema, “Mungu aliipenda sana dunia” (ktk Yohana 3:16). Yesu alikazia tena na tena kwamba hakuwa na mpango wa kufikia kisehemu kidogo au watu wachache – mpango Wake ulikuwa ni dunia nzima. Yeye ndiye nuru pekee ya kiroho kwa ajili ya kila nchi na kwa ajili ya kila mtu aliyeko katika kila nchi duniani.
Inasemekana kwamba askari wa jeshi la Napoleon walikuwa wanabeba ramani ya dunia katika mikoba yao, pamoja na bendera ya Ufaransa. Walikuwa ni wafungwa, mateka, watumwa wa wazo la kuiteka dunia kwa ajili ya Ufaransa. Enyi ndugu zangu Wakristo na dada zangu – Bwana wetu Mwenyezi ameweka maono yanayowaka ya dunia nzima mbele ya macho ya watu Wake na amewaomba kila mmoja kuyaruhusu yawake mpaka yachome moyo. Na haya maono yanapaswa kushika mawazo yetu kila wakati, mipango yetu, ndoto zetu, shughuli zetu kwa muda wote tunaoshi. Mara maono yatakapoanza kutushika, tutatambua kwamba Yesu aliweka mpango kwa ajili yetu – wewe na mimi kama watu binafsi – ili kutekeleza na kukamilisha maono yenyewe. Kufanya wanafunzi wenye maono ndiyo hilo! Unalionaje hilo?
Hebu tafakari swali hili kwa moyo wako wote. Je, Biblia na Ukristo vilitokea katika jimbo mojawapo kati ya majimbo hamsini ya Marekani? Hapana. Ukristo uliingizwa Marekani. Yesu hakuzaliwa
57
nyumba ya jirani na kwetu, wala katika mtaa wetu. Biblia haikuwa imeandikwa kwa Kiingereza au Kiswahili tangu mwanzo. Sisi Wakristo wa Tanzania (au wa Afrika) ni matokeo ya wamishenari Wakristo. Je, na sisi tumejitoa kufanya katika sehemu zingine za dunia yale ambayo hawa wamishenari walitutendea sisi? Kama ungekuwa mmojawapo wa waliopotea katika Bara la Asia, Afrika au Marekani ya Latin, ungetamani mtu akuletee ujumbe wa Nuru na Uzima? Hakika sisi Wakristo wenye ubinafsi na wenye kujali zaidi taasisi na “makanisa ya kujikimu” lazima tutubu hasa na kuomba huruma na msamaha wa Bwana wetu, kwa sababu tumejaribu kumfanya Yeye kuwa mali yetu (kama Wayahudi walivyofanya) badala ya kuruhusu atutawale na kutumiliki kabisa. Na toba yetu lazima iwe ya kiwango cha ndani sana kiasi cha kufikia mahali pa kusahihisha hii hali ya “Ukristo wa kibinadamu” (neno langu, ambalo hata hivyo linapingana katika maana yake).
Ndugu John Oxenham katika kitabu chake kiitwacho Bees in Amber, aliandika hivi:
Nasikia sauti dhahiri kabisa ikiita, ikiita,
Inaita wakati wa usiku, hivi:
Enyi mnaoishi katika Nuru ya Uzima,
Tuleteeni na sisi hiyo nuru!
Tumefungwa katika minyororo ya giza,
Macho yetu hayapati kuona,
Enyi ambao hamjawahi kufungwa wala kuwa vipofu,
58
Tuleteeni nuru!
Haiwezekani – hamwezi kutusahau,
Sisi tulioko katika usiku wa giza kuu zaidi,
Sisi ni watu tunaozama, sisi ni watu tunaokufa,
Tuleteeni – Jamani, tuleteeni Nuru!
Sasa Mkristo, usije ukaanza kutafuta maandiko ya kunipinga au ya kuthibitisha kwamba watu pasipo Mungu wamekufa na hawawezi kusema hivyo! Najua hayo yote – amini hivyo! Hivyo sivyo watu wasiomcha Mungu wanavyoishi, wanavyofikiri au wanavyozungumza – lakini, ndivyo kila aaminiye anavyotakiwa kufikiri! Hatuwezi kuwaeleza watu waliokufa habari za kifo, wala hatuwezi kutazamia dalili za uhai, matendo na maneno kutoka kwao. Wala hatupaswi kuwatazamia wao kufufuka toka kwa wafu pasipo kuisikia sauti inayofufua wafu! Warumi 10 inaweka wazi kabisa kwamba, hakuna tangazo kwa waliopotea pasipo waliotumwa ili kutangaza ujumbe. Hakuna kusikia bila tangazo, hakuna imani pasipo kusikia, na hakuna wokovu pasipo imani (ktk Warumi 10:12-17)! Katika uhalisi, mambo yanaanzia wapi? Kwenye kutuma na kwenye kusema! Je, kanisa lenu liko katika shughuli ya kutuma? Je, linatumia fedha ili kutuma ili ujumbe uweze kusemwa? Uchaguzi pekee ni kutokutii amri ya Mfalme wa Wafalme na Bwana wa Mabwana. Je, tutajisikiaje na tutafikiri nini tutakapohudhuria mbele ya Kiti cha Hukumu cha Kristo kama tulitumia huduma zetu
59
tukikazia wale “Nyuki Wanaoua” – majengo, bajeti, miili, vipeperushi, majigambo, na kadhalika?
Kabla ya karne iliyopita kufika katikati, Charles Kingsley alitembelea visiwa vya New Hebrides huko Bahari ya Pacific ya Kusini na kushangazwa na ukatili na ulaji watu vilivyokuwepo. Aliporudi Uingereza aliandika makala kali iliyosema kwamba serikali ya Uingereza ingefanya huduma muhimu sana kwa binadamu kama wangetuma merikebu ya vita ili kuwaangamiza hao “washenzi” waishie baharini kama nzi wasumbufu, kwa kuwa hawakuwa binadamu na hakuna kitu ambacho kingeweza kufanyika ili kuwainua kutoka kiwango walichokuwa nacho.
Lakini, walikuwepo watu wengine ambao hawakukubaliana kabisa na tathmini ya Kingsley. Miongoni mwao alikuwepo Mkristo aliyempenda Mungu sana, jina lake John Paton kutoka Dumfries, Uskochi. Paton aliamini kwamba Injili ya Yesu ni nguvu ya Mungu iletayo wokovu (ktk Warumi 1:16), na kwamba Injili ina nguvu za kuhuisha, kuwafufua wale waliokufa katika dhambi (ktk Waefeso 2:1). Baada ya safari ndefu, Paton alifika kisiwa cha Tana huko New Hebrides, na akiwa hatarini daima ya kuuawa, alimhubiri Kristo kwa hao watu. Namwalika msomaji yeyote mwenye mashaka afanye utafiti wa matokeo yeye mwenyewe. Paton alipokufa, wenyeji wa kule walitengeneza kumbukumbu juu ya kaburi yake, iliyokuwa imeandikwa hivi: “Alipokuja, hapakuwa na nuru. Alipokufa, hapakuwa na giza”. Wapendwa – leo hii tunaweza kupenyeza kwa
60
urahisi katika dunia nzima, kwa gharama ndogo kabisa na matatizo madogo tu ya usafiri. “Tumeketi” juu ya rasilmali kubwa sana ambazo zingeweza kutumika kwa ajili ya kuwainjilisha na kuwafanya wengi sana kuwa wanafunzi hapa duniani. Maelfu ya Wakristo, makanisa, na watu waliopotea wangekaribisha na kuitikia upendo wetu katika nchi za karibu na mbali, nasi mara nyingi tunaketi tu katika hali ya kujidanganya katika makanisa yaliyokufa na yanayokufa mahali tulipo. “Mahali ambapo hakuna maono, watu huangamia.”
Siku ile ile Bandari ya Pearl Harbor iliposhambuliwa na madege ya kivita ya Japani, mishenari aliyerudi kutoka Mashariki ya Mbali alikutana na rafiki yake ambaye alikuwa hamwungi mkono katika anachofanya, naye akimtazama kwa jicho la kejeli na kuzungumza kwa sauti ya dharau alisema, “Ehe! Unasemaje kuhusu WaJapani wako sasa?” Yule mishenari akamjibu kwa upole na utaratibu, na kwa ujasiri kabisa, kana kwamba anamchoma upanga, “Nashukuru. WaJapani wangu hawajambo, wametulia katika neema ya Mungu. Kama unazungumza juu ya wale waliopiga mabomu meli za KiMarekani, hao ni WaJapani wako – wale ambao wewe unawajibika nao, lakini hukufanya chochote juu yao. Wao ndiyo wenye kuleta matatizo yote hayo. Lakini WaJapani wangu wanaendelea vizuri tu, wakidumu katika kumtumaini Bwana Yesu Kristo”. Wapendwa – vipi kuhusu WaBrazili “wetu”, au WaZaramo, au WaFipa, au WaDigo, n.k.? Vipi kuhusu WaRundi “wetu”,
61
WaNyarwanda “wetu”, WaKongo “wetu” na kadhalika? Ndugu aitwaye Frank Laubach alisema hivi: “Kama Marekani wangetumia fedha nyingi kwa ajili ya umisheni Japani kabla ya Vita Kuu ya Pili ya Dunia kama zilizotumiwa kujenga merikebu moja ya kivita kati ya zile zilizozamishwa hapo Pearl Harbour, pengine hiyo vita isingetokea kabisa.” Je, wewe unajihusisha kwa namna yoyote katika kuigusa dunia? Je, unakwenda kama aliyetumwa ili kumfanya Kristo ajulikane? Kama hapana, ni kwa nini?
William James ambaye ni mwanasaikolojia wa Chuo Kikuu cha Harvard Marekani, aliandika juu ya nyumba aliyoishi huko Chocorua, jimboni New Hampshire akiwa mtoto mdogo. “Aah! Ni nyumba ya kupendeza sana katika nyumba ulizowahi kuona. Ina milango kumi na nne, na yote inafunguka kuelekea nje.” Ile kanuni ya usalama inayowekwa na serikali za mitaa kuhusu majengo yetu ya kanisa inazungumza mengi sana yenye hekima kwetu sisi. Mkristo, kanisa, maono yanayomshika mtu, yenye kufanya kazi na milango yote ikifunguka kuelekea nje ni kitu “cha kupendeza sana”, lakini kwa kweli, Mkristo mwenye kutazama ndani tu, na kanisa lenye kutazama ndani tu, inatakiwa liwe likiwa hai na ile hali yake ya kukata tamaa, kuchanganyikiwa, kushindwa kufanikiwa, na kushindwa kabisa!
Dunia yetu imekuwa ikipungua ukubwa kama puto ambalo halina upepo. Ndege siku hizi zinakwenda kasi kiasi cha kumwezesha mtu asafiri mapema asubuhi kutoka London hadi New
62
York. Sijawahi kusafiri nchi za ng’ambo bila ya kukutana na idadi kubwa tu ya wasafiri wenye kuzunguka dunia. Sauti inayonaswa kwa redio inasikika upande wa pili wa dunia haraka sana kuliko inavyosikika mwisho wa chumba ambapo maneno yake yanatamkwa. Tukio linalorekodiwa na televisheni huonekana nchi za mbali wakati huo huo linapotokea. Tunaishi katika chumba cha mbele cha dunia. Dunia nzima imekuwa ujirani mdogo tu. Je, tunafanya nini kuhusu jirani zetu?
[USHUHUDA WA MWANDISHI – Natazama nyuma kwenye kanisa langu la mwisho nililochunga kwa miaka kumi, na kujaribu kukumbuka njia tulizotumia ili kutengeneza maono ya dunia na mguso wa dunia kwa washirika wetu.
(1) Tulitumia mpango tuliouita “weka akiba chenji yako”. Kila mshirika alitiwa moyo kila mwisho wa kila siku kutoa chenji yote iliyokuwa imebaki mfukoni na kuitenga kwa ajili ya umisheni, ila abakize noti moja (au sarafu basi) ya kila kiwango. Mwezi Desemba, tulifanya “maandamano ya umisheni” na katika hayo tuliweka sadaka hizo zote mbele za Bwana kwamba aziongeze kwa ajili ya kufikia mwisho wa dunia.
(2) Tulitumia mpango tuliouita “Dola Moja Kwa Juma Kwa Ajili Ya Umisheni”. Tulimwomba kila mshirika atoe dola moja zaidi kwa juma kwa ajili ya umisheni wa kuifikia dunia. (Mmarekani gani ataona amepoteza kitu?)
63
(3) Tulitumia mpango wa “Kamati Ya Umisheni Inayotenda Kazi”. Tuliwachagua washirika wenye maono na roho ya umisheni, na kuwaomba “waweke dunia mbele yetu” daima. Tulitenga ibada kila baada ya miezi mitatu kwa ajili ya kukazia umisheni – na wasemaji walikuwa wamishenari (na wake zao na watoto wao), na kusoma barua za wamishenari, maombi maalum kwa ajili ya wamishenari “wetu”, na kadhalika.
(4) Tulitumia mpango wa “nyumba ya umisheni”. Tulikuwa na nyumba mbili ambazo tulizitumia kuwaweka wamishenari waliokuwa wamerudi nyumbani kupumzika na tukawaomba “wajaze” kanisa letu kwa habari walizo nazo na ushawishi walio nao.
(5) Tulitumia mpango wa “kutafiti dunia yetu”. Tuliomba taarifa za kijiografia, kisiasa, kiuchumi na kadhalika kuhusu mataifa mengi ya dunia. Sana sana tulijitahidi kujifunza kuhusu maeneo “yaliyoiva”, yaani, ambayo yanaitikia zaidi Injili.
Katika kufafanua, tulitumia hoja kama hii. Tuseme kwamba una shamba la matunda. Katika eneo A, mtenda kazi angevuna ndoo tano kwa saa. Katika eneo B, kuvuna ndoo moja kunaweza kuchukua masaa matano. Katika eneo C, hakuna cha kuvuna kwa sababu matunda bado mabichi. Kama una wafanya kazi thelathini leo, ungewatuma wapi? Nadhani ningetuma ishirini na tisa kwenda eneo A ili nisipoteze matunda pale. Halafu yule mmoja ningemtuma eneo B akafanye kinachowezekana hao, na pia kutazama eneo C. Wajibu
64
wa huyu mmoja ungekuwa kunijulisha wakati hayo maeneo mengine yameiva ili niweze kuwapanga upya wale watenda kazi. Yesu alijiita “Bwana wa Mavuno” (ktk Mathayo 9:39). Je, hajasimamia vizuri kazi Yake? Hapana kabisa, ila – kama kawaida – watenda kazi Wake hawajamsikiliza Yeye. Je, WEWE umekuwa ukimwomba Bwana wa mavuno kwamba “apelike watenda kazi katika mavuno Yake”? Kumbuka hivi: “Shamba ni dunia nzima” (ktk Mathayo 13:38).
(6) Tulitumia mpango wa “tuma mishenari”. Mimi kama mchungaji ningetoshekaje kama Mungu angekuwa hawaiti vijana kutoka kanisani kwangu au katika eneo langu la ushawishi kwenda kufanya umishenari katika vituo mbalimbali duniani? Hakika ningekuwa na mashaka na huduma yangu. Hivi karibuni tulikuwa na mgeni nyumbani kwetu ambaye amerudi kutoka Mashariki ya Mbali (katika nchi “iliyofungwa”). Karudi nyumbani kwa muda mfupi tu ili atafute misaada zaidi na kuongezea ujuzi wake wa kufundisha ili aweze kuwa “mishenari wa kawaida” (ambayo ni kichekesho maana maono ya umisheni yamemtawala kabisa!) katika hiyo nchi anayohudumia. Kiasi cha mwaka mmoja uliopita, alihusika sana na kumleta kijana mmoja kwa Kristo na kumfanya mwanafunzi, na tayari, huyo kijana amekwisha leta kumi wengine kwa Kristo – katika nchi “iliyofungwa”! Huyu “mishenari” alimaliza chuo kikuu akiwa na shahada ya ufundi umeme, kisha akarudi chuoni tena baada ya miaka minne jeshini ili kujifunza sayansi ya kompyuta kusudi aweze kupata nafasi ya kufundisha katika chuo kikuu cha nchi hiyo hiyo
65
Mashariki ya Mbali. Ninapoandika maneno haya, amerudi tena nyumbani, akiboresha taaluma yake ya kompyuta na ujuzi ili awe mwalimu bora wa chuo kikuu. Kwa nini? Kwa sababu amepata maono ya kufanya wanafunzi yenye kuigusa dunia. Aliniambia tena juu ya safari yake katika mpango wa kufanya watu kuwa wanafunzi (na jinsi anavyoshukuru) pamoja na kuambukizwa maono ya kuigusa dunia yaliyokuwepo katika kanisa nililokuwa nalichunga.
(7) Tulitumia mpango wa “kutuma wamishenari wa muda”. Sasa hivi dunia iko wazi kwa ajili ya upenyo wa umisheni wa muda wa vikundi vidogo vidogo vya watu kutoka makanisa mbalimbali ya nchi za Nje. Bado mlango wa dunia uko wazi. Mto wa kudumu wa Wakristo wanaokua, wenye furaha, waliohamasika, wenye kugusa dunia, unapaswa kuwa ukielekea kwenye maeneo mbalimbali hadi miisho ya dunia. Baadhi ya “makanisa makubwa” yanapaswa kuwa yanatuma haidhuru watu 200 hadi 500 kila mwaka kwenda kwenye miradi ya umisheni ya kuzunguka dunia. Mimi binafsi nimehusika katika safari kubwa zaidi mia moja za kimisheni huku nikiendelea na ratiba yangu nzito kabisa nyumbani. Hivi karibuni, mlei mmoja aliyekuwa anatembelea mji wetu aliniambia hivi: “Ningeogopa sana kwenda nchi yoyote nje ya Marekani”. Kuogopa? Hilo halipaswi kukaa katika akili ya Mkristo aina yoyote. Hebu jisomee 2Wakor. 11:23-33, uone ni hofu kiasi gani iliyotawala maisha ya Mtume Paulo. Cha kusikitisha ni kwamba, rafiki yangu alikuwa anakiri kushindwa kwa kanisa lake kumwingizia Agizo la Kristo.
66
(8) Tulitumia mpango wa “jifunze dini za ulimwengu”. Huu unajieleza wenyewe, na kila ilipowezekana, tulitafuta kusikia shuhuda kutoka kwa watu waliokuwa wahusika katika dini zingine, wakaokoka.
(9) Tulitumia mpango wa “onyesha umisheni”. Wakati Agizo Kuu linapolipuka katika akili ya mchungaji, kwamba ni nguvu ya Injili, hakika atawashirikisha watu wake jambo hilo katika kila nafasi. Atajifunza mahusiano ya kila itikadi kwa mpango huu. “atatoa damu” ya mkazo huo katika kila mahubiri na kila nafasi anayopata ya kutangaza Injili. Atawafanya watu wake wajue kujitolea kwa umisheni kwa waaminio wenye maono. Yeye mwenyewe atakwenda kwenye maeneo mengi ya umisheni kiasi anachoweza, na kuwachukua ndugu zake Wakristo wengi kiasi anachoweza, ili waende naye. MWISHO WA USHUHUDA]
Ewe Mkristo – je, “unaota ndoto” na “kuona maono” kuhusu kuifikia dunia? Kwa Kiyunani – “ta ethne” – makundi yote ya watu, mataifa yote – ng’ambo ya barabara na duniani kote. Je, Mungu amekuvamia kwa “Shambulizi la Ramani” – ili “ubebe” dunia nzima kwa ajili Yake? Je, unafuata mkakati wa Mwokozi, au umekubaliana na mbadala wa kijanja sana wa Shetani?
Kongamano kuhusu Kristo na kazi Yake ya ukombozi liitwalo “Summit III” lilifanyika mjini Chicago mwezi Desemba mwaka wa 1986. Dakta Ralph Winter, ambaye ni Mkurugenzi Mkuu wa Kituo cha Marekani cha Umisheni Duniani, alihudhuria.
67
Mwishoni mwa kongamano, yeye alikuwa miongoni mwa watu wawili waliotakiwa kutoa maitikio yao kuhusu kiini na mambo yaliyosemwa. Katika itikio lake, Dakta Winter alionyesha kwamba maelezo yote hayakuwa yamegusia kazi ya Wakristo na Kanisa ya kumshuhudia Kristo na kazi Yake kwa dunia. Yaani, wajibu wa waaamini kushuhudia dunia haukuwa umetajwa.
Baada ya majibu yake, mwenyekiti wa kikao ambaye naye ni Mkristo msomi maarufu na anayejulikana sana, alimtazama Dakta Winter kwa macho ya kejeli na kusema, “Sawa. Tulipaswa kujua kwamba ungetaja kitu kuhusu jambo lako unalopenda sana, ukipewa nafasi.” Swali: Je, kuigusa dunia ni jambo wanalopenda mashabiki wachache tu wenye mzigo, au linapaswa kuwa mapigo ya moyo wa kila – KILA – Mkristo? Hivi kweli tunaweza kukiri kwamba Yesu Kristo ni Bwana na wakati huo huo tupuuze wajibu pekee aliotupa sisi kama amri ya kusonga mbele? Zaidi – je, kundi lolote la Wakristo linaweza kujadili kwa usahihi au inavyotakiwa Nafsi na Kazi ya Kristo bila ya kutaja kuhusu mkazo Wake kwa dunia nzima? Ni kitu kinachotupasa sisi kutafakari maswali hayo mpaka mwisho kabisa, kwenye kupata jibu lenye kuridhisha. Ukweli ni kwamba kila Mkristo anapaswa kuwa Mkristo wa dunia nzima. Yeye anapaswa kuwajibika kuwa”ambukiza” wengine, kuombea wamishenari, maeneo ya umisheni, na Wakristo wengine, anapaswa kuivamia dunia, anapaswa kupata na kutawanya habari, na kwa njia hiyo
68
kumkaribisha Mungu aongeze maisha yake kwa ajili ya kuifikia dunia.
Rafiki zangu, dunia inawaka moto – moto wa mabadiliko, vurugu, hofu, mapinduzi, fujo, vita – mambo yanayofaa kabisa kwa ajili ya Injili. “Mapinduzi kila dakika” yanatokea. “Je, si kitu kwenu, enyi wote mnaopita tu?”
Hadithi moja maarufu sana katika kitabu cha Washington Irving kiitwacho Sketch Book ni ya mtu aliyeitwa Rip van Winkle. Huyu jamaa alilala usingizi wa miaka ishirini – ili aepukane na hali yake ya kutokuwa na faida, uzembe, pamoja na mke aliyekuwa mkorofi. Alipopata usingizi na kulala, jimbo lake la New York lilikuwa koloni la Uingereza, lililokuwa linapigania haki na uhuru wa watu kujitawala ili kupinga ukandamizaji. Lakini, “ukandamizaji mkubwa” ule haukumsumbua Rip, uliokuwa unamsumbua ni ule mdogo, wa mahali pamoja, wenye ubinafsi wa nyumbani kwake. Lakini kwa kulala mara moja tu na kwa muda mrefu, Rip alikombolewa kutoka ukandamizaji wote. Ee Mkristo, unasikiliza hilo? Hadithi hii ya Rip ni mfano uliofichika. Wachungaji wanateseka kutokana na ukandamizaji mdogo, wa mahali pamoja, na mara nyingi huingia katika usingizi uletwao na “dawa” (hakuna maono, hakuna nguvu, hakuna kuigusa dunia) kiasi kwamba wala hawana habari na ukandamizaji wa duniani, ambao ni utawala wa nguvu juu ya dunia nzima unaofanywa na Shetani (ktk 1Yohana 5:19b). Sasa, ikawaje katika hadithi? Rip akalala usingizi mzito, na
69
hakuamka mpaka baada ya miaka ishirini. Akiwa amelala, vita ya Kimapinduzi ikapiganwa. Rip alipokwenda kulala, alikuwa anatawaliwa na George wa Tatu wa Uingereza – mfalme. Alipoamka, alikuwa anaishi katika jamhuri ya kidemokrasia, na George mwingine – Jemadari George Washington – alikuwa anajiandaa kutawala. Rip Van Winkle alifunga macho yake na kulala wakati wa mapinduzi! Je, Mkristo, unasikia hilo? Mtu hawezi kujua anachokosa akiwa amelala. Ndiyo maana Shetani anataka wewe ujione mwenyewe – utazame kujisikia hatia kwako, ujali maombi yako, kusoma Biblia kwako, imani yako tu, ushuhuda wako tu, uaminifu wako tu, huduma yako tu, kanisa lako tu, dhambi zako tu, hofu zako tu – Ukristo wa kibinadamu, wenye kutafuta kujikimu. Amka ewe Mkristo, umtazame Mwokozi wako, utazame Biblia yako, utazame dunia yako, utazame nafasi na fursa ulizo nazo kupitia macho mapya kabisa!
Mbadala Wa Shetani
Turudi kwenye hoja yetu ya tatu kuhusu Agizo, katika Mathayo 28:18-20. Tumekuwa tukitazama kwa upana sana mkakati wa Mwokozi chini ya kichwa hiki: “Panua Maono Yako”. Sasa, hebu kwa kifupi tutazame mbadala anaotoa Shetani hapa. Daima Shetani anarudisha usikivu wetu kwenye mapambano yetu sisi, kujikimu kwetu, taasisi ya mahali ambapo tunatumika (na mafanikio yake), na kadhalika. Daima anatafuta kupunguza maono yetu yawe kitu cha
70
kawaida, yaendane na taasisi yetu au ubinafsi wetu, na kwa njia hiyo wingi wa watu duniani wasipate nafasi ya kusikia hata habari za Kristo na Injili. Yesu alitupa mpango wa kuigusa dunia nzima, lakini tunakubali kupokea mbadala mdogo, wenye kupotosha, na usiozaa matunda aina yoyote. Je, wewe unafuata mpango gani, mkakati wa Mwokozi ambao kwa huo, wewe – naam, WEWE – unaweza kuifikia na kuigusa dunia, au mbadala wa Shetani wenye kufanikisha punguzo linalodumu la jamii ya Kikristo na kuhakikisha kwamba mabilioni ya watu watapotea pasipo kupata habari?
4. KUWASHUHUDIA WAHUSIKA
Hoja ya nne katika Agizo Kuu ni Kuwashuhudia Wahusika. Agizo Kuu lina maneno saba ambayo ni matendo, lakini amri pekee ni “kuwafanya watu kuwa wanafunzi”. Katika fungu zima (Mathayo 28:16-20), neno tendaji pekee ni hilo – “kuwafanya watu kuwa wanafunzi”. “Uinjilisti” huu ni wa aina fulani maalum – si kupata watu “watakaokata shauri kumfuata Kristo” bali ni kupata “wanafunzi”watakaoipindua dunia.
Mkakati Wa Mwokozi
Fikiri jambo hili kwa makini sana: Kwa kuwa ni amri ya Yesu – Agizo Lake pekee kwa Kanisa Lake kwamba Lisonge Mbele – bila shaka haiwezekani kuwa mwanafunzi wa kweli kama hufanyi watu kuwa wanafunzi – kulingana na matakwa Yake na mkakati
71
Wake. Kipengele hiki cha “kufanya wanafunzi” si nyongeza kwenye mpango wa Yesu, bali ndiyo amri yenyewe. Swala si kupata “waongofu” bali ni kupata “wanafunzi”. Basi, mkakati wa Mwokozi hapa si kuokoa roho za watu tu, bali ni kufanya watu kuwa wanafunzi. Maana yake ni kwamba, kile ambacho Yesu alifanya kwa wanafunzi Wake Mwenyewe, aliwaagiza nao wakafanye kwa wengine. Walipaswa kutenda mkakati ule ule, nidhamu zile zile, na taratibu zile zile kwa wengine, ambazo Yesu Mwenyewe alikuwa amezitumia kwao. Rafiki yangu mpendwa: Hebu soma fungu hili lote polepole, kwa makini sana, na katika hali ya maombi mara kadhaa kabla ya kuendelea mbele. Tutalitazama neno ”mwanafunzi” kwa upana zaidi hapo baadaye.
Mbadala Wa Shetani
Nini mpango mbadala wa Shetani kuhusu kufanya watu kuwa wanafunzi? Sehemu moja ya mpango wake ni kuhakikisha kwamba waliopotea wanaendelea kupotea, au, kuwazuia kuokoka. Sehemu ya pili ni kuwazuia waaminio kuwa wanafunzi wenye maono ya dunia yote, na wanaotaka kuigusa dunia yote. Au basi, kama waaminio wakiwa wanafunzi, kusudi la Shetani ni kuwafanya wawe wanafunzi wa wazo lao wanalopenda tu, au utaratibu wao wanaopenda tu – mradi kitu chochote ili kuwazuia wasiwe wanafunzi wa kweli, wanaofanana na Kristo, kama inavyotakiwa na Agano Jipya.
72
5. KUWAHUSISHA WALIOSHUHUDIWA
Hoja ya tano katika Agizo Kuu ni Kuwahusisha Walioshuhudiwa. “Mkiwabatiza katika jina la Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu”.
Mkakati Wa Mwokozi
Mkakati wa Mwokozi kwa ajili ya kila aaminiye ni kujitambulisha na Yesu Kristo kwa njia yenye kudhihirisha kifo kwa kila kitu ambacho huyo mwamini aliishi kwa ajili yake kabla ya hapo, na ufufuo wenye kumaanisha kwamba sasa anamwishia Kristo tu. Kwa kubatizwa, amwaminiye Kristo anakiri kufia wakati wake uliopita – dhambi zake za zamani, ubinafsi wake wa zamani, motisha yake ya zamani, mtindo wake wa maisha wa zamani, jinsi alivyokuwa anafikiri zamani – wakati wake wote wa zamani, na anakubali kwamba sasa ana lengo na kusudi moja tu la maisha – Kusudi lenye kutawala kila kitu na kumwishia Huyo Yesu Kristo mtukufu. Ubatizo ni kuingia katika kaburi la maji, ambayo ni picha ya kuingia katika kifo cha Kristo, na kufufuka tena kutoka kaburini humo, ambayo ni picha ya kushiriki pamoja na Kristo katika kufufuka Kwake. Basi, ubatizo hudhihirisha kujiunga kikamilifu kabisa na kuhusika kikamilifu kabisa katika uanafunzi wa Kikristo. Ukweli kwamba unafanywa “katika jina la Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu” maana yake ni kwamba mwamini huyo anaingizwa katika kuhusika kikamilifu katika Mpango kamili na Nafsi ya
73
Mungu. Hakuna kitakachohifadhiwa katika maisha ya mtu kwa ajili ya makusudi yake mwenyewe. Kifo kimefutilia mbali uwezekano huo. Ufufuo umesababisha mwelekeo mwingine kabisa kwa ajili ya maisha yake. Sasa, kila rasilmali na uwezo ulioko katika nafsi yake iko kwa ajili ya Bwana Yesu Kristo.
Mbadala Wa Shetani
Katika hoja hii ya Agizo Kuu, nini mbadala anaotoa Shetani? Shetani anatafuta kusukuma mawazo ya wanadamu kwenye sehemu mbili, ambazo zote ni zaidi ya kawaida. Kwa upande mmoja, anasema ubatizo ni zoezi la kimwili, lisilofanya chochote rohoni, na ambalo ni taratibu tu. Basi, halina maana yoyote. Kwa hiyo – kwa mfano – dhehebu la Quakers halibatizi kabisa watu – kwa sababu hiyo. Kwa upande wa pili, Shetani analeta wazo kwamba ubatizo ni muhimu sana kuliko kitu chochote, na kwamba wenye dhambi hawawezi kuwa na uzima wa milele wasipobatizwa. Basi – kwa mfano – madhehebu mengi tu yanafanya ubatizo kuwa ndiyo jiwe kuu la pembeni kwa habari ya wokovu. Hapo katikati, kuna wanaoshikilia wazo dhaifu kabisa kwamba ubatizo ni “ishara tu – ni mfano” – kama makanisa mengi, pamoja na WaBaptisti.
Mwanamume mmoja alifika kazini siku moja akiwa amevimba macho na uso mzima. Mwenzake wanayefanya pamoja akamwuliza, “Vipi? Ulipatwa na nini?” Jibu likatoka, kwa sauti ndogo sana, “Mke wangu alinipiga”. Yule mwenzake akasema,
74
“Unataka kuniambia uliruhusu mwanamke tu akutendee hayo?” Jamaa alijibu hivi, “We! Mke wangu si ‘mwanamke tu’!” Wapendwa – tunaposema kwamba agizo lolote la Yesu ni “mfano tu”, si tunaunga mkono upande mbadala wa Shetani? Hakuna chochote alichowahi kusema Yesu ambacho ni “kitu tu”! Je, umeona ukubwa wa kuungana kwako na Yesu Kristo na kuhusika kwako na Yesu Kristo?
6. KUWAELIMISHA NA KUWAJENGA WALIOJIUNGA
Hoja ya sita katika Agizo Kuu ni Kuwaelimisha na Kuwajenga wote waliojiunga. “Mkiwafundisha kuyashika (kutii) yote niliyowaagiza ninyi.” Hapa tena, neno tendaji ndiyo linalotangulia. Linaonyesha shughuli inayoendelea, ya kudumu, isiyokoma, isiyokatizwa.
Mkakati Wa Mwokozi
Hakuna wakati wowote katika maisha yangu kama Mkristo ambapo siwi katika kufundisha! Iwe ni kwa mfano wa makusudi, kwa tamko la wazi, kwa kufuata mtaala ulioandaliwa, kwa ushawishi wa kimya, katika hali iliyopangwa au isiyopangwa, mimi ninapaswa kuwa mwasilishaji wa Yule ambaye ni uzima wangu. Kila aaminiye anapaswa kuwa mwalimu, awe na karama ya kufundisha au asiwe nayo. Njia za mawasiliano zilizoko leo ni nyingi mno na zenye kutenda kazi vizuri kabisa kiasi kwamba Mkristo hana udhuru wa
75
aina yoyote wa kutokufundisha. Kuna kanda za sauti ambazo zina kila aina ya mada ya Kikristo unayoweza kutaka, zilizoandaliwa na wataalamu wa mawasiliano Wakristo wanaomcha Mungu. Kuna mikanda ya video ya hali ya juu sana na yenye mada nzuri tu. Kuna maktaba kubwa sana za vitabu ambavyo vinaweza kupatikana kwa kuazima au kununua. Kuna chapisho mbalimbali zenye makala nyingi tu za mafundisho, na kadhalika. Nyumba ya kila Mkristo inapaswa kuwa ghala na kituo cha kusambaza vitu hivyo vya kufundishia. Kila Kanisa la Kikristo linapaswa kuwa kituo cha kusambaza kweli ya Injili, kwa kutumia kila mbinu iwezekanayo na kila mwanachama apatikanaye ili kupenya na kuingia katika mioyo, nyumba, jumuiya mbalimbali na kadhalika, kwa ajili ya kufikisha kweli kamili ya Injili. Kila Mkristo anapaswa kuwa makini kwa ajili ya kufanya watu kuwa wanafunzi na kufundisha jinsi ya kufanya watu kuwa wanafunzi, bila kikomo. Maono ya dunia nzima na huduma kwa dunia nzima vinapaswa kuwa mbele za kila Mkristo na kila kanisa. Nini lengo la yote hayo? Ili kila Mkristo na kila kanisa kupata moyoni mwake kile kilicho moyoni mwa Mungu – kugusa dunia nzima kwa kuwajenga na kuwasambaza Wakristo wenye maono ya dunia nzima, na watakaoigusa dunia yote.
Mbadala Wa Shetani
Shetani ana mbadala gani kwa mpango huu? Kwanza, anatafuta kuzuia mafundisho yenye upako ya kweli kuu za Biblia.
76
Halafu anatafuta kuwafanya Wakristo “waonja mahubiri”. Kwa hali hiyo, hawataathirika na Ukristo wa kweli kwa sababu wamepokea chanjo ndogo tu. Au anawafanya waaminio kuwa wachambuzi na wachuja ukweli, wakidhani kwamba wanaweza kupambanua na kutambua ukweli pasipo msaada wa Roho Mtakatifu. Basi, wanajifanya wakuu juu ya kweli na juu ya mwalimu afundishaye kweli. Neno hupokonan katika Agano Jipya, yaani “utii”, maana yake ni “kusikia chini ya,” na picha itokanayo na neno hilo ni mtu anayesikiliza kweli ya Mungu akiwa kwenye hali ya kudumu ya unyenyekevu. James M. Barrie alisema hivi: “Maisha ni somo moja refu sana, la unyenyekevu”, na ni kweli kabisa hasa katika maisha ya Kikristo. Lakini, mkakati wa Shetani ni kufutilia mbali uwezekano huu wa kusikiliza kweli kwa unyenyekevu, na basi kumfanya mwamini arudie maisha yake ya kujitawala mwenyewe, kwa kujijali mwenyewe, na kujipa umuhimu.
Mpango wa Shetani kwa ajili ya mwamini uko wazi sana kwa Mkristo msikivu na mwenye kutambua mambo. Hebu nitumie neno lenye kuonyesha mwisho au hatima ya mpango wa Shetani. Ni neno “kuning’iniza mbele ya”. Shetani anafurahi sana wakati aaminiye anapokwenda kanisani Jumapili kwa Jumapili na kuruhusu kweli ipite mbele yake bila kuifanyia chochote. Anapofanya hivyo mara ya kwanza, bila kupokea kwa unyenyekevu kweli hiyo iingie katika udongo laini wa moyo mnyenyekevu, mtii na wenye kusikia, anakuwa amepuuza kweli hiyo. Ni rahisi kuona kwamba hiyo ndiyo
77
kawaida ya mshirika wa kawaida kanisani Jumapili kwa Jumapili, juma baada ya juma, mwezi baada ya mwezi, na mwaka baada ya mwaka. Amekwisha amini kwamba kuhudhuria kanisani na kusikiliza mahubiri NDIYO maisha ya Kikristo. Jambo hilo likiendelea hadi mtu asiweze kukubaliana na ukweli wenyewe kwa unyenyekevu, kuvunjika na utii katika kuomba, Mungu huingia katika hali hiyo na kumgeuzia msikilizaji kibao. Anakuwa “mkaa kitini” asiye na uhai, asiye na nguvu, asiye na maono katika kanisa la mahali. Anaweza kuleta matatizo kwa kanisa na mchungaji wake – au asilete – kutegemeana na kiwango cha kujisikia hatia kwake juu ya jinsi alivyo. Ni hivi: Watu waliokuwa wanakwenda kanisani kila wakati na kila mara “wakaushika” ukweli ndiyo waliokuwa na hatia ya mawazo ya kurudi nyuma na hatimaye dhambi isiyosameheka. Ni wale Waandishi na Mafarisayo, watu waliokuwa bora sana na wenye kushika dini sana katika siku zao (ona Mathayo 12). Kwa hiyo, Shetani anataka sisi tuwe “Wakristo wa kwenye foleni ya chakula”, ambao daima wanatazama na kupima ukweli, wenye kuchagua na kuchukua kulingana na kweli zetu tunazopenda, na wahubiri wetu tunaowapenda na mahubiri yetu tunayopenda. Basi, hoja ya sita katika Agizo Kuu inabatilishwa kwa mkakati mbadala wa Shetani.
Ewe Mkristo – uko upande gani? Je, unafuata mkakati wa Mwokozi kwa juhudi zote za roho yako yenye unyenyekevu, au “unakanyaga na kuchafua nyua za Mungu” kama msikilizaji wa siku
78
zote ambaye hazai matunda kwa aina yoyote katika kutimiza Agizo Kuu?
7. TUMTARAJIE KUTENDA KAZI
Hoja ya saba katika Agizo Kuu ni Kumtarajia Yesu Kristo Kutenda Kazi. “Tazama, Mimi niko pamoja nanyi siku zote, hata mwisho wa dunia”. Neno “tazama” ni baada ya neno “enendeni”. Ahadi ya uwepo maalum wa Kristo katika mstari huu ni kwa wale tu ambao wanatoa na kumimina maisha yao katika shughuli zote zilizotajwa, ili kutimiza Agizo Kuu. Yaani, huwezi kudai kihalali hiyo ahadi kama hufuati huo mpango. Hatutapata nguvu ya Agano Jipya mpaka tutakapofuata taratibu za Agano Jipya. Basi, maombi yetu mengi kwamba tupewe Roho Mtakatifu na nguvu Zake yanapotea tu. Ni hivi: Tunataka hizo nguvu kwa ajili ya kitu gani? Kwa nini tunaomba tujazwe Naye? Ni ili Mungu akubaliane na mipango yetu? Au ni ili tukuze kujulikana kwetu? Au ni ili tupate kiasi fulani cha mafanikio katika juhudi zetu kwa ajili Yake? Usisahau jibu la Mungu kwa maombi ya yule mhubiri maarufu: “Mwanangu! Huhitaji nguvu Zangu kwa mipango midogo kama yako.”
Mkakati Wa Mwokozi
Nini mkakati wa Mwokozi? Kuhusika Yeye Mwenyewe Binafsi katika kila juhudi za kila mtu mwenye kufanya watu kuwa
79
wanafunzi, na kumpaka maishani mwake na katika shughuli zake kwa nguvu kuu za Roho Mtakatifu. Yesu alisema, “Na tazama, Mimi Mwenyewe (neno hilo ni la mkazo sana) niko pamoja nanyi siku zote, mpaka mwisho wa wakati.” Kila Mkristo ni mwakilishi asiyefaa, asiyeweza, asiyetosheleza, asiye na nguvu wa Yesu Kristo, kama hii ahadi haitimii. (Hiyo si ahadi tu, ni kitu halisi – ni ukweli). Lakini kila mtu anayeanza katika kila eneo la utendaji anajua jinsi ambavyo inatia moyo na kumwezesha sana wakati anapokuwepo yule mtaalamu pamoja naye. Je, Yesu alimaanisha nini aliposema, “Mimi Mwenyewe niko pamoja nanyi”? Alimaanisha kwamba Uwepo halisi wa Yesu uko pamoja na yule mwenye kufanya wengine kuwa wanafunzi. Roho Mtakatifu anaeleweka vizuri zaidi kuwa ni “Nafsi nyingine” ya Yesu. Alimaanisha kwamba Uwepo wa Yesu wa kudumu, unaokaa utakuwa pamoja na yule mwenye kufanya watu kuwa wanafunzi. Hakuna wakati, hakuna hali, hakuna mazingira ambapo mwenye kufanya wanafunzi ataishi katika kutimiza Agizo la Kristo ambapo hatakuwa na Uwepo wa Mwana wa Mungu Mfufuka, Mwenye Nguvu. Siku haitafika ambapo Bwana Yesu hatakuwepo kwa nguvu nyingi sana katika maisha ya mtakatifu Wake anayefanya watu kuwa wanafunzi. Alimaanisha kwamba mwenye kufanya watu kuwa wanafunzi anao Uwepo tendaji wa Yesu pamoja naye wakati wote. Yesu hayuko nasi kama mwenzi mkimya au asiyejulikana au asiyefanya chochote. Mstari wa mwisho wa Injili ya Marko unasema kwamba “walikwenda na kuhubiri kila
80
mahali, Bwana akitenda kazi pamoja nao, na kulithibitisha Neno kwa ishara” (ktk Marko 16:20, TLR). “Ishara” zinaweza kuwa za aina mbalimbali na za hapa na pale, lakini Uwepo wa Yesu unadumu wakati wote!
John Wesley White alisema hivi: “Ukijawa ‘enendeni takatifu’, umejazwa na ‘Roho Mtakatifu’.” Mara nyingi watu hutumia ahadi hii nje ya mantiki yake. Wakiwa katika mambo magumu, wanautumia mstari huu kusema kwamba Bwana yuko pamoja nao daima. Lakini, mstari huu si dawa kwa ajili ya nyakati ngumu. Kuna mistari mingi sana katika Maandiko, ya kutumiwa kwa kusudi hilo – si huu – isipokuwa kama wakati mgumu unatokana na kutimiza Agizo Kuu. Huu mstari ni kwa ajili mwenye kufanya wanafunzi. Yaani – kama utatamani mahali pa kumpata Yesu leo, lazima utafute mahali ambapo wanafunzi wanazaliwa. Yeye hupita kando ya makanisa mengi tu ambayo yanahubiri mahubiri (hata mahubiri mazuri sana), mahali ambapo watu wanaomba (tena maombi ya dhati kabisa), na mahali ambapo makundi yanakusanyika (na yanaweza hata kuwa makundi makubwa sana) na kwenda Zake kuthibitisha na kuweka upako juu ya mtu yeyote anayefanya wanafunzi kulingana na utaratibu Wake wa Agano Jipya.
Je, ungependa kujua Yesu atahudhuria ibada wapi Jumapili ijayo? Mtafute katika kanisa ambapo wanaandaliwa watu wenye maono ya dunia, wenye kuigusa dunia ambao nao watazalisha wengine wa aina hiyo. Kumbuka: Si “Wakristo wazuri” tu, kwa
81
sababu huo ni Ukristo wa kibinadamu. Yesu hahudhurii na kutia mafuta makanisa mengi na maisha ya waamini wengi kwa sababu moyoni mwao hawana kile kilichoko moyoni mwa Mungu, “kuwafanya watu wote kuwa wanafunzi katika mataifa yote”. Kwa upande mwingine, wakati Mungu anapoliona kanisa lenye kufanya watu kuwa wanafunzi (kuwajenga wanafunzi kwa kufuata utaratibu Wake na kwa kumtegemea Yeye Mwenyewe kikamilifu kabisa katika shughuli hii), anajihusisha kikamilifu kabisa hapo. Anaingia ndani, kulia, juu, chini na kwa kila njia anasisimka na kufurahia sana jambo hilo – na anajiunga na kanisa hilo mara moja. Naye atakutana na watu wa kanisani humo muda wote anaoweza kuwa hapo na kufurahia.
Hatuhitaji uthibitisho mkubwa zaidi wa ukuu wa Agizo kuliko kuona maneno ambayo Yesu alitanguliza na kufuatisha. “Mimi nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani.” Halafu, “Tazama, Mimi Mwenyewe niko pamoja nanyi siku zote, mpaka ukamilifu wa dahari.” “Siku zote” – za hatari au usalama, siku za kushindwa au za ushindi, za uhuru au kuzuiwa, za amani au za vita, za kupanda au za kuvuna, za kujifunza au za utendaji. Hakuna siku hata moja ambapo kweli hii haitatimia.
Wakati Fretyof Nansen, mgunduzi maarufu wa Norway aliposafiri mwaka wa 1896 kwenda kutoboa theluji iliyoko kaskazini mwa dunia ili kujifunza na kutafiti mwendo wa theluji hiyo, kila mtu alijua ameingia kwenye shughuli ngumu na hatari. Alichukua idadi
82
kubwa tu ya njiwa wenye uwezo wa kusafiri kurudi alikotoka, na kupeleka habari. Alipofika kila kituo kikubwa cha safari hiyo hatari, alimwachilia njiwa mmoja akiwa na ujumbe mguuni. Kitabu cha Bibi Nansen cha kumbukumbu nyumbani kilikuwa na maneno haya: “Nilifurahi sana kila mara nilipomwona njiwa mmojawapo akiwa ametua dirishani kwangu. Nilipomwona huyo ndege, nilijua kwamba mume wangu yu hai na ananikumbuka.” Miaka elfu mbili na zaidi iliyopita, Bwana Yesu Kristo aliyetukuzwa alimwachilia Njiwa wa Mbinguni – Roho Mtakatifu – nafsi yake Nyingine – kuja duniani Siku ile ya Pentekoste – kuachilia kwa Nguvu kamili ya Mungu kwa ajili ya utimizwaji wa Mpango wa Mungu. Tunapomtii na kuona utendaji wa Roho Wake mwenye nguvu, tunajua Yu hai na ni mzima, na anatukumbuka, na yuko pamoja nasi akitenda kazi. Ni shauku Yake na raha Yake kutenda hivyo wakati wote. Huo ndiyo mkakati Wake.
Mbadala Wa Shetani
Nini mbadala wa kijanja wa Shetani hapa? Yeye hujaribu kutupotosha ili tujenge taasisi na mambo mengine ambayo si ya maana sana, na kwa njia hiyo kuondoa utendaji wa Roho Mtakatifu pamoja nasi. Au, anajaribu kutushawishi kwamba tuko peke yetu kabisa, wala hakuna anayesikia tunapoomba. Anajaribu kutufanya tusiojua habari za Roho Mtakatifu, au kutomjali Yeye, na uwepo
83
wake na nguvu Zake, au kujishughulisha kutafuta ujuzi mbadala, wenye kuwa na msingi wake juu yetu wenyewe.
Mpendwa Mkristo – unaangukia upande gani katika hili? Agizo Kuu, au Kuacha Kukuu?
Tumelitazama Agizo ambalo linaamua wajibu au majukumu yetu. Kumbuka, ndiyo amri ya kusonga mbele pekee aliyowahi kutoa Bwana Yesu kwa Kanisa Lake. Lakini, Shetani siku zote anajaribu kuupinga huo Mpango wa Mungu kwa kuhakikisha mpango wake unatenda kazi. Popote ambapo Kanisa LINAPOTOSHWA na kuingia katika ujenzi wa taasisi, au katika kujihifadhi, au katika kufanya “Wakristo wazuri” tu, mkono wa Shetani ni wazi hapo. Kwa hali hiyo, Agizo Kuu limekuwa “Kuacha Kukuu”. Jamani – wakati haujafika turudishe Agizo Kuu mahali pake?
Nilifundisha somo hili kuhusu Agizo Kuu miaka kadhaa iliyopita, katika darasa la wenye ndoa vijana. Mwishoni mwa somo, mama mmoja kijana mwenye ndoa aliomba sala hii ambayo niliitoa kwenye kanda baadaye.
Baba! Ninashukuru kwamba kuna mtu – mwanadamu – mbinguni kwa ajili yetu wakati huu. Na kama YUPO na BADO ni mwanadamu kweli, basi bila shaka anazo hisia za kibinadamu. Anaweza kufurahia, kushukuru, kuumia na kuteseka. BILA SHAKA MOYO WAKE UNASIKITIKA anapotafuta kuendeleza kazi Yake hapa duniani, lakini anaona mwili Wake wa hapa duniani ukifuata
84
mkakati ambao ni KINYUME KABISA kwa kila hali, na ule mkakati aliowapa wanafunzi Wake.
Je, ni Agizo Kuu au ni Kuacha Kukuu? Wakati haujafika turudishe Agizo Kuu katika nafasi yake?
85
Sura Ya 3
Wazo Lenye Kuamua Njia Tutakayotumia
“Mkawafanye watu kuwa wanafunzi ….” Mathayo 28:19
Kama kweli tunataka kuwa watii kabisa kwa Yesu Kristo na kwa Agizo Lake Kuu, ni lazima tujilazamishe kuwa sahihi kabisa katika kuelewa Agizo hilo. Hatuwezi kujiruhusu starehe ya ujinga au kutokujua ipasavyo. Tunaishi kwa “kila neno litokalo kinywani mwa Mungu” na hakuna mahali popote ambapo neno hilo linatufunga kama kwa habari ya Agizo Kuu. Kwa kuwa amri pekee katika Agizo hilo ni “kuwafanya watu kuwa wanafunzi”, maswali kadhaa muhimu sana yanapaswa kuulizwa. La kwanza ni hili: Mwanafunzi ni mtu wa namna gani? La pili ni, Nini maana ya kuwafanya watu kuwa wanafunzi? Na la tatu ni hili: Tunafanyaje hilo? Siwezi kufikiri maswali mengine ambayo ni muhimu kwa ajili ya kanisa la leo. Vinginevyo, tunaendelea kufuata kwa ujinga kabisa “mbadala wa Shetani” badala ya kutii mkakati wa Mwokozi.
Tumeona jinsi ambavyo maono ni muhimu kwa ajili ya utendaji wa kiroho, na tumetazama kwa makini sana Agizo Kuu, ambalo ndilo lenye kutupa sisi wajibu wetu. Sasa, tutachunguza dhana au wazo lenye kuamua mbinu au njia tutakayotumia. Dhana ni hiyo ya kufanya watu kuwa wanafunzi. Ili tuelewe dhana hiyo kikamilifu kabisa, tunahitaji kuchunguza maneno yenye kuhusiana nayo. Baadhi yake yanapatikana na yanatumika katika Biblia, na
86
baadhi yake yanatokana na maneno yanayotumika katika Biblia na jinsi yanavyotumiwa.
KUFANYA WANAFUNZI
Dhana inayoamua njia yetu ni uanafunzi. Yesu aliamuru hivi: “Wafanyeni watu kuwa wanafunzi.” Maneno kadhaa inabidi tuyatazame vizuri sana.
MWANAFUNZI
Neno moja muhimu ni “mwanafunzi”. “Wanafunzi ni watu wanaompendeza Bwana na watu watakaoifikia dunia. Basi, kitambulisho dhahiri cha mwanafunzi ni muhimu. Kuelewa mwanafunzi ni nini na mwanafunzi anafanya nini ndiyo mambo makuu muhimu kwa ajili ya kanisa. Cha kushangaza katika kanisa ni kwamba, tunalitumia neno ‘mwanafunzi’ ovyo ovyo tu kwa uhuru, na mara nyingi pasipo kulifafanua. Hali hiyo ni sawa na kiwanda cha viatu kujaribu kutengeneza kitu bila vipimo au kufuata masharti. Kitakachotokea mwisho huko ni cha ajabu sana.” (Maneno ya Bill Hull katika kitabu kiitwacho The Disciple Making Pastor, uk. Wa 54).
Neno hili “mwanafunzi” kwa bahati mbaya sana limepunguzwa nguvu yake katika kanisa la kisasa. Inasemekana ni “mwongofu” hadi kuwa “aaminiye mwenye kukiri”. Kwa kawaida, “kufanya watu kuwa wanafunzi” hufafanuliwa kuwa ni “kuleta watu
87
kwa Kristo”. Kuleta watu kwa Kristo ni sehemu muhimu, sehemu ya kwanza, sehemu ya lazima katika kufanya watu kuwa wanafunzi, lakini ni mwanzo tu. Kama utaratibu mzima utakomea kwenye kuleta watu kwa Kristo tu, mwenye dhambi mhusika “hajaletwa” kabisa.
Katika Agano Jipya, neno lenyewe linatumiwa katika njia kadhaa za jumla, halafu kwa maana inayozidi kulengwa. Kwanza, linatumiwa kusema kuhusu msikilizaji wa kawaida tu. Wale wote waliofika kumsikiliza Yesu mwanzoni mwa huduma Yake wanaitwa “wanafunzi”. Halafu, linatumiwa kumwelezea msikilizaji aliyesadiki – mtu ambaye anakubali kwamba kile anachosikiliza ni kweli, ingawa anaweza asibadilishe maisha yake au mtindo wake wa kuishi kwa sehemu kubwa. Soma Yohana sura ya 6 kwa makini sana, ukitazama hasa mstari wa 63 hadi 66. Wale wasikilizaji wa kawaida na ambao walikuwa wamesadiki, walipokuwa bado hawajawa wafuasi halisi, walimwacha Yesu, “wasifuatane naye tena”. Ni hivi wapendwa: Kanisa leo limejaa watu ambao wanatosheleza maelezo hayo. Hawa ndiyo sehemu kubwa ya “waketi vitini” wanaojaza makanisa yetu Jumapili baada ya Jumapili, lakini ambao hawana nguvu na Mungu katika kubadilisha dunia, kwa sababu wao wenyewe hawajabadilishwa kwa undani na kwa ukweli.
Matumizi ya tatu ya neno “mwanafunzi” katika Agano Jipya yanaeleza mtu anayejifunza maisha yake yote, aliyejitolea, na anayefuata. Haya matumizi ya mwisho ndiyo anayokusudia Yesu katika Agizo Kuu, na ndiyo amri yetu ya kusonga mbele. Tunapaswa
88
kwenda kila mahali na “kuwafanya watu kuwa wanaojitolea, wanaojifunza maisha yao yote, na wafuasi wa Yesu Kristo.” Hii ndiyo maana iliyo katika neno “mwanafunzi”. Mwanafunzi ni anayeshikamana (sawa na gundi, kwa mwingine) au ni mwenye kujifunza kwa Yesu Kristo. Pima kila neno vizuri kabisa. Tumia muda kutafiti maneno hayo. Mwanafunzi ni mtu aliye katika mafunzo. Au, ni kiongozi aliye mafunzoni.
Tertuliano, mmoja kati ya viongozi wa kanisa la kwanza, aliwaita Wakristo “wanafunzi katika shule ya Mungu”. Mwanafunzi kwanza huzaliwa, kisha hutengenezwa. Anazaliwa kwa Roho wa Mungu akiwa na vifaa vyote vinavyohitajika ndani yake. Lakini, lazima ajengwe, afunzwe, afundishwe na kuelekezwa ajitolee kwa Yesu Kristo.
Waldron Scott, mtu maarufu katika kufanya wanafunzi, aliandika hivi: “Shughuli ile ya kutengeneza hali mpya za moyo, kupata utaalamu mpya, kuanzisha mahusiano mapya, kugundua, kuthubutu, kutafuta, kurekebisha, kufanya upya – yaani, kujifunza – hufanya maisha kuwa kitu cha kusisimua kama Yesu alivyoahidi. Kama hujifunzi, ni kwamba huishi. Ni rahisi tu kiasi hicho.”
Lakini, pamoja na maneno mazuri kiasi hicho kutoka kwa mtu wa hali ya juu hivyo, bado tunapaswa kuwa makini sana. Kuna kitu kinachotakiwa kuongezwa katika maneno ya Ndugu Scott, hivi: Mkazo wa huko kujifunza na kuishi unapaswa kuwa Yesu Kristo, na matokeo yanapaswa kuwa kufanana na Yesu Kristo kihalisi kabisa.
89
Mwanafunzi wa Agano Jipya amevaliwa kabisa na Yesu Kristo na mawazo yake yote ni kwa Yesu Kristo kiasi kwamba hali yake hiyo inameza kila jambo lingine dogo linalowezekana. Basi, naye anazidi kuwa kama Kristo zaidi na zaidi kihalisi kabisa – anayefundisha daima, anayehudumu daima, anayejenga maisha ya watu daima, anayerekebisha daima kila inapotakiwa, na anayekwenda duniani kote daima!
Basi, kuwa kama Kristo kihalisi si ile hali ya kuwa na tabia ya upole, ya uoga, ya kutokutaka kufanya kitu ambayo tumeiruhusu kuwepo katika kanisa la siku hizi – bila ya kufikiri. Dada Eugenia Price alikaribia kweli muhimu sana aliposema, “Dhambi kuu zaidi ya kanisa la leo ni kumfuga Yesu Kristo.” Sam Shoemaker, aliyesifiwa na Billy Graham kwamba, “Alikuwa mtu wa maana kwa kanisa kama taasisi duniani kote kuliko yeyote mwingine wa kizazi chake” aliwahi kuandika hivi: “Si kazi kubwa ya kanisa kufanya kazi nyingi, kuwa na orodha ndefu ya washirika, au kuchangisha fedha nyingi. Kazi kubwa ya kanisa ni kuwatengeneza watu wenye tabia kama Yesu Kristo – na huo si mtindo wa maisha dhaifu, wala si jinsi watu wasivyotenda. Hawa watu watakaofanana na Kristo hawawezi kuchongwa kutokana na makundi makubwa ya watu wa kawaida tu. Inabidi watengenezwe mmoja mmoja.”
Hebu fananisha makanisa yetu ya siku hizi na mikakati yake, ambayo utaratibu wake ni sawa sawa na kulipua bonge la majabali na kutazamia kupata sanamu kadhaa zilizochongwa na kusadifiwa
90
vizuri. Shoemaker aliendelea kusema hivi: “Makanisa yetu yanapaswa kupunguzwa mpaka yawe mashirika madogo yenye uwezo wa kutoa nafasi kwa wachungaji na walei kujifunza utaalamu mkuu wa kiroho wa kuwaleta wengine kwa Yesu na kuwafundisha. Inaonekana kuwa ujuzi wa dunia nzima kwamba, mtu asipoweka kazi hii kuwa ya kwanza katika maisha yake, itafukuzwa maishani mwake kabisa mwisho wa siku. Akili zetu, hisia zetu, masaa ya siku zetu – vyote hivyo vinapaswa kujawa na kundi maalum la watu wakati wote – watu ambao tunatafuta kuwavuta, watu tunaotaka kuwafundisha wachukue wajibu, watu ambao sisi wenyewe tunawahitaji kwa ajili ya kushirikiana kiroho, na kupata msaada.” Mtindo huo wa maisha ndiyo Yesu aliofuata, na unatakiwa kuigwa na sisi mpaka tuujue kabisa.
Knofel Staton aliandika vizuri kabisa, kama ifuatavyo: “Nani aliye mwanafunzi wa Yesu, na tunafanyaje ili mtu awe mwanafunzi wa Yesu? Bila ya kuwa na picha dhahiri ya malengo yetu, tutapoteza wakati tu mahali pamoja, na kutumia muda wetu na nguvu zetu, na bado hatutakuwa na wanafunzi.” Neno “mwanafunzi” linatumika mara 270 katika Injili na Kitabu cha Matendo ya Mitume. Halafu, neno hilo halitokei tena katika vitabu 22 vilivyosalia vya Agano Jipya. Kulikoni? Mbona neno hilo litoweke? Roho Mtakatifu anasema nini hapa? Katika Luka 6:40, Yesu alisema hivi: “Utaratibu ukikamilika, mwanafunzi atakuwa kama mwalimu wake”. Kwa hiyo, tutazamie maneno mengine kujitokeza yenye kuonyesha hali ya
91
kuendelea. Na kweli – Neno “Mkristo” linaanza kutumika. Neno “mtakatifu” – mtu ambaye ametengwa kimaalum kwa ajili ya kutawaliwa na Kristo – linaanza kutokea. Neno “aaminiye” – mtu ambaye ni mwamini wa kudumu na mwenye kuendelea kumwamini Yesu Kristo, kumshika Yeye na kufuata makusudi Yake katika maisha yake ya kila siku binafsi – linatumika mara nyingi na mara kwa mara.
MWENYE KUFANYA WATU KUWA WANAFUNZI
Neno kuu la pili ni neno “afanyaye wanafunzi”. Huyu ni mtu “anayewafanya watu kuwa wanafunzi”. Huyu ni mwanafunzi anayekomaa, maana mtu hawezi kuwa mwanafunzi wa Yesu huku anapuuzia amri pekee ya kusonga mbele ambayo Yesu aliitoa kwa kanisa Lake. Yaani, ni kitu kisichowezekana kuwa mwanafunzi pasipo kuwa mwenye kufanya watu kuwa wanafunzi. Afanyaye watu kuwa wanafunzi ni mwanafunzi mwenza, anayewatafuta na kuwaongoza wengine, huku wakijifunza pamoja.
KUFANYA MWANAFUNZI
Neno la tatu muhimu ni “kufanya mwanafunzi”. Amri ya Yesu kwamba “mfanye watu kuwa wanafunzi” imejaa vitu vingi sana, kutokana na mfano wa Yesu Mwenyewe, na mafundisho Yake. Hii ni harakati ya kuwajenga watu wawe wanafunzi. Christopher Adsit katika kitabu chake kiitwacho Kufanya Wanafunzi Kibinafsi
92
anafafanua jambo hilo kuwa ni “kutafuta kutimiza amri ya Agizo Kuu kwa kufanya juhudi za makusudi kuwasaidia watu waelekee kwenye ukomavu kiroho – kwa kutumia nguvu na maongozi ya Roho Mtakatifu, kutumia rasilmali za kanisa la mahali, na kutumia kikamilifu karama, vipawa na ujuzi ambao umepatikana kwa miaka na miaka.”
Kitendo cha kufanya mtu kuwa mwanafunzi hufanywa na mwingine, si na kitu fulani. Hufanywa na watu, si mipango. Hufanikishwa na watu binafsi, sio taasisi. Kimsingi, kufanya mtu kuwa mwanafunzi ni tendo la Mkristo mmoja akimgawia au kumwingizia mtu mwingine maisha yake yote, kwa njia ya mfano, uongozi na mahusiano. Ni uhamishaji maisha siku zote.
Kuna tofauti kubwa sana kati ya kuwasafisha wenye dhambi na kuwafanya watakatifu kuwa wanafunzi. Kazi nyingi za kanisa – kazi ya kichungaji, kuabudu, juhudi za kuelimishana, juhudi za kuhamasishana na kadhalika – husababisha kusafisha wenye dhambi kwa kiasi kidogo sana, na wala hakuna kiasi kikubwa cha kuwafanya watakatifu kuwa wanafunzi. Unataka uthibitisho wa hilo? Rahisi kabisa. Wakristo wengi katika makanisa mengi hawana “uzito kiroho” wa ziada kwa ajili ya Kristo kuliko ule waliokuwa nao kabla ya kuokoka!
Kusafisha wenye dhambi humfanya mwenye dhambi aokoke, halafu humwingiza katika kisanduku cha kiroho cha akiba, na anapotokea humo anatokeza kama mwanadamu mwungwana,
93
aliyefugwa na kufundishwa vizuri. Kinyume chake, kuwafanya watakatifu kuwa wanafunzi ni tendo la ujenzi mzuri wa mtu aliyeokoka ili aweze kubadilisha dunia kwa njia kubwa sana, kwa kuendeleza utaratibu huo huo.
Tofauti itaonekana katika mfano huu, ambao unalinganisha kuhubiri na kufanya watu kuwa wanafunzi. Hebu tuseme kwamba una mtu amesimama nyuma ya mstari fulani akiwa ameshikilia ndoo ya maji. Mbele ya mstari huo, kiasi cha mita 10, kuna chupa ishirini ndogo za maziwa. Kuhubiri ni sawa na kutupa maji kutoka kwenye ile ndoo nyuma ya mstari, kwa matazamio kwamba kiasi fulani cha maji kitaingia katika zile chupa. Lakini, mafanikio ya tendo hilo yanatabirika sana: si maji mengi yatakayoingai katika zile chupa. Na hata kama yataingia, yatafyonzwa upesi na jua kama hayatatumiwa kwa faida. Lakini, tendo la kufanya mtu kuwa mwanafunzi ni sawa na kwenda na ile ndoo yenye maji mpaka kwenye kila chupa na kumimina maji ndani ya chupa mpaka ijae. Ni dhahiri kwamba mafanikio makubwa yako hapo.
Au, kuhubiri ni kama kuchukua kifuniko cha chupa ya dawa na kusimama dirishani katika gorofa ya tatu, na kuimimina huko chini kwa matazamio kwamba itamwingia mtu jichoni. Lakini, kufanya watu kuwa wanafunzi ni tendo la kumkaribia mtu na kumtilia dawa moja kwa moja jichoni, mkiwa ana kwa ana.
Pasipo kuwa na kiwango maalum cha kufanya watu kuwa wanafunzi, tutagawa kweli kwa ujumla na kwa wingi na kuwahesabu
94
watu – ingawa tunaweza kuwa tunazaa watu wachache sana wenye maana. Kufanya watu kuwa wanafunzi kwa mtindo ambao Yesu aliutumia kutarekebisha tatizo hilo. Wakati wanafunzi walipomsikia Yesu akisema kwamba wanapaswa “kuwafanya watu kuwa wanafunzi”, walitakiwa kuelewa kwamba walitakiwa kuwafanya wengine kuwa kama Yesu alivyowafanya wao. Kufanya watu kuwa wanafunzi ni pamoja na kufuata utaratibu mzima wa kufanya watu kuwa wanafunzi – tangu kuongoka mpaka kufikia mtu afanyaye wengine kuwa wanafunzi, aliyefundishwa. Hicho ndicho kiini cha yale ambayo Kristo anatazamia kwa Kanisa Lake.
NIDHAMU
Neno muhimu la mwisho hapa ni “nidhamu”. Nidhamu ni maeneo katika maisha yenye kudhihirisha gharama ya uanafunzi. Hudson Taylor, mwanzilishi wa China Inland Mission na mmoja kati ya wamishenari maarufu sana wenye maono makubwa, aliandika hivi: “Mtu anaweza kuwa amewekwa wakfu, amejitoa na anamaanisha, lakini hatakuwa na thamani kubwa kama hana nidhamu.”
Je, wajibu alitooa Kristo ni wa dhati kiasi gani? Je, kanisa limeshindwa kiasi gani kutii amri moja tu ya Agizo hilo? Je, kuna ushahidi wowote halisi kuhusu kushindwa huko? Ninaamini kwamba kuna ushahidi tele na wa kudumu kabisa.
95
[USHUHUDA WA MWANDISHI – Nilikuwa katika kikao zamani na Mkristo mzee mwenye mvi, ambaye amekwenda Mbinguni kupumzika zamani. Yeye na mimi tukawa peke yetu ofisini mwake kwa muda, na hapo akaniuliza “ninafanya nini siku hizi” katika kanisa nililokuwa nachunga. Nikamwambia, “Ninafanya kila ninachojua ili kuwageuza washirika wa kanisa kuwa wanafunzi wenye maono ya dunia ambao nao wanazalisha wanafunzi wengine wenye maono ya dunia pia.” Kwa huzuni sana akanijibu, “Ndugu Hodges, sikuwa na mafanikio yoyote katika kuzalisha watakaozalisha wengine katika kanisa lolote nililochunga.” Nikauliza, “Basi, ulifanya nini?” Alijibu kwa masikitiko sana, “Niliendelea na kujitahidi kufanya kazi yote mimi mwenyewe.” Alijihukumu mwenyewe, na ilikuwa kitu cha kusikitisha sana!
Nilikuwa nimeketi katika mgahawa mmoja nikiwa na wachungaji watatu tukisubiri tuletewe chakula. Tukawa tunazungumza (kwa maelekezo yangu nadhani) kuhusu kufanya watu kuwa wanafunzi. Mchungaji mmoja mzuri tu katika kundi letu akatoa tathmini ya ukweli kuhusu historia yake ya utumishi (na alikuwa mchungaji mzuri tu na maarufu sana, mwenye kuamini Injili). Alisema hivi: “Herb, ninatazama katika makanisa yangu mawili niliyochunga kwa muda mrefu, na ninaona watu wawili tu katika kila kanisa wanaoweza kustahili kuwa aina ya watu wale unaowataja”. Hakuwa anazungumza kwa kulaumu au kwa hasira, bali kwa uchungu na huzuni tu. Inasikitisha sana, lakini ndiyo kawaida!
96
Tukijitahidi sana, tumekuwa tukizalisha “Wakristo wazuri” ambao mara nyingi maana yake ni watu wenye kujitazama sana ndani, badala ya wanafunzi na wenye kufanya wengine kuwa wanafunzi wanaogusa dunia na kuzalisha wengine. MWISHO WA USHUHUDA]
Lengo dhahiri la Yesu lilikuwa kuzaa “wanafunzi” ambao wangekuwa “wafanya wanafunzi”, wanaojihusisha katika kazi ya “kuwafanya wengine kuwa wanafunzi” katika maisha yao yote na kutekeleza zile “nidhamu” ambazo ni muhimu kwa ajili ya kutimiza kusudi hilo.
KUFANYA WANAFUNZI KUNAKOSABABISHA HUDUMA YA MAONGEZEKO
Halafu, Agano Jipya linaongeza jambo lingine muhimu kwa jukumu letu. Tunatakiwa kuhusika katika kufanya uanafunzi wenye kuzalisha huduma ya maongezeko. Ni dhahiri kwamba ilikuwa nia ya Kristo kwamba kila mwanafunzi ahusike katika huduma ya maongezeko. Nini maana ya maongezeko? Ni wakati wanaofanya watu kuwa wanafunzi wanapoanza kuzaa wanafunzi wengine wanaofanya watu kuwa wanafunzi wenye maono, na wenye kugusa dunia. Ni hivi: Mpango wa Mungu ni kuifikia dunia kwa mtindo ule ule uliotumika kuijaza – kwa kuongezeka. Katika Mwanzo 9:1 Mungu alisema, “Zaeni mkaongezeke, na kuijaza dunia”. Kuna mtu aliyesema kwamba hiyo ndiyo amri ya kwanza iliyowahi kutolewa
97
kwa mwanadamu, na ndiyo pekee aliyoitii. Agizo la Yesu la kiinjilisti ni sawa na lile la Mungu la kimwili.
Kwa nini watu wanashindwa kuongezeka kimwili?
1. Wengine hawaingii katika ndoa, au, hakuna muungano kati ya wanaume na wanawake. Basi, maongozeko hayawezi kutokea.
2. Wengine wana maradhi au matatizo katika sehemu muhimu za mwili, zinazohusiana na uzazi.
3. Wengine hawaongezeki kwa sababu hawajakomaa. Sidhani kama kuna anayefahamu wazazi wenye umri wa miaka mitatu! Viungo vya uzazi vipo, lakini havijakomaa kiasi cha kutosha kuruhusu maongezeko – au kuzaliana. Watoto hawazai.
Mapungufu hayo hayo yanahusika kwa ajili ya kushindwa kuongezeka kiroho. Mahali ambapo hakuna muungano kati ya Mkristo na Yesu Kristo kwa hali inayodumu na kuendelea, hapawezekani kuwepo na maongozeko yoyote kiroho – labda kidogo sana. Kuwepo kwa dhambi katika maisha ya mwamini pia kutazuia mkakati na mpango wa maongezeko. Pamoja na hayo, kupoa kwa Mkristo katika utoto wa kiroho kutazuia kuongezeka. Paulo alisema, “Niliwaandikia kama watoto katika Kristo”, na Wakristo watoto huko Korinto walikosa nafasi ya viwango vya kugusa dunia kwa maongezeko kiroho.
Maongezeko kiroho ni maono yaliyopangwa na Mungu kwa ajili ya kuifikia dunia yetu ya wakati huu na vizazi vyote vijavyo kwa wale tunaowaleta kwa Yesu na kuwafundisha wakati huu. Mkakati
98
wa huduma ya Yesu ulikuwa wazi: Aliwatazama makundi ya watu kupitia mtu mmoja, halafu akamjenga huyo mtu afikie makundi ya watu. Yeye alimhudumia kila mtu aliyekuwa mbele Yake – lakini aliwaita kwa ajili ya Ufalme Wake tu. Sisi tumepotosha kabisa viwango hivyo katika kujenga taasisi badala ya kuwajenga watu. Yesu alipenda kila mtu binafsi – hakika – lakini siku zote alitazama mbele kuliko wanafunzi Wake na kuwaona watu ambao wangewafikia na kuwafundisha (ona ktk Yohana 17:20).
Katika Matendo 2:41, 47 na 5:14, neno “akaliongeza” linafafanua mkakati wa Mungu kihesabu, tangu mwanzoni mwa historia ya kanisa. Lakini katika Matendo 6:1, tunasoma kwamba “idadi ya wanafunzi ikaongezeka sana, hata kundi kubwa la makuhani likajiunga na imani.” Halafu tunapofikia Matendo 9:31 tunasoma kwamba, “makanisa yakaongezeka sana.” Bila shaka, kanisa halikurudi tena kwenye majumlisho madogo madogo isipokuwa lilipotoka kwenda mstari wa mbele na kuanza tena, na hata huko lilirudi haraka sana kwenye kuongezeka.
Watu tunaolingana umri tunapokutana na mwanafunzi mwenzetu wa chuo kikuu au chuo cha Biblia ambaye hatujaonana tangu shuleni, maswali muhimu huulizwa. “Vipi, umeoa/umeolewa?” “Je, mna watoto?” “Wangapi?” “Mna wajukuu?” Na kama wahusika ni wazee kiasi, wanaulizwa, “Je, mna vitukuu?”
Tutakaposimama mbele ya Kiti cha Hukumu cha Kristo, pengine tutasikia maswali kama hayo hayo. “Je, una watoto? (Na
99
kama huna, kwa nini?)” “Watoto ni wangapi?” Halafu kipimo halisi cha ushiriki wetu katika mpango wa Yesu unaanza. “Je, una wajukuu – watu ambao wamekuwa Wakristo kwa sababu ya jinsi ulivyowajenga watoto wako mwenyewe wa kiroho?” “Na je, una vitukuu wa kiroho?” Haitaridhisha kujua kwamba tuliwahudumia watu wengi sana, na wachache tu ndiyo wakawa wazalishaji. Itatosheleza tu ikiwa tutakuwa tumetoa maisha yetu tukitafuta kuwafanya wanafunzi wetu kuwa kama Yesu alivyowafanya wa Kwake.
Ili tuwe na uhakika kwamba tunaona vizuri kiwango halisi na kuelewa udhati wa kushindwa kufuata kiwango hicho, hebu tumalizie sura hii kwa namna nzito – naam, hata ya kinyume kabisa.
Kitabu kiitwacho The Bridge Over River Kwai kinasimulia habari ya kanali Mwingereza aliyetekwa na WaJapani wakati wa Vita Kuu ya Pili ya Dunia. Katika kambi ya wafungwa wa kivita iliyokuwa katikati ya msitu mkubwa huko Burma, mamia ya wafungwa wasio na matumaini walikaa tu wakisubiri kifo. Huyo afisa Mwingereza akapata wazo la ubunifu ili kuinua hamasa na kuwapa waliotekwa sababu ya kuishi. Hapo karibu na kambi, adui walikuwa wanajenga daraja la treni. Wafungwa wakasema wao ndiyo watakaojenga. Watafanya kazi kwa ubora na kuonyesha WaJapani kitu ambacho kingefanywa na mafundi wa Kiingereza! Akijitolea na askari wake kuifanya ile kazi, yule kiongozi wa Kiingereza aliona mabadiliko katika motisha. Lengo la kujenga
100
daraja hilo likawa kitu kinachomsukuma, tena kizuri. Hatimaye, daraja likakamilika na treni ya kwanza ya KiJapani iliyokuwa imebeba vitu ikawa inavuka. Kanali huyo aliyejivunia kazi yake aliona makomandoo wa Majeshi ya Muungano wakiwa chini ya lile daraja, wakijiandaa kulibomoa. Kwa sababu ya jinsi alivyokuwa amehusika kibinafsi, alipiga kelele ya kumtaarifu yule mkuu wa Kijapani, halafu akakimbia kama mwenda wazimu kuelekea mtoni, ili kujaribu kuwazuia wale waliotaka kulilipua daraja.
Bila shaka mfano uko wazi kabisa hapo, sivyo? Makanisa mengi hukaa katika hali ya kukaribia kifo. Basi, viongozi wao wanazaa mpango mmoja baada ya mwingine, ratiba baada ya ratiba, ili kuboresha motisha na kuwapa washirika kitu cha kuwahamasisha. Yaani, wanaingia katika mikakati ya kujikimu na kujihami, ambayo ndiyo kawaida kabisa katika ujenzi wa taasisi. Kama hadithi ilivyokuwa, adui anao mpango wake, na anafurahi sana kutuingiza sisi katika “kuutimiza”. Mara nyingi tunaupokea mpango wake na kuufanyia kazi kwa bidii kabisa. Lengo la “kujenga daraja” linakuwa kitu kinachotusukuma kweli kweli. Mtu yeyote akisema kwamba huo ni mpango mbadala wa Shetani, na kwamba si mkakati wa Mwokozi, tunamgeukia kana kwamba ni adui yetu. Tumeshikwa sana na mipango hii ya kujenga taasisi mpaka tumesahau kwamba kuna vita kubwa zaidi kuliko ujenzi wa daraja. Kama watoto wadogo wanaocheza michezo ya kujifanya, tunaendelea kuishi tu bila ya kutambua kwamba tunakosa agizo halisi la Yesu.
101
[USHUHUDA WA MWANDISHI – Mwanzoni mwa mwaka wa 1991 nilikaa juma zima katika kanisa moja huko Texas, nikihubiri mikutano ya jioni kuhusu mada ambazo zinaunga mkono mkakati huu wa kufanya watu kuwa wanafunzi, na kufundisha kwenye ibada za mchana taratibu au hatua zenyewe. Mchungaji wa kanisa hili alitokana na huduma ya kanisa ambalo niliwahi kulichunga. Jioni ya mwisho, wanandoa vijana wakanijia muda mfupi kabla ya ibada kuanza, na tulipokuwa tunazungumza, yule mke akanipa barua iliyokunjwa. Sehemu ya barua hiyo ilisema hivi: “Sijui kama unafahamu au vipi, lakini, mimi ni mmoja katika wajukuu zako kiroho. Mchungaji wetu amekuwa akitufanya wanafunzi mimi na mume wangu kwa karibu miaka minne.” Halafu kukawa na sehemu ya maelezo binafsi, na sehemu nyingine ambapo alifanya kama muhtasari au marudio wa mahubiri ya kila jioni kwa juma hilo. Ndipo akaandika tena, hivi:
Asante sana kwa muda wa ziada ambao umeutumia kutufundisha juu ya uanafunzi. Japo mimi niko kama yule ndugu aliyekiri kwa machoni katika ibada ya mchana kwamba amekuwa Mkristo kwa muda mrefu, lakini hakuwahi kumfanya mtu yeyote kuwa mwanafunzi. Nimewashuhudia watu kadhaa baada ya kujifunza na kuwa na mchungaji wetu, lakini kwa sasa nina shauku ya kumpokea mwanafunzi wangu wa kwanza maishani mwangu. Juma hili limekuwa muda wa kubadilika katika maisha yangu, nami ninafurahia jinsi ambavyo wewe umemruhusu Mungu akutumie
102
kunihudumia na kunihimiza na kunihamasisha. Ninapanga – na Yesu akifanya kazi kupitia kwangu, nikufanye uwe babu-babu wa kiroho. Asante sana kwa kuja kwako! Ni mimi dada yako na mjukuu katika Kristo, (sahihi). MWISHO WA USHUHUDA]
Mambo halisi katika Agano Jipya yaliyotajwa katika hii barua yanaonyesha amri ya kusonga mbele ambayo Yesu aliitoa kwa kanisa lake. Ongezea maeneo ya kuzaa kiroho, maono ya dunia, na taratibu halisi za kuwafanya watu kuwa wanafunzi, nawe unakuwa umepiga hatua kubwa sana kuhusu kutimiza Agizo Lake.
Katika gazeti la chuo cha Biblia cha Kibaptisti toleo la mwezi Mei 1983, kulikuwa na kisa cha kusikitisha sana. Majina ya wahusika yamehifadhiwa, japo katika gazeti lenyewe yalitajwa. “Wakati wamishenari ….. walipoandika kitabu juu ya kufukuzwa kwao nchi ya Ethiopia, walilazimishwa kujiuliza ni kitu gani walichoacha nyuma. Jibu likawashtua kabisa. Walitambua kwamba walichofanya ni kumwaga mbegu tu – hawakuzipanda. Cha kushtua zaidi kikawa utambuzi wao kwamba Wakristo kila mahali walikuwa wanafanya makosa yale yale: wanabatiza makundi makubwa ya watu, lakini hawafanyi watu kuwa wanafunzi. Mishenari mmoja akasema katika ibada ya wanafunzi, ‘Hatukufanya yeyote kuwa mwanafunzi. Tumeona watu wanaokiri imani tu. Na tunao hao katika viti vya kanisa kila mahali Marekani, na duniani kote. Ni rahisi sana kubatiza watu. Ni vigumu zaidi kufanya watu kuwa wanafunzi. Mimi naona kanisa na Mungu wana mipango miwili tofauti ya utendaji.
103
Kanisa lina wasemaji na wasikilizaji, na wote hao hakuna anayetenda kile Yesu alichowaitia Wakristo kuwa. Tunahitaji kuingia katika mpango wa Mungu.”
Pengine maelezo haya yanajumlisha tatizo kana kwamba Wakristo wote wanastahili kulaumiwa, pamoja na kurahisisha ufumbuzi wa tatizo lenyewe. Hata kitabu hiki kina hatia katika eneo hilo. Lakini, kinashughulikia kushindwa kwa muhimu sana katika kanisa kwa ujumla, na kinatukumbusha juu ya mkakati mmoja tu ambao Yesu alitoa.
Ukitaka kuanza kufanya kilicho sawa, huwi umechelewa – yaani yale ambayo tumeagizwa kufanya. Mtu yeyote anaweza “kurudi mwanzo kabisa” na kuanza ule utaratibu wa kuongeza. Lakini, wengi wetu tungehitaji kujitoa wenyewe mara moja ili kuingia katika shughuli ya kujifunza maisha na huduma ya Yesu, tukiuliza hivi: “Alifanyaje na watu Wake?” na pia kujifunza mbinu za kufanya wanafunzi na kuwaongeza, kama zitolewavyo katika vitabu vingi maarufu.
Naona jeshi linalozidi kuongezeka la waongezaji wenye maono ya dunia nzima na mguso wa dunia nzima ambao historia yao yote ni kujitoa kwao kutimiza Agizo la Yesu la “kuwafanya watu kuwa wanafunzi.” Mungu awapate na kuwatuma wanajeshi hao mbele ya macho yetu
104
Sura Ya 4
Ufunguo Ulioko Mlangoni Mwa Historia Ya Kanisa
“Kitabu kile cha kwanza nalikiandika, Theofilo, katika habari ya mambo yote aliyoanza Yesu kufanya na kufundisha, hata siku ile alipochukuliwa juu, alipokuwa amekwisha kuwaagiza kwa Roho Mtakatifu wale mitume aliowachagua; wale aliowadhihirishia nafsi yake, kwa dalili nyingi, baada ya kuteswa kwake, ya kwamba yu hai, akiwatokea muda wa siku arobaini, na kuyanena mambo yaliyouhusu ufalme wa Mungu. Hata alipokuwa amekutana nao aliwaagiza wasitoke Yerusalemu, bali waingoje ahadi ya Baba, ‘Ile ambayo mlisikia habari zake kwangu; ya kwamba Yohana alibatiza kwa maji, bali ninyi mtabatizwa katika Roho Mtakatifu baada ya siku hizi chache.”
Matendo 1:1-5
Tutaanza somo hili “mlango wa mbele” wa “Matendo ya Mitume”. Historia ya Ukristo imekuwa na mjadala si mdogo kuhusu jina la kitabu hiki katika Biblia. Bila shaka unajua kwamba majina ya vitabu vya Agano Jipya hayajavuviwa. Yaliongezwa miaka mingi sana baada ya kukamilika kwa Agano Jipya. Kuna wanaoamini kwamba kinapaswa kuitwa “Matendo ya Baadhi ya Mitume,” kwa
105
sababu ni huduma za Petro, Yakobo, Yohana na Paulo tu ndiyo zinazotajwa. Wengine wanadhani kinafaa kiitwe “Matendo Ya Roho Mtakatifu” ili kukazia Mtendaji Mkuu na kuwaficha wale watendaji wadogo. Lakini, kila mmoja anabakiza neno “Matendo” katika jina la kitabu. Ona kwamba si nia, wala mipango, wala matumaini, wala matakwa, wala mafunzo, wala tafakari, wala mahubiri ya Mitume. Ni matendo ya mitume. Kama mitume wangekwamia kwenye hayo tuliyotaja hapo kabla, hata kama ni moja tu, kitabu hicho kisingeandikwa. Basi, ni maombi yangu kwa ajili yetu kwamba, tunapofungua mlango wa mbele wa kitabu chenyewe, “tukamatwe katika Matendo yenyewe”!
Tutaanzia kwenye mtazamo mpana wa mstari wa kwanza kabisa wa kitabu. “Kitabu kile cha kwanza nalikiandika, Theofilo, katika habari ya mambo yote aliyoanza Yesu kufanya na kufundisha.” Hebu niingize muhtasari wa mstari huu. Kwanza, kuna kitabu kingine kinachotajwa hapa (“kitabu kile cha kwanza”). Halafu, kuna mwanafunzi binafsi anayetambulishwa hapa (“Theofilo”) . Mwisho, kuna tamko la wazi kuhusu kusudi la kuandikwa kwa kitabu kile cha kwanza, na vivyo hivyo, tamko la kusudi kwa ajili ya kuandika kitabu hiki cha sasa.
KITABU CHA KWANZA KINACHOTAJWA
Hebu tufikiri kuhusu kitabu kile kingine kinachotajwa hapa. Hicho “kitabu kile cha kwanza” ni kipi? Tafsiri za Lugha Rahisi
106
zinakiita “maelezo ya kwanza niliyoandaa”. Hicho kitabu cha kwanza ni Injili kama ilivyoandikwa na Luka. Injili ya Luka ni mojawapo katika Injili nne katika Agano Jipya. Inazo sura 24 katika Biblia yako, na imejengwa kwenye kweli kama kumi hivi za kihistoria kuhusu Bwana Yesu Kristo. Hizo kweli ni kama ifuatavyo: Kuzaliwa Kwake na Bikira; Maisha Yake Yasiyo na Dhambi; Kubatizwa Kwake; Kujaribiwa Kwake; Kubadilika Sura Kwake; Mapambano Yake Katika Bustani ya Getsemane; Kusulubiwa na Kufa Kwake; Kuzikwa Kwake; Kufufuka Kwake; na Kupaa Kwake.
Ili ufahamu jinsi hayo ni ya ajabu, ona cha kwanza kabisa katika hizo kweli za kihistoria juu ya Yesu – kuzaliwa Kwake na bikira. Kumbuka kwamba Luka alikuwa tabibu – daktari. Si rahisi kwa madaktari kuamini uzazi wa bikira, lakini maelezo yenye kutosheleza kabisa kuhusu kuzaliwa kwa Yesu na bikira katika Biblia nzima yametolewa na Dakta Luka. Anatuambia mwenyewe katika sura ya kwanza ya Injili yake kwamba alikuwa amefanya utafiti wa habari za kihistoria kuhusu Yesu kwa ukamilifu kabisa, na kwamba aliandika alichoandika kwa msingi wa aliyopata kwenye utafiti. Hivyo basi, tunapata ushahidi mkubwa mwingine kuhusu ukweli na uhakika wa habari za Yesu Kristo.
107
LUKA ALIKUWA NANI, NA ALIINGIAJE KWENYE HABARI HII?
Hivi, Luka ni nani? Na alipataje kuingia katika hadithi ya Injili? Yeye alikuwa mtu wa Mataifa – yaani, asiyekuwa Myahudi – na jina lake linaonyesha hilo. Alikuwa tabibu aliyeitwa “Luka, tabibu mpendwa” katika Wakolosai 4:14. Wakati mwingine tunawaza kwamba kila mtu katika dunia ya siku zile alikuwa mshamba, mtu asiyekuwa na elimu, na asiyejua mengi kama tunavyojua sisi leo. Sivyo kabisa. Luka amekosolewa mara kwa mara kuhusu kuwa mwanahistoria na kuhusu kuwa tabibu, lakini yeye na vitabu alivyoandika vimevunjilia mbali nyundo nyingi sana, yaani, wakosoaji wake. Ukweli ni kwamba, katika kila hoja ya ukosoaji inayotolea, maandishi ya Luka yamesimama vizuri na kushinda barabara, kihistoria na hata kitabibu.
Vitabu chungu nzima vimeandikwa kuhusu Luka, kama mwanahistoria na kama tabibu. Kwa mfano: Dakta Hobart alichapisha kitabu kikubwa tu kinachoitwa The Medical Language of Luke, kinachokubaliana na ubora na usahihi wa lugha ya kitaalamu ya kitabibu katika vitabu vyake vyote viwili. Kama ilivyo kawaida, wakati wanasayansi wanapofanya utafiti kwa kuzingatia ukweli, hatimaye wanaifikia Biblia!
Lakini – huyo tabibu alihusikaje na uandishi wa Injili na matetezi ya Maandiko mpaka kufikia kuandika vitabu viwili ambavyo vinapatikana katika Agano Jipya letu? Hebu tuunganishe
108
historia, ufunuo na uwezo wetu wa kufikiri kwa kifupi. Paulo na Sila walifika katika eneo la Galatia wakati wa safari yake ya pili ya kitume (ktk Matendo 16:6). Walipokuwa huko, inaonekana Paulo alipata ugonjwa mbaya sana wa macho (au, ugonjwa aliokuwa nao hapo nyuma ulilipuka mpaka kufikia hali ya hatari). Alipowaandikia Wagalatia baadaye, alisema hivi: “Oneni jinsi nilivyowaandikia barua kubwa, kwa mkono wangu mwenyewe” (ktk Wagalatia 6:11, TLR). Tafsiri za Lugha Rahisi zinaeleza kwa njia nyingine. Moja inasema, “Oneni jinsi ninavyoandika herufi kubwa”. Nyingine inasema, “Mnaona hizo herufi kubwa?” Nyingine inasema, “Nimeandika kwa herufi kubwa kwa ajili yenu.” Kwa hiyo, unamwona Paulo akihangaika kuandika kwenye karatasi lake, akitengeneza ‘maherufi’ makubwa kwa sababu haoni vizuri kiasi cha kuandika kawaida.
Katika Wagalatia 4:13-15, Paulo aliwaambia hivi, “Mnajua jinsi ambavyo kwa udhaifu wa mwili wangu niliihubiri Injili kwenu mara ya kwanza. Na jaribu langu lililokuwa mwilini mwangu hamkulipuuza wala kulikataa; bali mlinipokea kama malaika wa Mungu – naam, hata kama Kristo Yesu … Kwa sababu ninawashuhudia kwamba, kama ingewezekana, mlikuwa tayari kung’oa macho yenu, ili mnipe mimi.” Ona kwamba Mungu hakumponya Paulo tatizo hili zito sana. Yeye alikuwa na kitu bora zaidi na kikubwa zaidi kuliko kumponya Mtume Wake! Alikuwa
109
anajipanga kumwita (kwa njia ya ugonjwa wa Paulo) mmoja kati ya wasemaji Wake wakuu!
Paulo na timu yake wakasonga mbele kutoka Kusini Mashariki hadi Kaskazini Magharibi katika “ukanda” wa Asia Ndogo mpaka wakafika Troa, mji wa pwani uliokuwa upande wa kaskazini wa Bahari ya Uyunani. Yawezekana alishindwa kulala usingizi vizuri, maana hapo ndipo “Paulo akapata maono usiku. Mbele yake alisimama mtu kutoka Makedonia, akamsihi akisema, ‘Njoo Makedonia, ukatusaidie’.” Hapo ndipo uinjilishaji wa Ulaya Kusini ulipoanza.
Wakati Paulo anasubiri huko Troa, alijua alihitaji kumwona tabibu. Kuna wasomi wa Biblia wanaoamini kwamba Paulo na Luka walikuwa wamefahamiana kabla, kwa sababu chuo maarufu cha utabibu siku hizo kilikuwa mjini alikozaliwa Paulo. Wengine wanapendekeza kwamba pengine Paulo aliulizia tabibu mzuri yuko wapi, na akaelekezwa kwa Luka (ambaye kwa kweli alikuwa tabibu mzuri sana – bingwa). Vyovyote ilivyotokea, ninaamini Paulo alimwona Luka ili apate matibabu ya tatizo lake.
Akiwa huko, Paulo (kama kawaida) alimshirikisha huyu tabibu Mmataifa mwenye ujuzi na akili nzuri sana habari za Kristo na Injili Yake, na “Mungu akawasha taa” ndani ya roho yake. Dakta Luka akaokoka na kuwa Mkristo. Aliaminishwa kuhusu dhambi zake na kuamua kumfuata Mwokozi. Mara ile ile Paulo alianza kumfanya mwanafunzi, lakini muda ulikuwa mfupi sana.
110
Paulo na Sila walikuwa “chini ya amri”. Walikuwa kwenye utume, na ratiba yao ilikuwa inapangwa na Roho Mtakatifu. Paulo akamwambia Luka kwa upole, “Ndugu, lazima tuondoke sasa.” Pengine Luka alijibu hivi: “Mwondoke? Mwende? Jamani, si ndiyo mmefika tu? Tena, umeniongoza kwenye jambo kuu kuliko yote niliyowahi kuyafahamu na kuyajua, ambalo ni uzima wa milele katika Yesu Kristo. Ndiyo unasema lazima mwondoke sasa? Hiyo haiwezekani!”
Lakini Paulo alipokaza juu ya jambo hilo, Luka alifikiri hali yenyewe kidogo halafu akasema, “Je Paulo, unaonaje ukipata msafiri mwingine katika timu yenu ya utume?” Bila shaka ari ya Paulo iliongezeka, lakini pengine alimjibu hivi: “Kuna uwezekano mzuri tu! Ila, itakuwaje kuhusu kazi yako ya utabibu?” Luka alijibu kwa utulivu kabisa, “Aa! Mbona hiyo si kikwazo? Kazi yangu imekaa vizuri. Itakuwa rahisi kuuza.” Ndipo Paulo akatambua kwamba Luka alikuwa amemaanisha kabisa. Pengine aliuliza hivi: “Yaani unamaanisha kwamba uko tayari kuuza kazi yako na kufuatana nasi katika safari hii, sehemu iliyiosalia? Nashindwa kuamini.” Labda Luka naye akajibu, “Lakini Paulo, unahitaji kuwa na tabibu wa kudumu sasa hivi, nami ninakuhitaji kwa kadiri unavyonihitaji na mimi. Naam – naona nitafanya hivyo!”
Je, unadhani natunga mawazo hayo? Hapana. Mpaka mstari wa 10 wa Matendo 16, maelezo ya mwanahistoria huyo (yaani, ya Luka) yanatumia neno “Wao” anapoandika kuhusu hiyo timu ya
111
kitume. Lakini unapofika Matendo 16:10 (anapozungumzia mambo ya Troa ktk mstari wa 8), maelezo yanasema, “Mara tukakusudia kwenda Makedonia” na ndiyo mwanzo wa sehemu za “tuka” katika Matendo. Luka, mwandishi wa kitabu cha Matendo, alijiunga na timu ya Paulo huko Troa!
TAFAKARI
Hebu tukatishe hadithi yetu na kuona kweli nzuri sana zinazofaa kutafakari. Ni hivi: Tendo la kufanya watu kuwa wanafunzi halielekei upande mmoja tu. Wakati Paulo anamfanya Tito kuwa mwanafunzi, Tito naye anamfariji Paulo (ktk 2Wakor. 7:5, 6). Wakati Paulo anampa kijana Timoteo hekima yake ya muda mrefu, Timotheo kijana anamhamasisha mzee Paulo. Wakati Paulo anamfanya Dakta Luka kuwa mwanafunzi katika maisha ya Kristo, Dakta Luka anampa mwanatheolojia Paulo ujuzi na utaalamu wake wa kitabibu.
Je, umewahi kujiuliza mahali Paulo kama mwanadamu alikopata mfano wake wa Kanisa kuwa ndiyo “Mwili wa Kristo” halisi? Kibinadamu, hilo hata halifai kuwa swali. Bila shaka Luka – kikawaida kabisa – angezungumza kuhusu utendaji kazi wa kushangaza sana wa mwili wa mwanadamu. Pengine angefafanua hii mashine ambayo ni mwili wa mwanadamu wakati akimtibu maradhi yake Paulo – kama ambavyo angefanya nyakati zingine pia.
112
Labda siku moja alisema hivi: “Hivi Paulo, una akili kiasi gani katika mwili wako, baada ya kichwa? Una hekima kiasi gani katika mwili wako chini ya kichwa chako? Pengine Paulo angesema, “Kweli sijawahi kufikiri sana juu yake, lakini bila shaka jibu sahihi ni kwamba, ‘sina’.” Na Luka angejibu, “uko sawa kabisa. Lakini basi, viungo vilivyoko chini ya kichwa chako vinajuaje kitu cha kufanya kama havina hekima au akili ndani yake? Jibu ni muujiza mwingine wa mwilini.”
Akaanza kumpa somo. “Ni kwamba una mfumo wa mishipa ya fahamu katika mwili wako, yenye kuunganisha viungo vya mwili na akili. Mishipa itokayo kwenye akili au ubongo hadi mwilini hupitisha amri zitokazo kwenye akili hadi kwenye viungo vya mwili, na kama viungo vyote viko katika hali nzuri kiafya, vinatii mara moja na kutuma ujumbe wa kukubali kurudi kwenye akili, unaosema, ‘Sawa. Kazi unayotaka tutaitenda.’ Unaona huu mkono wangu wa kuume ulionyooshwa? Kiganja kiko juu na vidole vimetawanyika. Na mkono utabaki hivyo hivyo mpaka niuachie ufanye kitu kingine. Kwa nini? Kwa sababu, muunganiko kati ya akili na kiungo uko timamu – afya ni nzuri na unafanya kazi.”
Muda wote huo wakati Luka anazungumza, Roho Mtakatifu anafanya kazi kwa nguvu sana katika akili ya Paulo. Ghafula anasema hivi: “Hivyo ndivyo Kanisa linavyofanya kazi pia. Sawa na jinsi ambavyo mwili wako ni chombo kwa ajili ya kujieleza, kanisa nalo ni Mwili wa Kristo, na chombo kwa ajili ya Yeye kujieleza.”
113
Na Roho Mtakatifu anaendelea kufafanua fundisho kuhusu kanisa kama mwili wa Kristo kwa Paulo mwanatheolojia, akipitia kwa Luka, mishenari tabibu wa kwanza!
Muda mrefu baadaye, huyu tabibu Mmataifa – Luka – aliyefanywa mwanafunzi kibinafsi na kwa upana sana na Paulo, mtume mkuu wa Kikristo, alikuja kuandika vitabu viwili vya ajabu sana ambavyo vinapatikana leo katika Agano letu Jipya. Iitokeaje kuwa hivyo? Na inadhihirisha nini kwetu kuhusu wajibu wa kufanya watu kuwa wanafunzi utolewao na Agizo Kuu?
Jiandae basi kupokea kweli hii kuu, ifuatayo: Ingawa Luka aliandika vitabu viwili tu kati ya vile ishirini na saba katika Agano Jipya, hivyo vitabu viwili ni kama moja ya nne (au robo) ya maelezo yote ya Agano Jipya. Viliandikwa kwa ajili ya nini? Je, Dakta Luka alikuwa na wazo lolote kwamba hivyo vitabu viwili vingekuja kupatikana katika Biblia? Au katika Agano Jipya? Hakika hapana, kwa sababu yeye hata hakujua kwamba “Agano Jipya” lingekuja kuchapishwa. Basi, kwa nini aliandika hivyo vitabu viwili vya ajabu na kushangaza sana?
114
MWANAFUNZI BINAFSI ANATAMBULISHWA
ROBO YA AGANO JIPYA ILIANDIKWA KWA MTU MMOJA!
Pili, hebu tufikiri sasa juu ya mwanafunzi binafsi ambaye aliandikia vitabu hivi viwili. Jina lake ni Theofilo. Linatushangaza sana. Kwa kweli, majina yanatushangaza.
Familia moja ilipata mtoto. Baada ya kutafuta jina kwa miezi kadhaa na kuchagua jina lenye kuvutia, walimpa jina la ajabu – “Theofilo” – baada ya kuzaliwa kwake. Rafiki yao mmoja akauliza, “Kwa nini? Mbona baada ya kuchagua jina zuri tu mlifikia uamuzi wa kumwita ‘Theofilo’?” Yule baba akajibu, “Tulimwita Theofilo kwa sababu ni mtoto mwenye sura mbaya tuliyepata kumwona!”
Jina la huyu Theofilo ni muungano wa maneno mawili katika lugha ya Kiyunani. Sehemu ya kwanza – “Theos” – maana yake “Mungu”. Sehemu ya mwisho – “philo” – maana yake “upendo”. Kwa hiyo, jina lake linaweza kumaanisha “mwenye kumpenda Mungu” au “anayependwa na Mungu”. Kwa sababu ya hiyo maana, watafsiri wengine wa Maandiko wamesema kwamba labda si jina la mtu mmoja binafsi, bali kundi la watu. Lakini si hivyo. Mpokea kitabu anaelezwa vizuri sana na Luka kwamba ni mtu binafsi, katika sura ya kwanza ya Injili ya Luka.
115
Kumbuka kwamba Injili kama ilvyoandikwa na Luka, na Kitabu cha Matendo mwandishi wake ni mmoja, mpokeaji ni mmoja, na vyote vina mada moja kimsingi.
Sasa, kweli kuu ya pili ni hii: Robo moja ya Agano Jipya iliandikwa kwa mtu mmoja tu! Hapo ndipo kwenye utaalamu wa Injili ya Kristo, tena kwa herufi kubwa kabisa! Injili ya Kristo hukuza thamani, kusudi, maana, faida, na wajibu wa kila mtu binafsi. Ukitaka kuona tumepotoka kiasi gani kwenye wazo na msukumo wa Injili ya Biblia, jiulize mwenyewe swali hili: Je, umewahi kusikia juu ya mtu yeyote hivi karibuni aliyeandika kitabu cha aina yoyote ile na kukituma kwa mtu mmoja ili amlete huyo kwa Kristo?
Siku moja yenye jua kali ambayo haina mawingu, chukua kioo cha kukuza maandishi na lundo la magazeti, uende nje ukafanye jaribio. Kunja-kunja kurasa kadhaa za magazeti. Halafu, shikilia kioo kile cha kukuza herufi juu ya hizo kurasa. Ingawa unakuza nguvu za mionzi ya jua kupitia hicho kioo, huwezi kuanzisha moto – ikiwa utasogeza kioo mara kwa mara. Lakini, ukikishikilia hicho kioo kwa utulivu na kulenga sehemu moja tu na kutoa nafasi kwa hicho kioo kukuza mionzi ile kwenye kitu kimoja, utapata nguvu za jua na kuanzisha moto. Na moto siku zote huenea kwenye kitu chochote kinachoungua! Katika hadithi yetu, Yesu ndiye jua, Luka ndicho kioo cha kukuza herufi, na Theofilo ndiye sehemu iliyolengwa. Na moto unawaka, tena, bado unaenea!
116
KWA NINI LUKA ALIANDIKA HIVYO VITABU VIWILI KWA MTU MMOJA?
Turudie swali letu la awali: Kwa nini Luka aliandika hivyo vitabu viwili kwa mtu mmoja huyu? Je, tuna jinsi ya kufahamu hilo? Ndiyo!
Nini hali ya Theofilo wakati Luka alipomwandikia Injili yake? Bila shaka alikuwa amepotea, mwenye dhambi ambaye hajaokoka. Luka anamwita “mtukufu Theofilo” (ktk Luka 1:3). Hivyo ndivyo mtu mkuu wa Kiyunani alivyokuwa anaitwa, kwa hiyo, huyu Theofilo alikuwa mtu mkuu wa Kiyunani, mwenye cheo na wadhifa mkuu. Hakuna Mkristo yeyote ambaye ameitwa hivyo katika Agano Jipya, kwa hiyo, bila shaka mtu huyu alikuwa amepotea dhambini. Pengine alikuwa amesikia Injili kiasi fulani (ktk Luka 1:4), lakini hakuwahi kusadiki. Kumbuka kwamba “Wayunani hutafuta hekima” (ktk 1Wakor. 1:22), na si wepesi kukubali wazo lionekanalo haliwezekani kwa jinsi ya kibinadamu, kama Injili (unapoisikia mara ya kwanza). Kwa hiyo, Theofilo alishtuka na kuhofu ukweli wakati alipoambiwa. Lakini Luka naye alikuwa mtu wa Mataifa (yaani, asiyekuwa Myahudi), na pia alikuwa na matatizo ya kiakili kwa habari ya Injili. Lakini, Luka akawa ameshawishika kabisa kuhusu uhakika na ukweli wa Yesu Kristo na Injili Yake, basi, akajitolea kuandika maelezo fasaha yenye utaratibu mzuri kuhusu kweli za Yesu na Injili kwa Theofilo, mtu huyo ambaye hakuwa amekubali ukweli.
117
Basi, nini kusudi la Luka kuandika? Kumleta huyu mtu mmoja kwa Kristo, apate kumwamini! Utafiti wa muda mrefu, kazi ngumu na uandishi wote huo – kwa sababu ya mtu mmoja tu – ili awe na “uhakika wa mambo hayo, ambayo alikuwa amefundishwa”. Je, Injili ya Luka ilifanikiwa katika hilo? Ndiyo! Tunajuaje? Kwa sababu katika mstari wa kwanza wa kitabu cha pili, Luka anaondoa lile jina la cheo chake na kumwita “Theofilo” tu. Basi, hii kazi kubwa ya uinjilisti ilifanikiwa kwa njia ya ajabu sana. Tabibu mmoja Myunani, mtaalamu bingwa, alifanya utafiti kuhusu Injili kwa ukamilifu kabisa na akamwandikia mkuu wa Kiyunani ili kumshawishi juu ya Yesu na kumfikisha kwa Kristo na wokovu wake. Na, ilitokea.
Basi, kwa nini Luka aliandika hii barua ya pili – Kitabu cha Matendo (sura zingine 28 katika Agano Jipya lako)?: Kama huyo mtu alifanikiwa kumwamini Kristo kutokana na barua ya kwanza, kwa nini itakiwe ya pili? Ndugu zangu: Jibu la swali hili linadhihirisha kushindwa vibaya sana kwa kanisa la siku za leo. Kusudi la Kristo linakuwa ndiyo limeanza tu wakati mtu anapo-okolewa! Nia ya Kristo ni kumhusisha kila mmoja katika wafuasi Wake – waaminio wote waliozaliwa mara ya pili – katika shughuli ya kuwafanya watu kuwa wanafunzi, wenye maono ya dunia, na wenye kuigusa dunia yote. Mpango Wake ni kwamba kila mwamini awe mzalishaji wa wazalishaji huku akidumisha mtazamo wake wa kutaka kufikia “mwisho wa nchi”. Nia Yake ni kwamba tufuate
118
mpango au mfano Wake – kuwaona watu makundi kwa njia ya mtu mmoja, na kumjenga huyo mtu mmoja ili kuwagusa makundi. Basi, Kitabu cha Matendo kiliandikwa na Dakta Luka ili kumtambulisha Theofilo – katika dhana na mwenendo – aingie katika mkakati wa kuifikia dunia wa Yesu Kristo.
Je, iliwezekana? Je, Theofilo alifanyika mwanafunzi mfanya wanafunzi, mzalishaji wa wazalishaji? Kweli hatujui, na ni vizuri zaidi kwa sababu, maana yake ni kwamba kila aaminiye anapaswa kupewa nafasi zote kwa kuhusishwa kibinafsi, kuwezeshwa kibinafsi, na kutumwa au kupelekwa kibinafsi - awe anazalisha au hazalishi. Tunao ushahidi kiasi fulani kwamba Theofilo alishikwa na amri ya kuwafanya watu kuwa wanafunzi maana, si tunasoma Kitabu cha Matendo leo? Kwa hiyo, Luka aliandika kitabu kingine cha pili, kirefu tu (sura 28 katika Biblia yako) ili kumwingizia mtu mmoja wazo na kuteka moyo wake na kumkaribisha ashiriki katika kazi kuu kuliko zote duniani.
Kama Roho Mtakatifu wa Mungu anaonyesha huku kuhusika kwa hali ya juu sana katika maisha ya watu binafsi wa Agano Jipya, wewe na mimi je, hatupaswi kuwa na kiasi kidogo cha watu binafsi ambacho tutakuwa tunamimina na kuweka maisha yetu na maono yetu kwao? Je, mimi sipaswi kuishi na ufahamu wenye kuwaka moto kuhusu Agizo Kuu, na kutafuta kila njia ya kuufafanua na kuushirikisha na makundi ya “watu waaminifu, ambao wanaweza kuwafundisha wengine pia” (ktk 2Timotheo 2:2)?
119
USHUHUDA BINAFSI (wa mwandishi)
Hebu niingize ushuhuda wangu binafsi hapa. Nikiwa na maono ambayo yamekuwa yakipanuka mara kwa mara kwa zaidi ya robo karne, nimetumia muda mwingi sana na watu binafsi wengi sana, na makundi madogo madogo mengi sana, na makundi mengi sana ya wachungaji na wamishenari, na makusanyiko ya makanisa, nikitafuta kuingiza haya ninayosema. Nimeona mafanikio makubwa sana kiasi kwamba watu ambao nimefanikiwa kuwashawishi wametapakaa katika sehemu mbalimbali kwa sasa katika dunia – wakiwaleta watu kwa Yesu na kufundisha wanafunzi. Vile vile nimeona kushindwa sana (na hata mwenyewe nimeshindwa kwa njia ambazo hakika zilimhuzunisha Roho Mtakatifu). Ninaweza kujaza kurasa nyingi sana kwa maelezo yenye kuthibitishwa kirahisi kuhusu wanafunzi ambao wamekwenda ili kuzalisha aina hii ya wanafunzi katika maeneo yao ya huduma. Wengi wao ni wachungaji (nami nimepata fursa kubwa sana ya kuwafundisha na kuwatia moyo wachungaji wengi zaidi na kuwatia moyo wale ambao wako katika huduma tayari), baadhi yao ni wamishenari katika nchi za nje nyingi tu, na wengine wengi ni “walei” wenye maono hai ya kufanya wanafunzi mahali ambapo wanakaa, wanafanya kazi na kuabudu. Ninamshukuru Mungu kwa ajili ya fursa hii ya kipekee, nami nimejizatiti zaidi leo kuliko wakati mwingine wowote kuhusika na “kuwafanya watu kuwa wanafunzi”.
120
TAMKO LA WAZI LA KUSUDI LA KUANDIKA VITABU VYAKE
YOTE AMBAYO YESU ALIANZA KUFANYA NA KUFUNDISHA
Sasa tunatazama sehemu ya mwisho ya muhtasari wetu wa Matendo 1:1 – tamko la wazi la kusudi la kuandika kitabu cha kwanza, yaani Injili ya Luka. Luka anasema kitabu hicho kinahusu “mambo yote ambayo Yesu alianza kufanya na kufundisha”. Ona maneno tendaji matatu: “alianza” “kufanya” na “kufundisha”. Maneno mawili hayo yanatupa mtazamo wa jumla wa huduma nzima ya Yesu. Yesu ndiye mtu pekee katika historia ambaye amefanya mlingano kati ya shauku ya KiMungu ya kufanya na kufundisha. Katika kila huduma nyingine, iwe ya kanisa au ya Mkristo binafsi, kumekuwepo na kutokulingana kwa maeneo hayo mawili.
Hebu fikiri kuhusu makanisa unayofahamu wewe. Mengine yamezidisha sana eneo la kufanya. Kanuni yao ya utendaji ni kama inawaambia hivi, “Okoka, halafu shughulika”. Wamekazia zaidi shughuli lakini hawana mkazo kwenye mafunzo. Wako mbele kwenye utendaji lakini wako nyuma sana kwenye kanuni na mafunzo. Mtu mmoja alinieleza kichekesho kuhusu kanisa lake mwenyewe kwa kusema hivi: “Ndugu, utagundua kwamba kanisa letu lina upana wa maili 5, na kina cha robo inchi tu”. Alimaanisha kwamba shughuli ya kukimbizana kwao inaongeza idadi ya watu
121
daima katika kanisa, lakini kwamba kina chake kiroho hakilingani na kukua kwake kiidadi.
Kwa upande mwingine, yapo makanisa ambayo yamekazia kupita kiasi jambo la kufundisha. Daima wanalishwa Neno la Mungu lakini hakuna mlingano unaofaa katika shughuli tendaji za huduma. Washirika wa makanisa hayo wanaingia kwenye “kuwa na ugumu wa moyo” ambayo ni aina fulani ya kuridhika na kujisikia kunakoweza kupelekea majigambo na hatimaye hali ya kujihesabia haki. Makanisa hayo yanakua kiasi cha kuridhisha, lakini Agizo Kuu si ajenda muhimu ndani yao. Watabishana kuhusu maana ya kidole cha tatu cha mguu wa kushoto kwenye sanamu ya Danieli, lakini hawatajali hata kidogo mabilioni ya watu ambao bado hawajafikiwa na Injili katika dunia yetu.
Yesu alikuwa na mlingano kamili kati ya kutenda na kufundisha katika huduma Yake, na kila mmoja wetu anatakiwa kutafuta hali hiyo kwa njia ya maombi katika maisha yetu na makanisa tunayohudhuria na tunayofanya huduma.
Tunafikia kwenye neno “kubwa” tendaji katika Matendo 1:1. Hilo ni neno “aliyoanza”. Injili ya Luka ilikuwa inahusiana na mambo “yote ambayo Yesu alianza kufanya na kufundisha”. Hayo matukio ya kihistoria katika maisha ya Yesu yanayotajwa mapema ni mwanzo tu! Kama ni hivyo, yaani, kama “kitabu kile cha kwanza” kilihusiana na mambo ambayo Yesu “alianza kufanya na kufundisha,” basi kitabu hiki cha sasa, yaani Kitabu cha Matendo ya
122
Mitume, kitakuwa kuhusu mambo yote ambayo Yesu anaendelea kufanya na kufundisha. Lakini hapa tunapata tatizo mara moja. Katikati ya sura ya kwanza ya Kitabu cha Matendo, huyo “mtendaji na mwalimu” – yaani Yesu, anatoweka! Sasa, aliendeleaje kufanya na kufundisha katika sura ishirini na saba na nusu zaidi kama ameondoka machoni pao?
YESU ANAFANYA NINI WAKATI HUU?
Hebu tupanue hilo swali, hivi: Yesu anafanya nini kwa wakati huu wa sasa? Anaendelea kufanya na kufundisha kwa kiwango cha nia na kusudi Lake katika dunia yetu siku hizi, kama alivyofanya tu wakati akiwa hapa siku za mwili Wake. Lakini, sasa anafanya vipi na huku haonekani? Anafanya kwa njia ile ile aliyofuata wakati akiwa hapa katika mwili Wake wa kibinadamu. Je, mbinu hiyo ilikuwa ipi? Tunaiita “kufanyika mwili” ambayo maana yake ni kwamba “Neno (logos, ‘wazo la Mungu’) alifanyika mwili, akakaa katikati yetu”. Kwa hiyo, Mungu alishuka mpaka kiwango chetu kama binadamu katika Nafsi ya Mwana Wake mpendwa, Yesu, na akaishi, akatenda na kufundisha miongoni mwa watu. Je, siku hizi anatumia mtindo gani? Huo huo kama wakati ule, ila, kuna marekebisho kidogo, kama ifuatavyo:
1. Anakaa katika miili ya waaminio wote waliozaliwa mara ya pili, kwa kusudi la kuendeleza utendaji Wake na kufundisha Kwake kupitia kwao;
123
2. Tofauti na Yesu ni kwamba, kila mmoja wao (yaani sisi) ni mwenye dhambi;
3. Kuna tofauti katika sifa kwa maana ya kwamba hakuna yeyote kati yetu ambaye ni Yesu. Yeye ni Mwana wa Mungu wa kipekee, mmoja tu.
Kwa marekebisho hayo kidogo, kila aaminiye anatakiwa kuwa nyongeza ya Yesu Kristo kufanyika mwili! Mara tu mwenye dhambi anapookolewa, Yesu Kristo huingia ndani kabisa ya maisha ya mtu huyo kwa Uwepo na nguvu za Roho Mtakatifu. Roho Mtakatifu ameelezwa kama “Nafsi Nyingine Ya Yesu” na anaweza kueleweka kwa urahisi tu kwamba ni Yesu pasipo mwili”. Basi, kila aaminiye ni kasha lililo hai la Uwepo Binafsi wa Mwana wa Mungu, na kusudi la msingi kwa ajili ya hilo ni ili huyo aaminiye awe mwendelezo wa kudumu wa utendaji na mafundisho ya Yesu.
JE, YESU ALITUMIA WATU AINA GANI?
Hii inasabisha swali lingine, tena la muhimu sana. Je, Yesu alitumia watu wa aina gani katika Kitabu cha Matendo, ili kuendeleza utendaji na mafundisho Yake baada ya kupaa Kwake? Cha kufurahisha ni kwamba, katika ile mistari ya kwanza ya Kitabu cha Matendo tunapata jibu kamili la swali hilo. Mistari hiyo inatupa picha nzuri tu ya wafuasi wa kwanza wa Kristo. Hebu tuchore picha zao.
124
1. WATU WA KAWAIDA
Cha kwanza ni kwamba, walikuwa watu wa kawaida. Tunahitaji kukumbuka tu yote tuyajuayo juu yao kutoka katika Injili kuona ukweli huo. Walikuwa ni mchanganyiko kutoka katika jamii, watu wa kawaida kabisa. Wote isipokuwa mtu mmoja walitoka Galilaya, na huyo mmoja alikuwa “yai bovu” – Yuda Iskariote. Galilaya lilikuwa jimbo dogo lililodharauliwa sana katika Dola ya Kirumi, na watu kumi na moja wa kwanza kabisa waliomfuata Yesu walitoka huko. Walikuwa kundi la watu ambao “si chochote wala lolote”, lakini akawatengeneza mpaka wakawa mashujaa Wake. Hili linapaswa kumfanya kila mmoja wetu ajisikie vizuri sana kwa sababu Yesu Kristo hahitaji kitu chochote kwetu kwa ajili ya kufanikisha kusudi Lake kupitia kwetu isipokuwa kujitoa kwetu – sisi ambao ni udongo wa kawaida tu.
2. WATU WALIOCHAGULIWA
Kinachofuata ni kwamba, walikuwa watu waliochaguliwaa. Tazama mstari wa 2 wa Matendo sura ya kwanza. Watu Wake wa kwanza wanaitwa “Mitume aliokuwa amewachagua”. Walichaguliwa kwa ajili gani? Neno “mitume” linatupa kuona mambo makubwa sana. Neno “mtume” linamaanisha “mtu aliyetumwa”. Aliwachagua ili awatume popote alipotaka waende ili waweze kuwa, waseme na kufanya chochote alichokitaka! Na hii ndiyo sababu alikuchagua wewe na mimi! Ona lile neno “aliowachagua” mwishoni mwa mstari
125
wa pili. Kila neno tendaji la Kiyunani hutumika katika sauti tatu: sauti ya kutenda, kutofanya chochote, na sauti ya katikati. Katika sauti tendaji, mhusika hutenda, kama vile “Ninakimbia,” “ninasimama,” “unatembea”, “unazungumza”. Katika kila tukio, mada hutenda. Kutofanya chochote maana yake ni kwamba mhusika hutendewa. Kwa mfano, “Nilikanyagwa!” Sauti ya katikati huunganisha zile zingine mbili kiasi kwamba mhusika hutenda, lakini kwa njia ambayo matokeo ya tendo humrudia yeye.
Sasa hili neno tendaji “waliochaguliwa” ni la sauti ya katikati na hutupa kweli moja ya muhimu na ya kushangaza sana. Maana yake ni kwamba, wakati Mungu alipokuchagua wewe, alikuchagua, si kwa sababu ya wewe kufaidika – yaani upate afya, mali na furaha, bali alikuchagua kwa ajili Yake Mwenyewe! Wewe ni Mkristo kwa ajili ya Kristo! Uko hai kwa ajili Yake! Basi, wewe si Mkristo ili mahitaji yako yatoshelezwe, au ili ujitosheleze mwenyewe na kujiridhisha, bali ili utumiwe na kutumwa na Yesu Kristo kama mwendelezaji wa utendaji Wake na kufundisha Kwake.
Nilipokuwa mvulana mdogo, baba yangu alinifundisha kupenda mchezo wa kandanda. Kujua kwangu mchezo huo kulitoka kwa baba, na ushindani wangu katika mchezo huo ulitoka kwa mama yangu. Watoto wa pale mtaani walikuwa wanacheza kandanda mara nyingi siku za Jumamosi katika sehemu iliyokuwa wazi kando ya nyumba yetu. Nakumbuka jinsi nilivyokuwa nawakasirikia wakuu wa timu kwa sababu, juma baada ya juma sikuwa nachaguliwa kuingia
126
kwenye timu, na kwa sababu hiyo, sikupata kucheza. Lakini pia nakumbuka siku ya kwanza nilipochaguliwa kucheza. Hawakuwepo wachezaji wa kutosha, ndipo mimi nikachaguliwa! Sikuhitaji muda mrefu kutambua kwamba yule kiongozi wa timu hakunichagua kwa sababu alinipenda. Yeye alinichagua kwa sababu alifikiri kunichagua kungemsaidia ashinde mchezo.
Sijui kama mfano huo unaeleweka. Yesu Kristo ananipenda, na hakuna ninachoweza kufanya kitakachomfanya aache kunipenda! Hanipendi kwa kuwa ninapendeka, au ni mzuri, au nina upendo. Ananipenda kwa sababu Yeye ni upendo – basi! Lakini, hakunichagua kwa sababu alinipenda tu, pamoja na kwamba upendo Wake ni mkubwa kama ulivyo. Alinichagua (pia) kwa sababu alijisikia kwamba kunichagua mimi kungesaidia upande Wake kushinda mchezo! Sasa je, kushiriki kwangu katika utume Wake wa dunia nzima kunaweza kumfanya aone kwamba uchaguzi Wake “ulistahili”? Au je, mimi “nimetulia huko Sayuni” tu, bila ya kufanya chochote kuhusu kusudi la Kristo la dunia nzima?
Kila Mkristo asomaye maneno haya anapaswa atulie hapa na kujiambia hivi: “Nimechaguliwa na Mfalme wa Wafalme wote! Nimechaguliwa na Bwana wa utukufu! Je, ninatimiza kusudi Lake la kunichagua?”
127
3. WATU WALIOSADIKI
Halafu, walikuwa watu waliosadiki. Tunasoma hivi katika Matendo 1:3, “Yesu Mwenyewe alijidhihirisha kwao akiwa hai baada ya kufa Kwake kwa uthibitisho mwingi sana (yaani, ushahidi usioweza kupingwa), akionekana nao kwa muda wa siku arobaini.” Ndiyo maana baadaye, mmoja wao alikuja kuandika hivi, “Tumeliona Neno la Uzima sisi wenyewe, kwa macho yetu” (ktk 1Yohana 1:1, TLR).
Vile vile kuna kipengele kingine cha haya maneno machache tu kutoka Matendo 1:3 ambacho kinahitaji kutazamwa kwa makini. Kinatokana na neno la Kiyunani “dia” ambalo maana yake “kati ya”. Yesu “alionekana nao kati ya siku arobaini”. Hee! Mbona ni neno la ajabu hilo! Nini maana yake? Maana yake ni kwamba kuonekana Kwake na wanafunzi hakukuwa moja kwa moja katika siku zote arobaini. Alionekana na kutoweka kama alivyopenda Mwenyewe kwa hizo siku arobaini. Alitokea akaonekana, halafu akatoweka asionekane, kama alivyopenda mwenyewe katika kipindi hicho cha siku arobaini.
Hebu tuseme kwamba mimi na rafiki yangu tuko katika mazungumzo mazito. Katika hali hiyo tunatazama vizuri. Lakini ghafula, mwili mwingine unatokea katikati yetu! Wee! Kitu cha aina hiyo kinashtua sana! Ndiyo maana ilikuwa kawaida kwa Yesu kuanza mawasiliano Yake kwa maneno haya, “Msiogope” au “amani iwe kwenu”. Sasa, mimi na rafiki yangu tunasahau kabisa
128
mazungumzo yetu na kushikwa kabisa na huyu mtu “aliyeingilia kati”. Na hebu tuseme kwamba, tukiwa tumemkazia macho kiasi hicho, mara tena anatoweka! Hayo ndiyo yaliyotokea mara kwa mara katika kipindi cha siku zile arobaini baada ya kufufuka Kwake. Yesu alitokeza na kutoweka tena na tena katika kipindi hicho.
Kitu cha ajabu hicho! Kwa nini alifanya hivyo? Alikuwa anataka wanafunzi Wake wajue bila ya mashaka wala maswali kwamba, awe anaonekana au haonekani, alikuwa pamoja nao wakati wote! Na ni kweli hata siku hizi. Yesu Kristo yupo sana katika Nafsi ya Roho Mtakatifu, kiasi kwamba anaweza kutokea katika umbo la mwili – akitaka kufanya hivyo. Lakini kusudi Lake alilotamka ni kwamba kila aaminiye ampe Yeye “mwili” kwa kuutoa mwili wake kuwa “hekalu”, kuwa “Patakatifu pa Patakatifu”, kuwa mahali teule kwa ajili ya Yesu kujionyesha Mwenyewe.
Unaonaje? Si ungesadiki kabisa kama ungemwona Yesu kama wao walivyomwona? Kuwa mwangalifu sana hapo. Yesu Mwenyewe alionyesha kwamba, kwa sababu ya Uwepo wa Roho Mtakatifu, sisi ndiyo wenye faida, wala si wale waaminio wa kwanza (ktk Yohana 16:7).
Swali: Wewe unasadiki kiasi gani kuhusu uhalisi wa Yesu? Kuhusu uhalali wa madai Yake? Kuhusu ukweli wa nafsi Yake? Kuhusu uwezo alio nao na mamlaka Yake? Kuhusu kusudi Lake la utume duniani kote? Hakuna kazi kubwa ya Mungu iliyowahi
129
kufanyika kupitia watu wasiosadiki. Mungu na afungue macho yetu kwa upya na kwa ukamilifu kuhusu Nafsi na kusudi la Yesu.
4. WATU WALIOPEWA AMRI
Kisha, walikuwa watu walioamrishwa. Matendo 1:2 inasema kwamba, “Yesu kwa njia ya Roho Mtakatifu aliwapa amri”. Mstari wa 4 unaongezea yafuatayo: “Baada ya kukutanika nao, Yesu aliwaamuru kwamba wasiondoke Yerusalemu, bali waingojee ahadi ya Baba, ambayo, kama alivyowaambia, ‘Mmeisikia kutoka kwangu’.” Hiyo “ahadi ya Baba” ni Siku ya Pentekoste, siku ambapo nguvu za ukombozi kamili za Roho Mtakatifu zilitolewa, siku ambayo ingefuata muda si mrefu baada ya hapo.
Je, unaweza kufikiri kidogo mawazo ya mtu kama Simoni Petro, mtu asiyetulia, asiye na subira kwa wakati huyo? Pengine alisema hivi: “Yesu! Mbona huamui unachotaka? Umetumia miaka mitatu kutuandaa twende, na sasa unatuambia tungoje!” Lakini, hakuna hoja kama hiyo iliyotolewa. Kufikia wakati huu, Mitume walikuwa wamekwisha jifunza kwamba Yesu si wa kubishana Naye. Maana, Yeye ambaye ni Bwana Mkuu wa ulimwengu wote, yuko sahihi wakati wote! Kanisa la leo lipate hekima kama hiyo! Linatakiwa kutumia muda wake mwingi katika kuomba na kuchunguza Biblia ili lisadiki kwamba linatenda kulingana na Akili ya Kristo, halafu litumie muda wake mwingi kumtii Yeye!
130
Waarabu wa kale walikuwa wanazalisha aina maalum sana ya farasi, na wakati mwingine walikuwa wanaitwa “farasi wa KiArabu”. Hapo kwanza walikuwa wanazalishwa kwa ajili ya kupandwa na wafalme tu. Sasa – kama sehemu ya mafunzo yao, mfundishaji alikuwa anabeba firimbi na kamba ya ngozi kwenye shingo yake. Kwa muda wa miezi mingi sana, farasi alikuwa anafundishwa kuacha kufanya kila kitu akisikia firimbi ya mwalimu. Alitakiwa kumwelekea yeye. Ilikuwa lazima kutii kikamilifu. Kukataa kidogo tu kulihesabiwa ni kutokutii kabisa. Ndipo kwa muda wa siku tano farasi angenyimwa chakula, na kwa siku tatu angenyimwa maji ya kunywa. Katika kipindi hicho cha kumalizia mafunzo, alikuwa anafungiwa katika zizi.
Siku ya mwisho, vyombo vyenye chakula na maji viliwekwa mahali panapoonekana, kiasi cha mita kama hamsini hivi kutoka zizini. Farasi angejitahidi kukifikia chakula na maji, kwa sababu ya kuwa na njaa. Halafu ghafula, mlango wa zizi ungefunguliwa, na yule farasi aliyeshangaa angeanza kuelekea kwenye vyombo vyenye chakula na maji. Lakini akiwa anakaribia kufika, mwalimu aliyesimama pembeni angepuliza filimbi! Farasi yule angechanganyikiwa. Ilibidi afanye uchaguzi kwa haraka. Wa aina gani? Je, aende kwenye vyakula na maji, au amfuate mwalimu? Kama farasi angeendelea kwenda kwenye vyombo na kutosheleza njaa yake na kiu yake, na kwa kufanya hivyo awe amekataa kumtii mwalimu, basi angeanza upya mafunzo, au angetolewa katika
131
utaratibu huo wa mafunzo. Kama farasi huyo angechagua kinyume cha hisia na kujisikia kwake na kumtii mwalimu na kufuata utaratibu wa mafunzo kwa kumwendea mwalimu kwanza, basi aliruhusiwa kwenda kunywa maji na kula chakula kilichokuwepo.
Wapendwa: Kila siku sisi tunakabiliwa na uchaguzi kama huo. Tutachagua nini – vyombo vya chakula, yaani kujitosheleza, au amri za Mwalimu. Hao walikuwa watu walioamrishwa, na Yesu anatazamia na sisi tufanye hivyo hivyo kama wao.
5. WATU WALIOTAWALIWA
Hatimaye, walikuwa watu waliotawaliwa. Katika mstari wa 4, Yesu alisema nao kuhusu “ahadi ya Baba” iliyokuwa inahusu ujio wa Roho Mtakatifu kwa ajili ya kuliwezesha Kanisa Lake Siku ile ya Pentekoste.
Katika mstari wa 5 alisema hivi, “Mtabatizwa katika Roho Mtakatifu siku si nyingi zijazo”. Tulisema Roho Mtakatifu ni kama “Yesu asiye na mwili”. Basi, atafanya mambo yale yale, atafuata makusudi yale yale na kujenga watu aina ile ile ambayo Yesu alijenga, alipokuwa hapa katika mwili. Kama Yesu alitoa watu wasio na mwelekeo na wasiosikia la mtu, basi na Roho Mtakatifu atatoa watu aina hiyo hiyo. Lakini, Yesu hakutoa watu wa namna hiyo. Alitoa watu waliokuwa wameandaliwa vizuri kitaaluma, wenye ujuzi, na wenye kuhusika. Walikuwa watu ambao wangeweza kumwakilisha Yeye katika hali yoyote. Walikuwa watu
132
walioshughulikia mambo yote kuhusu Neno la Mungu na kulifanyia kazi vizuri kabisa katika kila hali.
Na sasa, tangu Siku ya Pentekoste, Roho Mtakatifu ni “Rafiki Anayekaa Nasi” aliyeko kila wakati na aliye tayari kutawala na kututia nguvu kwa ajili ya Utume wa Bwana wetu. Je, umejazwa na huyo Roho Mtakatifu aliye mkuu na mpole? Je, unatawaliwa na Yeye kwa ndani ili aweze kuamua tabia yako, mwenendo wako, na ratiba utakayofuata maishani – au unayofuata maishani?
133
Sura Ya 5
Vinavyotakiwa Ili Kufanya Wanafunzi
Au
Dawa Ya Daktari Kutibu Tatizo La Kuacha Agizo Kuu
“Kwa kuwa watu wengi wametia mikono kutunga kwa taratibu habari za mambo yale yaliyotimizwa katikati yetu, kama walivyotuhadithia wale waliokuwa mashahidi wenye kuyaona, na watumishi wa lile Neno tokea mwanzo, nimeona vema mimi nami, kwa kuwa nimejitafutia usahihi wa mambo hayo yote tangu mwanzo, kukuandikia kwa taratibu, Theofilo mtukufu, upate kujua hakika ya mambo yale uliyofundishwa.”
Luka 1:1-4
“Maana (kama inavyojulikana vizuri tu) wengi wamechukua jukumu la kupanga kwa utaratibu na kuandika maelezo (kamili) ya matendo yaliyothibitika na kutimizwa kwetu na katikati yetu, kama tulivyosimuliwa moja kwa moja na wale ambao tangu kuanza (rasmi kwa huduma ya Yesu) walikuwa mashahidi waliojionea kwa macho yao wenyewe na wahudumu wa lile Neno (yaani, fundisho kuhusu kupatikana kwa wokovu katika ufalme wa Mungu kwa njia ya Kristo)
134
. Nilipoona kwamba ni vizuri na kitu cha kutamanika kwangu pia (nimekusudia), na baada ya kufanya uchunguzi kwa bidii na kufuatilia mambo yote kwa ukaribu na kwa usahihi, kuanzia mwanzo kabisa, yale mambo makubwa hadi madogo kabisa, kukuandikia maelezo yenye kufuata utaratibu mzuri, Ewe Theofilo mheshimiwa, (kusudi langu ni) ili upate kujua kweli kamili, na kuelewa kwa uhakika na kwa usalama dhidi ya makosa maelezo (au historia) na itikadi za imani ile ambayo ulijulishwa, na ambayo ulifundishwa kwa kuelezwa tu.”
Tafsiri Ya Biblia Fafanuzi
“Kwa kuwa waandishi wengi wamechukua jukumu la kuandika masimulizi kuhusu kweli ambazo zilithibitishwa miongoni mwetu, kama ambavyo mashahidi walioona mambo hayo ambao walikuja kuwa wahudumu wa ujumbe huo walivyotuambia, mimi nami, Ee mheshimiwa Theofilo, kwa kuwa nimechunguza yote kwa makini sana tangu mwanzo, nimejisikia niyaandike kwa mfululizo mzuri kwa ajili yako, ili uweze kujua vizuri uhakika wa mambo hayo uliyofundishwa.”
Tafsiri ya Biblia ya Williams
135
“Mwandishi, kwa Theofilo:- Waandishi wengi wamejitahidi kuandika maelezo ya matukio yaliyotokea miongoni mwetu, wakifuata mapokeo tuliyopewa na wale walioyaona kwa macho yao wenyewe na watumishi wa Injili. Basi na mimi kwa zamu yangu, Ee Mheshimiwa, kama mtu aliyepitia kwa makini sana mambo hayo yote, nimeamua kuandika simulizi lenye umoja kwa ajili yako, illi nikupe maarifa hakika kuhusu mambo ambayo umeambiwa.”
Tafsiri Ya Biblia Mpya Ya Kiingereza
Katika Zaburi 119:18 kuna sala hii: “Fungua macho yangu Ee Bwana, nipate kuona mambo ya ajabu yaliyo katika sheria Yako”. Hebu nikushauri wewe pia uombe sala hii daima unaposoma na kujifunza sura hii. Halafu, tunasoma hivi katika Zaburi 119:130, “Neno Lako linapoingia, linaleta mwanga; linatoa ufahamu kwa asiyekuwa na ufahamu.” Na iwe hivyo tunapojifunza kwa pamoja.
Basi tuanze mafunzo yetu kwa kutazama kwa makini sana mtiririko ulioko kwenye mchoro huu:
NENO  MWILI  NENO  MWILI  NENO  (weka jina lako hapa)  NENO  MWILI.
136
Mtiririko huu unawakilisha jinsi ambavyo Injili huenea miongoni mwa watu katika historia ya Ukristo (ktk Warumi 10:14). Unaanzia kwa “Neno” – “Logos” – kufanyika mwili na kukaa katikati ya wanadamu (ktk Yohana 1:14). Baada ya hapo, kila kuenea (au kusonga mbele) ni mtindo ule ule ambao umerekebishwa kidogo, yaani, Neno kufanyika mwili. Katika muda muafaka, kwa muujiza wa neema ya Mungu na uwezo Wake, wokovu Wake “ulifanyika mwili” ndani yako. Hapo, jina lako likaingia katika mtiririko kama ilivyoonyeshwa hapo juu – na mwelekeo wako wa maisha pamoja na kazi vikabadilika milele. Sasa, swali muhimu sana: Kwa kuwa jina lako limeingizwa katika mtiririko huo, je, mtiririko utaendelea kupitia kwako? Au kiunganisho hicho kitakatikia kwako utakapokufa? Je, mtiririko unaweza kuwa kama ifuatavyo? MWILI  NENO  MWILI  …? Je, mtiririko uliokusudiwa kuendelea utakomea kwako?
Hebu kabiliana na hilo swali kwa mara nyingine tena: Je, mtirtiriko utaendelea katika historia kutokana na nafasi au sehemu yako uliyofanya wakati ukiwa hai? Ili mtiririko uendelee na wewe, kuna kazi ambayo lazima ujifunze, nayo imekwisha fafanuliwa na kupangwa kwa ajili yako vizuri sana katika Neno la Mungu. Kama utakachofanya ni kumleta mtu kwa Kristo tu, kiunganisho kinaweza kukatikia kwa huyo mtu utakayemleta kwa Kristo. Kama utamleta mtu kwa Kristo na kumfundisha pasipo kufahamu kikamilifu na kutekeleza kile “kiwango” (cha kufanya wanafunzi wenye maono ya
137
dunia, mguso wa dunia, na wenye kujiongeza), huenda huo mtiririko ukakatikia kwa huyo utakayemleta kwa Kristo na kumfundisha. Ukweli ni kwamba, utamfanya kuwa “Mkristo bora” tu. Ni pale unapomleta mtu kwa Kristo na kumfundisha kulingana na kiwango kilichofunuliwa katika Biblia ndipo Mungu atakapohakikisha kwamba mtiririko ule hautakatika, na wewe mwenyewe utahakiksha kuendelea kwake kwa kuweka msingi kwa ajili ya vizazi vingi vya baadaye.
Injili ya Luka, iliyoandikwa na mtu pekee ambaye hakuwa Myahudi, ni kitabu kikubwa sana chenye kujaa shughuli ya kufanya wanafunzi watakaofikia dunia nzima. Kufanya wanafunzi wenye maono na watakaofikia dunia nzima ndicho kiwango cha kuendelea mbele kwa Injili katika Agano Jipya. Kumbuka kwamba Luka hakuwa mtume, hakuwa mhubiri, hakuwa mwinjilisti, wala hakuwa hata shemasi. Luka alikuwa mtu wa Mataifa – asiyekuwa Myahudi. Alikuwa mwanasayansi, tabibu na mwanahistoria asiyekuwa mtaalamu ambaye aliwezeshwa na Roho Mtakatifu kuandika kitu ambacho hakina makosa. Luka alifanya aliyofanya kwa sababu ya kupenda shughuli hiyo. Dakta Luka ni mfano mkuu wa milele wa kile kiwango cha NENO KUWA MWILI KUWA NENO katika Agano Jipya. Mistari minne ya kwanza katika Injili kulingana na Luka inafanyika utangulizi wa kitabu hicho, na ni kama iliandikwa baada ya kitabu chote kukamilika (kutokana na jinsi maneno
138
yalivyopangwa). Katika hiyo mistari, tunaona mfano mmoja mkuu sana wa kufanya mwanafunzi upatikanao katika Biblia.
Katika utangulizi wake wa ajabu sana, Dakta Luka anaonyesha tabia nne muhimu sana za mtu anayefanya wengine kuwa wanafunzi, aliye na maono ya dunia na mwenye lengo la kugusa dunia na kujiongeza. Mwanafunzi yeyote anayetaka kujua uhalisi wa ukubwa wa maono ya Mungu yeye mwenyewe na kwa ajili ya kizazi chake na vizazi vifuatavyo, lazima aingize tabia hizo na kuzifanya zake katika maisha yake, na ni lazima naye azijenge na kuzitia ndani ya kila mwanafunzi ambaye Mungu atampa.
Dakta Luka alikubali wajibu binafsi kwa ajili ya kumjenga Theofilo. Aliingia katika utafiti mzito kwa niaba ya Theofilo. Aliandaa vitendea kazi thabiti kwa ajili ya kumwezesha Theofilo, na alifanya kila kilichowezekana kibinadamu kuzalisha kwa mpango wa kudumu wanafunzi wengine wenye maono ya dunia, wenye mguso wa dunia na wenye kujiongeza, kwa njia ya Theofilo. Soma sentensi ya mwisho kwa makini sana, ukifikiri vizuri kabisa – “Yatafakari ninayosema, na Bwana akupe ufahamu katika mambo yote” (ktk 2Timotheo 2:7).
WAJIBU BINAFSI
Kama wewe unataka kufuata kiwango cha Agano Jipya, lazima ukubali kuwajibika kibinafsi kwa ajili ya kuwajenga watu kuwa wanafunzi kulingana na Agano Jipya.
139
Luka alianza kwa kukubali juhudi nzuri za wengine, katika kutayarisha maelezo kuhusu maisha na huduma ya Yesu. Ingawa wengine walikuwa wamefanya kazi kubwa na ngumu ili kuandika masimulizi kuhusu Yesu, Luka alisema, “Niliona ni vizuri hata mimi pia …” Roho Mtakatifu alikuwa anafanya kazi kwa njia ya Luka ili atende zaidi ya jinsi Luka alivyoweza kufikiri. Luka aliona mtu mmoja tu – Theofilo. Mungu aliona vizazi vingi sana – mpaka na sisi! Luka aliandika kitabu kimoja kwa mtu mmoja. Mungu aliandaa Injili ya ajabu sana kwa ajili ya vizazi vyote vya wakati ujao! Sisi tunawea kuona mwanafunzi mmoja tu, lakini Mungu anaona makundi ya watu ambao watafikiwa na kuguswa na huyo mwanafunzi mmoja.
Historia ya Kanisa la Kikristo inathibitisha kwamba hii dhana ya KiMungu ni rahisi sana kiasi cha akili za kibinadamu kushindwa kuiona. Usipofanya watu kuwa wanafunzi, ni kwamba hukubaliani na kiwango cha Yesu, na unaacha kutii amri ya Yesu. Usipowajenga wanafunzi wako kufikia kiwango cha kuwa na maono ya dunia nzima, kuweza kuigusa dunia nzima, na kukamilisha utaratibu wa kufanya wanafunzi wanaoweza kujiongeza wenyewe, hujakubaliana wala kulingana na kiwango cha Yesu – pasipo kujali mengine yote yanayoendelea katika maisha yako! Injili yenyewe imejengwa kwenye kukubaliana na Mungu (ktk Warumi 10:9; Mathayo 10:32, mahali ambapo “kukiri” maana yake kukubaliana na) kuhusu sisi kutolingana na kiwango Chake. Basi, tunaletwa na Roho Mtakatifu
140
kwenye kukubaliana na Mungu kuhusu jinsi anavyomwona Mwana Wake, Yesu Kristo. Maisha yetu yote baada ya hapo yanapaswa kuwa ni makubaliano na Mungu na mapenzi Yake. Tunapotazama amri Yake na kiwango Chake, tunaona kwamba haitoshi kwa Mkristo binafsi kuanza tu kuwahudumia watu, kuwa mtu mzuri kwa watu, kutafuta kukutana na mahitaji ya watu, au kuwa mhudhuriaji mzuri tu na mwaminifu kanisani. Lazima tuamue kati ya sisi wenyewe (“kujikana wenyewe,” ktk Mathayo 16:24) na kukubaliana na Mungu. Na kwa kuwa tunaambiwa kulitimiza Agizo la Yesu “tukiwa tunakwenda”, hatupaswi kupiga hatua hata moja bila ya kutekeleza Agizo Lake na Mbinu Zake pia.
Fikiri maneno ya Bwana wetu katika Yohana 15:16, “Ninyi (mkazo mkubwa kabisa) hamkunichagua Mimi, bali Mimi (mkazo mkubwa) ndiye niliyewachagua ninyi na kuwaweka, ili ninyi (mkazo mkubwa) mwende na kuzaa matunda (tendo linaloendelea, mkazo mkuu) na kwamba matunda yenu yapate kudumu (kitu kinachoendelea wakati huo huo), ili chochote mtakachomwomba Baba kwa jina Langu, aweze kuwapa.” Je, nini kazi ya matunda? Mti unaozaa matunda hauli matunda yake wenyewe; ni kwa ajili ya mwingine. Sehemu moja ya tunda ni ili kuliwa, lakini sehemu nyingine ya tunda ni ili kuzaliana. Mbegu katika tunda huendeleza utaratibu wa kuzalisha chakula na kupatikana kwa matunda mengine. Je, katika embe kuna mbegu ngapi? Moja tu! Lakini, kuna maembe mangapi katika hiyo mbegu moja? Mungu tu ndiye ajuaye!
141
Umeingizwa katika Ufalme wa Mungu ili uwajibike kibinafsi kwa ajili ya mtu anayekuja. Lakini, hakuna kitakachotokea tu! Leo utakutana na watu wengi wasiohesabika katika makundi ya maishani, ambao wanaweza kupatikana kwa ajili ya shughuli ya kufanya watu kuwa wanafunzi (wakiingizwa kazini vizuri, na wakipata habari sawasawa, na kufundishwa sawasawa) – na pengine hutamjali hata mmoja wao. Bila ya “kuona na kusikia” kwa mtazamo wa Mungu hutaweza kutimiza wajibu wako binafsi kwa ajili ya mtu anayefuata.
Naomba nikukumbushe kwamba, lile swali “Kwani mimi ni mlinzi wa ndugu yangu?” lilitolewa kwa Mungu kutoka moyoni mwa muuaji wa kwanza duniani, aliyekuwa anajitetea na mwenye kujaa chuki moyoni! Nisipojiunga na Yesu katika kuwajibika kibinafsi kwa ajili ya kumjenga mtu anayefuata ili afikie dunia nzima, mimi ninajiunga na mawazo ya muuaji. Jibu la Mungu kwa swali la Kaini likawa, “Ndiyo. Wewe ni mlinzi wa ndugu yako. Tena – muhimu zaidi – wewe ni ndugu ya ndugu yako!” Sasa, unafanya nini kuhusu Habili wako? Hebu useme pamoja na Luka kwamba, “Niliona ni vizuri na mimi pia. Ninachukua wajibu binafsi kwa ajili ya mtu ambaye Mungu kanipa.”
UTAFITI MZITO
Kama unataka kufuata kiwango cha Agano Jipya, lazima uingie katika utafiti mzito wa Neno kwa ajili ya mwanafunzi wako. Yesu alisema hivi: “Ninajitakasa mwenyewe kwa ajili yao”, na
142
maisha yako lazima yalingane na Yake. Haitoshi tu kujifunza Biblia. Kuna watu kila mahali ambao wamo katika kujifunza Biblia ambao hawatawahi kumjenga mtu mmoja anayefanya watu kuwa wanafunzi ambaye anajiongeza, atakayeigusa dunia. Kwa nini? Sababu ni rahisi tu: mtazamo wa mwalimu wa Biblia na hata wa mwanafunzi anayejifunza Biblia hiyo hawana maono kwa ajili ya kuigusa dunia. Wale wanaohusika katika kujifunza Biblia hawaioni kama njia kwa ajili ya kuifidia dunia, wala hawatengenezi mtaala kutokana na kujifunza Biblia kwao ili kuwajenga watu watakaoigusa dunia kwa makusudi. Badala yake, wanajifunza Biblia ili “kujua zaidi” na kuwa “Wakristo bora zaidi”. Mpaka inafikia mahali pa kutiliwa mashaka ikiwa kweli hayo ni makusudi mazuri na yanayofaa kwa ajili ya Mkristo. Yanaonekana kama ni malengo ya “kuufanya Ukristo kununulika kwa mteja”. Kibaya zaidi ni kwamba, hilo huzalisha kuingia kubaya kwa Injili, badala ya upandaji utakaozaa, wenye kusababisha mavuno makubwa sana ya kiroho hadi miisho ya dunia, mpaka wakati wa mwisho kabisa. Mtu yeyote anaweza kujisomea Biblia kwa faida yake mwenyewe. Lakini, uwezo wa kuigusa dunia unatokana na maisha ya wale ambao kwa makusudi kabisa wanaingia katika utafiti wa dhati kabisa kwa ajili ya kusudi la kumjua na kumfuata Kristo kweli kweli na kumfanya Yeye ajulikane kwa wengine.
Tazama Luka 1:3 na utazame lile neno “kuchunguza”. Hili neno lina uzito sawa na “kutumia kwa uhalali” katika 2Timotheo
143
2:15, na ndiyo neno “kujulikana kabisa” katika 2Timotheo 3:10, ambapo Paulo alimwambia Timotheo hivi: “Wewe umeyajua vizuri mafundisho yangu, jinsi ninavyoishi, makusudi yangu, imani yangu, uvumilivu wangu, upendo wangu na subira yangu …” Neno la Kiyunani litumikalo katika Luka 1:3 na 2Timotheo 3:10 ni parakolutheo, ambalo maana yake ni “kutembea na mtu mguu kwa mguu, kufuata kwa karibu, kusikiliza kwa makini sana.” Katika lugha ya mfano, neno parakolutheo linamaanisha kufuata kwa karibu njia ya kifikra iliyowekwa wazi na mtu ambaye ameipitia sana, akichunguza kila kitu na kutokuacha kugeuza jiwe lolote. Hebu msomaji na atafakari kwa kirefu sana juu ya hiyo sentensi ya mwisho. Na kwa mara nyingine tena, “Fikiri hayo ninayosema, na Bwana akupe kuelewa mambo yote” (ktk 2Timotheo 2:7). Hii njia ya kifikra katika mstari huu ni yale matukio halisi yenye kumhusu Yesu Kristo tangu milele hadi milele. Wakati Yesu alipotoka mbinguni na kuingia katika wakati, alianzisha njia mpya katika ardhi ngumu yenye vingi, ya kihistoria. Kila Mkristo anapaswa kuifuata njia hiyo kifikra na kiroho, akichunguza kila jambo ili aweze kuzalisha hayo mambo katika maisha yake mwenyewe na kujenga kutokana na hayo somo na mtaala kwa ajili ya wanafunzi wake mwenyewe. Hii itahitaji utafiti mzito.
Neno parakolutheo lina maana nyingine. Linamaanisha “kufuatilia”. Wazo hapo ni kama vile mtoto mdogo anavyofuatisha mchoro kwenye karatasi. Anachofanya ni kuweka karatasi nyepesi
144
juu ya kile anachotaka kukichora, na kwa utaratibu na uangalifu sana anafatisha kila mstari, kila kitu kinacho-onekana. Matokeo yake ni nakala halisi kabisa ya kile kilichokuwa kinaigizwa. Basi, Luka anajitokeza ili kufuatisha tabia na kuzalisha moyo na shauku ya Yesu wa Nazareti. Wakati Luka alipoondoa chombo alichotumia kuandikia Injili ya Luka kwenye ukurasa wake wa mwisho, uzuri wa Yesu, na ubinadamu Wake na huruma Yake kwa ajili ya wanadamu vilidhihirishwa kwa hali ya juu sana. Kazi ya Luka iliyokamilika haifanani na yoyote nyingine ya mwandishi wa Injili. Roho Mtakatifu ndiye aliyeongoza kalamu ya Luka kufuatisha mfano wa Mungu ulioko katika ubinadamu wa Yesu. Sisi nasi tunapaswa kufuata mwongozo wa Luka katika kufuatisha tabia ya Yesu, njia aliyofuata, na mtaala alioutumia katika kuwagusa watu – na tunapaswa kwenda na kufanya vivyo hivyo!
Mapema kidogo tulitaja 2Timotheo 2:15. Neno la Kiyunani linalotumiwa hapo na kutafsiriwa “kutumia kwa usahihi” linahusiana na neno letu parakolutheo. Ni neno orthotomeo. Hebu lifikiri kidogo. Neno lenyewe ni maneno mawili – orthos lenye kumaanisha “sawa, sahihi,” na temno lenye kumaanisha “kukata, kugawa, kutumia kwa utaalamu”. Hakika, Luka alikuwa tabibu mwenye ujuzi na utaalamu sana, ambaye alifahamu maana ya kuwa makini na kujali vitu muhimu kutokana na kazi na taaluma yake. Luka alielewa kwamba kama ishara moja au dalili moja ingeshindikana kuonekana, mgonjwa wake angekufa. Alikuwa mtumiaji mwenye kuwajibika wa
145
ujuzi na habari na matumizi ya taaluma katika maswala ya uzima na kifo. Naye alijua kwamba mada yake aliyokuwa anaishughulikia wakati huo ilikuwa swala la uzima au kifo – kwenda mbinguni au kwenda jehanamu!
Utafiti bora zaidi kihistoria unaonyesha kwamba Luka alikuwa amefundishwa sayansi na kuelimishwa katika matibabu katika kile chuo cha uganga kilichokuwa Tarso. Kuna wasomi wengine wamefikia mpaka hatua ya kupendekeza kwamba Paulo, Luka na Theofilo walikuwa wanafunzi pamoja katika chuo kikuu cha Tarso. Basi, alikuwa amepata mafunzo bora zaidi kwa habari ya utabibu yaliyokuwa yanapatikana wakati ule. Vyovyote vile, yawezekana kwamba Luka, mwanafunzi bora sana wa utabibu, alimfahamu Sauli, aliyekuwa mwandishi na mwanatheolojia stadi, kabla ya kukutana katika Kitabu cha Matendo (ktk Matendo 16). Inaonekana kwamba Paulo, kwa sababu ya tatizo kubwa la kiafya (na kitabu cha Wagalatia kinaonyesha lilikuwa tatizo kubwa sana la macho) alikwenda kutafuta msaada wa Dakta Luka. Inawezekana pia kwamba Paulo (pengine katika kuhudumiwa) alimshirikisha Dakta Luka Injili na habari za Kristo. Wakati Luka alipokuwa anamtibu Paulo macho ili kurekebisha tatizo lake, Mungu Roho Mtakatifu alipenya katika giza la upofu kiroho wa Luka na kuleta “nuru tukufu ya Injili ya Kristo, aliye mfano wa Mungu” (ktk 2Wakor. 4:4). “Mungu” huyo huyo, “aliyeamuru nuru ing’ae gizani”, aliangaza katika moyo wa huyo daktari, “ili kutoa nuru ya maarifa ya utukufu
146
wa Mungu katika uso wa Yesu Kristo” (ktk 2Wakor. 4:6)! Baadaye kidogo, wakati Paulo alipotamka nia yake ya kuondoka Troa akiwa na timu yake ya utume kwenda eneo lingine walilopangiwa, Luka akaomba kuambatana naye. Pengine Paulo alisema hivi: “Lakini Daktari, mbona una hospitali yako hapa? Huwezi kuiacha tu!” Na pengine Dakta Luka akajibu hivi: “Hapana, ila, ni nzuri, na ninaweza kumwachia mtu mwingine kwa urahisi tu.” Basi Luka akaiuza hospitali yake pengine, na kujiunga na mtume Paulo katika safari zake za kitume zilizokuwa zimesalia!
Luka ndiye mwandishi pekee wa Injili aliyekuwa amesomea sayansi ya udaktari. Sasa, anaingiza mafunzo yake yote na utaalamu katika kukusanya kweli za habari ya Kristo kutoka kwa wale waliokuwa mashahidi, waliojionea mambo ya Yesu. Katika kusafiri kwake na Paulo, na bila shaka katika safari zake binafsi, alikutana na hao watu waliojionea mambo hayo katika Asia Ndogo, katika sehemu mbalimbali za Palestina, na hasa huko Yerusalemu. Kidogo kidogo, madaftari ya Luka yakaanza kujaa kutokana na mahojiano binafsi mengi aliyokuwa amefanya. Hii ni kawaida kabisa, kwamba: alama moja ya mtu anayefanya wanafunzi wenye maono ni daftari linaloendelea kujaa! Daftari la Luka liliendelea kujaa maneno aliyosema Yesu na mambo aliyofanya. Kila alipokutana na mtu yeyote ambaye alikaa na Yesu kwa muda fulani, au aliyekutana na Yesu au aliyeona miujiza ya Yesu, angeuliza maswali muhimu ya kutafiti: “Je, wewe ulimjua Yesu kibinafsi?” “Alikuwa anafanya nini
147
wakati ulipomwona?” “Je, Yesu alisema nini?” “Niambie kila kitu unachojua kuhusu Yeye.” Baadhi ya watu aliowahoji kwa karibu sana ni Petro, Yakobo, Yohana na wengine katika wale Mitume wa kwanza. Bila shaka alizungumza na Yohana Marko kwa ukaribu sana, ambaye naye alikuwa anamalizia Injili yake wakati huo (yaani, Injili ya Marko). Kuna ushahidi mzito kabisa kwamba Luka alifanya mazungumzo ya hali ya juu sana na Mariamu, mama yake Yesu. Daktari aliandika maelezo mapana sana kuhusu kuzaliwa kwa Kristo na bikira kuliko mwandishi yeyote mwingine wa Biblia, na madaktari si wepesi kuamini sana kwamba bikira huzaa! Kuna mwandishi mmoja anayeitwa William Hobart aliyeandika kitabu kikubwa tu kuhusu lugha ya kitabibu ya Dakta Luka, na ndani yake anaonyesha zaidi ya maneno mia nne maalum kabisa ya kitabibu ambayo Luka aliyatumia alipoandika Injili yake na Kitabu cha Matendo. Ni kwamba Daktari huyu aliamini kabisa kuhusu kuzaliwa kwa Kristo na bikira kutokana na ushahidi wenye nguvu na usioweza kupingika. Aliweza kuona na kupata habari kamili kuhusu kuzaliwa kwa Yesu kupitia mahojiano ya moja kwa moja na Mariamu mwenyewe.
Sasa – kwa utaalamu wa hali ya juu sana kisayansi, tabibu huyo maarufu na mwenye utaalamu aliandika simulizi lenye mpangilio mzuri sana kuhusu maisha ya Bwana Yesu. Anatoa taarifa yenye upana na maelezo mazuri kuhusu kuzaliwa Kwake, maisha Yake na mafundisho, kifo Chake, kufufuka Kwake, baadhi ya
148
matukio katika zile siku arobaini baada ya kufufuka Kwake, na kupaa Kwake. Ni wazi kwamba Luka alifanya juhudi kubwa sana kutafiti kuhusu Nafsi, mafundisho, matendo na mafanikio ya Yesu. Katika Luka 1:3, neno “kamili” linatokana na neno la Kiyunani akribos, ambalo maana yake ni “kwa bidii, kwa makini, au kwa uangalifu sana.” Luka alimtafiti Yesu kuanzia juu (akron – kiwango cha juu kabisa) hadi chini (abussas – chini kabisa, shimoni). Luka anasema, “Ee Theofilo, sikuacha kujitahidi katika kumtafiti Yesu tangu maelezo ya hali ya juu zaidi hadi kweli za ndani kabisa.” Luka alikuwa na uhakika kwamba amefanya juhudi zake zote kutafiti kila kitu kuhusu maisha ya Yesu – tokea juu hadi chini.
Zile Injili nne za Agano Jipya hazikuandikwa katika utupu usio na uchafu wowote, bali katika purukushani za kawaida za maisha. Ingawa kila Injili imevuviwa na Roho Mtakatifu, inazo alama pekee na vidokezo vya mwandishi wake. Yohana inasikika kama Yohana, Marko kama Marko, Mathayo kama Mathayo – ingawa kila mmoja anaandika kitabu ambacho ni kamilifu, na hata ingawa kila kitabu ni juu ya Mhusika kamili. Katika Luka 1:1, Daktari alisema kwamba maelezo yake yana mambo kuhusu Yesu ambayo yalitimizwa na kukamilishwa mbele ya watu wa wale aliokuwa amewahoji. Yohana ambaye ni mwandishi mwingine wa Injili alisema katika barua yake ya kwanza kwa watu wote kwamba hao mashahidi walikuwa wamemwona, kumsikia na kumgusa Yesu. Hivyo, walitoa ushahidi wa mambo waliyoona, waliyosikia na
149
waliyogusa wenyewe. Neno “shahidi aliyeona” kwa Kiyunani, litumikalo katika Luka 1:1 ni autoptes, ambalo ni maneno mawili yenye maana ya “kujionea mwenyewe”. Maelezo ambayo Luka alisikia toka kwa hao watu waliojionea kwa macho yao wenyewe mambo hayo yalikuwa na nguvu sana kumshawishi yeye mpaka akawa na uhakika kwamba yangeshawishi, kusadikisha na kumtosheleza yeyote ambaye angeyatafiti mwenyewe kwa ukamilifu zaidi. Katika Kitabu cha Matendo, anayaita “vithibitisho vingi visivyotiliwa mashaka” au ”ushahidi usiopingika” (ktk Matendo 1:3). Anaandika Injili yake ili kutoa huo ushahidi wenye nguvu sana utokanao na maelezo hayo.
Tena, Luka anatuambia kwamba alitafuta habari na ushahidi toka kwa wale watumishi wa mwanzo kabisa wa Kristo, wengi ambao walikuwa wametoa maisha yao au wangekuja kuyatoa baadaye, kutia muhuri ushuhuda wao kuhusu Yesu kwa damu zao wenyewe. Neno “watumishi” linalotumika katika Luka 1:2 kwa Kiyunani ni huperetes, ambalo maana yake ni “mpiga makasia wa chini”. Neno hili lilitumika kusema kuhusu mtumwa aliyefanya kazi katika merikebu, aliyekuwa anaketi mahali pa chini kabisa kwa ajili ya kumfikisha mtu mwingine mahali alipotaka kwenda.
Mtumwa wa kwenye merikebu alipelekwa mpaka pande za chini za merikebu hiyo na kufungwa mnyororo hapo, kwa ajili ya kufanya kitu kimoja tu. Kazi yake pekee ilikuwa ni kumtazama yule akida mpiga ngoma na kuvuta makasia kwa kushirikiana na wale
150
watumwa wengine kwa amri ya akida. Hawa “watumishi” walikuwa wamesadiki kabisa kuhusu enzi na Nafsi ya Yesu Kristo kiasi cha kuwa watumwa wapiga makasia kwenye ile “merikebu njema ya Neema,” wakiishi kwa ajili ya kumtazama na kumtii Nahodha wao, Bwana Yesu Kristo. Kusudi lao pekee lilikuwa kumfikisha mwingine mahali alipotaka kwenda. Luka anaonyesha kwa nguvu sana kazi hiyo yao na mtindo wao wa maisha wakati alipotafiti habari za Yesu na kuandika hiki kitabu cha ajabu na kushangaza sana kwa ajili ya kumfikisha mtu mmoja – Theofilo – hadi mwisho mzuri katika maisha haya, na mwisho mzuri katika maisha yajayo. Injili ya Luka na Kitabu cha Matendo vimejaa mfano wa mtu anayefanya watu kuwa wanafunzi – mtu mwingine, mtu mwingine, mtu mwingine …. Kila Mkristo anapaswa kujiona kama mtumwa aliyefungiwa katika merikebu, anayefanya kila linalowezekana kuijua hii Injili, kufuata maagizo yake, kutengeneza mtaala, na kujenga wanafunzi, vyote hivyo kwa ajili ya kumfikisha mtu mwingine mahali anapotaka kwenda – mwisho mzuri.
VITENDEA KAZI THABITI, VINAVYOFAA
Ukitaka kufuata kiwango cha Agano Jipya, lazima uandae vitendea kazi thabiti, vinavyofaa, kwa ajili ya kuwajenga wanafunzi wengine. Luka aliahidi kumpa Theofilo maelezo yaliyoandikwa ya Injili ya Yesu Kristo ambayo ni makamilifu, yenye kufuata utaratibu. Hapa katika mstari wa kwanza Luka anatumia neno la kijeshi,
151
anatassomai, ambalo maana yake ni kupanga askari, au vitu, au kweli fulani, katika utaratibu na mpango wake. Luka alitafuta kupanga kweli kuhusu Yesu katika mpango mzuri unaofaa kama jeshi la askari lililoandaliwa na kupangwa kwa ajili ya kuiteka dunia nzima. Luka akamkumbusha Theofilo kwamba alikuwa ametafiti habari za Yesu kutoka juu hadi chini na kuweka mambo aliyogundua katika “mtiririko” au “mpangilio mzuri”. Hakuna mwanafunzi mwenye kufikiri vizuri anayeweza kuepukana na kusudi dhahiri la Luka la kuweka mpango mzuri katika mtaala kwa ajili ya kufanikisha kikamilifu malengo yake katika maisha ya mtu mwingine.
Luka – kama Paulo, aliyemfanya yeye kuwa mwanafunzi – alianza mkakati wa kuwajenga watu ambao wangeweza kutumia kwa usahihi Maandiko (ktk 2Timotheo 2:15). Paulo alimwambia Timotheo katika 2Timotheo 3:10 kwamba, “umeijua kabisa itikadi yangu.” Paulo alikuwa amepanga vizuri sana kweli kuu za Injili kwa ajili ya Timotheo, ili aweze kuzishika vizuri na kusimikwa kwa uthabiti ndani yake, na kuzieleza kwa usahihi na ufasaha kwa mtu mwingine. Luka alifanywa mwanafunzi na Paulo, na sasa anatoa mfano mkamilifu mzuri kabisa wa sheria ya Yesu aliyesema hivi: “Utaratibu ukikamilika, mwanafunzi atakuwa kama mwalimu wake” (ktk Luka 6:40). Vile vile, Luka anatuonyesha katika mistari hii mfano mkamilifu wa mwanafunzi anayetayarisha mtaala kwa ajili ya kufanya wanafunzi wengine. Yeye “aliandaa maelezo sahihi” na “kwa utaratibu” kuhusu kweli za Yesu kwa ajili ya kufundisha,
152
kuingiza kazini, kujenga na kumtuma mtu mmoja ili afikie dunia. Mwalimu maarufu aitwaye F.F. Bruce anasema kwamba “maneno hayo yanaonyesha mfuatano wa maelezo katika utaratibu, kimada au kufuata matukio, badala ya maelezo tu yasiyo na mpangilio.” Kabla ya barua hii, Luka (au pengine Mkristo mwingine) alikuwa “amemfundisha” (Luka 1:4) Theofilo kwa ushuhuda wa maneno tu kuhusu Yesu. Neno katecheo ni neno la Kiyunani ambalo maana yake ni kufundisha kwa utaratibu na mpangilio, hasa kwa maswali, majibu, maelezo na marekebisho. Luka anaonyesha umuhimu mkubwa sana kwa ajili ya kueleza Injili kwa maneno kwa mpangilio ili kumleta mwanafunzi kwa Kristo, na umuhimu wa kuwa na mtaala ulioandikwa kwa mpangilio kwa ajili ya kumjenga mwanafunzi huyo katika imani na maisha ya Kikristo na huduma.
Luka alifanya hayo yote ili Theofilo afikie kwenye ufahamu kamili wa Yesu Kristo, na kusababisha uhakika usiotikisika juu Yake. Alfred Plummer alifafanua neno “kwa uhakika” katika mstari wa nne hivi: “Theofilo atajua kwamba Injili ina msingi usiovunjwa wa kihistoria.” Sisi nasi tunapaswa kuanza kuandaa mtaala na kutayarisha jedwali la vielelezo (hebu tazama mifano (au hekaya) itolewayo na Yesu ambayo Luka ameiandika katika Injili yake), kutumia kila kitu kinachofaa KiMaandiko tunachoweza kupata ili kuwajenga wanafunzi wetu juu ya msingi usiotikisika wa Injili tukufu ya Bwana wetu Yesu Kristo.
153
Kuna Wakristo wengi wazuri, wenye nia njema tu, na wenye kujua mengi sana ambao hawatalenga kumjenga mwanafunzi mmoja mwenye maono ya dunia, mwenye kuigusa dunia, na mwenye kujiongeza. Kwa nini? Kwa sababu, hawatajali sana juu ya jukumu lao la kujenga (au basi kupata) mtaala unaofaa, wenye utaratibu mzuri kwa kusudi la kufikisha mtu mwingine kwenye hatima yake ya mwisho. Ili hata mtu wa kawaida asije kukwepa kweli hiyo, F.F. Bruce anatukumbusha kwamba Luka alikuwa “mtu wa kawaida tu, asiyekuwa Myahudi na asiyekuwa mhubiri”. Luka alikuwa tabibu maarufu na mzuri sana, mwenye ratiba iliyombana sana! Lakini alipata wakati (yaani, alitengeneza wakati) ili “kuandika kwa utaratibu” maelezo “yenye mpangilio” kuhusu maisha ya Bwana wetu, huduma Yake, mafundisho Yake, mambo aliyofanikisha, na kazi Yake – kwa ajili ya mtu mmoja tu.
MPANGO WA KUDUMU WA KUZALISHA
Kama unataka kufuata kiwango cha Agano Jipya, lazima ufanye kila liwezekanalo kibinadamu kuwa na mpango wa kudumu wa kuzalisha wanafunzi. Kila mtu anayefanya wengine kuwa wanafunzi, mwenye maono, lazima afanye kila linalowezekana kibinadamu, kwa kumtegemea Mungu kabisa, kufanikisha na kuendeleza uzalishwaji wa wanafunzi. Hawa wanafunzi lazima waone dhahiri kwamba dunia nzima ni eneo lao la kazi, na lazima waishi kwa makusudi kabisa ili kuigusa dunia hiyo. Mwanafunzi
154
yeyote mwenye maono anajua kwamba hawezi kumfanya mtu mwingine yeyote aone kiwango au afuate lengo pasipo uwezo wa Mungu wa kimuujiza, lakini pia anajua kwamba kama yeye mwenyewe hatakimbia hadi kiwango cha nuru yake na uwezo wake katika kufukuzia kiwango hicho, Mungu hatamfanya mtu mwingine yeyote akimbie pamoja naye. Kanuni ya Agustino bado ni halisi: “Pasipo Mungu, sisi hatuwezi; pasipo sisi, Mungu hatafanya”.
Luka ametupa mfano usioweza kusahaulika wa mtu anayefanya wengine kuwa wanafunzi, mwenye moyo na bidii. Alielewa kikamilifu kabisa umuhimu wa kile alichokuwa anafanya. Luka alifanya uchunguzi kwa bidii kabisa kuhusu maisha ya Yesu wa Nazareti, akatafuta kwa makusudi kuwa sahihi katika maelezo yake, na alijua umuhimu wa mpangilio au utaratibu. Luka alijitia katika kazi hiyo kwa bidii, akakusanya kweli zote zilizokuwa zinaweza kupatikana (zilizoandikwa na za mdomo), kisha akaandika kitabu hiki kwa mtu mmoja aliyepotea – Theofilo.
Theofilo alifanya nini na kitabu hicho? Alisadiki kabisa kuhusu ukweli wake mpaka akakipokea, akamwamini Yule aliyetajwa humo pamoja na ujumbe wake, na akatafuta kukihifadhi na kukifikisha kwa wengine. Japo kitabu hiki kiliandikiwa mtu mmoja tu, wewe unayo nakala yake! Ni mfano ulioje huo wa kiwango cha Yesu cha kufanya mtu kuwa mwanafunzi ili kuigusa dunia nzima – kiwango ambacho anamwamuru kila mmoja katika wafuasi Wake kukifuata. Amri Yake hiyo inaitwa “Agizo Kuu”.
155
Luka alimleta Theofilo kwa Yesu Kristo kwa kumwandikia kile tunachoita sasa “Injili Kama Ilivyoandikwa Na Luka”. Wakati Theofilo alipomwitikia Kristo kwa imani binafsi, Luka akaanza mara ile ile kumfanya Theofilo kuwa mwanafunzi kwa kuandika kitabu kingine chenye sura ishirini na nane, tunachokiita Kitabu cha Matendo, ili kumtambulisha Theofilo kwenye wajibu na mtindo wa Yesu wa kuigusa dunia. Ni mfano wa kushangaza vipi na wa ajabu sana wa kile kiwango cha Mungu cha Neno kuwa mwili! Kumbuka kwamba kiwango hiki kilitendwa na mtu wa kawaida tu aliyekuwa tabibu ili kujikimu kimaisha, lakini ambaye kazi yake kubwa ilikuwa ni “kuwafanya watu kuwa wanafunzi”.
[USHUHUDA WA MWANDISHI – Mchungaji mmoja rafiki yangu aitwaye Jim Davidson alinishirikisha mfano huu, ambao nami nakushirikisha wewe kikamilifu kabisa.
Babu yetu mzaa babu aliyeitwa Isaac Kilgore alijiunga na jeshi la Majimbo ya Kusini ya Marekani mwaka wa 1862 akiwa na umri wa miaka kumi na nane. Vita yake ya kwanza kubwa ilikuwa mahali palipoitwa Shiloh. Ili upate picha ya ukali wa hiyo vita ni kwamba, baadaye, wakati wowote askari aliposimulia jinsi vita ilivyokuwa mbaya, alikuwa anasema hivi: ‘Yaani! Niliogopa kuliko nilivyo-ogopa kule Shiloh.’
Mzee Izaki aliendelea, akapigana huko Chickamauga, Chattanooga, Mlima wa Kennesaw, Atlanta, Franklin na Nashville – kwa uchache. Zote zilikuwa vita kali. Na kwa muda, yeye alikuwa
156
mbeba bendera wa kikosi, na kwa maana hiyo alikuwa rahisi kabisa kupigwa risasi, lakini alipona hata hilo. Watu zaidi ya laki sita na ishirini elfu walikufa katika vita hizo zote. Hebu fikiri jinsi hilo lilivyoathiri idadi ya watu leo.
Baada ya Mzee Izaki kutoka jeshini mwisho wa vita, alitembea kwa miguu kutoka jimbo la Carolina Kaskazini hadi eneo la Walker huko Alabama. Akaoa mara mbili na kujipatia watoto kumi na saba. Hebu fikiri jinsi hilo lilivyoathiri idadi ya watu leo! Na kwa kuwa hakufa vitani, alipata wazao na kuongeza vizazi. Mmoja wao ni mimi, nami nina watoto wawili, ambao bila shaka nao watapata watoto. Lakini je, ingekuwaje kama Mzee Izaki angekufa vitani?
Siri ya hayo yote ni hii: Kama utapata mafunzo sahihi kama anavyopaswa askari, na kama hutakufa vitani – na tuko vitani – utazaa wakati wote, kizazi baada ya kizazi kwa ajili ya Yesu Kristo. Lakini, lazima ufikiri na hili pia: Utazaa vizazi hivyo kwa ajili ya Yesu Kristo ikiwa tu utakubali kuifia nafsi yako. Yesu alisema hivi: ‘Mbegu ya ngano isipoanguka ardhini na kufa, inabakia peke yake. Lakini ikifa, inazaa mbegu nyingi sana na kunakuwa na mavuno mengi sana’.” MWISHO]
Je, utakubali kuwajibika kibinafsi kwa hilo na kuingia katika utafiti mzito ili kulifanikisha? Utakubali kukuza na kutumia rasilmali thabiti na za uhakika kwa ajili ya kuwajenga wanafunzi wa Agano Jipya, na kujitoa mwenyewe kwa Mungu kuhakikisha kwamba kuna
157
uzalishaji wa kudumu katika vizazi vijavyo? Mungu anakusubiri, na dunia ya wanadamu pia!
158
Sura Ya 6
Mpango Wa Mungu Wa Kuongeza
“Na mambo yale uliyoyasikia kwangu mbele ya mashahidi wengi, hayo uwakabidhi watu waaminifu watakaofaa kuwafundisha na wengine.”
Matendo 1:1-5
Kuanza kwa safari ya kiroho uliosababishwa na Siku ya Pentekoste kukawa kumekamilika. Kanisa la kwanza lilikuwa lisukumwe na nguvu na uwezo wa jambo hilo hadi miisho ya dunia ya wakati ule. Petro alikuwa amemalizia mahubiri yake, akieleza Injili ya Kufa na Kufufuka kwa Yesu na kuja kwa Roho Mtakatifu, halafu katika mstari wa 41 wa Matendo sura ya 2 tunasoma hivi: “Ndipo wao waliolipokea neno lake kwa furaha wakabatizwa, na siku hiyo hiyo wakaongezeka kwao kama watu elfu tatu.” Du! Nyongeza kubwa sana! Hakuna mchungaji yeyote duniani ambaye asingefurahishwa na kuokoka kwa watu elfu tatu kwa siku moja baada ya kuhubiri Injili. Jali sana neno “wakaongezeka” maana linatumika tena katika mstari wa 47 wa sura hiyo hiyo. Pitia kwa haraka mstari wa 42 hadi 47a, halafu sikiliza sentensi hii: “Na Bwana akaliongeza kanisa kila siku, kwa watu waliokuwa wanaokolewa”. Umeona tena neno “kuongezeka” hapo?
159
Sasa hebu tuone Matendo 5:14. Kisa cha kusikitisha sana cha dhambi na hukumu ya akina Anania na Safira kimemalizika kusimuliwa. Mstari wa 13 unasema, “Na katika waliosalia hakuna mtu aliyethubutu kujiunga nao, ila watu waliwatukuza na kuwapa heshima kubwa.” Ungejisikiaje kuwa mshirika wa kanisa lenye nguvu sana kiroho kiasi kwamba watu wanaogopa kujiunga nalo? Lakini tena katika mstari wa 14 tunasoma hivi: “Na waamini wakazidi kuongezeka zaidi kwa Bwana, makundi ya wanaume na wanawake.” Ile “mashine ya kuzidisha” imeharibika! Hawawezi tena kuwahesabu kwa sababu wengi sana wanaongezwa kwa Bwana.
Sasa ona badiliko muhimu. Katika sura ya sita, mkakati wa Mungu kihesabu kwa ajili ya kukua kwa kanisa la kwanza bila shaka unaongezeka kwa kasi kubwa. Katika mstari wa kwanza tunasoma hivi: “Na katika siku zile, idadi ya wanafunzi ilipozidi kuongezeka, kulitokea manung’uniko ya Wayunani kinyume cha Waebrania, kwa sababu wajane wao walikuwa wanapuuzwa katika huduma ya kila siku. Unaona utaratibu huo? “Kuongezeka,” “kuhudumiwa,” na hatimaye “kunung’unika”. Washirika wanapoongezeka kanisani, huduma za ziada lazima zifuate, ili kuwahudumia na kuwapa shughuli ya kufanya, na baada ya hapo – hakika kabisa kama nuru inavyofuata giza, manung’uniko yatafuatana na maongezeko. Ni kitu halisi kabisa kwamba watu zaidi siku zote maana yake ni matatizo zaidi. Kwani, si hata wewe ni tatizo kwa namna moja au nyingine?
160
Angalia asili ya tatizo lenyewe. “Ushemasi” wa kila siku (maana hasa ya neno ‘huduma’) ulikuwepo ili kugawa chakula, vitu na fedha kwa idadi kubwa ya Wakristo wapya waliojikuta katika matatizo ya ghafula kiuchumi na kijamii kutokana na wao kumwamini Kristo. “Wayahudi wa Kiyunani” walikuwa Wayahudi waliozungumza Kiyunani, waliokuwa wamezaliwa nje ya Uyahudi na waliokuwa wamerudi nyumbani karibuni tu kwa ajili ya sikukuu ya Pasaka na Pentekoste. “Wayahudi wa Kiebrania” walikuwa ni wazaliwa wa nyumbani, waliosema Kiaramu, lugha ya Wayahudi waliokaa Palestina. Wale wa Kiyunani walikuwa ndiyo wachache, na wale Waebrania walikuwa ndiyo wengi.
Basi, manung’uniko yalitoka kwa wale waliokuwa wachache (kihalali kabisa) kama hoja kuhusu wajane wao kupuuzwa katika ugawaji wa kila siku wa vitu. “Walio wengi walikuwa wanawajali watu wao kiasi cha kuwapuuza na kuwanyanyasa walio wachache”. Ili kushughulikia tatizo, Mitume waliwachagua watu saba, na wote walikuwa na majina ya Kiyunani. Hiyo ni busara, sivyo? Kutatua tatizo na kumaliza malalamiko, watu kutoka miongoni mwa walalamikaji walichaguliwa kusimamia ugawaji wa vitu. Tatizo likawa limetatuliwa, “na Neno la Mungu likazidi kuenea, na idadi ya wanafunzi IKAONGEZEKA sana Yerusalemu, na idadi kubwa ya makuhani wakaitii imani” (Matendo 6:7). Maongezeko yalikuwa makubwa kiasi cha kuwepo na wingi waliotoka katika ukuhani wa Wayahudi kuingia katika jamii ya wanaomwamini Yesu huko
161
Yerusalemu. Ona kwamba kuanza sasa, kuongezeka ndicho kiwango cha kawaida kwa ajili ya kukua kwa kanisa la kwanza.
Katika sura ya 9, kasi inaendelea. Sura ya tisa ni masimulizi ya kuokoka kwa Mkristo mkuu kuliko wote – Sauli wa Tarso. Baada ya vurugu zilizotokana na kuokoka kwake na mahubiri yake ya kwanza kumalizika, tunasoma hivi katika mstari wa 31: “Ndipo makanisa yakapumzika katika Uyahudi yote na Galilaya na Samaria, tena, yakajengwa. Na, yakitembea katika kumcha Mungu na katika faraja ya Roho Mtakatifu, yalizidi kuongezeka sana.” Kwa kuwa sentensi yenyewe imekaa ilivyokaa, inaweza isiwe rahisi kuona kiwango cha kuzidishwa hapa. Sasa makanisa yanaongezeka! Swali: Je, Ukristo wa namna hiyo ulipotelea wapi? Hawakuwa na mashirika ya kimishenari, wala kamati za kuanzisha makanisa na watenda kazi wa kamati hizo. Hawakuwa na wamishenari wa ndani na nje ya nchi waliokuwa rasmi, lakini makanisa yalizidi kuongezeka. Tunauliza tena: Ukristo wa aina hiyo ulipotelea wapi?
Jibu linaweza kuonekana kwa urahisi kabisa ukifanikiwa kuhudhuria makongamano au mikutano yoyote ya wachungaji. Wahubiri wanaoanza kukutanika, wanauliza maswali kadhaa ya kawaida kabisa. “Vipi, Jumapili yako ilikuwa nzuri?” Jibu: “Naam – ilikuwa nzuri kabisa.” Swali linalofuata ni lipi? “Umekuwa na watu wangapi walio-ongezeka?” Wapendwa: Hatuwezi kuwagusa wakazi wa dunia hii wanaozidi kuongezeka kwa sisi kuongeza makanisa yetu, hata kama maongezeko yetu yatakuwa makubwa kiasi gani.
162
Kasi ya kuzidishwa haiwezi kufikiwa na maongezeko kamwe! Kuna mtu mahali katudanganya kuhusu kitu cha muhimu sana. Mungu ametuita kuongezeka!
Hatupaswi kupuuza thamani na umuhimu wa watu kuokoka (au, kuongezwa) katika jamii ya Wakristo, lakini, inabidi tujilazimishe kukabiliana na kosa kubwa sana katika taratibu zetu za utendaji kazi kama huko kuongezeka hakutakuwa mwanzo wa kuzidi kwa jamii ya Wakristo duniani kwa ujumla.
Amri pekee ya kusonga mbele iliyowahi kutolewa na Yesu kwa kanisa Lake inaitwa Agizo Kuu. Kuna maneno tendaji saba katika Agizo hilo, lakini moja tu ndiyo amri. Kuna neno moja tu zito, lenye nguvu, ambalo ni amri moja, katika Agizo Kuu! Neno tendaji hilo linatafsiriwa “kufundisha” ingawa hapo tena ni dhahiri kwamba kuna jambo tunalofichwa hapa. Kwa sababu, maana ya neno hilo ni zaidi ya kufundisha tu! Maana ya neno tendaji hilo ni “kufanya wanafunzi”. Tunahitaji kuacha kuuliza, “Umepata maamuzi mangapi katika ibada yako?” na kuanza kuuliza hivi: “Je, unajenga wanafunzi wangapi?”
Kanisa la kwanza lilijizidisha kwa kutumia mfumo na utaratibu uliokuwa umeonyeshwa vizuri na kwa ukamilifu kabisa katika huduma ya miaka mitatu ya Yesu Kristo na wale mitume Wake kumi na mbili. Yeye ndiye wa kwanza kufanya watu kuwa wanafunzi, na utaratibu aliofuata lazima uchunguzwe, tujifunze, tuufahamu na kuuiga kama tunataka kuzalisha wazalishaji kama
163
Yeye alivyofanya. Mimi binafsi siamini kwamba mtu anaweza kuwa mwanafunzi bila ya kuwa mwenye kufanya watu kuwa wanafunzi pia. Kutii kwetu UBwana wa Yesu Kristo unahusisha kuweka kipau mbele kwenye kutimizwa kwa Agizo Lake Kuu. Ninaamini kufanya watu kuwa wanafunzi ni kitu kilichomo ndani ya mkataba wetu wa kuwa mwanafunzi. Kama mtu ni mwanafunzi kulingana na Agano Jipya, basi atakuwa mwenye kufanya watu kuwa wanafunzi pia.
PICHA YA MWANAFUNZI ANAYEJIZIDISHA
Sasa fungua Timotheo wa Pili sura ya 2. Katika sura hiyo, tunapata picha saba nzuri sana za mwanafunzi, na maelezo yanayofaa sana ya mpango wa Mungu wa maongezeko. Kwaanza, tuangalie picha za mwanafunzi. Kila moja katika zile saba inatoa sehemu ndogo ya picha ya mwanafunzi wa Agano Jipya.
NI “MWANA”
Kwanza kabisa, mwanafunzi wa Agano Jipya ni “mwana” (ktk mstari wa kwanza). Yeye ni mwana wa Mungu kwa kuzaliwa kutoka juu, lakini hapa ni mtoto wa kiroho wa aaminiye atakayemleta kwa Kristo. Paulo alimwita Timotheo “mwanangu” kwa sababu alimwongoza kumjua Kristo. Katika safari zake, Paulo alifika kwenye mji ambako Timotheo alikuwa anaishi, katika safari zake za kitume. Akakuta familia yenye wanafunzi wawili maarufu
164
sana wa Agano la Kale, bibi mmoja aliyeitwa Lois, na mama mmoja aliyeitwa Eunike (ktk 2Tim. 1:5).
Eunike alikuwa na mtoto mchanganyiko aliyeitwa Timotheo. Baba yake alikuwa Myunani. Alipogundua jinsi kijana huyo alivyokuwa amefundishwa Biblia vizuri, alimwongoza kwa Kristo kwa urahisi sana. Alipoanza kumfanya kuwa mwanafunzi, akaona uwezo mkubwa sana wa kiroho ndani ya yule kijana, ambao ulikuwa wa kipekee sana. Paulo alipoondoka kuendelea na safari yake ya kitume, alimtia moyo kijana huyo kukua katika mwendo wake na Kristo. Paulo aliahidi kumwombea kila siku, na pia aliahidi kwamba angerudi ikiwezekana.
Baadaye sana, katika safari nyingine ya kitume, Paulo alirudi mjini kwa Timotheo. Alipomfuatilia yule kijana, ndoto zake kuu zikawa zimetimizwa. Kijana alikuwa amekua kiroho kuliko Paulo alivyokuwa ametazamia. Alipokaribia kuondoka, Paulo alisema, “Sasa Timotheo, unaonaje? Ungependa kusafiri na mimi?” Pengine Timotheo akatekewa. “Mimi? Nisafiri na wewe?” Paulo akamjibu, “Ndiyo.” Timotheo akauliza, “Huko safarini tutafanya nini?” Pengine Paulo alimjibu hivi, “Wewe nitazame mimi, niombee, halafu tutazungumza usiku.” Unapokuwa Mkristo mwenye maono, huko ni kumfanya mtu kuwa mwanafunzi!
Je, mwana au mtoto mzuri anafanyaje? Anajifunza kutoka kwa mzazi wake, anampenda mzazi wake, anamtii mzazi wake, na
165
kuongeza au kukuza tabia za familia. Ndivyo na mtoto wa kiroho anavyofanya.
NI “ASKARI”
Pili – mwanafunzi wa Agano Jipya ni “askari”. “Hakuna apigaye vita ajitiaye katika shughuli za dunia, ili ampendeze yeye aliyemwandika awe askari.” Je, askari mzuri hufanya nini? Anaachana na mipango yake yote na makusudi yake yote, ili kutimiza jukumu alilopangiwa. Anaingia katika mafunzo kwa bidii na udhati mkubwa sana. Anatetea maslahi ya nchi yake. Anapigana inapokuwa lazima. Kwa kifupi ni kwamba, yuko tayari kwa ajili ya mapambano na kujitoa, ambavyo ni vitu muhimu kama atafanikisha jukumu lake.
Ee Jemadari mpendwa, ulijeruhiwa vitani.
Mimi nisishangae kama nitaumizwa kidogo.
Badala yake, Ee Bwana, hebu swali langu kuu liwe
Je, nitapata kujeruhiwa vitani pamoja Nawe?
NI “ASHINDANAYE” (Mwanariadha)
Tatu – mwanafunzi wa Agano Jipya anafananishwa na “mwanariadha” ashindanaye. Mstari wa 5 unasema hivi: “Hata mtu akishindana katika machezo, hapewi taji, asiposhindana kwa halali.” Imekisiwa kwamba katika Agano Jipya, mashindano ya mbio yametajwa zaidi ya mara hamsini. Je, mwanariadha mzuri anafanya
166
nini? Anajitia kabisa katika mchezo wake, anafanya mazoezi magumu na kwa mpangilio, anapata ujuzi unaotakiwa, anajitahidi kuwa na nidhamu kiakili pamoja na kimwili, na anafanya juhudi ili ashinde. Mwanafunzi Mkristo hatafanya pungufu ya hapo katika kumfuata Kristo.
NI “MKULIMA”
Nne ni kwamba, mwanafunzi wa Agano Jipya anafananishwa na “mkulima” (ktk mstari wa 6). Je, mkulima mzuri hufanya nini? Anafanya kazi kwa bidii. Anatifua udongo, anapanda mbegu, analima, na anavuna mavuno aliyolima. Pia anatenga mbegu kwa ajili ya kupanda baadaye, kuvuna, na kuongeza mazao yake. Shughuli hizo zote zina mifano inayofanana na iliyo wazi kabisa katika zoezi la kiroho la kuwa mwanafunzi na kuwafanya wengine kuwa wanafunzi.
NI “MTENDA KAZI”
Kitu cha tano ni kwamba, mwanafunzi wa Agano Jipya ni “mtenda kazi” (ktk mstari wa 15), tena, mtenda kazi bingwa. Yeye anapaswa kuwa “mtenda kazi asiyekuwa na sababu ya kutahayari, akilitumia kwa uhalali neno la kweli”. Ili kufanya hayo, lazima “kujifunza ili kujionyesha kuwa amekubaliwa na Mungu”. Kama wanafunzi Wakristo, sisi tupo ili tufanye kazi kwa bidii, sio kuzembea.
167
NI “CHOMBO”
Cha sita ni kwamba mwanafunzi wa Agano Jipya ni “chombo” (ktk mstari wa 20 na 21). Je, chombo ni nini? Chombo ni kitu chenye nafasi, iliyokusudiwa kujaa kitu au mtu. Sisi kama Wakristo, tumekusudiwa kumjaa na kufikisha uzima wa Kristo Mwenyewe kwa watu. Je, chombo kizuri hufanya nini? Kinaketi kabatini kwa mwenyewe, kikiwa kitupu na chenye kupatikana, na kumsubiri mhusika akijaze, akipenda. Mwanafunzi Mkristo hawi katika hali ya kujiuliza ikiwa Bwana wake anataka kumjaza au vipi. Waefeso 5:18 inamwagiza “kujazwa na Roho”. Chombo kikishajazwa, kinamsubiria mwenyewe akimimine. Yaani, kinasubiri tu akitumie kama vyombo vinavyotumika. Ndivyo tunavyopaswa kuwa na sisi kama wanafunzi wa Kikristo.
NI “MTUMISHI”
Mwisho, mwanafunzi wa Agano Jipya ni “mtumishi” au mtumwa wa upendo. Mtumwa hana mapenzi yake mwenyewe, hana ratiba yake mwenyewe, hana haki zake, na hana mali yake. Yeye ni mali ya bwana wake. Lakini, hana kupungukiwa katika rasilmali. Hazina yote ya bwana wake inatosheleza kazi yoyote ile anayoweza kupewa na bwana wake. Ndivyo ilivyo pia kwa mwanafunzi Mkristo.
168
UTARATIBU WA KUZIDISHA WANAFUNZI
Sasa, baada ya kuona picha ya mwanafunzi kama itolewavyo katika 2Timotheo 2, hebu sasa tutazame utaratibu wa kuwazidisha wanafunzi. Mimi nimeuita “mpango wa Mungu wa kujiongeza.” Huo unapatikana katika mstari wa 2, pale ambapo Paulo alimwambia hivi Timotheo: “Na mambo yale uliyoyasikia kwangu [mimi] mbele ya mashahidi wengi, [wewe] wakabidhi watu waaminifu, watakaoweza [nao] kuwafundisha na wengine pia.” Hapo tunaona vizazi vinne vya wanafunzi katika mstari huu mmoja: “Mimi … wewe … watu waaminifu … wengine pia”. Kama inavyooneshwa kwenye mchoro huu.
Watu Waaminifu Wengine
Paulo Timotheo Watu Waaminifu Wengine
Watu Waaminifu Wengine
Bila shaka unapata picha kwamba mpango huo ni sawa na kitu kinachozidi kupanuka, sehemu ndogo ikiwa pale ambapo Paulo na Timotheo wamesimama. Kila kitu kinaanza na “mimi” na “wewe”, Paulo na Timotheo, na hiyo hali ya muungano inaonyesha vitu viwili muhimu sana kuhusu kuwafanya watu kuwa wanafunzi.
(1) Umuhimu wa mtu mmoja, na
(2) Umuhimu wa mahusiano mazuri.
169
Ondoa yeyote kati ya hao watu wawili – Paulo au Timotheo – na utaratibu wote unaporomoka tangu mwanzo. Hakuna kuongezeka kunakoweza kutokea pasipo mshikamanishaji hapo mwanzo, na wengine wa kuunganisha nguvu naye.
Paulo na Timotheo lazima wawe watu ambao ni wa sifa au hali aina fulani na wenye msimamo kama wanafunzi, ikiwa kuongezeka kutafanyika. Halafu, lazima wawe na mahusiano kwa jinsi ambayo ni ya wazi, yenye kuaminika na ya kipekee. Loo! Kanisa linahitaji kutafiti na kufanyia kazi theolojia ya mahusiano kwa hali ya juu sana! Hiyo ni dunia nyingine nzima ambayo haiguswi hata kidogo na kanisa kwa jumla. Kama Paulo na Timotheo hawakuwa na mahusiano yaliyojengwa kwenye kuaminiana na kupatikana, mnyororo ungekatikia pale mwanzoni kabisa. Lakini kwa neema ya Mungu na kwa faida yetu sisi na vizazi vyote vya baadaye, Paulo alikuwa balozi mzuri sana, wa kuvutia, mwenye uwezo mkubwa wa kutenda kazi kwa ajili ya Kristo. Na Timotheo naye alikuwa mwanafunzi mwaminifu, anayepatikana na mwenye kufundishika kwa urahisi.
UTARATIBU HUO UNAMFIKIAJE MWANAFUNZI?
Swali: Je, Paulo “alimfikishiaje” Timotheo? Utaratibu huo ulimfikiaje Timotheo? Yeye aliwezaje kupata hali ya Paulo mpaka naye akaweza kuiendeleza? Paulo alisema hivi: “Mambo yale ambayo wewe umeyasikia kwangu …” Je, ni swala la kusikia tu? Je,
170
mtaala ni dhana za kielimu tu, au mawazo ya kifilosofia tu, ambayo yanawea kufundishwa darasani kutoka kizazi hadi kingine? Hapana kamwe! Sasa basi, neno “kusikia” lina maana gani katika Agano Jipya? Mbona kusikia kunasimamishwa ili kuonyesha kuingizwa kwa mambo ya kiroho badala ya kuona, au kunusa au kuonja au kugusa? Ni kweli kwamba kuna mifano kiroho inayolingana na hizo hisia za kimwili. Basi, mbona kusikia kunatengwa na kukaziwa zaidi? Je, yaweza kuwa ni kwa sababu kusikia ndiyo hisia ambayo kwa hiyo utambuzi halisi huenda moja kwa moja hadi ndani ya mtu? Katika upokeaji wa hisia zingine zote, lazima kuwe na tafsiri. Picha zinazoonekana na macho lazima zitafsiriwe ili kueleweka kama mawazo na dhana, ndipo zifike ndani ya mtu. Ni kweli hata kuhusu vitu tunavyogusa, kunusa au kuonja. Lakini katika kusikia, mawasiliano ya moja kwa moja yanafanyika. Basi, “imani huja kwa kusikia, na kinachosikilizwa ni Neno (rhema, ujumbe muhimu, uliosemwa kwa upendo) la Mungu.”
JE, MPANGO WA KUSIKIA UNAHUSISHA NINI?
Katika mpango wa kufanya watu kuwa wanafunzi, huko “kusikia” kunahusisha kitu gani? Katika 2Timotheo 3 kuna mistari miwili inayoweza kutudokeza kidogo maana yake (ms. 10 na 11). Paulo aliandika hivi: “Wewe umejua kabisa (Paulo aliishi maisha ya wazi kabisa mbele ya Timotheo – uwazi … kufikisha ujumbe … mabadiliko, ndiyo utaratibu) mafundisho yangu, maisha yangu
171
(mtindo), kusudi langu, imani yangu (au, uaminifu katika utendaji), uvumilivu wangu (uwezo wa kuteseka kwa muda mrefu), upendo wangu, subira na mateso yangu (kumbe Paulo hakumficha Timotheo ukali wa dhiki yote aliyopata).”
Hayo ni matokeo ya kawaida kabisa ya kanuni ile inayoitwa “pamoja naye, pamoja nami”. Yesu aliwaweka kumi na mbili ili wawe pamoja naye” (ktk Marko 3:14). Kuwa mwanafunzi na kufanya wengine kuwa wanafunzi ni mtindo wa maisha ambao hunaswa zaidi ya kufunzwa. Hebu fikiri – kuna mtu anayeweza kusafiri safari ndefu na Paulo bila ya kubadilishwa na safari hiyo?
BAADA YA MWANAFUNZI KUWEZESHWA, ANAFANYA NINI?
Sasa basi, baada ya Timotheo “kuwezeshwa” au “kukamilishwa” au “kufundishwa ipasavyo”, anafanya nini? “Mambo yale uliyoyasikia kutoka kwangu mbele ya mashahidi wengi, wewe nawe uyakabidhi hayo kwa watu waaminifu”.
Maneno mawili hapo ni muhimu sana katika kufafanua nafasi na kazi ya Timotheo. Yeye anapaswa kukabidhi (ile imani yote, mtindo wa maisha na kujitolea) kwa watu “waaminifu”. Hapa tuwe makini sana. Hili ni mojawapo kati ya mambo ya hali ya juu sana kuhusu akili ya Kikristo. Kitu hiki kinapofanya kazi sawasawa, siku zote wanapatikana viongozi wa kizazi cha pili na cha tatu. Hii ndiyo sababu ni muhimu sana sana kwamba mwenye kufanya watu kuwa
172
wanafunzi atafute tu kuingiza utaratibu huo katika watu waaminifu. Kama wanafunzi wake watakuwa si waaminifu, mpango mzima unaishia kwao, na vizazi vyote vya baadaye vinaweza kuachwa pasipo uongozi wa kiroho wenye ujuzi.
Neno lingine linalopaswa kutazamwa vizuri tu ni lile neno kuu katika mstari. Ni neno “wakabidhi”. Hapa tena, lazima tuwe makini sana kuelewa vizuri maana yake. Ni neno la kibenki. Maana yake halisi ni “kuweka fedha”. Unapokwenda benki kuweka fedha katika akaunti ya kuweka fedha, unatazamia kupata faida fulani. Ndivyo ilivyo unapofanya mtu kuwa mwanafunzi. Huwi unayemsafisha mwenye dhambi tu ili awe safi. Unafanya uwekezaji wa wingi na wa hali ya juu ambao utazaa faida isiyo na mwisho hadi umilele wote!
JE, NI UWEKEZAJI AU NI MATUMIZI?
Basi, hebu niulize swali zito: Je, maisha yako ya sasa hivi ni matumizi zaidi au ni uwekezaji? Je, unayatumia au unayawekeza? Fikiri kwa umakini kidogo hapa. Kama unayatumia, basi matumizi hayo ni mwisho. Hakuna faida kutokana na tendo hilo. Na ukweli lazima usemwe. “Shughuli nyingi za Kikristo” tunazojihusisha nazo – iwe ni kuhudhuria kanisani, kusoma Biblia, maombi, n.k. – ni matumizi kuliko kuwa uwekezaji. Ni shughuli za “kujihami” tu ambazo hutufanya sisi kuwa “Wakristo wazuri” badala ya kuwa
173
uwekezaji ambao utaigusa dunia hadi miisho ya nchi mpaka mwisho wa wakati. Hivyo, shughuli hizo zinasaliti Agizo la Yesu Kristo.
Timotheo alitakiwa achukue akiba yote ya maisha ya Kristo ambayo ilitoka kwa Paulo ikamfikia yeye, naye “aiweke” katika maisha ya watu waaminifu, na utaratibu huo haujafanikiwa mpaka nao waweze “kuwafundisha wengine pia.” Basi, utaratibu huo unatakiwa kuzidi kuongezeka mpaka uwe kitu kikubwa chenye kuhusika na eneo pana zaidi na zaidi na kuwahusisha watu zaidi na zaidi.
MIFANO YA KUONYESHA UMUHIMU NA UWEZEKANO WA MAONGEZEKO
Hebu tutumie mifano michache ya kawaida tu ili kuonyesha umuhimu na uwezo wa kuongezeka.
MWINJILISTI
Hebu tudhanie kwamba yupo mwinjilisti ambaye angeweza (na kweli wapo) kuleta watu elfu moja kila siku kwa Kristo. Kama idadi ya watu duniani sasa hivi “ingegandishwa” hapo ilipo – asiwepo mtu yeyote kuzaliwa na mtu yeyote kufa mpaka kila mtu afikiwe na kumfuata Kristo, muda ambao ungehitajika kufikia idadi ya sasa ya watu duniani ni zaidi ya miaka elfu kumi na tano! Na hapa tukumbuke kwamba, hao watakuwa wameokoka tu, si kwamba ni wanafunzi wa Yesu.
174
KILA SIKU IWE YA PENTEKOSTE
Au, tuseme kwamba kila siku ingekuwa Siku ya Pentekoste, wakiokoka watu elfu tatu kila siku. Ingechukua miaka kama elfu tano hivi kuwaleta watu wote walioko duniani sasa hivi kwa Kristo! Na, zingatia kwamba idadi ya watu haijanganda! Inaongezeka kwa kasi kubwa sana. Basi, mambo yanakatisha tamaa, sivyo?
Hii ndiyo sababu lazima tufanyie kazi kanuni ile ya Biblia ya kujizidisha. Sasa, mfano ufuatao ni wa kihesabu, wa kinadharia, na ni kitu kisichokuwepo, lakini utatusaidia kuona uwezekano wa kujizidisha kiroho. Tuseme kwamba mwanafunzi mmoja anayefanya wengine kuwa wanafunzi ameguswa kabisa na kuingiziwa uwezo wa kuwa mwalimu wa kufundisha wengine kuwa wanafunzi, naye amtafute mwanafunzi mmoja ili amfundishe kwa mwaka mmoja kwa njia ya kumwezesha na yeye kuwa na mwanafunzi na kumfundisha kwa mwaka unaofuata, na hayo yaendelee hivyo hivyo bila kubadilisha chochote katika utendaji na maongezeko, mpango huu ungempita yule mwinjilisti “anayeokoa watu elfu moja kwa siku” baada ya miaka 23, na (ni hoja tu) watu wote duniani wangefanywa kuwa wanafunzi katika muda wa miaka 35. Ona tofauti kati ya “waongofu” wa mwinjilisti na “wanafunzi” wa yule mzalishaji mwenye maono.
Onyo: Mifano kama hii isitumike kupambanisha shughuli za wainjilisti na wavuna roho dhidi ya wanaofanya watu kuwa
175
wanafunzi. Hizo ni nafasi zinazotegemeana, ambazo kila moja ni ya muhimu. Kwa kweli ni vizuri hata nafasi hizo zote mbili ziunganishwe katika kila mwamini anayekomaa na kuukulia wokovu.
Kwa nini kufanya watu kuwa wanafunzi kunaendelea kwa kusuasua sana? Ukweli ni huu: Mungu amekosa watu wanaofaa na wenye sifa za kuwa waanzilishi wa shughuli hiyo. Yaani, hakuna wazalisha wanafunzi wa kutosha kuanzisha mpango huo duniani kote. Lakini, hilo lisituvunje moyo. Tukiwa na maono na mawasiliano, jambo hilo linaweza kurekebishwa haraka sana kuliko tunavyofikiri. Tena kumbuka, mambo yanaanzia kwa Paulo kwenda kwa Timotheo, ambaye ndiye anayefuata. Na mpango au utaratibu mzima unategemeana na ubora, kujitolea, maono na utendaji wa hao watu wawili wa kwanza. Kwa sababu, kikawaida, wao ndiyo mifano inayoonekana pale mwanzoni kabisa na wenzao, pamoja na kwamba hilo ni jambo la kutisha.
Umuhimu wa maongezeko ya kila siku ni mkubwa sana kwa ajili ya kuhitimisha mpango mzima. Hakuna mtu anayetakiwa kushindwa. Mkristo mmoja akishindwa kufanikisha sehemu yake ya kuongezeka, anapunguza uwezo wa kutimiza Agizo Kuu katika kipindi cha uhai wake kwa nusu nzima. Lakini, kama Mkristo mmoja tu akifanikiwa (na kujizidisha), anaongeza mara mbili uwezo huo katika kipindi cha uhai wake.
176
MAONO YA KUIGUSA DUNIA NZIMA KWA KUFANYA WATU KUWA WANAFUNZI
Ewe Mkristo, unayo maono ya kuigusa dunia nzima kwa kufanya watu kuwa wanafunzi? Je, unawekeza vizuri kabisa ule mtindo wa maisha ya Yesu, maono ya Yesu, na kujitolea kwa Yesu katika maisha ya watu binafsi ili nao wawe na maono hayo hayo na kujitolea, na kuweza kuwapa wengine? Kuna mtu ambaye amesema hivi, kwa busara kabisa: Ili uweze kugawa maono kwa wengine, lazima wewe mwenyewe:
 Uyaone waziwazi,
 Uyaseme kwa ubunifu,
 Uyaonyeshe kila wakati,
 Uwashirikishe watu wengine kwa bidii, na
 Uyalinde kwa uangalifu sana.
177
Sura Ya 7
Hekima Ya Mkakati Wa Yesu
Tunaianza sura hii kwa kutazama andiko linaloonekana si kitu kabisa. Ukweli ni kwamba, unaweza kusoma barua ya Paulo ya Kwanza kwa Wathesalonike mara mia bila hata ya kujali mstari huu. Lakini – na hii ni kawaida katika Maandiko – mara nyingi Mungu huficha hekima ya Mbinguni katika maandiko yasiyokuwa wazi sana, na huu ni mfano mmoja. Katika mstari huu kumefichwa utukufu wote na hekima ya Ukristo. Mstari wenyewe ni 1Wathes. 3:8, unaosema hivi: “Kwa kuwa sasa twaishi, ikiwa ninyi mnasimama imara katika Bwana”.
Kumbuka kwamba Agano Jipya liliandikwa kwa lugha ya Kiyunani, na uzuri mmoja wa lugha ya Kiyunani ni kwamba mpangilio wa maneno katika sentensi hudhihirisha kama hayo maneno yana uzito, na kama ndivyo, uzito huo ni mdogo (mfano: Roho Mtakatifu anapandisha sauti Yake) au ni mkubwa (mfano: Roho Mtakatifu anapiga kelele). Sasa – katika 1Wathes. 3:8, maneno yamepangwa kwa njia kwamba neno moja limebeba mkazo, na ni mkazo mkubwa. Mara nyingi nimewauliza watu kukisia ni neno gani lililokaziwa, na wameshindwa. Ni hivi: Hatuwezi kwa akili zetu kama binadamu kukisia na tukapata usahihi kuhusu Mungu. Hata kama tutabahatisha jibu sahihi, jibu letu bado ni kosa kwa sababu
178
tulikisia. Hii ndiyo sababu imetupasa kujifunza Biblia, “tukilitumia kwa uhalali Neno la Kweli” (ktk 2Timotheo 2:15).
Neno moja ambalo limekaziwa (tena kwa mkazo mkubwa kabisa) ni neno “ninyi”. Hebu soma mstari wote kwa sauti, ukipaza sauti unapotamka neno “ninyi”. Je, sasa unaweza kuelewa maana yake? Je, sasa unaona hekima na akili ya Ukristo? Je, sasa unaona wazi kwa nini neno “ninyi” liwe ndiyo neno kuu? Hebu tuchunguze kwa upana zaidi mpaka tupate mahali panapofaa kushika na kufahamu.
Kuna namna mbili za maisha ambazo wanadamu wanaweza kuzifuata. Watu wengi hawatambui injili, lakini njia moja ni mtindo wa maisha wa Shetani, na njia nyingine ni mtindo wa maisha wa Mwokozi. Njia moja ndiyo mtindo wa maisha wa kawaida wa mwenye dhambi (na yawezekana kuwa ndiyo njia pekee ya maisha ambayo mtu aliyepotea anaweza kuishi), na ile nyingine ni mtindo wa maisha wa kawaida kabisa wa mtakatifu mtendaji. Nayatumia maneno haya kwa makini na uangalifu sana, kwa sababu mtu yeyote aliyeokoka anaweza wakati wowote kurejelea mtindo wa maisha wa Shetani.
Ngoja nichore mchoro utakaotuwezesha kuona vizuri mitindo hii ya kinyume ya maisha.
179
Nauita mtindo huu wa maisha wa “kutoka nje kuingia ndani”. Haya ndiyo maisha yasiyoepukika, ya lazima ambayo ni kawaida kwa kila mtu ambaye hajawahi kuzaliwa na Mungu. Anaishi kama sponji – siku zote ananyonya au kufyonza vitu kutoka katika mazingira yake kwa ajili ya faida yake binafsi. Huo ndiyo mtindo wa maisha wa Shetani. Hilo ndilo lililomfanya Shetani kuwa Shetani, kule kusema, “Nita”. Alirudia hilo tena na tena, akihamisha imani yake kutoka kwa Mungu mpaka kuwa kwake mwenyewe. Hiyo ndiyo tafsiri ifaayo ya dhambi – “Ubinafsi”. Dhambi ni “mkunjo binafsi” wa maisha unaomfanya kila mwanadamu kugeuzia kila kitu ndani yake mwenyewe. Dhambi ni jitihada za mwanadamu kutafuta maana na utoshelevu katika maisha kwa ajili yake binafsi na ndani yake mwenyewe – pasipo Mungu.
Sasa, ni lazima tukiri – japo inasikitisha – kwamba, mtu aliyezaliwa mara ya pili anaweza pia kurejea mpaka kwenye mtindo huo wa maisha. Kwa kuwa alichukua “mwili” na kuingia nao katika maisha yake mapya ndani ya Kristo, wakati wowote anaweza
180
kujiamini mwenyewe na kutafuta kujinufaisha badala ya kumwamini Kristo na kuishi kwa ajili ya utukufu wa Mungu. Wakati Mkristo anapoishi kwa ubinafsi, anatumbukia katika mojawapo ya makundi mawili. Anaingia katika kundi la kuishi “kwa ubinafsi” au katika maisha ya “kujiponya”. Kila kitu anachofanya kinamtia katika hali ngumu ya kuishi kwa ajili ya faida yake binafsi au kwa ajili ya kujiponya. Hata kama atasoma Biblia, aombe na kujaribu kumtumikia Mungu, atafanya hivyo kwa sababu fulani ya kibinafsi tu. Biblia inasema, hiyo ni hali “ya kimwili”.
Mtindo mwingine wa maisha unaweza kuonekana kwenye mchoro huu. Upande wa kushoto unamwakilisha Yesu na upande wa kulia ni mwamini aliyezaliwa mara ya pili.
Mtu aliyezaliwa mara ya pili anakuwa na mwenzi – Yesu Kristo. Huyu anakuwa amehamishia matumaini yake kutoka kwenye ubinafsi na juhudi binafsi, na kuyaweka kwa Kristo. Kumekuwepo na hali ya kuunganika na kuwasiliana kati yake na Kristo. Maisha ya Kristo yameingia ndani yake, na “kiini cha msimamo” ndani yake
181
kimehama kutoka kwake hadi kwa Kristo. Hii inaitwa “wokovu, kuongoka, kuzaliwa tena, kuzaliwa mara ya pili” kwa lugha ya Biblia na imani. Maneno hayo yote yanaonyesha muujiza kabisa wa Mungu ambao unamtikisa mwenye dhambi kutoka katika kiini chake cha utu na kumwondolea ubinafsi, na kumtia Bwana Yesu Kristo mtukufu katikati kabisa ya maisha yake badala ya yule nafsi aliyeingiliwa na Shetani, mwenye ubinafsi. Nasema tena, huu ni muujiza kamili wa Mungu! Watu ambao hawajaokoka siku zote hawataelewa vizuri kuzaliwa mara ya pili ni kitu gani. Wao wanafikiri ni mwanzo mpya tu au kuupuuza kwamba ni ushika dini wa kupindukia. Swali la kipuuzi: Je, mtu ambaye hajazaliwa, anaweza kweli kuelewa maisha ya mwanadamu?
Mchoro wa pili unaonesha picha ya mtindo wa maisha tunaweza kuuita “kutoka ndani kwenda nje” ambao ni mtindo wa maisha wa Mungu Mwenyewe. Yesu “alijitoa mwenyewe kwa ajili yetu” na hapo akatuonyesha jinsi Mungu anavyofanya kazi kikawaida kabisa. Na Mkristo mtendaji huishi katika mahusiano ya imani na Yesu Kristo, siku zote akipokea uwezo ule wa kushangaza sana wa maisha ya kweli kabisa ya imani ya kweli. Hayo yote hupitia kwake na kumtosheleza yeye, na kutoka na kumwendea mwingine pia.
Sasa, hebu tusome tena ule mstari wetu. “Kwa kuwa sasa twaishi, ikiwa NINYI mnasimama imara katika Bwana.” Wakristo wengine hawaelewi vizuri mstari huu, kwa hiyo wanafikiri hivi:
182
“Ninaishi kama ninaomba vya kutosha.” Kama Mkristo, “ninaishi kama ninasoma Biblia kiasi cha kutosha.” Au “ninaishi ikiwa nimejitoa kabisa.” Au, “ninaishi kama mimi ni mwaminifu kabisa.” Au, “ninaishi kama ni mwema kiasi cha kutosha.” Au “ninaishi kama nimehamasika kabisa”. Au, “ninaishi kama ni mtendaji mwaminifu”. Lakini, hayo maneno yote mazuri sana yana ule uwezo uliofichika wa kugeuza maisha ya mtu huyo kurudi kwake na ndani yake tena. Huu ndiyo ule mkunjo uliofichika sana wa ubinafsi utokanao na mwili, na huwadanganya watu wengi sana waliokwisha okoka.
Yesu alisema hivi: “Yeye atakaye kuyaokoa maisha yake mwenyewe (yaani, maisha ya kujitakia faida, kujijali, kujihami) atayapoteza, lakini yeye atakayetoa maisha yake kwa ajili Yangu na Injili, atayaokoa.” Basi kumbe, maisha yanayosimuliwa huko nyuma ni maisha ya hasara, lakini yale maisha ya kujisahau mwenyewe, kujitoa mwenyewe, kutojijali mwenyewe katika maelezo ya pili ndiyo maisha yaliyo-okoka.
Sasa hebu tubadilishe michoro kidogo. Kama ilivyo kwa watu binafsi, ni kweli pia kwa makanisa. Hata makanisa pia yanaweza
183
kujielekea yenyewe, yakaishi kibinafsi au kichoyo kwa ajili ya faida yao wenyewe au usalama wao pamoja na kwamba yanakuwa katika kutafuta watu, ila, ni kwa faida yao wenyewe ya ndani!), badala ya kukuza na kumaliza kabisa njia zao za kujisaidia kufikia kiwango kwamba wanasukuma na daima kupima rasilmali za miujiza ya Mungu.
Mtindo wa maisha ya Kikristo ni kuishi kwa mahusiano, bila ubinafsi, kwa kujisahau wenyewe, kuwafikiria wengine kiasi kwamba Mkristo mmoja anaishi kweli ikiwa mwanafunzi wake anasimama imara katika Bwana. Paulo alisema, “Mimi ninaishi ikiwa ninyi mnasimama imara katika Bwana.” Basi, Mkristo anaishi katika, kwa njia ya, kwa ajili ya, na kupitia wanafunzi wake!
Huo si ndiyo mtindo wa Yesu kabisa, na jinsi ya kuifikia dunia? Yeye alijijenga Mwenyewe katika watu kumi na mbili kiasi kwamba, baada ya kipindi cha mafunzo cha miaka mitatu, alisema, “Kwaherini! Sasa maisha Yangu yako katika uangalizi wenu. Mimi ninaishi kama mtasimama imara!” Wapendwa wangu, hiyo ndiyo hali nzima ya kufanya watu kuwa wanafunzi.
Inasemekana kwamba “Mazoezi Humfanya Mtu Kukamilika”. Hii kanuni imesemwa kana kwamba ni kitu kisichobadilika, kisichoonekana, na kisichopingwa. Lakini mimi naomba niulize swali lenye maana. Tuseme kwamba kiwango kinachofanyiwa mazoezi si kikamilifu. Yawezekana kweli mazoezi yote duniani yatakayofanyika yakibadili hicho kuwa “kikamilifu”?
184
Bila shaka hapana! Ni hivi: Mazoezi hufanya kitu kikae daima; haimaanishi kwamba kinafanya kila kitu kuwa kamilifu. Hebu tufafanue na kutoa maana. Bila shaka inawezekana kwamba kanisa la Yesu Kristo limetenda kwa kufuata kanuni za kawaida na mapokeo kiasi kwamba “kujizoeza” kwake kwote kunazidi kulikita katika kiwango kisichokuwa kamilifu.
Kama dhana ya mafunzo haya ni sahihi, kwamba Agizo Kuu linawakilisha “Amri ya Kusonga Mbele” ya pekee iliyotolewa na Yesu Kristo kwa Kanisa Lake, na kama jinsi ya kuelewa Agizo hilo Kuu kulikotajwa katika mafunzo haya ni sahihi, basi mkakati wa kawaida kabisa wa kanisa la kawaida una makosa. Je, kujenga taasisi badala ya kujenga watu kumechukua nafasi kubwa katika kanisa la leo? Kumbuka kwamba maana ya “kufanya watu kuwa wanafunzi” inatokana na njia na agizo la Yesu. Kazi Kuu anayotoa inatajwa vizuri sana katika amri moja iliyoko katika Agizo Kuu: “Wafanyeni watu kuwa wanafunzi.” Na njia Yake inaonyeshwa katika mkakati Wake wa kuwashirikisha watu binafsi katika kikundi kidogo – watu kumi na mbili.
Hebu tuulize tena swali hili. Je, Ukristo unaowakilishwa sasa na kanisa lako ungeweza kusababisha Kitabu cha Matendo ya Mitume? Hili swali linatia aibu, kwa hiyo halina jibu la haraka. Au tuseme kwa njia nyingine. Je, Ukristo wa Kitabu cha Matendo ya Mitume ungevumilia hali iliyoko duniani kwa sasa – hali kwamba karibu nusu ya binadamu wote wanaokaa duniani bado hawajasikia
185
Injili (miaka elfu mbili na zaidi baada ya Kristo!) na kwamba 4/5 ya binadamu wote wamesikia Injili kijuu-juu tu? Je, Ukristo wa Kitabu cha Matendo ya Mitume ungevumilia hali iliyoko kanisani katika kila nchi iliyofikiwa duniani, inayosimuliwa katika kitabu cha Patrick Johnstone kiitwacho Operation World hivi: “Nchi hii inahitaji sana viongozi walioelimika?” Jibu linalotia aibu la maswali hayo yote ni “Hapana!” ya sauti kubwa sana. Sasa basi, hii mikakati na njia za sasa vitarekebisha huku kushindwa? Mpaka kitabu hiki kinapoandikwa, haijafanikiwa. Sawa. Si basi tuziache, na kwa ujasiri mkubwa tupitie tena ule mkakati wa kwanza wa Yesu, na tuone ni tofauti zipi zimetuondoa kwenye huo mkakati Wake?
Kuna maneno ya kawaida kabisa yanayotumiwa kanisani, ambayo tumeyadhania tu. Maneno hayo ni “kama Kristo”. Nadhani Wakristo karibu wote wangekiri kwamba lengo la maisha ya Kikristo ni kumfanya mwamini binafsi kuwa kama Kristo. Ukweli ni kwamba, hilo ndilo lengo la Mungu ambalo limetamkwa wazi wazi kwa ajili ya kila mtoto Wake. Katika Warumi 8:29 tunaona kwamba hilo limekuwa lengo na kusudi la Mungu siku zote kwamba “tufananishwe na mfano wa Mwana Wake,” au, kutufanya kama Kristo. Lakini tena, tumepungukiwa sana na kiwango cha Biblia katika kufafanua maana yake. Sisi tunafafanua tu na kutoa maelezo kwamba linahusiana na “tunda la Roho” katika Wagalatia 5:22, 23. Lakini, nani anaweza kupingana na maelezo hayo? Kama mtu akizaa tunda la Roho, tabia yake ya ndani ni kama ile ya Kristo bila shaka.
186
Lakini, hebu tufuate mfano wa matunda. Je, tunda lina jinsi ya ndani tu, au pia lina umbo la nje? Tutumie mfano huu. Mnunuzi wa matunda anapokwenda kutafuta malimau, anatafuta “hali ya ulimau”? Hapana. Yeye anatafuta tunda dogo la mviringo, lenye rangi ya manjano na ganda gumu kidogo. Yaani, limau lina umbo lake halisi la nje, lenye kueleweka, ambalo ni tofauti na umbo la boga, embe au ndizi. Pendekezo langu ni kwamba, tunda la Roho ni mwanzo mzuri katika jitihada za kuwafafanua Wakristo. Je, kuwa kama Kristo kuna umbo la nje pamoja na jinsi ya ndani?
Ngoja niliseme vizuri kwa sentensi moja tu: hutaweza kufanya kitu chochote kitakachozidi lengo lako la kuwa kama Kristo kuliko kuwafundisha makundi ya watu kuishi katika umoja na Yesu Kristo kwa ndani, na kujiongeza, kujizidisha, na kuifikia dunia nzima kwa nje. Maneno muhimu kimkakati ni “kufundisha,” (kwa kutumia mkakati na mtaala uliotolewa na Yesu), “makundi” (kwa kufuata ukubwa wa kikundi uliotolewa na Yesu), “muungano au umoja” (kwa njia hiyo, kufanya maisha ya Kristo, huduma na motisha kuwa vyetu), “kujiongeza na kujizidisha” (ambalo ni jukumu la kila mtoto wa Mungu) na “kuifikia dunia nzima” (ambayo ni kama lengo la kila saa kwa ajili ya kila mtoto wa Mungu). Na hayo yote yataamua mikakati tutakayotumia kufanikisha hilo lengo.
Katika muda mtakatifu sana kihistoria unaotajwa na Yohana 19:30, Yesu alisema neno moja ambalo pengine ndiyo la maana kuliko yote yaliyowahi kusemwa. Neno lenyewe ni tetelestai,
187
“imekwisha” au “ni tayari”. Kazi iliyokuwa imekwisha na kukamilika wakati huo ni kazi ya ukombozi, neno moja linalojumlisha kila kitu ambacho Mungu amekifanya ili kuwaokoa wenye dhambi kabisa.
Yesu analitumia tena neno hilo katika Yohana 17:4. “Nimekutukuza hapa duniani, nimemaliza kazi uliyonipa kuifanya.” Je, Yesu alikuwa amemaliza kazi gani hapa? Wasomi wengi wanasema kwamba tamko hilo pia linahusiana na kazi ya ukombozi ambayo Yesu aliikamilisha pale msalabani, lakini sidhani. Yesu anatumia neno la wakati uliopita, na msalaba ulikuwa bado mbele Yake! Hapa hakuwa anasema kuhusu kazi ya ukombozi, bali kazi ya uzalishaji. Hapa, utaratibu Wake wote wa mafunzo kwa ajili ya watu Wake ulikuwa umekamilika. Kumbe Yesu alikuja duniani kufanya na kukamilisha kazi mbili muhimu sana: Ukombozi na uzalishaji. Bila kazi ya ukombozi iliyokamilishwa na Kristo kufa msalabani, kusingekuwa na kitu chochote cha kuzalishwa, lakini tena, bila kazi ya kuzalishwa kupitia kuongezeka kwa Wakristo, kazi ya ukombozi ingejulikana kidogo tu, au kwa sehemu tu, au kwa hali ya chini sana (ambayo ndiyo hali ya dunia ya leo, na hata ya kanisa la leo).
Hapa tena, swali muhimu. Nini maana ya “kuzalisha” kwa maana ya Agano Jipya? Ni watu wangapi wanaotazamiwa kuzalisha, na wanatazamiwa kuzalisha kiasi gani? Je, uzalishaji huo ni kufyatua tu (kiwango cha kuvuna roho, au kuwaleta wenye dhambi kwa Kristo) au ni kitu kinachotakiwa kusababisha maongezeko? Kama ni
188
maongezeko, yawe ya ukubwa gani? Na je, malengo halali katika hili yafikiwe vipi? Hapa tena, mbinu na njia ya Yesu viwe mwongozo wetu.
Hebu tuchukue mfano mmoja ili tuuchunguze kwa haraka. Je, Yesu alifuata mfano gani katika kuzalisha? Je, alizalishaje watu watakaowazidisha wengine? Je, aliwezaje kusababisha mtazamo na nia katika watu kumi na mbili uliopelekea dunia nzima kuguswa mpaka sehemu za mwisho kabisa za dunia ya wakati Wake katika kipindi cha miaka sitini tu baada ya kifo Chake? Soma tena sentensi hii ya mwisho na uiruhusu kweli yake iingie katika akili zako. Ruhusu swali lake lisisimue moyo wako? Ilikuwaje? Yeye aliwezaje? Aliwezaje kusababisha mtazamo na nia? Tena, katika watu kumi na mbili!!?? Ambavyo vilipelekea dunia nzima kufikiwa? Mpaka miisho ya dunia iliyojulikana siku zile? Katika kipindi cha miaka sitini tu baada ya kifo Chake? Yeye hakuwa na televisheni, uchangishaji wa fedha, simu, njia zozote za mawasiliano ya kisasa. Yeye alitumia mbinu ya mtu kumwambia mtu! Vipi? Ilikuwaje? Ilitokeaje? Hakuna chochote katika mpango Wake kilichotegemea watu wengi. Hakuna chochote katika mpango Wake kilichotegemea mahubiri (japo aliwasiliana na watu wengi kutoa huduma, kufundisha, na kuibua wanafunzi wa baadaye). Hakuna chochote katika mpango Wake kilichokuwa taasisi (na hapa tunachosema ni ukweli tu, si kwamba tunafanya tathmimi ya taasisi). Hakuna
189
chochote katika mpango Wake kilichojengwa kwenye kwenda kanisani (japo Mwenyewe alihudhuria kanisa kwa uaminifu).
Sasa basi MKAKATI WAKE ULIKUWA NINI? ALITUMIA MBINU GANI? ALITUMIA NJIA GANI?
Pengine tutapata dokezo kwa kutazama orodha za wale watu aliowaita “mitume” kama zinavyoonekana katika Biblia. Hebu tuseme kwanza kabisa kwamba Yeye aliwafundisha ili awatume mbali Naye, si ili aongeze makundi ya watu mahali alipokuwepo. Huu mkakati haufanani kabisa na kanisa la leo hata kidogo tu, ambalo lina tabia ya kutathmini kufanikiwa kwake (na mafanikio ya viongozi wake) kwa kawaida kupitia kipimo. Orodha zile nne za Mitume zinapatikana katika Mathayo 10, Marko 3, Luka 6 na Matendo 1. Hizo orodha peke yake zinapaswa kusababisha mafunzo mengi sana. Kuna masomo yasiyoelezeka na ya milele kutokana na kujifunza hizo orodha tena na tena. Tuzitazame hapa.
Mathayo Marko Luka Matendo
Simoni (aitwaye Petro) Simoni (aitwaye Petro) Simoni (aitwaye Petro) Petro
Andrea Yakobo wa Zebedayo Andrea Yohana
Yakobo wa Zebedayo Yohana Yakobo Yakobo
Yohana Andrea Yohana Andrea
Filipo Filipo Filipo Filipo
190
Batolomayo Batolomayo Batolomayo Tomaso
Tomaso Matayo Matayo Batolomayo
Matayo Tomaso Tomaso Matayo
Yakobo wa Alfayo Yakobo wa Alfayo Yakobo wa Alfayo Yakobo wa Alfayo
Tadayo Tadayo Simoni Mzelote Simoni Mzelote
Simoni Mzelote Simoni Mzelote Yuda wa Yakobo Yuda wa Yakobo
Yuda Iskariote Yuda Iskariote Yuda Iskariote
Ona yaliyo dhahiri hapa. Jina lile lile linatokea mwanzo kwenye kila orodha. Labda tuseme hivi, ni mtu yule yule, ingawa jina halifanani kila mahali. Kwanza, “Simoni Petro” halafu “Petro”. Turekebishe kidogo tena. Ni mtu yule yule – lakini ni dhahiri pia kwamba si mtu yule yule! Safari ya kuhama toka kwa “Simoni” mwenye kutawala, hadi kufikia kwa “Petro” mwenye kutawala ni somo kubwa sana kuhusu mkakati, mbinu, njia na utaratibu wa Yesu
191
katika kuwajenga wanafunzi. Je, hilo tu si ndiyo amri pekee iliyoko katika Agizo Kuu Lake alilotupa sisi (yaani, kuwajenga wanafunzi)? Kama ndivyo, basi tunatakiwa kufuata kwa makini sana na kwa kiasi tunachoweza mkakati, mbinu, njia na utaratibu wa Yesu (la sivyo, tutazamie matokeo tofauti – ambayo kwa bahati mbaya, ndivyo imekuwa katika kanisa la siku hizi). Ni mafunzo yenye maana sana kufuatilia tu ule utartatibu wa mafunzo ambao Yesu aliupitia kwa ajili ya Simoni Petro peke yake. Kama mafungu yale yenye kueleza jinsi Yesu na Petro walivyokutana, walivyozungumza na walivyofundishana, na kama yatakuwa ndiyo kiwango kwa ajili ya kujenga wanafunzi katika kanisa la siku hizi, basi ni rahisi kabisa kuona kwa nini tunateseka na hali ya kutokuwa na matokeo yafaayo (yaani, kuwa na Wakristo ambao hawajajengwa na kuwa na dunia ambayo kwa sehemu kubwa haijafikiwa). Ingewezekana kila Mkristo ajifunze somo hili ingekuwa vizuri sana. Kutazama utaratibu ambao kwa huo Yesu alimaliza “Simoni” (jina lake kabla hajaokoka, lenye kuonyesha hali yake ya kimwili) na kumwibua “Petro” (jina lake linalotumiwa kikawaida katika Kitabu cha Matendo) ni kitu kinachofungua macho ya mtu yeyote anayetamani kujua njia ya Yesu katika kuwajenga wanafunzi.
Unapotazama mstari wa pili kwenye ile orodha, utaona kwamba majina hayafanani. Ndivyo ilivyo kwa mstari wa tatu na wa nne. Lakini –– katika mstari wa tano jina ni lile lile. Hii ni muhimu ili kuelewa mkakati wa mafunzo aliotumia Yesu. Mstari wa sita
192
hauna jina moja, wala wa saba, wala wa nane. Lakini –tena – katika mstari wa tisa jina ni lile lile moja. Mstari wa kumi una majina tofauti, na wa kumi na moja, na wa kumi na mbili (kama utajaza nafasi iliyoachwa wazi na kifo cha Yuda Iskariote kwa kuandika jina la mtu aliyechaguliwa kumrithi, yaani Matiya).
Pengine mpaka hapo tumeanza kuona njia ya msingi kabisa iliyotumiwa na Yesu katika kujenga wanafunzi wenye maono ya dunia nzima, wenye uwezo wa kuigusa dunia nzima, na wenye kuzalisha wanaojiongeza kama wao wenyewe. Tunajua bila shaka yoyote kwamba mkakati wa Yesu ulikuwa umejengwa kwenye kundi dogo la watu kumi na mbili. Pia tunajua kwamba Yesu aliweka “mayai” Yake yote katika hicho “kikapu” Chake kidogo sana. Mpango Wake wote kwa ajili ya kuigusa na kuifikia dunia ulikuwa umewekwa katika mikono (na uzalishaji) ya watu kumi na mbili! Tena, orodha ya Mitume inaonyesha pia njia Yake katika kuwajenga watu hao. Bila shaka Yeye (na ni dhahiri ukitazama tu) aliwagawa watu Wake hao kumi na mbili katika makundi matatu yenye kulingana, yenye watu wanne kila moja, na kuweka kiongozi kwa ajili ya kila kundi. Tuna ushahidi gani kuhusu hili? Mbona ni mkubwa tu ushahidi huo? Haiwezi kuwa ni bahati au bahati mbaya. Watu wote katika kundi la kwanza (na hao tu) ndiyo walikuwa wafuasi wa Yohana Mbatizaji waliokuja kumfuata Yesu kwa sababu ya kutiwa moyo na kiongozi wao. Hao watu wote katika kundi la kwanza ni watu wenye uwezo na machachari, kama Simoni Petro,
193
kiongozi wao. Yakobo na Yohana waliitwa “Wana wa Ngurumo” na Yesu Mwenyewe! Kitabia walikuwa kama ngurumo inayotaka kuanza kazi. Andrea bila shaka ndiye mwenye uwezo mkubwa kuliko tunavyofikiri kwa kawaida. Yeye ndiye alikuwa mishenari wa kwanza kufanya kazi nyumbani (ktk Yohana 1:40-42), mtenda kazi kwa ajili ya vijana na kwa ajili ya jamii (ktk Yohana 6:8, 9), na ndiye alikuwa mishenari wa kwanza kufanya kazi nje ya nyumbani (ktk Yohana 12:20-22). Haiwezekani kwamba mtu mpole aliyezubaa angeweza kufanikisha mambo yote hayo ambayo yanatajwa katika maandiko hayo! Basi, hawa walikuwa watu wenye uwezo katika utendaji.
Kundi la pili linaongozwa na Mtume Filipo, ambaye katika Injili anaonekana kuwa mtu mfikiriaji, au mwanafalsafa. Na kila mtu katika kundi lake alikuwa hivyo hivyo – Tomaso “mwenye mashaka” na Lawi Matayo, aliyeandika Injili yenye mafundisho ya hali ya juu sana ya Yesu. Ona kwamba Yesu hakumweka mwanafalsafa kuwa kiongozi mkuu katika kundi Lake maana asingefanikisha chochote! Kwa kawaida, watu aina hiyo ni wenye mashaka sana, wenye maswali mengi, watafiti wakuu, wapinzani wakuu, wepesi kuzembea na ni wachangiaji wakubwa kuhusu utume wa Kikristo. Lakini, hawawezi kuwa viongozi wa kundi. Lakini, tusipuuze umuhimu na ulazima wa watu hawa tunapotafakari hoja hii. Ni kwamba tunaona tena jambo lingine kubwa na la maana sana katika mkakati wa Yesu.
194
Sasa – kaa tayari. Kundi la tatu lilikuwa na wanamapinduzi wa kisiasa tu! Kiongozi wao – Yakobo mwana wa Alfayo – pengine ndiye alikuwa mpole kuliko wote katika kundi hilo! Pengine jina la pili la Yuda, “Iskariote” laweza kutokana na kisu kidogo kilichokuwa kinabebwa na baadhi ya wanamapinduzi waliokuwa wamejizatiti kukitumia kumwua afisa yeyote wa Kirumi ambaye wangefanikiwa kumpata katika kundi la watu (au popote pale ikiwezekana). Hili ni jambo la ajabu. Kuna ushahidi mkubwa tu kwamba Yakobo na Matayo (ambao wote wanaitwa “mwana wa Alfayo”) walikuwa ndugu. Je, hili linakusisimua kiasi? Mbona mmoja (Matayo) akawa msaliti kwa kuunga mkono Rumi, akitoa maisha yake kulipisha kodi toka kwa Wayahudi kwa ajili ya serikali ya Kirumi, ambayo waliichukia? Mbona yule mwingine (Yakobo) akawa mzalendo hodari wa Kiyahudi? Je, kuna aliyeitikia maoni ya mwenzake ya kupita kiasi? Je, uzalendo wa Yakobo ulimfanya Matayo aisogelee Rumi? Au je, usaliti wa Matayo ulimfanya Yakobo kuingia katika matendo ya kisiasa na kimapinduzi? Au? Hoja yoyote tutakayotoa inadhoofishwa na ukimya wa Maandiko, lakini swali hilo linaibua maswali na fikira sana. Yule anayeitwa “Mzelote” anatambulishwa kwa jina lake na chama cha siasa kilichokuwa cha kizalendo sana, chenye uasi na ukatili sana kilichoitwa hivyo hivyo. Je, ulijua kwamba kama Simoni Mzetole angekutana na Matayo mtoza ushuru katika hali “ya kawaida” tu, angemwua upesi sana? Ndiyo maana nasema, Muujiza Mkuu wa Yesu haukuwa kuwalisha watu wenye
195
njaa kwa kuongeza chakula, au kuwaponya wagonjwa, au hata kufufua wafu. Kwangu mimi, Muujiza Wake Mkuu ulikuwa ni kujenga – kwa kutumia vifaa “visivyowezekana” – kundi la Watu Kumi na Mbili ambao wangetikisa dunia kwa Uzalishaji wa Kiroho hadi miisho ya dunia ya siku zile! Na, kama kanisa lisingebadilisha mkakati wa Yesu (wa kujenga watu) na kuweka kitu mbadala kinachowafaa wao, ambacho hakika kinatokana na chanzo kingine (kujenga taasisi zenye kujijali kwa ndani), mawimbi hayo yaliyoanzishwa na wanafunzi yangekuwa yanaitikisa dunia mpaka miisho yake hadi leo, na kuendelea kufanya hivyo bila kuzuiwa wala kupungua hadi mwisho wa dahari.
Charlie Chaplin – mchekeshaji maarufu sana duniani – alipokuwa hai, yalifanyika mashindano ya “Wanaofanana na Charlie Chaplina” huko nchi ya Monaco. Bwana Chaplin alisafiri mpaka huko, akaingia kwenye shindano hilo pasipo kujulikana, na akawa mshindi wa tatu! Kweli najiuliza Yesu wa kweli angeshika nafasi gani katika kanisa la siku hizi kama yangefanyika mashindano ya “Wanaofanana na Kristo”???
Usielewe hii sura vibaya. Hakuna amri ya wazi inayotulazimisha sisi kufuata mpango wa vikundi huo. Lakini, busara ya kawaida tu ingeshauri kwamba, “kama Kristo” maana yake “kama Kristo”. Hilo linaonekana jepesi kabisa, lakini ukweli wake umeshindwa kupatikana katika kanisa. Ukubwa wa kundi la Yesu unaonekana kuwa wa busara sana, pamoja na migawanyo yake,
196
maana inatoa nafasi ya uwajibikaji, mgawanyo wa kazi, ushirika na kadhalika. Lakini hakika, makundi hayo hayakuwa yamefungwa na yasiyoweza kubadilika. Matokeo yanathibitisha kwamba Yesu alikuwa Bingwa wa jinsi vikundi vinavyofanya kazi na kushirikiana. Mbona sisi tusiwe na hekima ya kufanya hivyo? Je, kweli sisi tuna hekima tusipofanya hivyo?
Narudia tena: wewe … na wewe … na wewe … hamtafanya kitu kama Kristo katika maisha yenu yote kitakachozidi kuwafundisha watu binafsi kwa kufuata mkakati wa Yesu (yaani, “kuwafanya watu kuwa wanafunzi”) ili kuifikia na kuigusa dunia nzima.
Je, wakati haujafika wa sisi kukagua shughuli zetu zote ili kuhakikisha kwamba tunatimiza lile Agizo la Yesu kikamilifu, kwa uzito na kwa mtiririko wa utaratibu unaofaa?
197
Sura Ya 8
Jinsi Kiwango Hiki Kifanyavyo Kazi Kanisani
“Lakini kila mmoja wetu alipewa neema kwa kadiri ya kipimo cha kipawa chake Kristo. Hivyo husema, ‘Alipopaa juu aliteka mateka, akawapa wanadamu vipawa.’ Basi neno hilo ‘Alipaa’, maana yake nini kama siyo kusema kwamba yeye naye alishuka mpaka pande zilizo chini za nchi? Naye aliyeshuka ndiye yeye aliyepaa juu sana kupita mbingu zote, ili avijaze vitu vyote. Naye alitoa wengine kuwa mitume, na wengine kuwa manabii; na wengine kuwa wainjilisti na wengine kuwa wachungaji na waalimu; kwa kusudi la kuwakamilisha watakatifu, hata kazi ya huduma itendeke, hata mwili wa Kristo ujengwe; hata na sisi sote tutakapoufikia umoja wa imani na kumfahamu sana Mwana wa Mungu, hata kuwa mtu mkamilifu, hata kufika kwenye cheo cha kimo cha utimilifu wa Kristo; ili tusiwe tena watoto wachanga, tukitupwa huku na huku, na kuchukuliwa na kila upepo wa elimu, kwa hila ya watu, kwa ujanja, tukizifuata njia za udanganyifu.”
Waefeso 4:7-14
198
Je, Ukristo ambao sasa unawakilishwa kanisani kwenu ungesababisha Kitabu cha Matendo ya Mitume? Hili swali ni kali na lenye uzito. Kuwa wazi ni kutoa jibu moja tu: Hapana! Basi, nini tofauti kati ya Ukristo uliosababisha Kitabu cha Matendo ya Mitume, na huu mbovu wa ajabu kabisa unaopatikana na kuonekana karibu katika kila kanisa?
Katika kanisa la kwanza, walifuata mfano wa Yesu katika kuwajenga watu muhimu, lakini siku hizi sisi tunahesabu watu katika makundi. Tuna kawaida ya kupima mafanikio kwa kutazama ukubwa na wingi wa watu. Tena, mfano tunaofuata sisi sana sana ni wa kusafisha wenye dhambi ili waishi maisha safi. Wao walifuata mfano wa kuwafanya watakatifu kuwa wanafunzi kwa ajili ya kuifikia na kuigusa dunia, ingawa pamoja na hayo, maisha masafi hayakupungua. Tunachofanya sisi ni kama kuwaweka walio-okoka katika sanduku la kuwahifadhi liitwalo “usalama wa milele” badala ya kila mwamini kuwekeza maisha yake yote katika watu wengine waliokolewa ili kutengeneza wazalishaji wenye maono ya dunia nzima, wenye kuigusa dunia nzima na kuifikia, ambao nao watawazaa wengine wenye maono ya dunia nzima, wenye kuigusa dunia nzima na kuifikia, ambao nao watawazaa wengine …..
Sasa – tofauti kati ya Ukristo wa mwaka wa 4BK na Ukristo wa mwaka wa 2008BK? Je, Yesu amebadilika? Hapana. Tunamwabudu na kumtumikia Yesu yule yule waliyemjua wao. Je, Roho Mtakatifu ni mwingine? Hapana. Roho Mtakatifu
199
tunayehusiana siku za leo ni yule yule “aliyekuja” kikamilifu kabisa katika uwezo wa ukombozi Siku ile ya Pentekoste. Je, Biblia ni tofauti? Hapa, uwe makini kidogo, kwa sababu jibu sahihi ni “ndiyo”. Wao hawakuwa na Biblia kamili. Walikuwa ndiyo wanamalizia kuandika Biblia kupitia shughuli zilizoandikwa katika Kitabu cha Matendo. Kwa hiyo, kama kuna faida ya kuwa na Biblia kamili iko kwetu, si kwao. Je, kulikuwa na tofauti katika teknolojia au mafanikio kwa habari ya usafiri? Aah! Swali gani tena hilo? Sisi tuko vizuri katika kila hali – wao hawakuwa vizuri katika kila hali. Mungu alikuwa ameandaa amani ya dunia nzima kupitia nguvu za kijeshi za Kirumi na akatayarisha mtandao wa barabara zilizofika kila mahali ambao ulijengwa na Warumi, lakini hayo yalikuwa machache sana ukilinganisha na manufaa ya leo tuliyo nayo sisi. Wao hawakuwa na simu, barua pepe, vipindi vya televisheni ili kuchangisha fedha – wao walikuwa na “mwambie mtu”. Hawakuwa na vyombo lakini walikuwa na KWELI MUHIMU! Lakini, na sisi pia tunazo! Sasa, kilichowawezesha wao kuigusa dunia nzima iliyojulikana wakati ule katika kipindi kifupi sana, wakati leo hii kiasi cha mbili kwa tano cha binadamu wote hakijasikia kabisa Injili, na kiasi kingine cha mbili kwa tano cha dunia nzima kimepata Injili kwa hali ya chini sana, ni nini? Halafu, idadi ya moja kwa tano iliyobakia ina uwezo mkubwa sana katika kila hali kuliko waliokuwa nao Kanisa la kwanza. Lakini, kwa faida gani? Je, tofauti kati yetu na wao ni ya kujitolea? Kuna ambao watatoa hoja ndefu na kwa sauti kubwa kabisa kwamba hiyo
200
ndiyo tofauti, lakini, si hiyo tu. Katika kanisa la kwanza, watu waliokuwa wamejitoa si wengi kuliko Mkristo wa kawaida wa siku hizi ambaye anahudhuria ibada kwa uaminifu mara tatu kwa juma pamoja na siku maalum – lakini bado hana ushawishi wa aina yoyote juu ya watu kama bilioni 2 nukta tatu ambao hawajasikia habari za Kristo siku hizi. Ukristo wa Kitabu cha Matendo usingeweza kuvumilia takwimu za jinsi hii, lakini kanisa la leo lina uwezo wa kuendelea katika shughuli zake zote za kawaida bila hata ya kujali hali ya kushindwa kwake iliyo kuu.
Sasa – nini tofauti basi kati ya Ukristo wa Iskanda, Rufo, Trofena na Andoniko wa karne ya kwanza, na ule wa Jo, Suzie, Samweli na Edwadi wa karne yetu? Mimi nasema hivi: Tofauti ni ya mkakati peke yake. Wenzetu walitenda kazi kwa kufuata mkakati tofauti na ule tunaotumia sisi!
Angalia mfano huu, ambao ni picha ya desturi ya taasisi ya makanisa ya leo. Fikiri kuhusu basi lenye kusafiri kwenda mahali, ambalo linabeba watu njiani. Kanisa ndiyo mfano wa hilo basi. Mchungaji ni kama dereva wa hilo basi. Dereva (yaani mchungaji) anawakaribisha abiria wapande kwenye basi (na yawezekana wakakaribishwa na abiria wenzao pia). Wanaketi na husimama ili kushughulikia maswala muhimu tu. Dereva (yaani mchungaji) anatoa maelezo kuhusu vivutio vinavyoonekana njiani wakati akiwaendesha abiria wasiofanya chochote, wenye kutazama (na pengine waliolala usingizi) kuelekea mahali walipokubaliana kwenda. Abiria wa
201
kawaida anavumilia hiyo safari, lakini kamwe hatafuti abiria mwingine, na mara nyingi hashuhudii kuhusu jinsi anavyofurahia basi lile, na kampuni ya hilo basi, na njia linakopitia, wala safari linalofanya. Yaani kwa kifupi ni kwamba, mafanikio ya safari yenyewe yako katika uwezo na ubora wa hilo basi, na utendaji wa dereva wake. Hii ni tofauti kubwa sana sana na ule Ukristo wa Bwana Yesu pamoja na wanafunzi wa kwanza. Ukristo wa Kitabu cha Matendo ulikuwa ni kitu cha watu (ktk Matendo 1:8; 8:1 na 4); haukuwa kitu cha mhubiri au kitu cha taasisi fulani.
Eneo la dunia liitwalo North Pole lina kiwango kikubwa sana cha barafu. Wanasayansi wanatuambia kwamba barafu hiyo ikitokea kuyeyuka basi sehemu kubwa ya dunia itajaa maji. Wakristo wengine wanaweza kuitwa “mali ya Mungu iliyoganda”. Kama hao wote watayeyuka mbele za Mungu na kupata joto la kutambua maono Yake, makusudi Yake, malengo Yake, na mkakati Wake, “dunia yote ingejaa maarifa ya Bwana, kama maji yajazavyo bahari.”
Mfano wa Mungu aliotoa ili Kanisa Lake liufuate unaelezwa kwa uwazi kabisa katika Waefeso 4:7-14. Mada ya jumla ya fungu hili ni karama za kiroho, lakini karama zinazotajwa hapa si zile za aina mbalimbali ambazo kwa kawaida hutajwa katika Agano Jipya. Orodha ya karama katika Warumi 12, 1Wakorinto 12 na 14 na 1Petro 4 ziko tofauti. Hizo ni matoleo kutoka mbinguni zinazowekwa katika waamini na Roho Mtakatifu. Karama hizi tunazotaja hapa sasa ni viongozi wenye vipawa ambao Roho Mtakatifu huwatoa kwa Kanisa
202
Lake kwa ajili ya makusudi maalum ya jumla katika kanisa, na kwa ajili ya kufanikisha au kutimiza malengo maalum.
Hebu nitoe muhtasari utakaotuwezesha kuona kwa ujumla fungu zima (yaani, Waefeso 4:7-14). Fungu hili linatuonyesha mtoaji wa hizo karama, karama zenyewe (yaani, watu waliopewa vipawa), na malengo ya karama hizo kutolewa.
MTOAJI KARAMA
I. Mtoaji Anatajwa – mstari 8-10
Kweli kuu tatu zinatolewa kuhusu Yesu:
A. Alishuka, ms. 9, 10.
B. Alipaa, ms. 8, 9, 10.
C. Yuko juu ya vyote, ms. 10b.
II. Karama Zenyewe (Watu) Zinaonyeshwa – mstari 11
Viongozi wenye vipawa wanne (au watano) wanatajwa:
A. “Mitume”
B. “Manabii”
C. “Wainjilisti”
D. “Wachungaji waalimu”
III. Malengo Ya Kutolewa Karama Yanatajwa – mstari 12, 13
A. Ili kupata viungo kwa ajili ya Mwili, ms. 12b.
B. Ili kuwezesha viungo katika Mwili, ms. 12a.
C. Ili kutumia viungo kupitia Mwili na zaidi, ms. 12-16.
203
Katika kile kipengele cha “Mtoaji Karama” ambacho ni mojawapo ya maandiko maarufu sana yenye kufafanua fundisho la Nafsi ya Kristo katika Agano Jipya, ona sheria moja inayojitokeza. Ingawa njia ya Shetani kwenda chini ni kupanda, njia ya Mungu kwenda juu ni kushuka. “Yeye ajiinuaye mwenyewe (kama Shetani) atashushwa, lakini yeye ajinyenyekezaye mwenyewe (kama Yesu) atainuliwa (kama Yesu).”
Hii orodha ya watu waliopewa vipawa (ktk mstari wa 11) inaweza kusababisha mafundisho na mawazo yasiyo na kikomo. Kwa mfano: Swali kuhusu zile karama mbili za kwanza ni hili: Je, zipo katika kanisa la siku hizi? “Mtume” kama nafasi rasmi iliweza kuwepo katika kanisa la kwanza tu kwa sababu sifa zake maalum zilizotakiwa (yaani, kumwona Yesu na kuwa pamoja Naye) hazipatikani kwa mwingine yeyote baada ya karne ya kwanza. Nafasi ya “nabii” inaonekana kuwa ya Agano la Kale tu. Pia, Waefeso 2:20 inasema kuhusu mitume na manabii kuwa “msingi” wa kanisa. Siku hizi, jengo hilo limekwisha panda sana! Kweli msingi ni wa muhimu, lakini, ukiwa katika nafasi yake tu, si katika kuta.
Ila, kufikiri hivyo sana kusikokuwa na faida kunaweza kutufanya tukose hoja kuu. Kuna kanuni ambayo imetajwa mara kwa mara, kwamba, “Mfuasi ni kama kiongozi wake”. Mfuasi atakuwa kama kiongozi wake (maneno ya Yesu Mwenyewe katika Luka 6:40). Basi, wakati Yesu alipotoa kwa Kanisa Lake viongozi wanne
204
wenye karama pekee na tofauti, bila shaka anatuambia waziwazi kile anachokusudia Kanisa Lake liwe.
MTUME
Neno “mtume” maana yake ni “mtu anayetumwa kuondoka”. Basi, anakusudia iwe hivyo kwa kanisa Lake lote (!!!), kwamba liwe ushirika wenye kwenda na kutuma waendao. Watu wengi hujiepusha na jukumu la kwenda kwa kubakia kwenye wazo la kutuma, lakini hii haiwezi kupata kibali katika Agano Jipya. Vipi kanisa la siku hizi? Limejaa watu wanaokuja – watu ambao Ukristo wao unaelezwa kwa uaminifu wao katika kuja na kutumika. Neno “mtume” kama lilivyo hutuambia ni kwa nini Yesu aliwachagua hao (ktk Waefeso 1:3; Matendo 1:3). Lile neno “aliwachagua” linamaanisha kwamba Yesu aliwachagua “kwa ajili Yake Mwenyewe”, wala si kwa ajili ya kukua kwao, afya yao, mali yao, furaha yao, au hata utoshelevu wao. Mkazo usiofaa umesababisha kuundwa “Ukristo unaofurahisha wateja”, ambao ni kusoma vibaya Agano Jipya. Agano Jipya linamwonyesha Mungu kuwa ndiye mteja, na sisi ndiyo watoshelezaji wa matakwa Yake. Ndugu aitwaye Jim Elliott aliomba kwa kumaanisha kabisa, hivi: “Ee Moto wa Mungu! Nifanye mimi kuwa ndiyo mafuta!” Je, Yesu alituchagua sisi kwa ajili gani? Ili twende mahali Yeye anapotaka sisi twende – “kuondoka” – siyo “kukaa” – ili tuwe, ili tuseme, na kufanya chochote Yeye anachotaka. Basi, lengo pekee lililo sahihi kwa ajili ya kila Mkristo lazima
205
lihusishe mkakati wa kuifikia miisho ya dunia. Tunawezaje kuona vikomo kwenye mkakati kama huo katika Kitabu cha Matendo? Walijaribu kuweka mipaka kwamba kiwe kitu cha mahali pamoja, kitu chao cha ndani, lakini Mungu alituma mateso yaliyowatawanya kama mbegu (ambalo ni neno linalotumiwa katika Matendo 8:1; 8:4 na katika 1Petro 1:1) kwenda nje na mbali mbali kabisa katika udongo mchanganyiko wa Dola ya Kirumi. Ee Mkristo – jihadhari, kwa sababu mateso makubwa sana ya siku zijazo yanakaribia kulijia kanisa la siku hizi. Uislamu wenye msimamo mkali na ukorofi umeanza kuivamia dunia, na kilichoko njiani ni kanisa maskini na dhaifu la Yesu Kristo. Maendeleo ya kiteknolojia na makufuru ya sayansi na ubinadamu vimezua watesaji kila mahali. Kwa hiyo, siku za Ukristo kukaa katika ngome yake salama kwa utulivu, zimekwisha. Utawanyiko mwingine wa Wakristo uko njiani. Na Mungu ndiye Mpanda Mbegu! Ni hivi: Ingawa sisi ni wagumu kwa hiari yetu kusikia kuhusu jukumu letu la kwenda, Mungu anamaanisha kabisa kwamba twende!
NABII
Neno “nabii” maana yake “mtangazaji” (pamoja na kwamba ni “mtabiri” wa ukweli). Nabii ni msema kweli, si msema kitu cha kupoza moyo. Nabii alikuwa “mtangazaji” au “mshuhuda”. Basi, Yesu alipotoa kwa Kanisa Lake manabii wenye vipawa, anachotuonyesha ni kwamba alikusudia kanisa Lake kuwa ushirika
206
wa watu wasiokoma, walio waaminifu siku zote, walio jasiri siku zote, wenye kuzungumza siku zote. “Waliokombolewa na Bwana na waseme hivyo.” Hii hutimiza makusudi kadhaa ya Mungu. Humkomaza msemaji, kwa sababu mtu yeyote atafuatilia ukiri aliotamka, hata kama ni ukiri gani. Humtukuza Mungu, kwa sababu anakaa ndani ya sifa na shuhuda za watu Wake. Na, hufikisha Injili kwa kila asikiaye. Mkristo asipime joto au mapigo ya moyo ya dunia kabla hajanena – la sivyo, hatasema kabisa! Kwanza kabisa, sisi husema kwa Mungu, na kuhusu Mungu, na kwa ajili ya Mungu. Basi, hatupaswi kunyamaza kimya kamwe. “Ninaamini, hivyo nimesema.” Manabii, wahubiri, waalimu na viongozi wa kanisa lazima waseme kwa ukamilifu, kwa uwazi na kwa ujasiri – na waamini wote vivyo hivyo!
MWINJILISTI
Neno “mwinjilisti” maana yake ni “msema mema,” yaani, mtu ambaye “anamsema vema” Yesu kwa watu, na watu kwa Yesu. Injili inakiri habari mbaya sana kuhusu Shetani na mbinu zake mbaya, mwanadamu na hali yake ya dhambi na utendaji wake, Mungu na itikio Lake takatifu kinyume cha dhambi, na kuzimu kama makazi ya mwisho kabisa ya mwenye dhambi anayejiona na kujifikiria mwenyewe. Lakini cha kusikitisha ni kwamba, kanisa limetangaza habari mbaya mara nyingi zaidi na kwa nguvu sana kuliko ambavyo limetangaza Habari Njema. Ujumbe mkuu na wenye
207
nguvu zaidi katika Maandiko unaitwa “Injili” – euaggelion – “Habari Njema”. Hakuna mtu aliyepokea habari njema kweli kweli mpaka ajisikie vizuri kuhusu Mungu, kuhusu Yesu, kuhusu Roho Mtakatifu, kuhusu yeye mwenyewe, kuhusu wokovu wake, kuhusu hali yake ya sasa na ya baadaye, na kuhusu matokeo ya mwisho kabisa ya mambo yote. Mungu analikusudia Kanisa Lake kuwa tukufu na lenye ushindi katika kueleza kwake habari njema.
MCHUNGAJI MWALIMU
Halafu neno “mchungaji mwalimu” linatoa kweli ya mwisho kuhusu kile ambacho Mungu anatazamia kwa Kanisa Lake. Neno “mchungaji” maana yake “mtunza mifugo” na linaeleza anakusudia watu Wake waongoze. Ili kuongoza, Mkristo lazima ajue kwa uwazi na kwa uhakika yeye ni nani, ana nini, anakwenda wapi, jinsi ya kufika aendako, kusudi lake leo na kila siku ni nini, na jinsi ya kufanikisha kazi yake. Mtu yeyote anayejua mambo hayo kwa uwazi na uhakika anaweza kumwongoza mtu mwingine. Neno “mwalimu” linaonyesha kwamba Yesu anakusudia Kanisa Lake kuwa ushirika wenye kueleza ukweli, kufundisha na kulisha. Na hii ndiyo kazi ya kila aaminiye. “Kwa njia zote” (ktk 1Wakor. 9:22) – neno la papo kwa papo, ushuhuda ulioandaliwa, mafundisho rasmi na mahubiri, ugawaji wa maandiko, vitabu, magazeti, barua ( na Mungu yuko juu sana kwa uandishi wa barua), kanda za sauti na video, redio na televisheni, kuonana uso kwa uso au kwa umbali – lengo la Mkristo
208
linatakiwa kuwa ni kushawishi, kugeuza, “kuwavuta baadhi” kwa shughuli zozote anazofanya.
Hizo ndizo karama zikionyeshwa; basi, kazi, wajibu na jinsi ya kanisa kuwa wazi na dhahiri kabisa.
MALENGO YA KUTOA KARAMA HIZI
KUPATA VIUNGO
Tunapaswa “kuujenga” Mwili wa Kristo kwa kutumia hawa watu wenye vipawa na wafuasi wao watakaopatikana. Hivyo, kiwango kipya cha kupata watu lazima kitumiwe na kanisa. Masharti yote ya kuwapata watu lazima yatumike mara moja na kanisa. Kila kitu katika “mkataba” wa Kikristo lazima kitamkwe na kukubalika tangu mwanzo kabisa – wakati wa kukata shauri – yaani, kujikana, kubeba msalaba (hayo ni masharti ya “pale pale mlangoni”, si nyongeza kwa kuwa mtu amekomaa), kuishi nje kama mtu alivyo ndani, kujisomea Biblia kwa ajili ya kujijenga na kwa ajili ya kutumika, kuabudu na maombi ya mapambano, na kadhalika. Na hayo hayawezi kufanyika sehemu ya maisha kwa mafunzo ya saa moja kwa juma, au masaa mawili, au matatu kwa juma.
Je, katika uinjilisti wetu, ni wapi penye kiwango na utendaji kwa ajili ya kumkataa kijana tajiri yule aliyekuwa anapenda mali yake? Kiwango hiki cha hali ya juu sana kilitumiwa na Yesu katika kumwondoa mtafutaji muungwana, wa dhati aliyekuwa anataka
209
kujua cha kufanya (hebu jisomee Mathayo 19:16-26 kwa makini sana). Tena ujue kwamba swali la huyu kijana – “Nifanye nini kizuri, ili niweze kuwa na uzima wa milele?” – Yesu aliulizwa mara mbili. Mwanasheria (“mtaalamu” wa Torati ya Musa) aliliuliza katika Luka 10:25 katika mantiki tofauti kabisa. Na hakuna wakati wowote ambapo Yesu alitoa jibu ambalo wengi wetu tungelihesabu kuwa ni “mpango wa wokovu unaofuata utaratibu”. Yeye aliweka “kipimo cha katikati” pale mwanzoni kabisa – penye mlango wa kuingilia!
Ni hivi: Neno “amini” ambalo linatumika kirahisi sana na sisi kueleza njia ya wokovu, ni muungano wa maneno mawili ambayo maana yake ni “kwa uzima”, au “kuishi kwa”. Unavyotenda ndivyo unavyoamini! Mengine yote ni mazungumzo tu ya kawaida kabisa, “si lolote si chochote”, maneno mazuri tu ambayo yamejaa “kelele na ghadhabu, yasiyo na maana yoyote ile”. Huu ni Ukristo wenye kujadili lakini hautendi. Ni Ukristo wenye “kujitukuza” bila ya kwenda, wenye “kufurahia” lakini usiotii, wenye kujitakasa wenyewe kwa ajili ya usafi lakini kamwe haujimimini wala kujitoa kwa ajili ya ushindi. Hujitokeza ili kujaza kanisa (Jumapili asubuhi) lakini haujimwagi ili kujaza na kugusa dunia mpaka pande za mwisho kabisa za nchi … Lazima tutaje waziwazi kama sharti la kuingia kwamba, Kuzaliwa Upya (kitu kinachofanywa na Mungu tu) lazima kufuatwe na Maisha Mapya) ambayo pia yanatendwa na kuwezeshwa na Mungu pia). Basi, tunahitaji kuwapata wanachama wapya katika kanisa la siku hizi, wanachama wenye kuelewa
210
mafunuo kamili ya Yesu. Kwa kawaida si inatakiwa mwenye kutia sahihi karatasi yoyote asome na kuelewa mkataba mzima kabla ya “kutia sahihi”?
KUWEZESHA VIUNGO
Halafu, kila mshirika anapaswa “kuwezeshwa” kwa ajili ya kazi yake binafsi ya “huduma” (ktk 4:12a). Sentensi hii ina neno moja pana sana na lenye mafafanuzi makubwa katika Agano Jipya. Ni neno “kuwakamilisha” ila, maana kamili ya neno hilo si rahisi kuipata. Kuna tafsiri moja ya Biblia inayosema kwamba hao watu wenye karama au vipawa wametolewa kwa kanisa ili “kuwawezesha” washirika. Nyingine inasema “kuwapa vitu vyote wanavyohitaji”. Kitu kimoja ni hakika kwa tafsiri yoyote ile: Wakristo wote – bila kukosa, bila kupendelewa, na bila kutengwa – wanapaswa kuwezeshwa hivyo, kupewa kila wanachohitaji. Mfumo wa taasisi yenye kutazama ndani ya kanisa la siku hizi ni kwamba, mchungaji ndiye mchezaji pekee kwenye jukwaa, na “walei – washirika” wanaachiwa kazi za hapa na pale kama wasaidizi wa jukwaani, wahusika na taa na walinzi. Mfumo huu lazima ubadilishwe mpaka ifikie mahali ambapo mchungaji atakuwa ndiye “mwezeshaji” wa watu, na watu wawe ndiyo watumishi. Kusudi la wazi kabisa lililotajwa hapa la kuwawezesha washirika ni ili kila Mkristo aingie katika “kazi ya huduma”. Ni hivi: Siku ile ulipo-okoka uliitwa kuingia katika huduma! Kanisa lingekuwa jeshi
211
kubwa, lenye ushindi sana, lenye kupenya, lenye kusonga mbele, lenye kuimba, na lenye kelele za shangwe kama wangejua hilo! Dada Eugenia Price alisema hivi: “Dhambi kuu kuliko zote ya kanisa la siku hizi ni kwamba, limefanikiwa kumfuga na kumdhoofisha yule Simba wa Yuda.” Tumezuia vitisho vyote, hatari yote na uwezekano wa kufia Ukristo visitokee katika Ukristo. Basi, michezo au tamasha za muziki ndiyo zenye kuweza kutoa changamoto, msisimko na hali ya kujali kuliko kusonga mbele kwa Kanisa la Yesu Kristo.
Neno “kuwezesha” au “kukamilisha” ni neno kubwa. Ukijifunza neno hilo katika Agano Jipya utashtuka na kushangaa. Kwa Kiyunani, neno hilo ni “katartismon”. Kipande chake ni neno “artis” na maana yake ni “fundi stadi”. Kumbe kazi ya kila mchungaji mwalimu ni kumfanya kila mwamini aliye chini ya uwezo wake kuwa fundi stadi katika kulitumia, kulielewa, kuliishia, kutawaliwa nalo, kuhudumia, n.k. kwa kutumia Neno la Mungu. Kazi hii ilimla Yesu sana, kama mkakati kwa ajili ya Watu Kumi na Mbili katika mafunzo kazini ya muda wote, kwa karibu, katika kipindi cha miaka mitatu tu. Hapo tena – nini maana ya neno “kama Kristo”? Tukiondolea mbali Mkakati Wake, na kuondoa Agizo Lake Kuu, na kupuuza Mfano aliotoa, kwa nini sisi tulalamike kuhusu hali ya kanisa na ya dunia? Ni kwamba tunaishi na tulichotengeneza wenyewe. Kumbuka kwamba Utambuzi hupelekea Taratibu, na Taratibu kupelekea Matokeo. Kama kilichotokana na mfumo mzima
212
ni kibaya, (na hakuna awezaye kukana kwamba sivyo), basi Utaratibu wetu lazima una makosa.
Angalia tena lile neno “kuwezesha”. Utafiti unadhihirisha kwamba lilikuwa neno la kawaida kabisa lililotumika katika dunia ya Kiyunani ya karne ya kwanza. Na lilikuwa na maana nyingi mbalimbali.
(1) Kutuliza mji uliokuwa umetengana.
(2) Kutibu kiungo kilichokuwa kimeteguka.
(3) Kuendeleza viungo fulani vya mwili kwa mazoezi.
(4) Kumrejeza mtu kwenye hali yake ya kawaida.
(5) Kuwapatanisha marafiki ambao walikuwa wametengana.
(6) Kumwezesha mtu au kitu kwa ukamilifu kabisa, kwa ajili ya kusudi fulani.
(7) Kuweka mambo kwa utaratibu, au kupanga vitu vizuri.
(8) Kuelekeza kitu kwenye mkono wa maendeleo.
Kabla ya kuachana na orodha hiyo kwa haraka, hebu tazama kila neno na ulifafanue kulingana na maelezo ya kazi ya viongozi wa Mwili wa Kristo. Halafu, tafsiri kila neno katika maisha na mwenendo wa wafuasi wote, kwa sababu wanafunzi watakuwa kama mwalimu wao (ktk Luka 6:40).
KUVITUMIA VIUNGO
Basi, zile nafasi za kawaida zilizozoeleka za “wachungaji” na “washirika – walei” lazima zibadilishwe. “Walei” wanakuwa ndiyo
213
askari walioko mstari wa mbele (wenye silaha kamili, wenye ufahamu kamili, na wenye utendaji kamili), na “wachungaji” na mkutano wa kanisa lote, wapo kwa ajili ya kuwaunga mkono. Ndugu Charles Colson alikuwa sahihi kabisa alipoandika hivi: “Kila mmoja wetu kama waamini lazima tujione kama watumishi wa Injili. Sisi si wahudhuriaji wa kanisa tu, walaji wa mambo ya kiroho.” Mkristo ambaye hana huduma binafsi yenye kupelekea mguso wa dunia yote kwa nguvu ni mfano potofu wa Mkristo. Lengo ni kumtumia Mkristo kila wakati katika kuishi maisha ya Kikristo na kupenya na kugusa dunia nzima kwa mkakati wa Yesu. Halafu tena, kujengwa kwa wanafunzi wenye kujizidisha, wenye maono ya dunia na wenye uwezo wa kuigusa dunia ndicho Kipau Mbele Kikubwa (kama katika Agizo Kuu). Ili kanisa liweze kurekebisha mawazo potofu yake, lazima lianze uandikishaji tofauti, liwe na uwezeshaji tofauti na mpya, na liwe na utumaji mpya na wa tofauti. Mungu na afungue macho ya mioyo yetu na kuijaza nuru (ktk Waefeso 1:17-19)!
Kumbe basi – kusudi la sasa katika ushirika wa waaminio ni “kuwawezesha watakatifu”. Hii inahitaji mafunzo ya hali ya juu, ya kikamilifu kabisa, kwa kila mwamini. Hatimaye, kusudi kuu ni “kulijenga kanisa” – kihali, kwa kulijenga kwa ndani, na kwa idadi, kwa kulipanua kutoka nje. Nje kwa kiasi gani? Kila kanisa lazima lione kwamba wajibu wake ni mpaka “mwisho wa nchi”. Kwa hiyo, lazima liongeze uwezo wake – watendaji, mapato, mipango, mikakati na utendaji wake – hadi mwisho kabisa wa nchi. Kumbuka kwamba
214
mwangaza unaong’aa mbali zaidi hung’aa kwa nguvu zaidi nyumbani.
MIFANO YA USHIRIKA WA WAAMINIO WA MAHALI PAMOJA
Tumalizie mafunzo haya kwa kuonyesha michoro miwili ya mifano ya ushirika wa waaminio walioko mahali pamoja. Mfano mmoja ni ule wa kawaida katika makanisa yetu mengi, na ule mwingine ndiyo ufaao, tunaosema juu yake katika maelezo yetu.
Kusanyiko/Waamini
Viongozi
Watendakazi
Mchungaji
Katika mfano wa kwanza, washirika ni watu wengi – waamini wasiotosheka – wasikilizaji, watazamaji, waunga mkono. Wakati hali ya kujitoa inaposhuka na kuwa nzito kidogo, yule aliyejitoa zaidi
Dunia
215
katika ushirika anafanywa kiongozi. Kadiri huko kujitoa kunavyozidi kuwa kwa hali ya juu (sana sana katika kanisa la mahali pamoja peke yake), wafanya kazi wa kanisani wanaanza kupatikana. Halafu, yule aliyejitoa kuliko wengine wote kanisani ndiye anaonekana kufaa kuwa mchungaji! Bila shaka upotofu wa huu mfano ni dhahiri. Basi, uzito wa mwili wote na majukumu yake yote unatulia juu ya mchungaji. Mchungaji anabeba majukumu yasiyohesabika katika mwili au kundi hilo, na wakati mwingine ndiye anayeona au kushughulikia majukumu ya nje ya mwili au kundi. Mipango maalum inawashawishi wale washirika waliojitolea kabisa kujihusisha na kazi zile “maalum” za kuleta watu kwa Yesu, kufanya utume, huduma za kawaida katika jamii na kadhalika. Lakini mzigo wa utendaji, mafanikio na hatimaye kuifikia dunia nzima humwangukia mchungaji zaidi.
Matokeo ya mfano huu ni matatu:
(1) Uongozi uliovunjika moyo kabisa. Zaidi ya wachungaji elfu moja kila mwaka wanaacha huduma. Wengine zaidi ya mia tatu kila mwezi wanaondolewa kwa nguvu kwenye madhabahu. Je hilo linatutia aibu? Kama hapana, linapaswa kututia aibu! Na, linaweza kurekebishwa kabisa.
(2) Wanachama wa kanisa ambao kwa sehemu kubwa ni “wa kimwili” (yaani, wenye ubinafsi, wanaotaka kujitosheleza wenyewe). Katika mfano huu, washirika hawajui kazi nyingine isipokuwa kuhudhuria kanisa, kuwa waaminifu kwa taasisi yao (au dhehebu
216
lao) na kutathmini mapato. Je, ni ajabu kwamba wanazidi kuwa kimwili?
(3) Dunia inayobaki bila kushuhudiwa. Sehemu kubwa ya binadamu duniani aidha hawajasikia kuhusu Jina la Yesu kabisa, au wamesikia “kidogo” tu. Ukristo wa Kitabu cha Matendo ulishughulika na hali iliyokuwa mbaya zaidi, wakaibadilisha kabisa kwa muda mfupi sana. Hali iliyoko inaweza kubadilishwa vivyo hivyo hata leo, lakini si kwa kuendeleza mfano huo mbovu.
Mfano ule wa pili ni kama kinyume kabisa cha ule wa kwanza.
Mchungaji
Watendakazi
Viongozi
Kusanyiko/Waamini
Dunia
217
Katika huu, mchungaji ndiye mwenye kuwajibika kwanza kabisa. Nafasi yake ni ya kuwajibika, si ya heshima! Wajibu wa nafasi kama hiyo ni mkubwa zaidi sana kuliko heshima au sifa yoyote inayoweza kupatikana kutokana nayo. Ukweli ni kwamba hiyo inaweza kuwa kama sheria: nafasi yoyote katika mwili inayopelekea kuendelea kukua kwa sifa ya kiongozi wake (kimafanikio, na kadhalika) itiliwe mashaka kabisa katika Ukristo! Mwili hutafuta kuonekana, kutambuliwa, kutuzwa – na hilo ni eneo moja tu la udhaifu ambalo mwili umerithi! Mwili hauwezi kuaminiwa na aina ya pongezi na sifa zinazotolewa kwa viongozi “maarufu” katika michezo au siasa.
Wajibu wa kwanza wa mchungaji katika mfano huu ni kuwawezesha na kuwaambukiza watenda kazi pamoja naye maono ya kufanya watu kuwa wanafunzi, ili kuifikia dunia nzima. Maono haya ya kawaida na ya wote yanapaswa kuamua huduma ya kila mtenda kazi kanisani, na kupanga malengo yake kwa ajili ya wanafunzi ambao yeye anawajenga. Mchungaji pia anawajibika katika kuwawezesha na kuwaambukiza viongozi maono yake, lakini sasa ana fursa pekee. Viongozi kwa wakati huu “wanawezeshwa mara mbili” kwa kupewa maono ya kawaida na mkakati – kutoka kwa mchungaji moja kwa moja, na kutoka kwa watumishi wa kanisa. Basi, mchungaji, watumishi wa kanisa na viongozi watakuwa na umoja katika kuwawezesha watakatifu wote kwa ajili ya kazi yao ya huduma. Wakati matarajio hayo yanapofanyiwa kazi, “mafuta ya ziada” yataondoka, na “vijana tajiri” watahama. Lakini, macho,
218
midomo, masikio, mikono, magoti na miguu ya mwili wenyewe vitakuwa vinaona, vinasema, vinasikia, vinatenda, vinapiga magoti na kutembea katika muungano kamili kabisa – siku zote kuelekea nje hadi mwisho wa dunia. Ushirika wa mahali pamoja ndiyo mahali pa msingi pa huduma (ingawa huduma nyingi hufanyikia hapo). Ndicho kituo chenye nguvu kwa ajili ya huduma. Watu pale wanaonyesha na kumshirikisha Kristo popote walipo, na kwa makusudi kabisa wanajenga mikakati kwa ajili ya wao binafsi kupenya hadi mwisho wa nchi.
Nini matokeo wakati mfano wa pili unapokuwa halisi? Hapa tena, matokeo ni matatu.
(1) Viongozi walio na msisimko na waliotosheka walioko duniani.
(2) Waamini “wa kiroho” wanaozidi kuongezeka (ambao Kristo ni wa muhimu kwao, wanamheshimu Mungu, wamejazwa Roho na ni watakatifu wanaogusa dunia).
(3) Dunia kuzidi kushuhudiwa.
Mikakati kwa ajili ya kufanyia kazi mfano huu wa pili imo katika Amri na Mfano wa Yesu, na Amri na Mfano wa Waefeso sura ya 4. Lakini, lazima tuwe waangalifu sana. Mwisho wa siku, makusudi ya Mungu yanategemea kutimizwa kwa makusudi Yake ya sasa. Je, wewe binafsi unafundishwa kwa utendaji wa karibu kabisa wa kazi za kuifikia dunia? Je, wewe unawajenga wengine – kwa karibu, kwa kuwapa kazi za kuifikia dunia?
219
Sura Ya 9
Maneno Yake Ya Mwisho, Wosia Wake
“Lakini mtapokea nguvu, akiisha kuwajilia juu yenu Roho Mtakatifu; nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, na katika Uyahudi wote na Samaria, na hata mwisho wa nchi.”
Waefeso 4:7-14
George Orwell, mwandishi maarufu wa kitabu kiitwacho 1984 na Animal Farm, aliwahi kuandika hivi: “Sasa tumezama kufikia kiwango ambacho wajibu wa kwanza wa watu wenye akili timamu ni kurudiwa kusemwa mambo ambayo ni ya kawaida.” Katika kanisa la siku hizi, kilicho kawaida ni kitu chenye kuleta mapinduzi na mabadiliko sana. Hakuna kitu kinachopuuzwa sana kama lile agizo “dhahiri” au la kawaida la Yesu. Tunapotaja kitu hicho kwa mara nyingine na kufanyia kazi, kanisa linatikiswa hadi misingi yake.
Agizo la Yesu lilitajwa katika kila Injili nne na katika Kitabu cha Matendo ya Mitume. Kitabu cha Matendo ya Mitume ni maendelezo ya habari zinazosimuliwa katika Injili. Kitabu chenyewe kimeandikwa kwa mtiririko mzuri na kinafuata utaratibu wa kijiografia ambao unaonekana kwa urahisi sana, utaratibu
220
unaopatikana katika Matendo 1:8: “Yerusalemu … Uyahudi … Samaria … mwisho wa nchi.” Kitabu cha Matendo kinaweza kugawanywa katika sehemu tatu kubwa (sura ya 1 hadi 7; ya 8 hadi 12; ya 13 hadi 28), huku sehemu ya kwanza ikionyesha jinsi kanisa la kwanza lilivyoendeleza huko Yerusalemu ile kazi ambayo Yesu aliianzisha (ktk Matendo 1:1). Sehemu ya pili inahusiana na maendeleo ya Injili katika Uyahudi na Samaria, na sehemu ya mwisho inahusu kuendelezwa kwa Injili hadi “mwisho wa nchi”.
Mstari wa nane katika Matendo moja unayo maneno ya mwisho ambayo Yesu Kristo aliyazungumza kwa wanafunzi Wake, muda mfupi tu kabla hajapaa kwenda mbinguni. Injili ya Luka na ya Yohana inadhihirisha kwamba mara ya kwanza Yesu alipokutana na wanafunzi Wake baada ya kufufuka, aliwaagiza kuwa mashahidi katika mataifa yote. Alirudia agizo hilo mara moja tena jioni hiyo hiyo. Akalirudia tena baadaye pale mlimani Galilaya, kama ilivyoandikwa katika Mathayo 28. Na sasa, yuko nje ya mji wa Yerusalemu, siku arobaini baadaye, muda mfupi tu kabla ya kupaa Kwake. Hivyo basi, agizo hilo linapaswa kuwa dhahiri kabisa kwetu sisi. Lakini, swali moja litafunua kwamba hatujajali sana agizo hilo. Je, unaigusa dunia nzima kwa kiasi gani katika mambo unayofanya, unayofikiri, unayosema, au unayotayarisha? Ni hivi: Yesu alishikwa sana na jambo la kuhusisha dunia nzima, lakini mtulivu sana kuhusu mbinu au njia. Sisi tumefanya kinyume! Tunakwenda kongamano
221
baada ya kongamano kujifunza kuhusu mbinu, lakini tunaepuka kule kuhusika kwenyewe, ambako ndiyo muhimu.
Amri ya Yesu ilidai matendo. Agizo Kuu halikutolewa ili watu wajifunze tu. Ni mpango wa utendaji. Katika somo hili, tutalitazama tena, tukitumia Matendo 1:8 kama msingi wetu. Lakini swali kubwa ni hili: Je, utakuwa tayari kupatikana katika kila hatua kwa ajili ya kutimizwa kwa Agizo Kuu?
MKAKATI KWA AJILI YA KUENDELEZA INJILI
Kwanza, tunaona katika tamko hili Mkakati kwa ajili ya Injili kuendelea kuenea. Mkakati upo katika neno “shahidi”. Hili ni neno muungano lenye mambo mengi ndani yake. Neno la asili kwa Kiyunani ni “martutia”, ambalo bila shaka si neno kimya. Neno hilo limezaa neno la Kiingereza “martyr” yaani, “shahidi mfia imani”. Kumbe basi, mtindo wa maisha unaotokana na neno hili ni kuishi maisha yenye kujihatarisha katika utendaji. Kuwa “shahidi mfia dini” ni mradi wa kuishi au kufa.
Dada mmoja aitwaye Virginia Owens aliandika hivi: “Kuwa Mkristo ni nafasi ya ajabu sana – si ya salama. Mtu hamfuati Kristo akiwa anatembea katikati ya barabara iendayo kwenye kuheshimika.” Mwanatheolojia mmoja, aliyekuwa ameanza kuelewa “nafasi ya kupita kiasi” ya Ukristo aliandika hivi: “Hebu tukusanye Agano Jipya zote zilizopo, tuzipeleke kwenye kiwanja mahali au juu ya mlima, halafu, wote tukiwa tumepiga magoti, mmoja wetu aseme na
222
Mungu hivi: ‘Kichukue Kitabu hiki tena. Sisi binadamu, kama tulivyo sasa, hatufai kushughulika na kitu kama hiki. Kinatuhuzunisha tu.’ Wazo langu ni kwamba, sawa na wakazi wa Gerasi, tumwombe Kristo ‘aondoke kwetu’.” Hao waandishi wawili wameanza kuelewa dai la Yesu kwamba tuwe “mashahidi wafia imani”.
Neno hilo “martus” linatokea zaidi ya mara 30 katika Kitabu cha Matendo, na ni miongoni mwa maneno makuu kitabuni. Hutujulisha kwamba tunapaswa kusahau mawazo yoyote ya mtindo wa maisha unaotilia maanani “usalama kwanza”. Tazama mifano ifuatayo.
Mkulima alikwenda kuwinda na mbwa wake porini, maili nyingi mbali na nyumbani. Akagundua kwamba amesahau kopo la kumlishia mbwa wake chakula. Aliweka bunduki yake chini na kumwambia mbwa wake akae hapo mpaka arudi. Alipokuwa amekwenda, moto wa pori ukatokea, na yule mbwa akafa. Baadaye, mkulima yule aliukuta mwili wa mbwa wake – ulioungua kabisa – kando ya bunduki yake. Kwa huzuni sana alisema, “Siku zote ilibidi niwe mwangalifu katika ninachomwambia mbwa wangu afanye, kwa sababu angefanya hivyo hivyo.” NDUGU WAKRISTO, Yesu Kristo anataka na sisi tujali sana kuhusu kufanya anachosema mpaka tusahau kuhusu moto wa porini unaowaka.
223
Profesa mmoja wa sayansi ya viumbe alitaja kanuni moja ya sayansi siku moja darasani. Alisema hivi: “Kujihami ndiyo sheria ya kwanza katika nguvu za asili.” Mwanafunzi mmoja Mkristo akamwambia baada ya darasa akiwa anatabasamu, “Inashangaza sana kuona tofauti kati ya nguvu za asili na neema. Sheria ya kwanza ya nguvu za asili ni kujihami, lakini katika neema, sheria ya kwanza ni kujitoa.” SAWA KABISA!
Jionee hali ya kujitoa mwenyewe ya Kalvari iliyo kiini cha neema ya Mungu, halafu ukumbuke kwamba kanuni ya kwanza ya uanafunzi wa Kikristo inapatikana katika maneno haya ya Yesu: “Mtu yeyote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe, ajitwike msalaba wake, kisha aje anifuate.” Kujikana mimi mwenyewe maana yake ni kujiambia yale maneno aliyosema Petro kwa habari ya Yesu wakati alipomkana: “Sijawahi kumsikia kabisa mtu huyo. Simjui mtu huyo mimi!”
Ndugu mmoja aitwaye Bruce Morgan aliandika hivi: “Tatizo la Wakristo ni kwamba hakuna mtu anayetaka kuwaua tena.” Dada Eugenia Price alikariri wazo hilo aliposema hivi: “Dhambi kubwa ya kanisa ni kwamba LIMEMFUGA Yesu Kristo na kumfanya mpole.”
224
Aina ya ushahidi ambao unatajwa katika Matendo 1:8 ni wa asili dhahiri kabisa kiasi kwamba unatuingiza katika matatizo kila wakati (lakini pia unaleta furaha ya daima ndani yetu, na huambatana na miujiza ya daima pia).
Mkutano wa mamia ya viongozi wa kidini kutoka Marekani yote ulifanyika, na ajenda kuu ilikuwa hii: “Tunawezaje kutumiwa ili kulirejeza taifa hili kwa Mungu?” Kila mhudhuriaji alipewa nafasi jioni moja kutoa jibu lake kwa kifupi. Kiongozi mmoja – Mmarekani Mweusi – aliinuka na kusema hivi: “Wapendwa. Wakristo wa Marekani hawatapata tena uwezo wa kuigusa jamii hii mpaka wapoteze hofu yao ya kifo.” Akakaa chini. Watu wengi waliohudhuria mkutano huo walisikika wakisema kwamba pengine jibu bora kuliko yote katika mkutano huo lilikuwa la huyo ndugu.
Miaka mingi iliyopita, mhubiri maarufu mishenari aliyeitwa Robert Wilder alitembelea Chuo kidogo kiitwacho Hope huko Jimbo la Michigan ili kuhubiri katika ibada ya wanafunzi kuhusu utume wa dunia nzima. Akaweka ramani kubwa sana ya India mbele ya kanisa, na akaweka kimulimuli mbele ya hiyo ramani. Katika mahubiri yake alitamka kwamba kila mara kimulimuli kilipowaka, mtu mmoja wa India alikuwa anakufa pasipo kusikia habari za Kristo. Siku hiyo, Kristo na maono Yake ya dunia nzima aligusa moyo wa mwanafunzi mmoja aliyekuwa karibu kumaliza hapo chuoni aliyeitwa Samuel
225
Zwemer. Maono hayo yalipowaka moyoni mwake, alimwomba Mungu amweke mahali pagumu kabisa duniani.
Muda si muda, alianzisha makazi katika Kisiwa cha Bahrain huko Ghuba ya Uajemi, katikati kabisa ya jamii ya dunia ya Kiislamu. Kisiwa hiki ni maarufu. Zwemer akaanza kuchapisha na kugawa vipeperushi vya Injili, japo hakuwa amepata kibali cha serikali ya Kiislamu ya mahali pale. Katika kipindi cha juma moja, binti wawili wa Zwemer – mmoja wa miaka minne na mwingine wa miaka saba – walikufa kwa sababu ya magonjwa na joto kali la mahali pale. Samuel Zwemer akaomba wakuu wa Bahrain ruhusa ya kuzika miili ya binti zake, lakini alinyimwa kibali kwa madai kwamba walikuwa Wakristo, na miili yao ingenajisi ardhi ya pale. Zwemer akakata rufani na akapata ruhusa – kwa sharti kwamba yeye mwenyewe achimbe makaburi. Alifanya hivyo, na baada ya maziko, aliweka jiwe la kumbukumbu lililosema, “Amestahili Mwanakondoo aliyechinjwa, kupokea utajiri.” Huo ndiyo mtindo wa kishujaa wa kutoa kila kitu hadi kufa, ambao Yesu alitaka watu waishi.
Shirika moja la zamani kidogo lililohusika na kutuma wamishenari lilituma wamishenari sabini kwenda nchi ya Kamerun, ambayo ni “kiungo” muhimu kati ya Afrika magharibi na Afrika kusini na kusini kati. [Waislamu kwa sasa wanajitahidi sana kujaribu kuipata Kamerun.] Katika hao sabini, sitini na nane walifia huko. Wastani wa uhai wao baada ya kufika huko ilikuwa miaka miwili na
226
nusu! Inasemekana wengi wao walisafiri pamoja na majeneza yao, wakijua kwamba uwezekano wa kurudi ulikuwa mdogo! Yesu alitaka mtindo huo wa maisha wa kishujaa, wa kutoa kila kitu hadi kufa!
Familia moja ya kimishenari ilikwenda Uchina kuhubiri Injili huko, chini ya “shirika la utume wa imani”. Walikwenda kama waalimu wa shule za kawaida. Waliporudi, walirudi kama wamishenari wa kawaida likizoni – wakiwa na boksi lenye picha na vitu mbalimbali vya kuonyesha. Walipomaliza kuonyesha maonyesho yao na kutoa maelezo yao, kipindi cha maswali na majibu kikatolewa. Mshirika mmoja wa kanisa alisimama na kuuliza hivi: “Mlipokuwa huko hamkuogopa kwamba mnaweza kufia huko?” Jibu la baba wa familia ile ya wamishenari lilitoka, hivi: “Hapana, maana KABLA HATUJAENDA TULIKWISHA KUFA.” Hii ndiyo maana ya neno “martus” au “shahidi mfia imani”.
Mchungaji Charles Crowe wa KiMethodisti alikuwa anaendesha gari lake mjini Chicago, kwenye mzunguko wa barabara, kama alivyokuwa anafanya mara nyingi tu. Jengo la kanisa lake lilikuwa maarufu sana hapo mjini kuwa ndiyo lenye kilele kirefu katika makanisa yote ya Marekani Kaskazini. Juu yake ulikuwepo msalaba mkubwa sana. Siku hii asubuhi, wakati Mchungaji Crowe anapita mbele ya jengo hilo, aliona kundi kubwa tu la watu wamesimama kando ya barabara mbele ya jengo, na wote
227
walikuwa wanatazama juu. Akainama kwa makini katika gari lake na kutazama juu aone walikuwa wanatazama nini. Akaingia kwenye eneo la kuegesha magari, akaharakisha kuweka gari lake katika sehemu yake ya kuweka gari, kisha akaharakisha kwenda mbele ya kanisa na kujiunga na waliokuwa wanatazama juu.
Juu ya msalaba palikuwa na mpaka rangi mwenye ndoo ya rangi. Alikuwa amefungiwa msalabani, na kwa utaratibu alikuwa anapaka rangi ule msalaba, akielekea chini. Msalaba wenyewe ulikuwa unayumba kwa utaratibu kila alipopaka rangi. Watu walikuwa wanatazama kazi yake hatari. Baada ya muda, Charles Crowe aliondoka kwenye lile kundi la watu na akaanza kuelekea ofisini kwake hapo kanisani. Mara Roho Mtakatifu akamwambia, “Mwanangu! Umepita hapo mara nyingi, na hapajawahi kuwepo mtu yeyote njiani akitazama juu kwenye ule msalaba. Nini kilichofanya tofauti leo? Ni hiki: LEO, MSALABA ULIKUWA NA MTU JUU YAKE! Siku zote, dunia itasimama kuona wakati mtu mkweli atakapokuwa msalabani.”
Leo hii kanisa linaambiwa na dunia maneno yale ambayo Tomaso alisema kuhusu Yesu katika mashaka yake na kutokujua: “Nisipoona alama za misumari mikononi Mwake, na kutia kidole changu katika alama hizo … sitaamini.” Wanatafuta kujitoa bila maonyesho kwa Mkristo ambaye Kristo ndiye kiini cha maisha yake, la sivyo, hawataamini.
228
Pengine ni vizuri tutulie kidogo hapa na kujikumbusha kuhusu mbadala pekee wa mtindo huu wa maisha ya Kikristo. Yesu alisema hivi: “Yeyote atakayeokoa (linda, tetea, hifadhi) maisha yake atayapoteza, na yeyote atakayepoteza maisha yake kwa ajili yangu atayapata.” Sehemu ya kwanza inafafanua ule mtindo wa maisha wenye kufikiri usalama kwanza, mimi ndiyo wa muhimu, nijiokoe mwenyewe kwa gharama yoyote ile. Sehemu ya pili inafafanua ule mtindo mwingine wa maisha – wa kuwekeza, wa kutojijali, wenye kujali wengine, wa kuwajenga wengine, uliojawa na Kristo – ambao ndiyo mtindo wa maisha wa Mkristo.
Wasafiri wawili walinaswa na tufani ya barafu walipokuwa wanasafiri sehemu ya kaskazini. Walipokuwa wanakabiliana na hiyo dhoruba, walimkuta mtu amegandia kwenye barafu, wakadhani amekufa. Mmoja akasema, “Nina matatizo ya kutosha kujisaidia mwenyewe. Nasonga mbele.” Yule mwingine akasema, “Siwezi kumpita binadamu mwenzangu katika hali hii wakati bado ana pumzi hata kidogo tu ya uhai.” Akainama na kuanza kumpa joto yule mtu kwa kumsugua kwa bidii sana. Hatimaye yule mtu akafungua macho yake, akarejelea uhai wake, akapata nguvu na kutembea pamoja na yule mtu aliyemsaidia. Walipoendelea na safari, walikuta nini? Walimkuta yule mtu aliyeamua kujishughulikia mwenyewe na kujitafutia usalama wake akiwa amekufa kwa baridi katika barafu.
229
Yule Msamaria Mwema alihifadhi maisha yake mwenyewe kwa juhudi zilizohitajika kumwokoa yule mtu mwingine. Msuguano ule ulisisimua damu yake na kumfanya hai. Sheria haibadiliki wala haishindwi: “Yeyote (Mkristo au kanisa) atakayeokoa maisha yake atayapoteza; na yeyote atakayepoteza maisha yake kwa ajili yangu atayapata.”
Mwandishi maarufu aitwaye C.S. Lewis alifanikiwa kunasa uzuri na msisimko wa maisha ya Mkristo katika kitabu chake cha “Chronicles of Narnia” kwa kumfanya mtu mmoja katika sehemu iitwayo The Last Battle (Vita ya Mwisho) aseme hivi: “Afadhali nife nikiwa napigania taifa la Narnia kuliko kuzeeka na kuwa mjinga nyumbani, na pengine nishindwe kutembea mpaka nitumie kiti na mwishowe nije kufa tu.” Rafiki zangu. Tutakufa kwa namna moja au nyingine. Kujitoa kwa Kikristo ni kwamba, “Kristo atukuzwe katika mwili wangu, katika uhai wangu au kwa kifo changu.”
Kwa maneno mengine, Yesu anasema hivi: “Ee mwamini! Wewe ndiye ushahidi wangu, vitambulisho vyangu, hoja zangu, wasifu wangu, mwenezaji wangu, matangazo yangu.” Na Msalaba ndiyo kiini cha uwakilishi wowote wa Kristo. Mtu mmoja aitwaye George Bernard Shaw aliuliza hivi: “Je, ni lazima Kristo asulubiwe katika kila kizazi kwa kuwa tu dunia haina ubunifu?” Jibu kwa swali lako, mheshimiwa, ni, “Ndiyo” nasi tunapaswa kuwa wale
230
wanakondoo wasiojijali wenyewe. “Ninyi ndiyo mashahidi wangu wafia imani.” Huo ndiyo mkakati wa Injili kusonga mbele.
CHANZO CHA USHUHUDA WA INJILI
Pili, tunaiona asili au chanzo cha ushuhuda wa Injili. Asili yake inaonekana katika matukio matatu ya neno “nanyi”. “[Nanyi] Mtapokea nguvu baada ya Roho Mtakatifu kuwashukia [ninyi], nanyi mtakuwa mashahidi wangu.” Maneno “nanyi” na “juu yenu” yako katika wingi. Agizo limetolewa kwa Mwili wote wa Kristo na linatimizwa na kila kiungo cha huo Mwili. Wewe Mkristo mpendwa, unahusika kabisa – kikamilifu kabisa – katika mkakati wa Yesu. Wewe ni asili au chanzo cha ushuhuda wa Injili.
Ona kwamba neno “nanyi” linazidi kutajwa kwa Roho Mtakatifu mara tatu katika mstari huu. Hii si kwamba inapunguza nafasi na jukumu Lake; bali huongeza wajibu wako. Hao “nanyi” ni akina nani? Si malaika, si watu wasiokuwa wa kawaida, si watu maalum. Andiko linadhihirisha “nanyi” hao katika mistari inayofuata. Matendo 1:2 inawataja kabisa kwamba, ni wale “mitume ambao Yesu alikuwa amewachagua”.
Ni hivi wapendwa: Mitume wote walikuwa wanaume. Hii haipunguzi nafasi ya wanawake, inaongeza tu jukumu la wanaume. Roho Mtakatifu bila shaka alitazamia matatizo ya historia ya Kikristo – kwamba ingekuwa rahisi kabisa kwa wanaume kukimbia wajibu wao na kuwaachia wanawake. Kwa hiyo , siku hizi katika makanisa
231
yetu tuna vikundi vya umisheni vya wanawake. Mungu ashukuriwe kwa ajili ya wanawake wanaojali na wanaomcha Mungu, lakini hili ni jukumu la wanaume kimsingi! Ni hivi: Ukifanikiwa kumpata mwanamume, kiongozi aliyewekwa na Mungu katika idara ya msingi katika jamii, unakuwa na nafasi bora sana ya kumpata kila mtu mwingine katika eneo lake la utawala. Lakini ukimpata mmoja wa watu wake kwanza (mke, watoto) unaweza kushindwa kumpata huyo kiongozi au wengine katika eneo lake.
Zamani kidogo Ijumaa Kuu moja usiku, jengo la kanisa liitwalo People’s Church huko mjini St. Paul jimbo la Minnesota, Marekani, lilishika moto. Ilikuwa baada ya usiku wa manane na idara ya zimamoto ilizuiliwa na barafu katika juhudi zake za kuuzima moto. Walipokuja kufanikiwa, jengo likawa limeungulia chini. Asubuhi iliyofuata, washirika wa kanisa hilo na wanamji ule walianza kukusanyika pembeni mwa lile jengo lililokuwa bado linafuka moshi. Jengo lenyewe lilikuwa aina fulani ya makumbusho ya picha za kidini pamoja na jengo la kanisa, hivyo lilikuwa maarufu sana kwa utalii.
Nyuma kabisa ya madhabahu ilikuwepo picha ya kuigiza ya “Kristo Anayesihi” – sanamu kubwa ya marumaru iliyokuwa na urefu wa futi nane, iliyoandaliwa na mchoraji maarufu Mdenish aliyeitwa Thorsvalden. [ZIADA: Mishenari maarufu wa India aitwaye Stanley Jones alikuwa anatembelea mji wa Copenhagen,
232
Denmark miaka mingi kabla. Mwongoza watalii akawa amewapeleka kwenye Kanisa moja la Kikatoliki huko Copenhagen, mahali ambapo sanamu ya hiyo picha tunayosema, ilikuwepo. Sanamu yenyewe inamwonyesha Yesu akiwa amesimama, uso umetazama chini, mikono imefunguliwa kwa dunia. Imetokana na Mathayo 11:28, kwamba, “Njooni kwangu ninyi nyote mnaosumbuka na wenye kulemewa na mizigo mizito, nami nitawapa pumziko.”
Sasa, walipokuwa wanaondoka hapo, yule mwongoza watalii aliuliza, “Je, kuna yeyote aliyefanikiwa kuuona uso wa Bwana Yesu” Jones akajibu, “Tungewezaje kuuona? Umeinamia chini.” Yule mwongoza watalii akajibu kwa sauti ya chini ya unyenyekevu, “Ndiyo hivyo Mzee. Ukitaka kuuona uso wa Bwana, lazima kwanza upige magoti miguuni Pake!” MWISHO WA ZIADA]
Sasa, lile jengo la kanisa lilipoungua, ile sanamu ilianguka na sakafu na kutumbukia shimoni katika vyumba vya chini ya ardhi. Siku ya pili yake, masaa ya asubuhi, baadhi ya watu wa kanisa walipata ruhusa ya kushuka na kuingia katika magofu ya kanisa ili kuona kama kuna vitu vya thamani vilivyopona moto. Wakaikuta ile sanamu, imepata alama za moto na majivu na moshi kidogo, lakini haikuwa imeharibika isipokuwa kipande kikubwa kilichobomoka kutoka sehemu ya sanamu kusimamia. Wakaiacha ipoe, halafu mchana ule wakaibeba taratibu kutoka huko chini na kuiweka pembeni ya barabara. Wakapanga watu sita kusimama kuilinda ili wapitaji na watazamaji wasiiharibu, halafu wakarudi tena chini
233
kutafuta vitu vingine.Waliporudi tena baada ya muda, kundi la watu lililokuwepo halikuwa linatazama tena lile jengo lililoharibiwa. Badala yake, walikuwa wanatafuta nafasi katika huo mviringo, wote wakiwa wanajaribu kuitazama hiyo sanamu maarufu.
Hebu niufanye huo mfano kuwa wa kiroho, ili kutilia mkazo jambo moja. Ni hivi: Yesu alikuwa katika hilo kanisa kwa muda mrefu tu, lakini alikuwa “amefungiwa minyororo madhabahuni,” na watu wa mtaani walikuwa hawajapata kumwona. Ni wakati tu kanisa liliposhika moto na kuungua (!) na baadhi ya watu wa kanisani (!) kumchukua na kumweka pembeni ya barabara (!) ndipo “watu wa nje” walipoweza kumwona kwa mara ya kwanza kabisa! Wewe, mwamini wa Kikristo, ndiye asili au chanzo cha ushuhuda wa Injili.
MADA YA USHUHUDA WA INJILI
Halafu, mstari wetu unatuonyesha mada ya ushuhuda wa Injili. Yesu alisema hivi, “Ninyi mtakuwa mashahidi WANGU.” Ushahidi wetu haupaswi kuelekea kwenye kanisa, au dhehebu, au itikadi, au fundisho, au ukiri fulani, au taratibu fulani. Unapaswa kumwelekea Kristo. Ni fursa yetu nzuri tu kumweleza Yeye kama alivyojieleza Mwenyewe katika Neno Lake, kwamba ni Mwokozi mwenye Kukomboa (ktk Matendo 1:3), kwamba ni Bwana Mfufuka (1:3 tena), na kwamba ni Mfalme Anayerudi (ktk 1:11). Mada hiyo haina mwisho! Tena, ni kweli kuu yenye kuvuta usikivu kabisa.
234
Picha kwenye ukuta wa jumba la maonyesho ya sanaa huko Ujerumani ni mfano mzuri wa sehemu hii ya kazi yetu. Picha hiyo inamwonyesha Martin Luther, Mjerumani maarufu aliyeleta Matengenezo ya Kanisa, akiwa anahubiri katika mimbari ya kanisa la Kijerumani. Mkononi mwake ameshika Biblia, na kwa mkono mwingine amenyoosha kidole, na mdomo wake uko wazi kana kwamba anatangaza kitu. Anaihubiri Injili. Unaweza kumwona mhubiri na wasikilizaji wake katika picha hiyo. Lakini ukitazama kwa makini sana, utaona kitu cha kushangaza. Hakuna msikilizaji wake hata mmoja anayemtazama mhubiri ambaye ni Martin Luther! Ukifuata mahali wanapotazama, unaona kitu cha kufurahisha sana. Pembeni mwa lile jengo, kuna umbo dhahiri japo liko mbali la Yesu Mwana wa Mungu – na kila jicho hapo linamtazama Yeye. Wanamsikiliza Luther, lakini wanamtazama Yesu!
Hayo ndiyo matokeo tunayotaka ya kumshuhudia Kristo kwetu. Tunamtangaza Yeye, Naye anajitambulisha mwenyewe kupitia ushuhuda wetu. Basi, usikivu wa kila “msikilizaji” hatimaye unamwelekea Yeye.
UPANA WA USHUHUDA WA INJILI
Mstari huo pia unadhihirisha upana wa ushuhuda wa Injili. Ona kwa makini sana maneno yake ya kumalizia – “Nanyi mtakuwa mashahidi Wangu katika Yerusalemu NA Uyahudi wote, NA
235
Samaria, NA mpaka sehemu za mwisho za dunia.” Sasa tuchambue kidogo.
Watu wa karibu ni kazi yetu – “Yerusalemu”;
Watu jirani ni kazi yetu – “Uyahudi”;
Watu waliopuuzwa ni kazi yetu – “Samaria”;
(Samaria ni mfano wa watu unaowachukia kabisa, unaowabagua); na
Watu wanaofuata ni kazi yetu – “mpaka mwisho wa nchi”.
“Yerusalemu” huwakilisha hali yako ya karibu. “Uyahudi na Samaria” huwakilisha hali yako ya jirani, na “mwisho wa nchi” huwakilisha maeneo ya kimataifa yanayokuzunguka. “Yerusalemu” huwakilisha ushuhuda wa mjini kwetu, “Uyahudi na Samaria” huwakilisha ushuhuda wa nchi yetu, na “mpaka mwisho wa nchi” huwakilisha ushuhuda wa dunia yetu.
Halafu, ona kwa makini sana kwamba si swala la “aidha au” kuhusu watu hawa. Ni swala la “pamoja na”. Yesu Kristo anatutazamia tuishughulikie dunia nzima – kweli kabisa, na kwa dhati kabisa! Kwa njia gani? Kwa kujifunza na kufuata ule mkakati wa kufanya watu kuwa wanafunzi ambao kwao tunaona makundi ya watu kwa njia ya mtu mmoja, na kumjenga huyo mtu awaguse hao wengi – ambao ndiyo mkakati aliotumia Yesu na wale Kumi na Mbili aliokuwa nao.
Kitabu cha Matendo ya Mitume ni kimoja katika vitabu vichache sana vya Biblia vyenye kujipanga vizuri. Sura ya kwanza hadi ya saba huonyesha ushahidi wa wanafunzi wa kwanza huko
236
Yerusalemu. Sura ya nane hadi kumi na mbili katika Uyahudi na Samaria, na halafu sura ya 13 hadi 28, “mpaka mwisho wa nchi”.
Kipimo cha kweli cha nguvu na uwezo wa Mwili wa Kristo katika mahali pamoja ni hiki: Je, ushawishi wake unafika mbali kiasi gani? Mungu kwa hakika kabisa analitazamia kanisa la mahali kushugulikia dunia nzima! Maana, Yesu aliweza kufanya hivyo na watu kumi na mbili, na alifanikiwa kabla ya kuwepo kwa siku, televisheni, na teknolojia aina zote. Yeye alikuwa na waeleza watu tu! Lakini, aligusa dunia nzima ya siku Zake kupitia kundi Lake hilo dogo, la watu wa hivi hivi.
Siku hizi tunafikiri kwamba lazima tuwapate watu wa jamii zetu nyumbani kabla ya kuanza kushughulika na wale tulioagizwa kuwafikia duniani. Lakini, mpango huo ni kinyume. “Nuru ing’aayo mbali zaidi inang’aa kwa nguvu sana karibu na nyumbani.” Kila kanisa linapaswa kuwa na mpango daima jinsi linavyoweza kufikisha Injili katika sehemu nyingi duniani kwa haraka kiasi iwezekanavyo, na lengo lake linapaswa kuwa kuwajenga wanafunzi ambao wana maono ya dunia, watakaoigusa dunia nzima hadi mwisho wake, hadi ukamilifu wa dahari. Mungu alisema hivi: “Niombeni, nami nitawapa ninyi mataifa kuwa urithi wenu, na sehemu za mbali za nchi kuwa mali yenu” (ktk Zaburi 2:8, TLR). Sasa, kwa nini hatujapata watu wa mataifa kuwa urithi wetu, na sehemu za mwisho za dunia kuwa mali yetu? Sababu pekee pengine ni kwamba, hatuombi! Ni dhahiri kabisa kwamba kanisa kwa ujumla halina kwenye moyo wake kile kilicho
237
moyoni mwa Mungu. Vipi kuhusu kanisa lenu? Kuhusu kanisa lako? Vipi wewe mwenyewe?
Ona pia kwamba, mstari wenyewe unasema, “katika Yerusalemu na Uyahudi yote, na Samaria, mpaka mwisho wa nchi”. Si swala la “aidha au” bali ni “pamoja na”. Tunapaswa kuwa tunashuhudia mahali pote hapo kwa wakati mmoja, na pote tunapaswa kupahifadhi na kupabeba moyoni. Kivipi? Kwa kujenga maono kwa ajili ya dunia nzima, halafu kwa kuwajenga watu wa kutekeleza maono hayo. Upana wa eneo letu la kazi ni dunia nzima.
SIRI YA USHUHUDA WA INJILI
Hatimaye, maneno ya Yesu yanadhihirisha siri ya ushuhuda wa Injili. Alisema, “Mtapokea nguvu, baada ya Roho Mtakatifu kuwajilia juu yenu.” Njia nzuri ya kumfikiria Roho Mtakatifu ni kwamba, Yeye ni Yesu pasipo mwili. Roho Mtakatifu ni mbadala wa Kristo hapa duniani, akifanya aliyokuwa anafanya, na kuendeleza kazi Yake.
Mvulana mmoja alimwuliza mama yake, “Mama! Mungu analetaje mvua?” Baadaye akawa kama amekumbuka, na kujibu swali lake mwenyewe. “Usijali, ninajua tayari. Yeye anamwambia Roho Mtakatifu afanye hivyo. Roho Mtakatifu ndiye anayefanya kazi yote!” Roho Mtakatifu ndiye Nafsi Mtendaji katika Uungu. Siku hizi, Yeye ndiye hufanya kazi yote!
238
Halafu fikiria kuhusu neno “nguvu”. Neno la Kiyunani linalotumiwa hapa ni “dunamis”, ambalo limezaa neno la Kiingereza “dynamite” au baruti. Lakini, kiunganisho hicho kinaleta tatizo la msingi kwetu. Kwa kawaida baruti ni kitu chenye mlipuko mkubwa. Basi, tuna kawaida ya kutazamia nguvu za Mungu kulipuka kwa hali ya juu sana kama kiwakilishi cha ahadi ya Yesu. Tatizo ni la aina mbili: kwanza, hakuna hali ya kulipuka katika Injili; na pili, Wayunani walikuwa hawana baruti. Baruti iligunduliwa na Alfred Nobel mwaka wa 1866, ambaye ndiye mwanzilishi wa Tuzo za Nobel. Basi, kulitafsiri neno hilo kwa msingi wa neno letu la Kiingereza la baruti kunaweza kutupotosha kidogo, kuwafanya Wakristo watazamie “mlipuko” badala ya kumruhusu Roho Mtakatifu kutengeneza na kuzaa ubora na tabia ya utulivu na utendaji iliyokuwepo katika maisha na huduma ya Yesu.
Nguvu ya Matendo 1:8 ni
Nguvu ya kubadilisha tabia,
Nguvu ya kuangaza,
Nguvu kwa ajili ya mawasiliano,
Nguvu kwa ajili ya utendaji wa dhati, endelevu.
Ni nguvu ya kushuhudia, pamoja na kuwa nguvu katika kushuhudia. Kuna mtu anayefafanua nguvu ya tabia kuwa ni “onyesho lenye nguvu la haiba ya mtu” na hiyo ndiyo tafsiri nzuri ya nguvu za Mungu. Ni onyesho lenye nguvu la haiba ya Mungu – jinsi
239
Mungu alivyo. Linaweza kuwa kitu mlipuko, lakini mara nyingi huonekana kama ushawishi ulioko ndani kabisa katika tabia ya mtu, na kusadiki kunakomgusa yeye na wengine wanaomzunguka. Kazi ambazo Yesu aliahidi kwamba zingefanywa na Roho Mtakatifu ---
Kusadikisha (ktk Yohana 16:7-11);
Kuangaza (ktk Yohana 16:13-16),
Mawasiliano (ktk Yohana 15:26), na
Kuifikia au kuigusa dunia (ktk Matendo 1:8)
-- zaidi sana katika eneo la ushawishi wenye nguvu kuliko eneo la maonyesho au madhihirisho “mlipuko”.
Ona kwamba nguvu hii “inapokelewa”. “Mtapokea nguvu”. Haipatikani kama malipo ya kazi, inapokelewa. Haifikiwi kwa juhudi zozote, inapatikana. Haihitajiki kipawa kikubwa sana ili kupokea chochote. Watu matajiri na maskini kabisa wanaweza kupokea kitu chochote kitolewacho. Bila shaka mtu anakipokea tu. Mungu anataka sana kukupa wewe nguvu ya Roho Mtakatifu – lakini kwa masharti Yake na kwa ajili ya makusudi Yake tu. Yeye amekuagiza ujazwe na Roho Mtakatifu, nafsi pekee ambayo ni nguvu za Mungu.
Tunasoma hivi katika 1Yohana 5:14 – “Huu ndiyo ujasiri tulio nao katika Yeye, kwamba, tukiomba chochote kulingana na mapenzi Yake, anatusikia.”
Kwa kuwa ametuagiza tujae Roho Mtakatifu, tuna uhakika kwamba ni mapenzi Yake. Basi, tukae katika hali ya kutazamia daima na kumwomba daima atujaze kwa Roho Wake, na tumpokee
240
tu katika utimilifu Wake. Ndipo kwa ujasiri kabisa tutaweza kujua kwamba Nafsi ya Roho Mtakatifu siku zote “anasafiri nasi” popote tuendapo, mradi tu tunaishi kutimiza Agizo Kuu la Bwana wetu.
241
Sura Ya 10
Mbweha Tally Ho!
Maana Ya Jina La Kitabu
Najisikia vizuri kupata nafasi ya kujibu swali hili, kwa sababu kazi yote ya Yesu kwetu inapatikana katika jibu nitakalotoa. Hebu kwanza nifafanue mfano uliozaa jina la hiki kitabu.
Mbwa wanapokuwa katika kundi, wanakimbia pamoja na kufanya moja au mengi katika haya manne yafuatayo:
1. Watalala.
2. Watajihami kwa manufaa ya usalama wao.
3. Kama hawatishiwi, watakaribisha wanachama wapya katika kundi lao.
4. Watapigana wao kwa wao.
Lakini, kuna kitu cha kutilia maanani, nacho ni hiki: HAYO YOTE WATAFANYA MPAKA MBWEHA APITE!
Sasa – “kanisa” ni nini? Ingawa tafsiri nitakayotoa hapa ni dhaifu, isiyopendeza na nyepesi sana, kanisa ni Wakristo katika vikundi, wanaokimbia pamoja. Theolojia imejaribu kueleza kanisa kwa njia ya hali ya juu zaidi kidogo inaposema kwamba “ni kusanyiko au ushirika wa waamini waliozaliwa mara ya pili na
242
walioitwa, walio katika Yesu Kristo, walioungana pamoja kwa ajili ya malengo ya kiroho yanayofanana.” Tafsiri yangu mimi ni nyepesi tu na rahisi kabisa na yenye kueleweka, lakini inaeleza hicho hicho. Lakini, kosa kubwa la maana au tafsiri zote hizo si mfano bali ni utendaji halisi. Makanisa mengi hayakimbii. Kweli “yanakimbizwa” (utasikia watu wakisema, “analiendesha kanisa lake”, au, “hao ndiyo wenye kuliendesha kanisa hili”. Au, “kanisa hili linaendeshwaje?”), lakini hayakimbii! Yanaendeshwa kama mitambo inavyoendeshwa, au kama biashara inavyoendeshwa, lakini yenyewe hayakimbii kufukuzia lengo ambalo yamepewa.
Haya – turudi kwenye tafsiri yetu. Kanisa ni Wakristo katika kikundi, wanaokimbia pamoja. Wakristo wanapokimbia pamoja katika vikundi (na ndivyo ilivyo), watafanya moja au mengi katika haya manne yafuatayo.
1. Watalala. Andiko linalofaa kabisa kusomewa makanisa mengi kabisa ni hili: “Amkeni enyi mlalao, mfufuke kutoka kwa wafu.” Miaka mingi iliyopita, mishenari aitwaye John Halsy aliandika maneno haya, mazito kabisa:
Kama ningekuwa mwandishi mwenye kutamani kujulikana kwa kuandika kitabu kifupi kuliko vyote, ningewaendea baadhi ya washirika walio katika makanisa yetu maarufu ya mjini, yaliyotulia, niwaombe kibali chao kuandika maelezo ya kile wanachomfanyia Kristo na kufanya kwa ajili ya dunia. Historia hiyo ingekuwa fupi kweli kweli! Pengine herufi moja au mbili tu zingetosha kueleza kila
243
kitu kinachofanywa na wengi wao kwa ajili ya Bwana aliyewanunua, na kwa ajili ya dunia inayoangamia! Kuna andiko ambalo linaweza kuwapa starehe sana baadhi ya watu wanaoitwa Wakristo. Ni hili – ‘Sisi tulioamini tunaingia katika pumziko.’ Lakini kumbuka kwamba hilo ni pumziko la mtenda kazi baada ya kazi, si pumziko la mvuvi kutokana na kazi. Ila, nina andiko lingine la kuweka pamoja na hili – ‘Ole wao waliopumzika huko Sayuni!’ Ndiyo! Ole, kwa sababu hiyo starehe ni mwizi anayeiba hali ya kujisikia hatia, ikiwaibia waamini na makanisa nafasi yao ya kushiriki pamoja na Kristo katika shughuli iletayo raha kuliko zote duniani.
Ufufuo au kupaza sauti kuamsha watu si vitu vibaya katika kufafanua hitaji la Wakristo wengi na makanisa mengi. Ninasema hivyo kwa aibu kubwa sana, kwa sababu mimi mwenyewe binafsi nimelala katika sauti za baragumu nyingi sana kutoka mbinguni, zilizotolewa ili kuniita niende mstari wa mbele kwenye makabiliano na mapambano mapya. Lakini, ukweli unabaki pale pale kwamba makanisa mengi yenye kukiri Jina la Kristo na kusema kwamba yamejipanga na kuungana na Ukristo ule uliosababisha Kitabu cha Matendo ya Mitume kuandikwa, yamekufa kama makaburi. Huku yakiwa yamelewa sana na dawa ya ubinafsi, na kuzoea sana (na kupenda sana pia) Ukristo usiokuwa na msalaba, na yenye shauku ya kuufanya Ukristo kupendwa sana na kuwa maarufu, wao (na sisi pia) huonekana kama hawana mwelekeo kabisa katika kumfuata Bwana Mkubwa (au, kama ndugu Mkristo mmoja mpendwa alivyosema,
244
“kumfukuzia Kristo hasa hasa”) au kufuata “Kusudi lile Kuu (ambalo ni kuifikia dunia nzima) au kutekeleza ule Mpango Mkuu (yaani, “kufanya watu kuwa wanafunzi” kwa kiwango cha Kristo na kwa kufuata mkakati Wake). Kwa hali hiyo, wanalala tu.
[MZAHA KIDOGO – lakini wenye lengo la kufikisha ujumbe.]
Jamaa mmoja alisema hivi, “Kama watu wote wanaolala kanisani wangepangwa mstari – wangejisikia vizuri zaidi!”
Mwingine ametafsiri mahubiri kuwa ni “mtu mmoja akizungumza katika usingizi wa mwingine”.
Mama mmoja alimpigia simu mchungaji wake saa tisa usiku akasema, “Mchungaji! Nina tatizo kubwa sana. Shida yangu ni kwamba sipati usingizi, hivyo silali kabisa. Naomba unihubirie kidogo!” (Yaani, akisikiliza mahubiri anapata usingizi.)
Uzuri ni kwamba hivyo ni vichekesho, ingawa “wakalia vitu kanisani” mara kwa mara hufanya hayo kuwa kweli. Ila sasa, tunapofikiri uhalisi wa kusikitisha sana wa Wakristo kuishi maisha yao kwa kujitakia mema na kujihudumia au kujihami, na makanisa nayo yakielezwa kwa uwazi kabisa na kwa uhalali kabisa kuwa ni “majitu yaliyolala” (ingawa ukweli ni kwamba si hivyo, na inasikitisha sana kwa sababu, watu wengi hata hawajui hilo jitu linapaswa kufanya nini au linaweza kufanya nini au lingeweza kufanya nini kama limeamka kabisa na kwa ukamilifu. Basi, wanaelewa kwa udogo sana jinsi ambavyo kanisa limelala kweli),
245
mbona hayo yanakuwa kama hukumu badala ya kuwa vichekesho. Kwamba kanisa ni “jitu lililolala” ni wazo la Shetani kabisa.
Sasa, tufikie sehemu ya pili ya kanuni zile tulizotaja.
2. Watahakikisha usalama wao wenyewe. Fikiri tofauti kubwa iliyo kati ya kujihami na kuishi tu, na huduma ya kweli. Tofauti hiyo mara nyingi haionekani kwa sababu kwa kawaida makanisa hujitia katika mpango ambao ni mchanganyiko wenye kupooza, ambao unatoka katika hayo mawili. Wana “ibada” na wanatoa “nafasi za kuhudumu” lakini je, matokeo yanakaribia utendaji na matokeo yaonekanayo katika Kitabu cha Matendo ya Mitume? Huduma ya kweli ina kujitolea, kujihatarisha na hali ya kutokujua kilicho mbele, na masharti yake yanapangwa na Yeye anayesimamia shughuli yenyewe. Wakati mtu anapoingia katika huduma ya kanisa la siku hizi, anainuliwa kwamba ni “Mkristo wa kipekee sana,” lakini mambo kama hayo yanaonyesha tu ujinga na kujipenda kwa mwamini “wa kawaida”. Labda tuulize swali hapa – je, Mkristo wa kawaida ndiye mbaya katika wazuri, au ndiye mzuri katika wabaya? Vyovyote vile, kanisa la kawaida ni wazi kwamba liko kwenye kujihami, likihesabu kondoo zaidi ya kuwalisha na kuwawezesha kondoo ili watumwe kwenda kama ‘kondoo katikati ya mbwa mwitu’. Kanisa la kawaida linajihusisha sana na majengo, bajeti, vipeperushi, idadi ya watu na Biblia – vitu ambavyo, ingawa ni vizuri sana vinapotumiwa sawasawa, husababisha “kifo” vinapokuwa lengo kuu.
246
Hivyo ni (au vinaweza kuwa) vitu muhimu vinavyoshikika kanisani, lakini kuchukuliwa navyo ni hatari kwa habari ya Makusudi Halisi ya kanisa. Kanisa linalojihami ni wazo la Shetani kabisa.
Tuangalie sehemu ya tatu.
3. Kama si tishio kwao, mbwa katika kikundi watakaribisha wanachama wapya. Wakati mwingine, makusudi nyuma ya kutafuta washirika wapya kanisani, kukua kwa kanisa na “mikutano ya uinjilisti” yanahitaji kuchujwa vizuri kabisa. Makusudi ni rahisi sana kupotoshwa na kuharibiwa kama yanakuza au kutukuza majina ya watu na kuonyesha mafanikio ya viongozi binafsi pamoja na mashirika au madhehebu au taasisi zinazo-ongozwa nao. Ile hali ya kujilinda na uhasama wa baadhi ya viongozi ni dalili ya kutambua kwao makusudi yao mchanganyiko yaliyoko nyuma ya wao “kujenga” majengo, taasisi, taratibu, makundi ya watu na kadhalika. Hakuna kusudi la mtu yeyote lililo safi kabisa, lakini kukua kwa kanisa kunaweza kukuza sifa ya mtu na kuficha hali ya kujipenda na kujisifu ya ndani, japo matangazo yatolewayo ni kwamba kuna nia safi na shauku safi kabisa ya “kumtumikia Bwana”. Sikuzote mwili uko karibu sana, na ni kitu hatari kilichojificha katika ngozi laini sana ya hali ya kiroho. Hapo ninakiri udhaifu wangu pia, na kusema ukiri wa wachungaji wengi walio wakweli na wacha Mungu ambao nimewafahamu. Ninajua makanisa mawili madogo sana ambayo yalijikuta katika jamii zenye kukua haraka. “Wazee” waliokuwa
247
katika makanisa hayo waliitikia kukua kwa makanisa hayo kwa njia za ajabu sana. Kote, viongozi walimwambia mchungaji wao, “Inabidi tuwe makini sana kuhusu hawa watu wapya wote wanaokuja maana, ikiendelea hivi, tutapoteza utawala wa kanisa letu.” (!!!) He! Hivi kweli, hali hiyo ya kujijali, kujifikiria na kujihami inaweza kudumu katika kanisa “linalokua”? Je, hoja kama hizo zinaweza kutoka kwa viongozi wa kanisa? Kila kiongozi mwenye cheo chochote kanisani au wadhifa amewahi kukabiliana na mambo kama hayo katika uongozi – na pengine yeye mwenyewe yuko hivyo. Hii ni namna moja tu ya sura ambayo mwili unaweza kuvaa. Kwa kawaida, mwili aidha unapenda utendaji au unapinga, na viongozi wa kiroho na washirika waaminifu kanisani wanalengwa na Shetani ili kusababisha maonyesho kama hayo, ya tabia ya mwili. Baada ya zaidi ya miaka arobaini katika huduma, nimegundua kwamba lazima kila mara nijitahidi kuuweka mwili “chini ya mamlaka”, na kuuhesabu (Warumi 5:6, 11; Wagalatia 2:20).
Lakini kumbuka mahali mambo yanapobadilika katika ule mfano wetu: MPAKA MBWEHA APITE! Mbweha akipita, na aonekane wazi kabisa na wale mbwa, hawapati nafasi hata ya kulala. Hawatashughulika na kujihami tena. Watawapokea wanachama wapya katika kundi lao wanapokuja, lakini mbwa watakaokuja ni wale walioko tayari kuingia katika mpango wa kumwinda yule mbweha na kujiunga na wale mbwa wengine wote watakaohusika. Ingawa mbwa wenyewe wanaweza kugongana kwa nguvu zaidi na
248
mara nyingi zaidi kuliko mwanzo, hawataona vidonda vyao na uvimbe wao – kwa sababu wana mambo makubwa zaidi ya kufanya kuliko kungurumiana, kubwekeana na kutaka kuumana. Mbweha akiwa anaonekana, mbwa hao watakimbia kwa pamoja wakiwa na maono yanayofanana na makusudi pia.
MBWEHA NI NINI?
Je, mbweha ni nini kwa Mkristo na kwa ushirika wa waaminio? Mimi binafsi nahesabu kuwa kitu muhimu cha kufukuzia katika maisha ya Mkristo ni Yesu Kristo. Kazi kubwa katika maisha ya Kikristo ni “kumfuata Yesu” au “kumtafuta Yeye kwa bidii zote”. Kwangu, hilo ndilo la mwisho kabisa. Lakini, utaratibu uliowekwa kwa ajili ya kuwaingiza wafuasi wengine ndiye huyo mbweha ambaye Yesu alimweka mbele ya wanafunzi Wake ajulikanaye kama “Agizo Kuu”. Viongozi wa Kikristo wana kawaida ya kuweka mbweha wadogo ili “watu wao” wawafukuzie – vitu kama mahudhurio, michango kwa ajili ya bajeti, mambo ya ujenzi, mikutano ya uamsho ya mara kwa mara, na mikazo mingine mbalimbali. Lakini hao “mbweha wadogo” wanaweza “kuharibu mizabibu”! Wanakuwa ndiyo kiini kikubwa na malengo makubwa, wakielekeza usikivu wa waaminio katika shughuli na mipango ambayo inawasaidia wao zaidi kuliko kuifikia dunia.
Wakulima kadhaa walikuwa wanapoteza muda wao wakijisifu juu ya mbwa wao wa kuwindia. Mmoja akasema, “Nadhani mbwa
249
wangu anaweza kusikia harufu ya miaka hamsini iliyopita.” Mwingine akasema, “Acha mchezo bwana. Hakuna mbwa anayeweza kusikia harufu ya zamani hivyo.” Yule aliyetangulia akasema, “Nadhani mbwa wangu anaweza.” Mwindaji wa tatu akasema, “Ninajua jinsi ya kupata ukweli. Nakumbuka Baba yangu akisema kwamba nilipokuwa mtoto mdogo palikuwa na mbweha mzee aliyekuwa anapita chini ya nyumba yetu kila jioni. Ni miaka arobaini na zaidi sasa. Si twende mpaka pale tuone kama mbwa wako anaweza kunusa hiyo harufu?” Basi, wakampakia mbwa kwenye gari na kwenda mpaka hiyo nyumba ya zamani. Wakamfikisha pembeni mwa nyumba hiyo na wakamzungusha mpaka kandoni. Mara yule mbwa akaanza kupiga kelele na kuonyesha dalili za kunusa na kufuata – akijivuta kwa nguvu atoke kwenye kamba iliyokuwa imemfunga. Mwenye mbwa akamwachia. Mara, mbwa yule akakimbia mbio, akavuka uwanja uliokuwa mbele ya nyumba. Alipokaribia kama yadi ishirini mbali na nyumba, mara aliruka juu kama futi sita! Mtu mmoja akasema, “Huyo mbwa ana matatizo gani?” Yule mkaazi wa pale akajibu, “Hana matatizo yoyote. Miaka arobaini iliyopita, hapo mahali kulikuwa na uzio, na yule mbweha alikuwa anarukia hapo!” Yule mbwa akaendelea kulia na kunusa huku akivuka ule uwanja. Mara akakata kulia na kufuata njia kando ya nyumba. Yule mkaazi wa zamani wa pale akasema, “Miaka arobaini iliyopita kulikuwa na kichaka hapo na miti, na yule mbweha alikuwa anaizunguka. Kweli, mbwa wako ananusa njia ya yule
250
mbweha wa zamani.” Mbwa akaendelea kwenda pole pole akinusa na kulia mpaka akapotelea kabisa. Wale wawindaji walikuwa wanamwangalia sana huyo mbwa, hawakuona akitoweka. Hatimaye mmoja akasema, “Hebu tumfuate, tuone atatufikisha wapi.” Wakafuata kweli, lakini pamoja na kumtafuta sana kila mahali, hawakumpata. Baada ya kumsaka mchana kutwa, ilibidi waachilie mbali shughuli hiyo, wakitumaini kwamba mbwa yule angerudi mwenyewe baadaye. Lakini haikuwa hivyo. Mbwa akawa amepotea, na hawakuweza kumpata popote. Baada ya kusubiri majuma kadhaa na kuendelea kumtafuta hapa na pale, na kuuliza, walikata tamaa na kuachilia mbali msako wao.
Miaka miwili baadaye, muda mrefu tu baada ya kuachilia mbali kumtafuta mbwa na baada ya kupoteza matumaini, yule mwenye mbwa akapigiwa simu jioni moja. Mpiga simu akasema, “Je, hapo ni nyumbani kwa Reks, mbwa mwindaji?” Mwenyewe akasema, “Ndiyo – alikuwa akikaa hapa, lakini amepotea kwa muda wa miaka kama miwili hivi. Wewe nani, na kuna nini?” Akajibiwa hivi: “Ni hivi mzee. Maelezo yangu yatakushangaza. Mimi ni meneja wa duka kubwa sana katika mji wa New York. Nimemtambua mbwa wako kwa jina na anwani yako uliyomwekea shingoni. Hapa dukani, amekaa analinda vazi la ngozi ya mbweha la zamani, na nimeshindwa kumtoa.” Mwenye mbwa akaacha kushangaa, akaifikiri kidogo halafu akasema, “Mheshimiwa. Unaweza kumrudisha mbwa wangu kwa gharama zangu?” Yule mwenye duka akasema,
251
“Nimefikiri hilo, na nimekwisha fanya utafiti, na gharama yake ni kubwa sana.” Mwenye mbwa akauliza, “Hiyo ngozi yenyewe ina thamani gani?” Mwenye duka akajibu, “Ni dola 65”. Baada ya kufikiri kidogo, mwenye mbwa alisema hivi, “Basi mzee, naomba unitumie hiyo ngozi, halafu uache duka lako wazi kwa dakika tano tu kesho”.
Wapendwa – wakati umefika – kwa ajili ya Mungu na kwa ajili ya Kristo na kwa ajili ya mabilioni ya watu waliopotea, na kwa ajili ya ushirika wa waaminio, na kwa ajili ya kila kitu kilicho kweli na kizuri na chema, kwetu sisi kurudi hadi “nyumbani kwetu” kiroho, tupate tena kunusa ile harufu ya zamani (yaani, Agizo Kuu) – harufu ambayo itakuwa na thamani na maana zaidi sana kuliko hivi vitu vingine tunavyofukuzia – dunia na mwili – na kuanza kumfuata Mbweha Mkuu.
Huyo Mbweha Mkuu ni nani? Ni kuifikia dunia yote. Dunia Yote. Kuifikia dunia yote kwa ukamilifu wake wote. Ndiyo Mbweha Mkuu wa Kristo – aliyewaagiza watu Wake wamfukuze. Kila Mkristo anapaswa atazame kwa makini sana na kwa muda mrefu sana huyo Mbweha Mkuu kila siku ya maisha yake. Kumtazama huyo Mbweha kwa muda mrefu kutapelekea kuelewa mambo kadhaa muhimu. La kwanza ni maono. Lingine ni mkakati. Lingine ni maongezeko yaliyohamasishwa, dhana ambayo bila shaka ilikuwa na sehemu muhimu katika kutokea kwa Kitabu cha Matendo. Na kitu cha mwisho ni kuelewa Ufikiaji Dunia Yote kwa ukamilifu, - lengo
252
la kuifikia dunia nzima, na lengo la ufikiaji ambao utakuwa kamili – yaani, wenye kuhusisha kila njia iliyoagizwa na kufunuliwa, ili kukamilisha kazi yenyewe.1
1 Hakuna chochote kilichosemwa katika hii sura fupi ambacho kinapaswa kuhesabika kuwa kinyume cha kanisa kwa namna yoyote ile. Tayari kuna kulipiga kanisa kwa kila namna – mimi sitaki kuwa na hatia ya kuongeza. Ila, tahadhari hii ichukuliwe kwa uzito wake. Kanisa tukufu la Mungu – Mwili na Bibi Arusi wa Kristo, Jengo la Mungu, “nguzo na msingi wa ukweli” linahitaji kuongeza idadi ya washiriki wenye kuomba, kwenda, kutoa na kuunga mkono mkakati huo kuliko wakati mwingine wowote. Lakini, kusudi mbadala au utaratibu bandia (“mbweha wadogo”) vitaharibu utukufu wa kanisa na kuliruhusu lilaumiwe kihalali kabisa, na kukataliwa na wengi. Tunaomba Mwili wa Kristo umpe Yeye kitu tendaji kabisa kwa ajili ya kutimiza Agizo Kuu! Tunaomba Bibi Arusi wa Kristo ampende Kristo sana kiasi kwamba kule kutajwa tu kwa Agizo Kuu kusukumwe na pendo la Kristo kulitimiza! Tunaomba Jengo la Mungu liwe Hekalu la kutosha kabisa kumwonyesha Mungu wetu kwa dunia nzima!
253
Kumalizia
Maisha Ya Mbwa Wa Mwituni
Wale watu ambao nimepata nafasi na fursa ya kufanya kazi nao katika kufanya watu kuwa wanafunzi, na utaratibu wa kuifikia dunia ni miongoni mwa Wakristo wenye motisha kubwa niliowahi kuwafahamu. Mfano mzuri sana ni mwanafunzi kijana aitwaye Ian Bowers. Amekuwa akisonga mbele na kuendelea katika ufahamu wa kuwafanya watu kuwa wanafunzi na kujihusisha kwa miaka kadhaa sasa. Wakati fulani aliwahi kutunga shairi kuhusu mfano wangu wa “Mbweha huyo!” Nimelisoma mara kadhaa. Niliomboleza wakati ujumbe wa shairi hilo uliponifikia na kunigusa moyoni. Kwa kibali chake, ninamalizia kitabu changu kwa shairi hilo. Naomba na wewe ubarikiwe kama mimi nilivyobarikiwa.
Maisha ya mbwa wa mwituni ni rahisi tu,
Ingawa si maisha ya starehe.
Hebu nitoe mtazamo mpya
Maana tunaishi maisha ya uhitaji.
Hayo mahitaji yanaonekana kututawala
Na kusimamia maisha yetu.
Lakini kila siku ninajiuliza
Ikiwa mahitaji hayo si uongo tu.
Ni hivi: Kila siku ni yetu ya kushinda
254
Hatuna ratiba yoyote ya kufuata.
Lakini, hili hitaji hutujia
Hitaji la kulala.
Katika uwanja au chini ya mti wa kivuli
Au chini ya mbingu iliyojaa nyota
Unatamani maisha ya mbwa
Unapotuona tumelala hapo chini.
Ila, usiache kuendelea na hadithi yangu sasa.
Sikiliza, na usikie vizuri sana.
Ugundue kwamba maisha ya mbwa anayelala
Ni hatua moja tu kutoka Jehanamu.
Maana nikiamshwa tu kwa dakika
Kitu fulani hujigusa ndani yangu
Nami nina njaa – njaa sana
Hitaji langu ni kula.
Mjini nitapata takataka kidogo
Msituni nitapata mnyama mdogo
Lakini nikisha tosheka
Ninarudi haraka tu kulala usingizi.
255
Na kwa hili wala sikutishwa
Nilihesabu kuwa ni hazina ya dhahabu
Wakati mbwa mvivu kuliko mimi
Alipokaribishwa kundini.
Je, bado ni maisha ya mbwa
Yanayotamaniwa na moyo wako?
Rafiki yangu, hujui hata kidogo
Maana, kuna zaidi ya hayo.
Hatimaye kisa changu kitakuwa dhahiri sana
Maana, sasa pokea mwanga
Upande mbaya wa maisha ya mbwa mwitu
Ni hitaji la kupigana.
Lakini, kupigana kwa sababu gani? Nikuulize sasa
Je, waweza kuniambia wakati
Wa kuinuka kinyume cha mbwa mwenzangu
Au pengine kumkomeshea maisha yake?
Yeye ni mbwa mwenye ngozi na mkia
Anayo meno na macho ya kuona
Lakini lazima athibitishe kwamba yeye ni bora
Au wakati mwingine ni mimi.
256
Basi, unguruma na ubweke, na ung’ate
Kiburi chetu kutosheleza
Mmoja atashinda hii vita ya kijinga
Na inawezekana hata mmoja akafa.
Na vita inapokuwa imekwisha
Sikuzote ni hasara, hakuna faida
Na kile tulichothibitisha
Ni kwamba mbwa wanaweza kuwa na kiburi sana.
Sidhani kama ni sahihi kusema
Kuna hitaji la kupigana
Nadhani badala yake ni kwamba tunakosa la kufanya
Na tuko hatua moja tu kutoka kwenye kufa.
Je, unasikiliza kwa makini?
Rafiki yangu, unasikiliza kweli?
Maana hadithi yangu haijaisha.
Sasa ndiyo tu imeanza.
Kuna hitaji moja ninalokubali
Tena nasema pasipo aibu
Huyu mbwa mwitu anapenda, na hata anaishi
257
Kwa ajili ya kukimbiza au kufukuza.
Lakini si kukimbiza tu, rafiki.
Ni kukimbiza ambako ni kuzuri sana
Kukimbiza kwenye kuhamasisha maisha yangu
Na kunakoshika akili yangu.
Si wale mbweha wadogo.
Hao nimewahi kuwafukuza wote.
Wao ni rahisi kuwashika na kuwamaliza
Nikawa nimechoshwa upesi nao.
Siku moja ikatokea
Kamwe sitasahau
Kulitokea harufu fulani hewani
Nikapata hamu kubwa.
Nikainua pua yangu angani
Nikasimama kwa miguu yangu
Ndipo nikawaona wale mbwa wengine
Wakiwa tayari kama mimi.
Kiongozi wetu ni Salvadori
Wa kikundi chetu cha mbwa kumi na mbili
258
Ngozi yake ilikuwa manjano kabisa
Na michirizi myekundu mgongoni.
Huyu ndiye mliyekuwa mnamsubiri
Ndivyo alivyosema, huku macho Yake yaking’aa
Huyu ndiye mbweha ambaye mkimshika
Hakika itagharimu maisha yako.
Inueni pua zenu hewani
Inuseni hiyo harufu
Jifunzeni muijue vizuri,
Jifunzeni muijue vizuri.
Na wakati msipoweza kuniona
Inuieni pua zenu juu
Pateni hiyo harufu na kuifuata
Mjue kwamba nipo.
Nikahisi moyo wangu unaongeza mapigo
Shinikizo la damu likaongezeka
Kadiri hiyo harufu ilivyozidi kuwa na nguvu
Nguvu zaidi.
Halafu bila ya maonyo
259
Kama radi ya umeme
Kiongozi wetu akageuka na kujitupa
Kuelekea katika giza la usiku.
Tulisimama kidogo tu
Na kutazamana machoni
Tukajua gharama itakayotukabili
Lakini hatukujua zawadi tutakayopata.
Na kama ni kumshika huyo mbweha,
Hatukupaswa kukawia zaidi.
Maana kazi ilikuwa ni kubwa sana
Harufu ilipoanza kupotea.
Lazima ibakie kwenye pua yetu
Kusudi letu lazima liwe wazi
Tutamshika huyu mbweha mwenye nguvu
Kauli mbiu yetu itakuwa HAYA TENA – MBWEHA HUYO!!
Pua zangu zikapanuka, misuli zangu zikakaza
Nikaruka kutoka mahali pangu
Miguu yangu ya mbele ikakutana na ardhi
Na mbio zikawa zimeanza.
260
Lakini rafiki yangu, usifikiri unajua
Nilichokuwa ninakimbilia
Zawadi haikupatikana katika mbweha
Ilikuwa kitu kingine zaidi.
Sikuwa naendeshwa na hitaji
La kulala au hata kula chakula
Badala yake, nilikuwa nimetawala kabisa
Kilichokuwa kinanishikilia hapo kwanza.
Je, unasikiliza kwa makini sana?
Je, rafiki yangu, unasikiliza?
Zawadi ni hii: Maisha sahihi
Niliyoishi kulingana na kusudi.
Ningepumzika nile, ningepumzika nilale
Uchovu uliniambia wakati wa kufanya hivyo
Lakini nguvu zilipokuwa zinanirudia tu
Ufukuzaji uliendelea.
Kwa habari ya kupigana, jifunze kweli hii
Hatukuwa tena na nafasi!
Tulikuwa tumepata changamoto ya maisha
261
Yenye kushika akili yetu.
Maana hatukufukuzia kitu bure tu
Yaani mbweha tusiyemwona
Tulijua yeye ni mjanja
Basi, tukafukuza kwa mkakati.
Hatukuhukumu wala kutishia
Wageni waliokuja kundini
Tuliwashirikisha maono yetu kwa ujasiri
Na kuwaingiza pia katika kumtafuta.
Hii njia, hiyo zawadi kuu
Mbwa wengine hawakuiona
Na wengine waliingia katika mbio
Isingekufa na mimi.
Sasa jifunze hili somo la mbwa mzee
Jifunze vizuri, vizuri sana
Kwa kila mbwa anayekufa
Watatu zaidi wajiunge.
Kwa hiyo usifikiri unaniona sasa
Mbwa dhaifu anayekaribia kufa
262
Nuru yangu itang’aa bado
Hata nitakapovuta pumzi yangu ya mwisho.
Kwa sababu nimewafundisha
mbwa wengine wa mwitu
Na nimewafundisha hilo vizuri sana
Nimewafundisha jinsi ya kuinua pua zao
Nimewafundisha jinsi ya kunusa.
Kitu kingine nilichowafundisha
Cha muhimu zaidi sana
Nimewafundisha wote mkakati nilioishi na kuufuata
“Ukimbiaji”.
Sasa mmesikia hadithi yangu.
Je, ulisikiliza kwa makini?
Je, unatamani maisha ya mbwa
Ambayo ni hatua moja tu kutoka Jehanamu?
Changamoto iko mbele yako
Je, utaongeza mfumuko?
Nenda uingie katika mbio
Kimbia na wewe, na UKIMBIE VIZURI!
- Mtunzi ni Ian Bowers
263
FAHIRISI
264
Muhtasari Wa Kila Sura
Sura Ya Kwanza Maono Ni Muhimu Kiasi Gani? (Mithali 29:18)
I. Dhana Ya Kiroho
A. Umuhimu Wa Maono
B. Maana Ya Maono
II. Hali Ya Kusikitisha
A. Hakuna Maono Madhabahuni
B. Hakuna Maono Katika Viti
C. Hakuna Maono Katika Maisha Ya Kila Siku
III. Matokeo Yake Mabaya
A. Watu Huacha Kujizuia – matokeo ya kiadili ya kutokuwepo kwa maono
B. Watu Husambaratika – matokeo ya kijamii ya kutokuwepo kwa maono
C. Watu Huwa Tayari Kuhukumiwa – matokeo ya kibinafsi ya kutokuwepo kwa maono
D. Watu Huangamia – matokeo ya kiroho, ya milele ya kutokuwepo kwa maono
Sura Ya Pili Agizo Lenye Kuamua Wajibu Wetu (Mathayo 28:18-20)
I. Uhakikisho Nyuma Ya Agizo Lenyewe
265
A. Mamlaka Ya KiMungu
B. Mamlaka Iliyotolewa
C. Mamlaka Stahili
D. Mamlaka Iliyofafanuliwa
II. Wajibu Katika Agizo Lenyewe
A. Amri Ya Kusonga Mbele Ya Pekee Kwa Kanisa (Kwa Mkristo Pia)
B. Kuligawa Agizo
1. Watenda Kazi Watumiwe
2. Kuingia Shambani
3. Kupanua Maono
4. Kuwashuhudia
5. Kuwaingiza Kazini Wanaopatikana
6. Kuelimisha Na Kuwajenga Walio Kazini
7. Kumtazamia Yeye (Bwana) Kutenda Kazi
C. Je, Ni Agizo Kuu Au Ni Kupuuza Kukuu?
Sura Ya Tatu Wazo Linaloamua Njia Tutakayotumia
(Mathayo 28:19)
I. Kufanya Wanafunzi
A. Mwanafunzi
B. Mwenye Kufanya Wanafunzi
C. Tendo La Kufanya Wanafunzi
D. Nidhamu Husika
266
II. Kufanya Wanafunzi Kunakosababisha Huduma Ya Kujizidisha
Sura Ya Nne Ufunguo Ulioko Mlangoni Mwa Historia Ya Kanisa
(Matendo 1:1-5)
I. Kitabu Cha Kwanza Kinatajwa
A. Injili Kulingana Na Luka
B. Luka Alikuwa Nani, Na Aliingiaje Katika Hadithi?
C. Kweli Za Tafakari
1. Mfano Wa Kanisa Kama “Mwili Wa Kristo”
2. Luka Aliandika Vitabu Viwili Vya Ajabu
II. Mwanafunzi Binafsi Anatajwa
A. Moja Ya Nne Ya Agano Jipya Iliandikwa Na Mtu Mmoja!
B. Kwa Nini Luka Aliandika Vitabu Hivi Viwili Kwa Mtu Mmoja?
C. Ushuhuda Binafsi
III. Tamko La Wazi Kuhusu Kusudi La Kuandika
A. Yote Ambayo Yesu Alianza Kufanya Na Kufundisha
B. Je, Yesu Anafanya Nini Sasa?
1. Anaendelea Kufanya na Kufundisha
2. Kila Aaminiye Ni Chombo Hai Cha Kuhifadhi Uwepo Wake
267
C. Je, Yesu Alitumia Watu Aina Gani?
1. Wa Kawaida
2. Waliochaguliwa
3. Walioamini
4. Walioamriwa
5. Waliotawaliwa
Sura Ya Tano Vinavyotakiwa Ili Kufanya Wanafunzi, au
Tiba Ya Daktari Kutibu Kuacha Kukuu
(Luka 1:1-14)
I. Wajibu Binafsi
II. Utafiti Wa Dhati
III. Vyanzo Sahihi
IV. Uzalishaji Unaodumu
Sura Ya Sita Mpango Wa Mungu Wa Kuongeza (2Tim. 2:2)
I. Picha Ya Mwanafunzi Mwenye Kuongeza Wanafunzi
A. Ni Mwana
B. Ni Askari
C. Ni Mwanariadha (mkimbiaji)
D. Ni Mkulima
E. Ni Mtenda Kazi
F. Ni Chombo
G. Ni Mtumishi
268
II. Utaratibu Wa Kuongeza Wanafunzi
A. Mpango Unamfikiaje Mwanafunzi?
B. Nini Kilichomo Katika Mpango Wa Kusikia?
C. Mwanafunzi Akisha Wezeshwa, Anafanya Nini?
III. Mifano Yenye Kuonyesha Umuhimu Na Uwezo
A. Mwinjilisti
B. Siku Ya Pentekoste “Kila Siku”
C. Kuongezwa Fedha
D. Maono Ya Kuifikia Dunia Kwa Kufanya Wanafunzi
Sura Ya Saba Hekima Ya Mkakati Wa Yesu (1Wathes. 3:8)
Sura Ya Nane Jinsi Kiwango Hiki Kifanyavyo Kazi Kanisani
(Waefeso 4:7-14)
I. Mtoa Vipawa
A. Alishuka
B. Alipaa
C. Yuko Juu Ya Vyote
II. Vipawa Vyenyewe
A. Mitume
B. Manabii
C. Wainjilisti
269
D. Wachungaji Waalimu
III. Malengo Ya Kutolewa Kwa Vipawa Hivi
A. Kupata Viungo
B. Kuviwezesha Viungo
C. Kuvitumia Viungo
Sura Ya Tisa Maneno Yake Ya Mwisho, Wosia Wake
(Matendo 1:8)
I. Mkakati Kwa Ajili Ya Kuenea Kwa Injili
II. Chanzo Cha Ushuhuda Wa Injili
III. Mada Ya Ushuhuda Wa Injili
IV. Upeo Wa Ushuhuda Wa Injili
A. Hali Yako Inayokukabili
B. Mazingira Yako Hapo Ulipo
C. Eneo Lako Kimataifa
V. Siri Ya Ushuhuda Wa Injili
270
Maswali Na Mapendekezo Kwa Ajili Ya Kujifunza Hiki Kitabu
Kwa ajili ya Sura ya Kwanza, “Maono Ni Muhimu Kiasi Gani?”
1. Toa maana mbili za maono ya KiMungu.
2. Nini matokeo yanayofuata, wakati watu wa Mungu wanapokuwa hawana maono?
Kwa ajili ya Sura ya Pili, “Agizo Lenye Kuamua Wajibu Wetu”.
1. Nini kazi saba za Agizo Kuu? Ngapi katika hizo ni amri?
2. Ni mpango gani mbadala ambao Shetani ametoa chini ya kila kazi, katika hizo saba?
Kwa ajili ya Sura ya Tatu, “Wazo Linaloamua Njia Tutakayotumia”.
1. Toa maelezo kuhusu kila moja katika maneno haya: “Mwanafunzi,” “Mfanya Wanafunzi,” “kufanya Wanafunzi,” na “Nidhamu”.
2. Nini tofauti kati ya Ukristo wa kawaida, wa kuhudhuria kanisani, na maisha ya Kikristo yenye kuzaa huduma ya maongezeko?
Kwa ajili ya Sura ya Nne, “Ufunguo Ulioko Mlangoni Mwa Historia Ya Kanisa”.
1. Toa maelezo mafupi kuhusu utaratibu wa kufanya wanafunzi wa Paulo hadi Luka hadi Theofilo.
271
2. Tuna ushahidi gani kwamba Theofilo “alishika” huo mkakati na “kukimbia nao”?
Kwa ajili ya Sura ya Tano, “Vinavyotakiwa Ili Kufanya Wanafunzi, au
Tiba Ya Daktari Kutibu Kuacha Kukuu”
1. Orodhesha na kueleza kwa kifupi mambo manne ambayo Dakta Luka alifanya, na mwanafunzi Theofilo.
2. Nini umuhimu wa kila hatua katika utaratibu mzima? Je, mfanya wanafunzi anaweza kupunguza hata moja katika hizi na kutazamia mafanikio katika kufanya wanafunzi? Je, ni hatua ngapi katika hizi ambazo wewe unafanyia kazi kwa sasa kwa ajili ya kufanya mwanafunzi?
Kwa ajili ya Sura ya Sita, “Mpango Wa Mungu Wa Kuongeza”.
1. Nini picha saba za mwanafunzi katika 2Timotheo sura ya 2? Je, ndiyo imekamilika, au ni pendekezo tu?
2. Eleza kidogo ule mkakati wa vizazi katika 2Timotheo 2:2, ukionyesha kilicho cha lazima ili “kuhakikisha” maongezeko ya vizazi vinne.
Kwa ajili ya Sura ya Saba, “Hekima Ya Mkakati Wa Yesu”.
1. Eleza hekima ya mkakati wa Yesu kiutaratibu, alipowafundisha Mitume Wake kumi na mbili.
272
2. Je, unaamini maelezo ya mfumo yaliyotolewa katika hii sura kuwa ni ya msingi, au ya bahati mbaya, au ya kubahatisha tu katika mkakati wa Yesu?
Kwa ajili ya Sura ya Nane, “Jinsi Kiwango Hiki Kifanyavyo Kazi Kanisani”.
1. Je, mkakati wa kufanya wanafunzi kwa vizazi ziaid ya kimoja unaweza kufanya kazi katika kanisa la siku hizi? Kivipi?
2. Fafanua kidogo yale maelezo ya mipango miwili yaliyotolewa katika sura hii – mfano wa kawaida na ule utolewao na Waefeso 4:7-14.
Kwa ajili ya Sura ya Tisa, “Maneno Yake Ya Mwisho, Wosia Wake”.
1. Ni neno gani moja katika Kitabu cha Matendo linalodhihirisha mkakati wa Mungu kwa ajili ya kuenezwa kwa Injili? Nini maana zake mbili? Nini uhusiano kati ya hizo maana mbili za neno hilo?
2. Nani aliye katika “kundi la watenda kazi” wa Mungu, na wanapaswa kufanya kazi katika maeneo gani?
3. Watenda kazi watafanikishaje kazi hiyo?
Kwa ajili ya Sura ya Kumi, “Haya Tena, Mbweha Huyo!”
1. Fafanua ule mfano wa “Mbweha”.
2. Je, mfano huo ni wa kweli kulingana na mambo uliyoona katika kanisa la mahali?
3. “Mbweha Mkubwa” ni nini?

No comments:

Post a Comment